Tuesday, December 27, 2011

Serikali hoi kifedha

Na Saed Kubenea


SERIKALI ya Rais Jakaya Kikwete iko taabani kifedha. Haina uwezo wa kuajiri watumishi wapya wala kupandisha vyeo wale waliopo, MwanaHALISI limegundua.

Sasa imeagiza ajira zote serikalini katika mwaka wa fedha wa 2011/2012 zipunguzwe kwa asilimia 50. Vilevile upandishaji vyeo upunguzwe kwa kiwango kilekile.

Kwa hatua hii, serikali inabadilisha maamuzi ya bunge lililoidhinisha mapato na matumizi yake Juni mwaka huu.

Serikali imekiri kutokuwa na uwezo wa kutekeleza bajeti iliyopitishwa na bunge, kuwa na vipaumbele tofauti na mashaka na vyanzo vyake vya mapato.

“Baada ya serikali kutafakari uwezo wake kwa kuzingatia vipaumbele na vyanzo vya mapato, imeamuliwa bajeti iliyokuwa imependekezwa kwa ajili ya mishahara ya watumishi wapya na upandishaji vyeo, ipunguzwe kwa takribani asilimia hamsini, umeeleza waraka wa ikulu.

Utekelezaji wa hatua hiyo ya serikali ulianza rasmi Novemba mwezi uliopita.

Waraka wa serikali umesainiwa na Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejementi ya Utumishi wa Umma, Habu Mkwizu na kupelekwa kwa makatibu wakuu wote wa wizara, wakuu wa idara na taasisi zake nyingine.

Matokeo ya uamuzi huu, waraka unaeleza, “ni kwamba kila mwajiri sasa atalazimika kuandaa upya mahitaji yake ya ikama (taratibu za ajira na malipo) kwa kuzingatia ukomo uliorekebishwa wa bajeti uliotolewa na wizara ya fedha kwa mwaka 2011/12.”

Kila mwajiri amepelekewa jedwali la viwango vya ajira mpya, mishahara na nyongeza; na kutakiwa kufuata mkondo huo wakati wa kuwasilisha maombi mapya ya vibali vya ajira mpya kwa mwaka huuwa fedha.

Waraka unaagiza waajiri kuweka kipaumbele katika kutenga “nafasi za kutosha kwa ajili ya wataalam wa sekta za Elimu, Afya, Kilimo na Mifugo.”

Nakala ya waraka wa ikulu imepelekwa pia kwa Katibu Mkuu Kiongozi na Msajili wa Hazina.

Jedwali elekezi linaonyesha kila wizara, idara na asasi/taasisi ya serikali itapata shilingi kiasi gani kwa ajili ya nyongeza ya mshahara, idadi ya ajira kwa mwaka huu na ukomo wa kiwango cha kulipa mishahara yote yakiwa katika eneo la punguzo la asilimia 50.

Kwa mfano ikulu imebakiwa na Sh. 18,961,106 kwa ajili ya nyongeza za mishahara; itaajiri watumishi 10 na itapewa jumla ya Sh. 2,314,917,441, linaonyesha jedwali.

Miongoni mwa waliodhinishiwa kuajiri watumnishi wengi zaidi ni Polisi (1,351), Magereza (485), Wizara ya Elimu (417), Kilimo (294), Jamii, Jinsia na Watoto (247), Maliasili (152) na Kurugenzi ya Makosa ya Jinai (111).

Wale ambao hawataajiri hata mtumishi mmoja ni Ngome, Mahakama ya Ardhi, Mahakama ya Kazi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Lakini miongoni mwa waliobakiziwa fedha nyingi kwa mujibu wa ukomo matumizi kwa mwaka huu ni pamoja na Ngome (288,708,794,879), Polisi (153,274,299,225), Jeshi la Kujenga Taifa (65,562,775,137), Magereza (60,900,159,845) na Elimu (35,997,981,200).

Kuibuka kwa taarifa ya ikulu kumekuja wakati serikali inadaiwa mabilioni ya shilingi na makandarasi wanaojenga barabara sehemu mbalimbali nchini; madeni ya walimu; kilio cha vyama huru vya wafanyakazi juu ya nyongeze ya mishahara na mikopo ya wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu nchini.

Aidha, upungufu huo wa kifedha, umeibua hofu ya kukwama kwa miradi ya maendeleo na ahadi nyingine zilizotolewa na Rais Kikwete wakati wa kampeni za urais muhula wa pili, zikiwemo ahadi za ujenzi wa barabara za ghorofa, ununuzi wa meli, viwanja vya ndege, bandari na reli.

Vilevile, kupatikana kwa habari hizi kumekuja wiki moja baada ya Rais Kikwete kunukuliwa akisema tatizo la ajira nchini, hasa kwa vijana, ni bomu linaloweza kulipuka muda wowote kuanzia sasa.

Kiongozi mmoja mwandamizi serikalini anasema kufutwa kwa ajira hizo mpya kutazidi kumuweka Rais Kikwete mbali na wananchi wake. Anasema wananchi wengi hawana imani na serikali kwa kuwa wanaona fedha nyingi za umma zinatumika kwenye semina na safari za viongozi.

Kwa mujibu wa waraka wa ikulu wa tarehe 18 Novemba 2011,wenye Kumb. Na. BC. 97/109/014/15, kila mwajiri sasa ametakiwa kuandaa upya mahitaji yake ya ajira kwa kuzingatia ukomo uliotolewa.

Waraka wa ikulu ambao umebeba kichwa cha maneno kisemacho, “Ajira mpya kwa mwaka wa fedha 2011/2012,” umetumwa pia kwa makatibu tawala wa mikoa, wakurugenzi wa halmashauri za miji, manispaa na halmashauri za wilaya.

Miongoni mwa wizara ambazo zitakuwa zimeathirika vibaya na uamuzi huo wa serikali, ni pamoja na tume ya kurekebisha sheria ambayo imepewa mamlaka ya kuajiri wataalam wasiozidi wawili na tume ya haki za binadamu na utawala bora na mahakama ya kazi ambazo zimezuiwa kuajiri kabisa.

Waraka wa serikali unaonyesha pia kwamba katika mikoa mitano mipya iliyotangazwa na serikali mwaka jana, ni mkoa wa Katavi pekee, ambako anatoka waziri mkuu Mizengo Pinda, ulioidhinishiwa kuajiri watumishi wapya. Umeruhusiwa kuajiri wafanyakazi wapya 46.

Haikuweza kufahamika mara moja sababu zilizofanya serikali kuruhusu mkoa wa Katavi peke yake kuajiri na kuacha mikoa mingine mipya bila hata kutajwa.

IGP aingilia kati dola kuyeyukia Polisi

MKUU wa Jeshi la Polisi nchini, Inspekta Jenerali Saidi Mwema, ameunda Tume maalumu
kuchunguza sakata la upotevu wa fedha za kigeni, dola za Marekani 50,000 (takriban Sh milioni 90) katika mazingira ya kutatanisha katika Kituo Kikuu cha Polisi Arusha.

Kwa mujibu wa vyanzo vya habari vya kipolisi katika Kituo Kikuu cha Polisi Arusha, Tume hiyo tayari imeshaanza kazi siku tatu zilizopita na baadhi ya askari kanzu wameshahojiwa juu ya upotevu wa fedha hizo.

Habari zilisema mbali ya askari Polisi wawili waliowekwa ndani kwa kutuhumiwa kuiba fedha hizo na kutoa maelezo yao, pia wako askari wengine wanne wametoa maelezo, lakini hawakuwekwa rumande.

Waliowekwa rumande wako nje kwa dhamana.

Vyanzo vya habari vilieleza kuwa kuundwa kwa Tume hiyo na IGP ni kutokana na majibu ya utata kwa baadhi ya viongozi wa Polisi mkoani Arusha kwa mmiliki wa Hoteli ya Kibo Palace aliyetambuliwa kwa jina moja la Laswai, juu ya upatikanaji wa dola hizo kwani viongozi hao hawatoi ushirikiano kupatikana kwa fedha hizo.

Fedha hizo dola 50,000 zilizooneshwa mahali ziliko na mmoja wa watu watatu wanaosadikiwa kuhusika na ujambazi kwa kutumia usafiri aina ya pikipiki maarufu jijini Arusha kwa jina la ‘toyo ama bodaboda’ zimeyeyukia mikononi mwa polisi katika mazingira ya kutatanisha.

Habari zilisema askari waliokwenda eneo ambako dola ziliko, walirudisha majibu kuwa dola zilizopatikana ni dola 900 tu, hatua ambayo inadaiwa kupingwa na mtuhumiwa wa ujambazi aliyeongozana na askari hao.

Kutokana na utata huo uongozi wa hoteli hiyo ulitaka kujua kwa kina juu ya upatikanaji ama kutopatikana kwa fedha hizo kwa maandishi na sio maneno.

Kwa mujibu wa nakala ya barua hiyo ambayo gazeti hili ilifanikiwa kuiona yenye kumbukumbu
KPH/VOL 1/06-09 ya Desemba 21, mwaka huu kwenda kwa Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Akili Mpwapwa, ilitaka kupata ufafanuzi wa maandishi juu ya dola za Marekani 50,000.

Nakala ya barua hiyo iliyosainiwa na R. H. Mbaga kama Meneja wa Utawala yenye kichwa cha habari ''Kukamatwa majambazi watatu na dola za Marekani 50,000,'' inamtaka Kaimu Kamanda kujibu kwa maandishi juu ya kuwa askari hawakukamata kiasi hicho kwa mmoja wa watuhumiwa wa ujambazi kwani Bodi ya Hoteli hiyo haiwezi kufanya kazi kwa mdomo, hivyo inataka maandishi.

“Ni matumaini yangu utatupa majibu kwa haraka ili niweze kuyawasilisha kwa Bodi ya Wakurugenzi kama nilivyoagizwa,” ilisema sehemu ya barua hiyo ya Mbaga.

Ujambazi huo ulifanyika kwa kutumia toyo na kumpora dereva wa gari la hoteli maarufu ya kitalii ya Arusha ya Kibo Palace, Onesmo Joseph (28) dola za Marekani 200,000 (zaidi ya Sh milioni 340).

Awali Mpwapwa alikiri kuwekwa ndani kwa askari hao na kuomba kuacha kutaja majina ya askari hao kwani uongozi wa Polisi unafanya upelelezi zaidi kwa sababu kuna taarifa kuwa kuna askari wengine wamehusika katika tukio hilo la kuiba fedha hizo kama ushahidi kwa watuhumiwa.

“Kwa sasa hata kama unayo hayo majina usiyataje acha kwani ukiwataja wengine wanaweza kuharibu ushahidi na mimi na wenzangu tutakuwa na wakati mgumu wa kuwatia hatiani wengine waliohusika kulichafua Jeshi la Polisi,” Kaimu Kamanda aliliambia gazeti hili wiki iliyopita.

Vita vya urais na kimya cha rais


Na Saed Kubenea

MJADALA wa kutafuta mgombea urais ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), unazidi kupamba moto. Jarida la Kimataifa la Uchunguzi nchini Uingereza (Economic Intelligence), limesema mrithi wa Rais Jakaya Kikwete mwaka 2015 atatoka Tanzania Zanzibar.
Jarida halikutaja jina la yule anayedaiwa atakuwa mrithi wa Kikwete na ambaye anatoka Zanzibar. Badala yake, Economic Intelligence limesema mwanasiasa mmoja mashuhuri kutoka miongoni mwa wale waliojitokeza kwenye kinyang’anyiro cha urais mwaka 2005, ndiye atakayekuwa mrithi wa kiongozi huyo.
Pamoja na kwamba hadi sasa, hakuna mwanachama wa chama hicho aliyetangaza hadharani dhamira ya kugombea nafasi hiyo, minong’ono imekuwa ikiongezeka siku baada ya siku.
Orodha ya wanaotaka kuwania nafasi hiyo ni ndefu. Lakini la muhimu ni hili: Kila anayetamani kuwa rais anasema, “Liwalo na liwe…”
Miongoni mwa wanaotajwa, ni viongozi wastaafu na wale waliopo bado madarakani; mawaziri na naibu mawaziri, rais wa sasa Zanzibar na yule aliyemaliza kipindi chake; makatibu wakuu na mabalozi walioko nje.
Baadhi ya wale wanaoutamani urais, tayari wameunda hadi makundi ya kuwafanyia kampeni – yale ya kumchafua yule na kumjenga huyu. Wengine wameunda hata mitandao ya kupanga safu ya kuingia ikulu. Wengine wameanza safari ya kutembelea baadhi ya mikoa na wilaya ili kutafuta uungwaji mkono.
Wengine wameanza kutafuta viongozi mashuhuri kutoka mikoa yenye wapigakura wengi – hasa eneo la kanda ya Ziwa Viktoria – kushawishi na ikibidi hadi kutumia “nguvu za giza” kutafuta uungwaji mkono. Baadhi yao tayari wameanza kupita mikoani na kujitambulisha kama “rais mtarajiwa.”
Kutokana na hali hii, sasa CCM inaonekana kuwa chama cha migogoro na kilichobeba watu wanaogombea madaraka.
Aidha, kuna wanaokiona kama chama cha watu wenye uchu wa madaraka; na chochote wanachokihubiri hakiwezi kwenda nje ya mstari huo. Wengine wanasema, hata mkakati wa chama kujisafisha, kupitia kilichoitwa “kujivua gamba,” umesukumwa na vita vya urais.
Swali la kujiuliza ni hili: Yuko wapi mwenye uwezo wa kuiokoa CCM kutoka katika hatari ya kusambaratika kutokana na vita hivi vya urais? Njia gani anayoweza kuitumia? Uwezo wake ukoje? Anaungwa mkono na nani?
Jibu ni moja: Anayeweza kuiokoa CCM na hatari ya kusambaratika, ni Rais Jakaya Kikwete pekee. Huyu ndiye mwenye uwezo wa kukinusuru chama hiki. Sababu ni nyingi.
Kwanza, pamoja na udhaifu wa Kikwete na kupoteza mvuto kwake ndani ya CCM, lakini kwa mfumo wa uendeshaji wa chama hiki, uwezo wake wa kuweka mgombea na chama kikabaki salama, bado ni mkubwa. Mgombea yeyote ambaye atakuwa mbali na Kikwete, fursa ya kushinda kinyang’nyiro ndani ya chama hicho ni ndogo mno.
Kikwete anajua kwamba hakuna mwanasiasa hata mmoja ndani ya chama chake, mwenye ujasiri wa kuthubutu kuhama CCM.
Hivyo basi, yeyote atakayetaka kumweka – awe dhaifu au jasiri; awe fisadi au mpinga ufisadi – atapita. Wale wote waliokuwa wamekasirika na wale waliokuwa wamefurahi wataungana kumpigia kampeni.
Hata chaguo lake hilo likishindwa, haitakuwa kwa sababu ya nongwa za ndani ya chama bali itakuwa ni kwa kukataliwa na wananchi. Hii ni kwa kuwa Kikwete anajua kuwa wengi wa wale wenye chuki kali dhidi ya ufisadi, wako nje ya chama chake.
Kwa mfano, Kikwete anafahamu jinsi Samwel Sitta alivyoshindwa kuondoka ndani ya chama hicho mara mbili. Pale alipotaka kufukuzwa hadi akaamua kuunda chama chake – Chama cha Jamii (CCJ), ambacho nacho kiliishia njiani; na pale alipoondolewa kwenye kinyang’anyiro cha uspika.
Pamoja na kufanya mazungumzo mara kadhaa na Dk. Willibrod Slaa, katibu mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Sitta alishindwa  kupata ujasiri wa kukata minyororo ya CCM.
Hata pale alipoteuliwa kuwa waziri wa Afrika Mashariki, Sitta aliendelea kuwasiliana na viongozi wa CHADEMA na kujiapiza kuwa hataenda kula kiapo cha uwaziri. Dakika chache baadaye alionekana kwenye runinga akiapa kulinda katiba na “kutii rais” aliyemteua.
Naye Edward Lowassa hana ujasiri wa kuthubutu kuondoka. Anachoweza kufanya ni kuishia kulalamika na kisha kufia humohumo ndani. Ni kwa sababu, Lowassa hawezi kukubaliwa na CHADEMA kwa jinsi alivyo sasa.
Angalia jinsi Rostam Aziz alivyokishambulia chama chake wakati alipojiondoa kwenye chama hicho mapema mwaka jana. Alisema ameamua kuondoka ndani ya chama hicho baada ya kuona siasa uchwara zimetawala. Akajiapiza hatakisaidia kwenye kampeni.
Rostam alikwenda ughaibuni kupumzika. Lakini alihudhuria mkutano wa ufunguzi wa kampeni Igunga katika uchaguzi mdogo wa kuziba nafasi yake ya ubunge. Ni yeye aliyetafuta na kulipia helkopta iliyotumiwa na CCM jimboni humo.
Lakini kuna hili pia. Pamoja na Kikwete kuwa na uwezo wa kukiokoa chama chake na mpasuko, lakini hana ubavu wa kuwalazimisha wananchi kuchagua mgombea anayemtaka yeye.
Hii ina maana kwamba yeyote anayetaka kumbeba, sharti awe mgombea safi, jasiri na mwenye uwezo wa kuhimili mikikimikiki ya siasa za ushindani.
Wala Kikwete na chama chake, wasije kufanya makosa kuwa mgombea mwanamke au mwanaume kutoka Zanzibar anaweza kunusuru chama.  Ukiondoa Dk. Salim Ahmed Salim, hajapatikana mwanasiasa mwingine mwenye ubavu wa kushindana na wagombea wa vyama vingine.
Hata hivyo, Dk. Salim – miaka sita baada ya Kikwete kuingia madarakani –  serikali ya CCM haijamsafisha Dk. Salim kwa madai ya viongozi wa chama hichohicho kwamba aliua rais wa kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani Karume.
Hadi leo hii, CCM hakijamsemea kuwa hicho kilichodaiwa hakikuwa na ukweli. Mtoto wa Rais Karume, rais mstaafu Amani Abeid Karume, hadi anaondoka madarakani, hakukana tuhuma kuwa baba yake aliuawa kutokana na njama za Dk. Salim.
Wachunguzi wa mambo ya siasa wanasema huenda viongozi wa CCM hawataki kujisahihisha na kumwondolea tuhuma Dk. Salim kwa kuwa hawataki awe rais.

Ufa wazidi kuongezeka CUF

Na Alfred Lucas


UFA ndani ya Chama cha Wananchi (CUF), umezidi kuongezeka. Wakati idara ya usalama ya chama hicho ikisema Hamad Rashid Mohammed, anatumiwa na Edward Lowassa katika mbio zake za kutafuta uongozi, Maalim Seif Shariff Hamad, anasema yeye mwenyewe ndiye anayesaka urais.

Kuibuka kwa taarifa za Hamad kutumiwa na Lowassa, kumekuja wiki mbili baada ya gazeti hili kuripoti madai ya baadhi ya viongozi wandamizi wa CUF kuwa mwanasiasa huyo anatumiwa na waziri mkuu Mizengo Pinda kukivuruga chama hicho.

“Baada ya Lowassa kuona hali ya kisiasa ndani ya chama chake (Chama Cha Mapinduzi) ni mbaya kwake, akatengeneza mpango wa kumtumia Hamad kutaka kuja kugombea urais kwa CUF,” unaeleza waraka huo uliotoka idara ya usalama ya chama hicho 4 Desemba 2011, kwenda kwa Profesa Ibrahim Lipumba.

Waraka huo uliosainiwa na mkurugenzi wa usalama wa chama hicho aliyetajwa kwa jina la Khamis Khassani, pamoja na mambo mengine unasema, “Lowassa ameona dhahiri hawezi kupata nafasi ya kugombea urais CCM mwaka 2015, hivyo akaamua kutengeneza mkakati na Hamad ili aweze kugombea urais kupitia CUF, huku yeye Hamad akiwa mgombea mwenza wake.”

Anasema, “…kiini cha haya, ni kwamba Lowassa anajua hawezi kupata nafasi hiyo kupitia viongozi wa sasa wa CUF kwa kuwa wanamuunga mkono Rais Jakaya Kikwete.”

Haikuweza kufahamika mara moja hicho kinachoitwa, “viongozi wa sasa wa CUF wanamuunga mkono Rais Kikwete,” kimelenga nini.

Hata hivyo, wachambuzi wa mambo ya kisiasa wanasema, kauli hiyo inathibitisha madai ya wengi akiwamo Hamad Rashid, kwamba CUF kimelala kwenye mnyororo wa CCM na ndiyo maana kinaitwa na CCM B.

Akiandika katika hali ya kumtoa hofu mwenyekiti wake, mkurugenzi hiyo wa usalama wa CUF anasema, “Lowassa anaona ili aweze kupata nafasi hiyo lazima kuwe na viongozi ambao watakubaliana naye lakini pia kwa makubaliano ya Hamad Rashid kuwa mgombea wake mwenza mwaka 2015.”

Anasema Lowassa ndiye anayefadhiri mpango huo; Hamad Rashid hana hata senti moja inayotumika kwa kazi hiyo. Anasema kadri siku zinavyokwenda mbele ndivyo anavyojikuta hana pesa na hivyo ameanza utaratibu wa kutafuta mikopo kutoka maeneo mbalimbali ndani ya nchi.

MwanaHALISI limeshindwa kumpata Lowassa kujibu madai hayo ya CUF.

Bali Hamad Rashid ameliambia gazeti hili juzi wakati linakwenda mitamboni, Wanaonifahamu wanajua kuwa mimi si mtu wa kutumiwa. Wanajua sijatumiwa na siwezi kutumiwa.”

Alipoulizwa kama yeye si mtu wa kutumiwa kwa nini anabebeshwa madai hayo alisema, “Ndugu yangu, nakuambia akutukanaye hakuchagulii tusi.”

Kwa upande wake, Maalim Seif anasema, anachokiona yeye ni kuwa Hamad Rashid anapiga hesabu za kutaka kuteuliwa kuwania urais wa Zanzibar iwapo atapata nafasi ya kuwa katibu mkuu wa chama hicho.

Akiongea kwa tahadhari kwenye mahojiano yake ya ana kwa ana na gazeti hili jijini Dar es Salaam, juzi Jumatatu, ambayo yatachapishwa kwa ukamilifu kwenye toleo letu lijalo, Maalim alisema, “Kuna watu wamemdanganya Hamad kwamba mimi niko mbioni kurejea CCM.

Anasema, “Ni kweli, CUF na CCM zimeunda serikali ya umoja wa kitaifa Zanzibar, lakini huko si kuungana” na wala hakuna maana ya yeye kurejea ndani ya chama hicho.

Maalim anasema Hamad Rashid ana mkakati wake, ambao ni kuingia ikulu ya Zanzibar. Anasema, “Si vibaya kuwa na ambition (ndoto). Bali means (namna) ya kufikia ambition hizo ndiyo tatizo.”

“Hamad anawaza kama akikosa urais chama kitashika nafasi ya pili basi atakuwa makamu wa kwanza wa rais. Watu wanamfahamu Hamad, hawezi kufanikiwa,” anasema Maalim Seif.

Katibu mkuu huyo wa CUF anasema, Hamad Rashid ambaye ni mbunge wa Wawi, kisiwani Pemba hatafanikiwa kwa sababu ya kuingia vibaya kwenye harakati hizo.

Waraka wa idara ya usalama uliokwenda kwa Profesa Lipumba unasema, sakata linaloendelea ndani ya chama hicho lilianza rasmi kwenye uchaguzi wa Igunga ambapo karibu wajumbe wengi wa baraza kuu walikuwepo huko, walishawishiwa na Hamad “kufanya uasi” kwenye kikao cha BKT cha mwezi wa tano hawakumuunga mkono Hamadi.

Anasema hali hiyo ilisababisha kuwapo chuki kati ya wajumbe waliokuwa Igunga na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, Tanzania Bara, Julius Mtatiro.

Anasema chuki hiyo iliongeza nguvu katika suala zima la Hamad ambaye hapo mwanzo alikuwa na wabunge wachache; siku za mwisho kuelekea upigaji kura kulifanyika vikao kadhaa vilivyowajumuisha baadhi ya wajumbe wa baraza kuu wakiwamo baadhi ya wabunge.

Anasema mara baada ya kurejea kutoka Igunga, wajumbe kadhaa wakiwemo Khassan Doyo, walijipanga kuhakikisha wanatengeneza hoja ambazo zingesababisha agenda zilizowasilishwa zikataliwe na hatimaye kuwa na agenda moja ya kutokuwa na imani na viongozi wakuu wa chama hicho kwa kisingizio cha kushindwa uongozi.

Anasema agenda hizo zingesababisha kuundwa kwa uongozi wa muda kuelekea mkutano mkuu.

Waliotarajiwa kuwa viongozi, ni mbunge wa Lindi Mjini, Salum Barwani aliyetajwa kuwa angekuwa mwenyekiti, mbunge wa Ole, Pemba, Rajab Mbarouk Mohammed, makamu wa mwenyekiti, Hamad Rashid katibu mkuu, Doyo naibu katibu mkuu Bara na Masoud kuwa naibu katibu mkuu Zanzibar,” anaeleza.

Awali akiandika kwa Maalim Seif, 10 Desemba 2011, saa 1:03 adhuhuri, Profesa Lipumba alisema, “…ubinafsi ni hatari sana. Anawapa watu kudhani ndani ya CUF kuna mgogoro…”

Ujumbe wa Profesa Lipumba ulilkuwa ukijibu ule wa Maalim Seif wa 9 Desemba 2011 ulioeleza juu ya Jubeir Shamte ambaye Hamad Rashid alimtumia ujumbe alioutuma kwa Profesa Lipumba kuhusiana na kushamiri kwa mgogoro ndani ya chama hicho.

Aidha, Profesa Lipumba alitaka kujua kutoka kwa Maalim Seif iwapo vyombo vya habari vimeripoti lolote juu ya barua hiyo.

“Ni kweli, gazeti la MwanaHALISI limeandika… Mwenyewe anawafanya wanachama wamuone ni msaliti,” anasema.

Anasema, Hamad Rashid amekutana na na Sheikh Issa Ponda na Sheikh Basaleh, na kwamba mazungumzo yao yamemfika yeye Maalim Seif.

Maalim akiandika kwa Profesa Lipumba anasema, “…jamaa yako (Hamad Rashid) amekutana na Sheikh Issa Ponda na amezua mambo mengi. Sasa anamtafuta Sk Basaleh (Sheikh Basalehe). Ponda anasema yeye anafahamu sana jamaa yako na ni muongo. Wameomba baadaye mimi nikutane nao ili kuwaleza ukweli. Nakwenda Lindi na Kilwa kuanzia kesho (10 Desemba 2011). Nikirudi inshallah nitawarafuta,” anasisitiza.

Maalim anasema, hii ndiyo hali, na kwamba Profesa Lipumba asiwe na wasiwasi inadhibitiwa.

Wiki mbili zilizopita, gazeti hili liliandika kwa ufasaha mvutano uliyopo kati ya Maalim Seif na Hamad Rashid. Mvutano huo ulifikia kuibuka kwa vurugu kubwa kwenye maeneo ya Manzese jijini Dar es Salaam, ambako Hamad Rashid alizuiwa kufungua matawi ya chama hicho kwa madai hakutoa taarifa makao makuu ya chama Buguruni.

Hamad Rashid amekuwa akikisitiza, CUF kinaendeshwa kama chama cha familia, na kwamba ukatibu mkuu ambao yeye anataka kuugombea umekuwa kama utume ndani ya chama hicho.

Saturday, December 24, 2011

Find out why these babes are dressed in bikinis in town


These girls were spotted in their bikinis not at the beach, but right in the heart of town. Five bikini babes strutted their stuff on the MRT trains and at Raffles Place and Orchard Road. Amused passers-by stopped to take photographs with them.

In their oversized shades and carrying bubble guns, a volleyball and stickers that read "I(heart)SBP" the girls attempted to drum up publicity for the upcoming Siloso Beach Party on New Year's Eve.
The girls themselves had the character "I(Heart)SBP" painted on their bodies.

Freelance model Hannah Lau, 23, who sported a 'P' sticker on her stomach told The New Paper that it did not feel like work but felt more like hanging with the "ladies".
Hailed as Asia's largest beach countdown party, the Siloso Beach Party will feature 12 hours of non-stop action at 5 party zones including Azzura Beach Club, Wavehouse and Cafe Del Mar.

Tickets are available at the Sentosa Ticketing Counters only. Each ticket is priced at $49 for event admission and includes one standard drink.
Various discounts are available for UOB cardholders.