Showing posts with label malima. Show all posts
Showing posts with label malima. Show all posts

Monday, August 22, 2011

Kikwete azidi kutoswa


WAZIRI wa Utawala Bora, Mathias Chikawe
WAZIRI wa Utawala Bora, Mathias Chikawe na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Adam Malima wako mbioni kuingiza nchi katika mikataba mitatu mikubwa ya kimataifa kwa maslahi binafsi, MwanaHALISI limeelezwa.

Mikataba ambayo Chikawe na Malima wanataka kuingiza taifa inahusu uchimbaji wa madini aina ya kopa (Copper), wilayani Mpanda mkoani Rukwa na mradi wa madawa ya virutubisho kwa wagonjwa wa ukimwi – Secomet V.

Kwa mujibu wa uchunguzi wa MwanaHALISI, Chikawe na Malima wamepanga kutekeleza miradi hiyo miwili kupitia kampuni ya Lion of Afrika Ltd., ambayo mtendaji wake mkuu ni Abdurazak Ebrahim.
Mradi mwingine, uliopangwa na vigogo hao wa serikali, unahusu usindikaji wa nyama pamoja na maziwa. Taarifa zinasema Abdurazak Ebrahim mfanyabiashara mwenye uraia wa Afrika Kusini, anasifika duniani kwa “ushawishi,” na kwamba anafahamika sana ndani ya serikali ya Rais Jakaya Kikwete kutokana na kubebwa na viongozi hao wawili.

MwanaHALISI limeelezwa tayari Malima “amenasa” katika mikono ya Abdurazak Ebrahim. Imeelezwa kuwa tarehe 27 Mei 2011 aligharamiwa usafiri kutoka Dar es Salaam hadi nchini Afrika Kusini, pamoja na malazi katika hoteli ya kimataifa ya Michelangelo iliyoko Cape Town. Aliondokea uwanja wa ndege wa kimataifa wa  Julius Nyerere jijini Dar es Salaam kwa ndege ya Shirika la ndege la Afrika Kusini (South African Airways) Na. SA 323.

Ziara ya Malima nchini humo ililenga kufanikisha mradi wa kuchimba kopa wilayani Mpanda unaofanywa na kampuni ya Abdurazak Ebrahim. Uthibitisho wa malazi (Confirmation of Accommodation) wa uongozi wa hoteli ya Michelangelo kwenda kwa Malima, tarehe 9 Juni 2011, unaonyesha kiongozi huyo wa serikali alilala katika hoteli hiyo kwa siku nne – kati ya tarehe 9 na 13 Juni 2011.

Kila siku alilipiwa na mwenyeji wake, fedha za Afrika Kusini, Rand 2, 830 (karibu Sh. 500,000).
Malima amejitambulishwa katika hoteli ya Michelangelo kwa jina la Johan Ernest Malima. Gazeti hili halikuweza kufahamu mara moja, kwa nini Malima anayetambulika nchini kuwa ni muumini mzuri wa madhehebu ya kiislamu, alikubali kutumia jina hilo linalotumiwa na waamini wa kikristo.

Katika uthibitisho huo wa hoteli, mwenyeji wake anasema, “…Dereva atakuja uwanja wa ndege wa Cape Town na kukuchukua... atakuwa na kibao chenye jina la hoteli ya Michelangelo... na wewe utajitambulisha kwake kwa jina la Ernest Malima.”

 Haikufahamika iwapo Malima aliwasiliana na ubalozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini na kueleza kuwa angalau kwa safari hiyo hatajulikana kwa majina yake rasmi kama anavyofahamika kwa aliyemteuwa na kwa Watanzania kwa jumla.

Abdurazak Ebrahim anafahamika nchini Afrika Kusini kuwa ni mwenye mahusiano na watu wengi ndani na nje ya nchi hiyo, “hususani katika mambo ya uwekezaji katika uchimbaji wa madini na biashara ya dawa za binadamu ...,” anaeleza kiongozi mmoja wa serikali ya Tanzania ambaye hakutaka kutajwa gazetini.
Alikuwa akijibu swali la gazeti hili iwapo serikali inafahamu mahusiano kati ya kigogo huyo na mawaziri wa Tanzania.

Gazeti limeshindwa kuwapata Chikawe na Malima. Wote wawili simu zao ziliita bila kupokelewa. Mwandishi alipowatumia ujumbe mfupi wa simu ya mkononi kuwauliza kuhusika kwao katika miradi hiyo, hakuna aliyejibu.

Ujumbe kwa Malima ulisema, “MwanaHALISI linataka kufahamu ni biashara gani unayofanya na Abdurazak Ebrahim hadi akulipie hoteli na tiketi ya kwenda Afrika Kusini, Juni mwaka huu, wakati wewe ni waziri?”
Aidha, gazeti lilikuwa limetaka kujua iwapo Adam Malima Kigoma, ndiye yuleyule Johan Ernerst Malima.
Naye Chikawe aliulizwa, “Tunataka utueleze jinsi unavyoufahamu mradi wa dawa za virutubisho kwa wagonjwa wa ukimwi ambao wewe unatajwa pamoja na Abdurazak Ebrahim.”

Nyaraka zilizoandaliwa na mmoja wa mawakala wa Abdurazak Ebrahim, Tosky Hans zinaonyesha “...kuthibitika kuwapo kwa madini ya kopa wilayani Mpanda, lakini uchunguzi wa jiolojia utakaonyesha wingi wa madini hayo bado haujakamilika.”

Katika nyaraka nyingine ambazo zinaitwa nyaraka za siri na za binafsi (private and confidential), inaonyeshwa kuwapo makubaliano ya pande mbili – kati ya Abdurazak Ebrahim kwa upande mmoja na Chikawe na Malima kwa upande mwingine.

Makubaliano kati ya vigogo hao yalifanyika 22 Machi 2011 na yanahusisha upatikanaji wa maeneo ya uchimbaji madini na nafasi katika uuzaji wa bidhaa mbalimbali kama dawa za banadamu katika ukanda wa Jangwa la Sahara.

Nyaraka zinasema, “makubaliano au mikataba itakayofanywa itakuwa ni kwa manufaa ya watu binafsi” na kwamba katika makubaliano hayo wahusika wameafikiana kuanzisha na kuendeleza mahusiano ya kibiashara kwa kuzingatia vigezo vya mkataba.

Makubaliano hayo pia yanahusisha hatua zote za maafikiano, majadiliano na mawasiliano pamoja na kuwahusisha baadhi ya watu walio katika mahusiano hayo ya kibiashara.
Nyaraka zinasema kuwa makubaliano hayo yatabaki kuwa siri baina ya pande mbili zinazohusika na utakuwa mkataba wa miaka mitano.

Kwa mujibu wa makubaliano, mikataba yote itasainiwa kwa kutumia sheria za Afrika Kusini.
 Kwa upande wa biashara ya virutubisho vya madawa ya binadamu kwa wagonjwa wa HIV – Secomet V – Chikawe na Malima wanatajwa kuanzisha biashara hiyo inayodaiwa kuwa inaweza kuwaingizia mamilioni ya shilingi kwa muda mfupi.

Katika andishi kwa njia ya barua pepe iliyotumwa 11 machi 2011 na Zak Ebrahim kwenda kwa Chikawe, mfanyabiashara huyo anasema “biashara hiyo inalipa vizuri.” Awali Chikawe aliambatanisha ripoti iliyoandikwa na Dk. L.M.M Chuwa wa hospitali ya St. Benard ya jijini Dar es Salaam. Anasema kuwa daktari huyo alikuwa na mazungumzo na Shelys Pharmaceutical mwaka 2007 na walimuagiza Dk. Chuwa kufanya majaribio watu 53 kwa kutumia Secomet V. Majaribio yamepangwa kukamilika katika kipindi cha miezi 6 hadi  9 kutoka sasa.

Hata hivyo, wataalamu wa dawa hiyo wanasema watumiaji wengi wa Secomet V, hali zao zimezidi kuwa mbaya.

“Kuna uniti 28000 zimeuzwa nchini Afrika Kusini kwa mwezi zikiwa na ongezeko la asilimia 20 kwa mwezi. Ni biashara inayojitosheleza na na inayoweza kuwa na uhitaji ndani wiki 8 mpaka 12,” anasema Abdurazak Ebrahim katika andishi lake kwa Chikawe.

Wabia hao wawili wamependekeza kutafuta namna ya kuizalisha nchini vimelea hivyo vya Secomet V.
“Ni muhimu tukapata baadhi ya mawazo toka Tanzania juu ya mipango tunayoitarajia. Kuna aina mbili ya Fulvic Acid ambayo ni ya vidonge na nyingine ni ya maji ambayo itakuwa na gharama kubwa katika usafirishaji dawa zote zinatakiwa kutumiwa na mgonjwa kwa dozi ya mara tatu kwa siku,” anaeleza.
Akiandika kwa njia ya kushawishi, Abdurazak Ebrahim anataka kufahamu kutoka kwa Chikawe kama serikali ya Tanzania ina fedha za kununua bidhaa hizo; “hii ni njia muhimu ya kupata mafanikio kama zikisambazwa Tanzania.”

Uchunguzi wa suala hili unaendelea.

Wednesday, July 20, 2011

Ngeleja, Malima watakiwa kujiuzulu

MBUNGE wa Arusha, Godbless Lema (CHADEMA) jana aliomba Mwongozo wa Spika akitaka Waziri na Naibu Waziri wa Nishati na Madini wawajibike katika sakata la wizara hiyo kuchangisha Sh bilioni moja kutoka idara na taasisi zake kwa ajili ya kufanikisha uwasilishaji wa Bajeti.

Lema aliomba Mwongozo wa Spika kwa kutumia kanuni ya 68(7) kwa kusema Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, David Jairo, asingeweza kuwa na ujasiri wa kuchangisha fedha hizo bila mawaziri husika kuwa na taarifa.

Mbunge huyo ambaye alitaja moja kwa moja bungeni kwamba Katibu Mkuu huyo alijihusisha katika vitendo vya rushwa kutokana na fedha hizo, alihoji kama kweli ndiye anapaswa kuwajibika pekee na si pamoja na Waziri mwenye dhamana, William Ngeleja na Naibu wake, Adam Malima.

Spika Anne Makinda hakukubaliana na hoja ya Lema kutokana na kile alichosema kwamba mjadala wa suala hilo umewekwa pembeni kutokana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuliomba Bunge juzi kwamba anakwenda kulifanyia kazi. “Naomba waendelee kufanya inavyostahili kiutawala,” alisema Makinda.

Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo (CCM), ndiye aliyeibua hilo sakata wakati akichangia hotuba ya Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kabla haijaondolewa bungeni juzi.

Shelukindo aliwasilisha barua bungeni iliyoandikwa na Katibu Mkuu Jairo ikizitaka idara na taasisi zote za wizara hiyo kila moja ichangie Sh milioni 50 kwa ajili ya kukamilisha maandalizi ya uwasilishaji wa hotuba ya bajeti.

Mbunge huyo wa Kilindi pamoja na Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka (CCM) kwa nyakati tofauti, walihoji bungeni mantiki ya fedha hizo takribani Sh bilioni moja na wakataka wizara ifafanue zimekusanywa kwa ajili gani.

Pinda katika hoja yake bungeni alikiri kwamba Jairo kawaudhi na kuwatibua wabunge na akaahidi kuwasilisha suala hilo kwa Rais Jakaya Kikwete aliyemteua ili achukuliwe hatua.

“Lazima nikiri hata mimi nilishtuka kweli sana tena si kidogo, kwani suala hili limegubikwa na maswali mengi hakuna namna ya kutetea,” alisema Pinda.

Wakati huo huo, baadhi ya wadau wa umeme nchini wamewatupia lawama watendaji wa Wizara ya Nishati na Madini na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuwa ndiyo chanzo cha matatizo ya umeme kutokana na kutotekeleza kivitendo, mipango ambayo ingesaidia kuondokana na tatizo hilo.

Watendaji hao pia wameshutumiwa kuwa mabingwa wa kupiga maneno na kufanya ujanjaujanja katika kushughulikia tatizo la umeme.

Pia wameshutumiwa kuwa wanapuuzia mchango wa sekta binafsi wakati ndio watumiaji wakubwa wa umeme.

Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Haji Semboja, alisema kinachokosekana kwa watendaji hao ni akili na ubunifu, badala yake alisema wanatanguliza ujanjaujanja na ni werevu wa kupiga maneno.

“Tatizo letu tunakwepa kuwatumia wataalamu katika masuala haya; badala yake tunawatanguliza wachekeshaji na wapiga porojo … katika hali ya namna hii, kamwe hatuwezi kuondokana na tatizo la umeme,” alisema Dk Semboja. Alisema kwa sasa suala si fedha bali ni akili ya kubuni mikakati ya kuondokana na tatizo hilo kama walivyofanya Kenya na Ethiopia.

“Kama suala ni fedha, Tanesco wanahitaji bajeti ya miaka 20 ijayo, kumaliza tatizo la umeme, lakini sasa tunahitaji ubunifu na akili.” Alitoa mfano kuwa ndani ya Tanesco na Serikali kuna wataalamu ambao wameshirikishwa katika mipango inayohusisha ushiriki wa jumuiya za kanda kama ya Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (Sadc) na ile ya Bonde la Mto Nile, lakini utekelezaji wake kwa Tanzania hautiliwi maanani.

“Mimi nimekuwa nashiriki miradi yote hiyo, lakini ushiriki wa Serikali yetu ni mbovu, ndiyo maana nasema tuna watu wenye uwezo, watafutwe tuachane na hawa wachekeshaji na wapiga maneno,” alisema Dk Semboja. Mwenyekiti wa Shirikisho la Wenye Viwanda (CTI), Felix Mosha, alisema Tanzania itaondokana na tatizo la umeme iwapo wataishirikisha sekta binafsi katika mipango yake.

Mosha alisema asilimia 85 ya watumiaji wakubwa wa umeme wa Tanesco ni wenye viwanda, hivyo alishauri Serikali kuwa inapaswa kuwahusisha katika mipango yote kuanzia ya muda mfupi, kati na mrefu ili nao watoe maoni yao ya namna ya kuondokana na tatizo hili. Alisema matatizo haya yanayoendelea ya mgawo wa umeme ni matokeo ya Serikali kuidharau sekta binafsi hasa kwenye suala la umeme.

“Hata pale jambo linalogusa sekta binafsi, Serikali haitaki majadiliano nasi na badala yake wamekuwa wanajadiliana wenyewe na kuamua mambo yao.” Mosha alisema: “Naamini kukwama kwa bajeti hii sasa itatoa fursa ya kutushirikisha, na sisi tuko tayari, kwani tuna mapendekezo yetu ambayo tutawapatia watu wa Serikali.”

Alisema, kama Serikali itaendelea kuwapuuza, ustawi wa viwanda nchini uko katika hatihati, kwani vingi vinategemea jenereta ambazo zilikuwa maalumu kutatua tatizo la muda mfupi na si ilivyo sasa kutokana na gharama zake kuwa juu kuliko umeme.

Mwenyekiti huyo pia alisema katika hali ya sasa, viwanda vya Tanzania havina ubavu wa kushindana na vya nchi zingine za nchi wanachama wa EAC kutokana na kutokuwa na nishati ya uhakika.

Alionya pia kuwa watu wengi watapoteza ajira, kwani viwanda vingi vinafanya kazi kwa siku mbili kwa wiki jambo ambalo linamwia vigumu mwajiri.