Showing posts with label kikeke. Show all posts
Showing posts with label kikeke. Show all posts

Tuesday, July 26, 2011

Kisa na mkasa na Salim Kikeke

Kumpata mke balaa

Bwana mmoja nchini Marekani hatimaye amefunga ndoa kwa mara ya kwanza, baada ya kusaka mchumba kwa zaidi ya miaka sabini.

Bwana huyo Gilbert Harrick mwenye umri wa miaka tisini na tisa sasa ambaye alipigana katika vita vya pili vya dunia amesema hakuwahi kukutana na msichana aliyempenda kwa miaka yote hiyo.
Bwana Gilbert amefunga ndoa na Bi Virginia Hartman mwenye umri wa miaka themanini na sita.
Gazeti la Rochester Cronicle limesema wawili hao kwa sasa wanaishi katika nyumba ya kutunza wazee, mjini New York.

"Tulitaka tuishi pamoja katika chumba kimoja, lakini walitukatalia hadi tufunge ndoa" amesema bwana Gilbert, "Kwa hiyo nikamuomba tuoane na yeye akakubali" ameongeza mzee huyo.
Kabla ya kuoana na kuishi katika chumba kimoja, wapenzi hao walikuwa wakiandikiana barua za mapenzi kila mara.

"Ni wazimu, lakini ndio raha yenyewe" amesema Bi Virginia, ambaye ana watoto watano katika ndoa yake ya awali.

Chupi si lazima

Mamlaka za magereza katika jimbo la Florida zimeamua kubana matumizi kwa kuacha kutoa bure nguo za ndani kwa wafungwa.

Badala yake, mkuu wa gereza la Polk amesema kuanzia sasa wafungwa watalazimika kununua chupi ambazo awali zilikuwa zikitolewa bure.
"Hakuna sheria inayotulazimisha kuwapa wafungwa vazi hilo" amesema Liwali Grad Judd, ambaye pia ndio mkuu wa gereza hilo.

Gazeti la Telegraph limesema vivazi hivyo vya ndani vitawagharimu wafungwa hao dola mbili na nusu hadi dola nne na nusu kutegemea aina na mtindo.

Hata hivyo utawala wa gereza umesema si lazima wazinunue, wasiotaka kuvaa, wataachiwa wafanye hivyo.
Chupi hizi pia zitapatikana katika rangi moja tu, nyeupe.
"Wanaotaka watanunua, wasiotaka, basi waache upepo uingilie mguu mmoja na utokee mguu mwingine wa suruali" amesema Mkuu wa gereza.

Pombe ikizidi...

Walevi wawili nchini Marekani waliingia matatani baada ya kuingia ndani ya karandinga la polisi ili wajipige picha kama vile wamekamatwa.

Wawili hao Ryan Letchford na Jeffrey Olsen waliingia katika gari la polisi lililokuwa limeegeshwa barabarani, na kuanza kupeana zamu kujipiga picha.

Hata hivyo shughuli hiyo iliingia doa wakati vitasa vya mlango wa gari vilipojifunga, wakati wawili hao wakiwa bado ndani ya karandinga.

Rafiki wa tatu wa jamaa hao alikuja kujaribu kuwatoa, lakini akashindwa na kulazimika kupiga simu polisi kuomba msaada.

Constable wa polisi Mike Connor ameliambia gazeti la kila siku la Philadelphia kuwa alifika na kuwafungulia walevi hao.
"Walikuwa wakiona aibu sana" amesema polisi huyo.
Hata hivyo wawili hao hawakuwa huru kwa muda mrefu, kwani walikamatwa na kushtakiwa kwa makosa ya kutaka kuiba gari la polisi, ukorofi wa kihalifu na ulevi hadharani.

Makahaba kuchumbiwa

Kituo kimoja cha televisheni nchini zambia kimeanzisha kipindi kinachosaidia wasichana waliokuwa makahaba zamani, kutafuta wachumba.

Wasichana hao wapatao kumi na wanane mbali na kusaidiwa kutafutiwa wachumba, watapatiwa zawadi ya dola elfu tisa kila mmoja na pia kulipiwa gharama zote za harusi.

Kituo hicho kiitwacho Muvi TV, kimesema kinataka kuwapa wasichana hao nafasi ya kuanza maisha mapya.
Kipindi hicho kinaitwa "tayari kwa ndoa".

Mhubiri mmoja Mchungaji Jeff Musonda ametoa baraka zake kwa makahaba hao wa zamani.
Kituo hicho cha TV kimesema kiliwatafuta wasichana hao kutoka mitaa mbalimbali ya nchi hiyo.
Baadhi ya washiriki wamesema walikuwa wakiuza miili yao ili kuwahudumia watoto wao.

Hata hivyo watu wamepokea kwa hisia tofauti kipindi hicho, wengine wakisema mtu akishakuwa kahaba ni vigumu kubadilika kwa muda mfupi, huku wengine wakisema, hakuna haja ya kuwahukumu kwa mambo waliyoyafanya siku za nyuma.

Kulipa kulala jela

Gereza moja nchini marekani mwishoni mwa wiki liliwatoza fedha watu kwa kulala ndani ya gereza.
Hiyo ilikuwa kwa watu waliokuwa wakitaka kuhisi maisha ya gerezani.
Gereza hilo Cole County, liliwatoza watu dola thelathini kwa usiku mmoja kwa watu waliotaka kuonja maisha ya jela siku ya Ijumaa na Jumamosi.

Maafisa wamesema nafasi hiyo imetolewa kwa wananchi ili kulijaribu gereza hilo jipya kabla halijaanza kazi rasmi ya kuwafungia wahalifu.

Shirika la habari la reuters limesema watu wapatao mia moja na sabini walifurika katika gereza hilo wakitaka kuona usingizi wa jela ukoje.

Baadhi ya watu waliofika kulala gerezani ni pamoja na mawakili na wanandoa waliokuwa wakiadhimisha miaka yao ya ndoa.

Watu hao walipitia misingi ya kuswekwa gerezani, ikiwa ni pamoja na kukaguliwa, kunyanganywa simu za mkononi, mikanda pamoja na vito walivyokuwa wamevaa.

Pia walipigwa picha kama wafungwa."Ingawa hakikuwa kifongo cha ukweli, lakini nilihisi kukosa uhuru" amesema Bob watson, mmoja wa watu waliolipa kulala jela.

Kila chumba kidogo ndani ya gereza hilo kina kitanda cha chuma na godoro jembamba, huku balbu yenye mwanga mdogo ikiwaka usiku kucha.

Hata hivyo kuna TV yenye channel moja ambayo haisikiki kutokana na kelele ndani ya gereza.
Na kwa Taarifa yako... Konokono anaweza kupita kwenye ncha ya wembe bila kujikata.

Wednesday, July 20, 2011

Kisa na mkasa na Salim Kikeke

Kikeke na kifua

"Mimi ni Dayo Yusuf wiki hii nikikuletea Kisa na Mkasa-- kwa sababu, Salim Kikeke, sauti yake imekauka kutokana na mafua.
Bwana Kikeke alisafiri kwenda Nairobi Kenya kwa ajili ya shughuli za kikazi na akapatwa na mafua hayo.
Bila shaka tutakuwa naye wiki ijayo..", ilisikika sauti ya Dayo Yusuf.

Bunduki kwenye besdei

Gun
Bunduki
Bwana mmoja nchini Marekani amefikishwa mahakamani baada ya kwenda na bunduki katika sherehe moja ya kuzaliwa mtoto wa jirani yake.

Bwana huyo aliwatisha watoto wa jirani yake huyo pamoja na watoto engine waliokuja kwenye sherehe hizo, kwa sababu watoto wake hawakupewa keki.

Mtandao wa news.com umesema polisi wa mjini Memphis wamesema bwana huyo Joseph Hayes alikasirishwa sana baada ya watoto wake kutopewa keki na Ice Cream katika sherehe hiyo.
"Kwa nini hamkuwapa watoto wangu keki na Ice cream" alifoka bwana Joseph na bastola yake.
Polisi waliitwa kutuliza mzozo huo, na Bwana Joseph mwenyewe kukanusha kuwa alikuwa na bunduki. Alisema alikuwa na kifaa tu kilichoonekana kama bunduki. Bwana huyo ameshitakiwa kwa makosa ya kutishia watu.

Mwizi wa mabegi

Begi
Mabegi

Polisi nchini Uhispania wamemkamata bwana mmoja mwenye mwili unaoweza kunyumbulika kwa makosa ya wizi.

Mwizi huyo inadaiwa alikuwa akijificha ndani ya sanduku, na sanduku hilo kuwekwa katika mizigo ya abiria kutoka uwanja wa ndege wa Girona wanaokwenda jijini Barcelona. Kwa mwezi mzima polisi walikuwa wakishangazwa na wizi unaotokea kwenye eneo la kuwekea mizigo ndani ya basi. Hivi karibuni wizi kama huo ulitokea tena ambapo masanduku yote ya abiria yalikuwa yamevunjwa na vitu kuibiwa.

Hata hivyo abiria mmoja aligundua kuwa sanduku moja tu ndio lilikuwa halijaguswa. Polisi waliitwa na walipofungua sanduku hili walimkuta mtu amejikunja ndani yake. Polisi pia walimkamata mwenzake na mwizi huyo ambaye alikuwa akimpeleka kama mzigo ndani ya basi hilo.

Mwenzi huyo alikuwa akinunua tiketi ya basi na kuweka sanduku lake hilo lenye mwizi mwenzake katika eneo la mizigo, ambapo wakiwa safarini, mwizi huyo hutoka ndani ya sanduku na kuanza kuvunja na kuiba masanduku ya abiria.

Kabla ya mwisho wa safari, bwana huyo mwenye mwili unaonyumbulika, alikuwa akiingia katika sanduku lake na kujifungia ndani tena, na kubaki kama mizigo mingine.

Baharia mlevi

Boat
Boti

Baharia mmoja mlevi nchini Sweden alizua sokomoko na kusababisha shughuli za uokozi kufanyika baharini baada ya kutoa taarifa kuwa mke wake ameanguka baharini.

Hata hivyo baada ya msako wa muda, polisi waligundua kuwa baharia huyo alikuwa amemsahau mke wake nyumbani. Baharia huyo akiwa katika chombo chake binafsi, alipiga ishara ya hatari katika eneo la Kalmar, nje kidogo ya mwambao wa kusini wa Sweden, akiamini kuwa mkewe ameangukia baharini na kuzama.

Baada ya kufanya msako, waligundua kuwa mke huyo hata hakuwahi kuingia katika boti hiyo, na alikuwa salama salimini katika nchi kavu. Bwana huyo na boti yake walivutwa na boti ya polisi hadi pwani, ambapo baada ya kufanyiwa vipimo, baharia huyo, vipimo vilionesha amelewa chakari.
Mtandao wa news.com umesema baharia hiyo ameshitakiwa kwa kuendesha boti huku akiwa amelewa.

Mafunzo ya kwenda choo

Choo
Choo

Kundi moja la wazazi nchini Uingereza London limekasirishwa, baada ya shule wanayosoma watoto wao kutishiwa kukatazwa kwenda shule iwapo hawatapewa mafunzo thabiti ya kutumia choo.
Mkuu wa shule hiyo iliyopo jijini Liverpool, Patricia Deus, amewaonya wazazi kuwa walimu wake wanapoteza muda mwingi kila siku kuwasaidia watoto wenye umri wa hadi miaka mitano kwenda kujisaidia chooni. Wanafunzi wengi bado wanavaa nepi, limesema gazeti la Daily Express.

Mkuu wa shule, Bi Deus ameandika barua kwa wazazi wa watoto wote mia tatu na thelathini na mbili wanaosoma katika shule hiyo. "Tuna watoto wanaojiunga na shule yetu ambao hawajafunzwa kutumia vyema choo" imesema taarifa ya mkuu huyo wa shule na kuongeza kuwa watoto wenye matatizo ya kiafya tu ndio watapewa msaada.
"Hili ni jukumu la mzazi. Watoto watabaki nyumbani mpaka muwape mafunzo ya kutumia choo vyema" amesema mkuu wa shule.

Hospitali bei chee

Bwana mmoja nchini Uchina, alipata furaha kubwa sana baada ya kwenda hospitali na kupatiwa matibabu, na ilipofika wakati wa malipo, aliambiwa alipe senti moja.

Gazeti la Xiaoxiang Morning Herald limesema bwana huyo wa mjini Changsha, katika jimbo la Hunan alikwenda hospitali akisumbuliwa na ugonjwa wa tumbo.

Baada ya kuhojiwa kwa muda na daktari, alipatiwa ushauri na dawa, lakini aligundua kuwa bili yote ni Yuan 0.01 ya Uchina, sawa na chini ya senti moja ya kimarekani.

Kwa mujibu wa Yang Li, mkurugenzi wa hospitali hiyo, amesema wanajaribu kuwaridhisha wagonjwa wao, na wameanza kwa kutoza fedha kidogo kwa ajili ya matibabu, ili kupunguza gharama za matibabu kwa wagonjwa.

Na kwa taarifa yako......

Binaadam wa kawaida huota kwa wastani, ndoto elfu moja mia nne na sitini kwa mwaka.
Tukutane Wiki Ijayo.... Panapo Majaaliwa