Showing posts with label kawambwa. Show all posts
Showing posts with label kawambwa. Show all posts

Thursday, August 11, 2011

Ripoti ya kunyanyaswa watoto Tanzania

Ramani ya Tanzania
Ramani ya Tanzania

Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na shirika linaloshughulikia maslahi ya watoto la UNICEF karibu theluthi moja ya watoto wa kike nchini Tanzania wanakabiliwa na unyanyasaji wa kijinsia na kuingiliwa bila hiari kabla hawajatimia umri wa miaka 18.

Shirika hilo linasema kuwa watoto wa kiume idadi yao inafika asili mia 13.4. Kinachotumika sana katika unyanyasaji huu ni kuwatomasa watoto ambako baadae hufuatiwa na jaribio lakutaka kuwaingilia.

 Tanzania ndio nchi ya kwanza kuwa jasiri kufichua tatizo hilo linalowakabili watoto wa kike nawakiume andy brooks
Afisa mmoja wa shirika hilo Andy Brooks amesema uchunguzi huu ndio uliokamilika zaidi na umeonesha kuwa serikali iko tayari kukabiliana na tatizo hili.

Uchunguzi huu pia uligundua kuwa wale ambao wamejihusisha na mapenzi kabla ya kutimia umri wa miaka 18, asili mia 29.1 ya watoto wa kike na asili mia 17.5 ya wale wa kiume wamesema kuwa mara ya kwanza wao kujihusisha na ngono haikuwa kwa hiari yao.

Unicef inasema hii ina maana walilazimishwa ama kushawishiwa kujihusisha na ngono. Waziri wa Elimu wa Tanzania Shukuru Kawambwa amesema kuwa serikali imejitolea kukomesha unyanyasaji wa kijinsia na kuingiliwa watoto.

Bw Brooks amesema uchunguzi sawa na huo utafanywa nchini Kenya, Rwanda, Malawi, Zimbabwe na Afrika Kusini.

Wednesday, July 20, 2011

Posho elimu ya juu yapanda kwa TShs 2, 500/=

SERIKALI itaongeza fedha za kujikimu kwa wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu nchini kutoka Sh. 5,000 ya sasa hadi Sh. 7,500 katika mwaka huu wa fedha.

Kauli hiyo ilitolewa bungeni jana na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Dk. Shukuru Kawambwa, alipokuwa akisoma hotuba yake ya Makadirio ya Matumizi ya Fedha kwa Wizara yake kwa mwaka huu.

Alisema, kiasi cha Sh. bilioni 77.8 kitatumika kwa suala hilo na wanafunzi 91,568 wa elimu ya juu wa mwaka wa kwanza na wanaoendelea na masomo na kwa wanaosoma shahada za uzamili na uzamivu, wanatarajiwa kupewa mikopo kwa mwaka 2011/12.

Alisema katika mwaka huu wa fedha, Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) itaimarisha utoaji na urejeshaji wa mikopo kwa kuainisha taarifa za wakopeshwaji na zile za Tume ya Vyuo Vikuu, Baraza la Mitihani na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa.

Alisema pia Bodi hiyo itasogeza huduma za utoaji mikopo karibu na wananchi kwa kuanzisha ofisi ya kanda Zanzibar.

Akisoma maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii kuhusu wizara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Margaret Sitta , alisema ili kuimarisha uwezo wa Serikali kuendelea kutoa mikopo kwa wanafunzi, Kamati yake ilishauri Serikali itafute mbinu mbadala za kupata fedha ili kuinua uwezo wa kutoa mikopo mwaka hadi mwaka.

Alisema, ili kuimarisha urejeshwaji wa mikopo iliyotolewa tangu mwaka 2006, kiundwe chombo mahususi chini ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, ili kufuatilia ukusanywaji wa marejesho ya mikopo iliyokwishatolewa.

Alisema, taarifa za mikopo husika zitambulike kwa walengwa ili kurahisisha ukusanyaji wa fedha hizo kwa ushirikiano wa mwajiri na Bodi ya Mikopo na kuwa fedha za marejesho ya mikopo hiyo zitambulike bayana, kwa kuonekana katika taarifa ya utekelezaji wa majukumu kila mwaka.

Pia Kamati ilishauri utoaji vitambulisho vya Taifa ukamilike ili kutambua wanafunzi wanaokopa na waliokopa na uraia wao, ambapo pia Kamati ilishauri kuwapo udhibiti wa karo hasa katika vyuo visivyo vya Serikali.

Mbunge wa Viti Maalumu, Diana Chilolo (CCM), alishauri kutokana na utata katika urejeshwaji wa mikopo, Serikali itoe fedha hizo bure kwa wanafunzi badala ya kuwakopesha.

Akiwasilisha maoni ya Kambi ya Upinzani, Msemaji Mkuu wa Kambi hiyo kwa Wizara ya hiyo Cristowaja Mtinda, alisema kutokana na muundo wa Bodi ya Mikopo na uendeshaji mbaya, kuna haja ikavunjwa kwani imeshindwa kuifanya elimu ya juu ipatikane kwa kila mwanafunzi anayestahili.

Alisema Bodi hiyo ilitoa mikopo kwa wanafunzi 91,568 mwaka uliopita, lakini ilikusanya marejesho ya mikopo yenye thamani ya Sh. bilioni 7.9 kati ya Sh. bilioni 21 zilizotarajiwa kukusanywa.

“Kutokana na sababu hizo, Serikali iazimie kuivunja Bodi hii, pamoja na kufanya uchunguzi huru wa fedha zilizotumika chini yake hadi sasa na kujiridhisha kama waliopewa dhamana hii hawakutumia nafasi zao kujinufaisha binafsi,” alisema.

Alisema baada ya Bodi hiyo kuvunjwa, Serikali iunde chombo kipya kitakachojulikana kama Mamlaka ya Taifa ya Kugharimia Elimu ya Juu (TAHEFA), ambacho kitachukua majukumu yote ya Bodi.

Thursday, June 16, 2011

Wanafunzi 9,000 Udom watimuliwa


ZAIDI ya wanafunzi 9,000 wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) wamefukuzwa kwa muda usiojulikana kuanzia jana kwa madai ya kuhamasisha mgomo usio halali.Habari zilizopatikana mjini hapa zimeeleza kuwa wanafunzi hao ni wa Kitivo cha Sayansi ya Jamii na Sayansi Asilia. Walitakiwa kuondoka chuoni hapo kabla ya saa 8:00 mchana.

Baada ya amri hiyo, Polisi wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) walionekana wakiwa wanarandaranda katika maeneo ya chuo hicho.hali hiyo ilichangia pia kuharakisha wanafunzi hao kuondoka chuoni hapo wakihofia kukumbana na kipigo.

Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Idriss Kikula alithibitisha kufukuzwa kwa wanachuo hao na kusema kuwa suala la kuwarejesha litatokana na utaratibu watakaoupanga baadaye.

Kufukuzwa huko kumekuja siku mbili baada ya kuanzisha maandamano yaliyoshinikiza kujiuzulu kwa viongozi waandamizi wa Serikali, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Waziri wa Mambo ya Ndani, Shamsi Vuai Nahodha na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa kwa madai kwamba wamewadanganya kuhusu malipo yao ya masomo kwa vitendo.

“Ni kweli kabisa kuwa tumewasimamisha kwa muda usiojulikana. Tutawarudisha kwa muda ambao tutaona unafaa,” alisema Profesa Kikula na kuongeza mtindo utakaotumika ni wa kuchambua na kurudisha mwanafunzi mmoja mmoja.

Katika madai yao, wanafunzi hao walisema wanasoma bila ya kufanya mazoezi ya vitendo kama ilivyo kwa vyuo vingine. Madai mengine ni pamoja na mazingira mabovu chuoni hapo pamoja na kutosoma baadhi ya masomo ambayo wanachuo wengine wanasoma.

Msimamo wa wanafunzi

Wakizungumza mara baada ya agizo hilo jana baadhi ya wanafunzi hao walisema kuwa hawaoni tabu kufukuzwa wakisema wao ni waathirika wanaotumika kwa maslahi ya wengine. Walisema kuwa kufukuzwa kwao ni kwa ajili ya kudai maslahi ambayo wamekuwa wakiyatafuta wakati wote bila ya mafanikio na kwamba kama itabidi itakuwa bora waondoke.

“Sisi tunaondoka na wenzetu wengine walishaondoka katika Kitivo cha Sayansi ya Kompyuta kwa hiyo kwa hali hii lazima chuo chote kitafungwa maana hali inakokwenda chuoni hapa ni siasa tupu,” alisema mmoja wa wanafunzi hao na kuongeza:

“Ni bora turudi nyumbani kwa kuwa huwezi kusoma bila ya kufanya mafunzo kwa vitendo. Ni bora tukae nyumbani tu,” alisema mmoja wa wanafunzi hao huku akiungwa mkono na wenzake.

Wanafunzi wa Kitivo cha Teknolojia ya Habari na Elimu Angavu walifukuzwa baada ya kugoma wakitaka walipwe fedha kwa ajili ya vifaa vya kujivunzia kwa vitendo.

Kufukuzwa kwa wanafunzi hao kulikuwa faraja kwa madereva wa teksi na pikipiki maarufu kama bodaboda ambao walifurika chuoni hapo kufanya kazi ya kuwasafirisha kwa malipo ya Sh10,000 kwa pikipiki na teksi Sh15,000.

Tuesday, June 14, 2011

Polisi yapiga wanafunzi mabomu



Jeshi la Polisi limetumia mabomu kuwatawanya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom). Milio ya mabomu ilisikika katika eneo la Bunge mjini Dodoma, baada ya polisi kuwatawanya wanafunzi wa Chuo cha Sayansi ya Jamii cha Udom, kuandamana hadi bungeni wakitaka kumuona Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, kushinikiza kulipwa posho za mafunzo kwa vitendo.

Mapema asubuhi, wanafunzi hao walikusanyika katika viwanja vya Nyerere Square mjini hapo na ilipofika saa 4.00 asubuhi walianza kuandamana hadi bungeni wakishinikiza kumuona Pinda na Kawambwa. Hata hivyo, jitihada zao zilishindikana baada ya polisi kuwaamuru kuondoka katika eneo hilo na walipokaidi amri hiyo ndipo walipopigwa kwa mabomu ya machozi yaliyofanya wanafunzi hao kukimbia ovyo.

Katika maeneo mbalimbali ya mji wa Dodoma hususan bungeni kulikuwa na ulinzi mkali wa askari wa Kikosi cha Kuzuia Fujo (FFU), waliokuwa wamebeba bunduki na mabomu ya kurusha kwa mkono.

Rais wa Serikali ya Wanafunzi Kitivo cha Sanaa ya Lugha na Sayansi za Jamii, Mwakabinga Philipo, alisema wameamua kuandamana kutokana na kutotekelezewa madai yao ambayo ni kupatiwa fedha za mafunzo kwa vitendo ambazo wamekuwa wakiahidiwa, lakini hawapatiwi.

Alisema Seneti ya Udom Juni 8, mwaka huu ilitoa taarifa kuwa tatizo la madai ya fedha za mafunzo kwa vitendo halitatokea tena. Alifafanua kuwa licha ya ahadi hiyo, wanashangazwa kuona mpaka sasa haitekelezeki ndio maana waliamua kwenda bungeni kuonana na viongozi hao.

Mwakabinga alisema kutokana na ahadi zilizotolewa na viongozi hao ndio maana waliamua kwenda kuonana na Pinda na Kawambwa ili kupata ufumbuzi wa fedha hizo. Baada ya kutawanywa na polisi, ilipofika majira ya saa 6:00 mchana, wanafunzi hao walikusanyika tena katika viwanja vya Nyerere wakidai kuwa Waziri Kawambwa angekwenda kuzungumza nao.

Baada ya wanafunzi hao kukusanyika, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, James Msekela, alifika katika eneo hilo kwa lengo la kuwatuliza, lakini jitihada zake ziligonga mwamba baada ya kumzomea na kumwambia “hatukutaki wewe, tunamtaka Waziri.” Baada ya Dk. Msekela kuzomewa, askari wa FFU walianza kuwatawanya wanafunzi hao na kukimbizana nao katika mitaa mbalimbali na kufanikiwa kuwakamata baadhi yao.