Showing posts with label lisu. Show all posts
Showing posts with label lisu. Show all posts

Thursday, May 26, 2011

Lissu na wenzake marufuku Nyamongo

Maiti wazikwa, wananchi wataka kurejesha majeneza polisi



 
















MBUNGE wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu, ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Katiba na Sheria, na wenzake saba ambao juzi walifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Tarime na kusomewa mashtaka matatu ya kuingia eneo la hospitali bila kibali, kufanya mkutano na kuzuia watu kufanya kazi, wamepata dhamana lakini wamezuiwa kutembelea maeneo ya Nyamongo hadi kesi inayowakabili itakapokwisha.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya wilaya hiyo, Yusto Roboroga alitoa uamuzi huo akisema ni kwa mujibu wa kifungu cha Sheria Namba 148 cha Makosa ya Jinai, kilichofanyiwa marekebisho mwaka 2002, ambacho kinatoa haki kwa watuhumiwa kupata dhamana. Alitoa uamuzi huo baada ya kupitia pingamizi lililowekwa na upande wa mashtaka kutaka wasipewe dhamana. Hata hivyo, alisema: “Washtakiwa wanazuiwa kutembelea maeneo ya Nyamongo mpaka kesi hiyo itakapokuwa imekwisha."

Hakimu huyo alisema kwa kuwa washtakiwa hao ni viongozi wakubwa wa chama walizuiwa ili kupunguza shinikizo la wanachama kutokana na tukio lililojitokeza, lakini kwa kuwa mazishi yameshafanyika, alisema wanaweza kudhaminiwa kama watakidhi masharti.

Hakimu Ruboroga alitaja masharti  ya dhamana hiyo kuwa ni kusaini mkataba wa dhamana wa Sh5 milioni kwa wadhamini wawili wanaoaminika.

Kwa wasio wakazi wa Tarime, alisema watatakiwa kupeleka mahakamani hati za mali isiyohamishika. Washtakiwa wote walikidhi masharti na kuachiwa kwa dhamana hadi Juni 26, mwaka huu kesi hiyo itakapotajwa tena.

Juzi, Lissu na wenzake, Waitara Mwita Mwikwabe, Stanslaus Nyembea, Anderson Deogratias Chacha, Andrew Andalu Nyandu, Mwita Marwa Maswi, Bashiri Abdalllah Selemani na Ibrahimu Juma Kimu walifikishwa mbele ya mahakama hiyo na kusomewa mashtaka hayo matatu na Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Casmir Kiria ambaye alisema, waliyatenda Mei 23, majira ya saa nne usiku. Wote walikana mashtaka hayo.

Wakati huo huo maiti wote waliokuwa wametelekezwa barabarani wamezikwa na ndugu zao huku baadhi ya familia zikikataa kuwazika kwa majeneza ya polisi na kutumia yale yaliyokuwa yameandaliwa huku wengine wakipanga kuyarudisha kwa Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Tarime, Constantine Massawe.

Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Kewanja, Om’tima Tanzania alisema kuwa mmoja wa marehemu hao, Chacha Ngoka alizikwa na jamii. Hata hivyo, alisema polisi waliweka mwili wake ndani ya jeneza bila kuweka sanda hali ambayo iliwalazimu kumweka ndani ya jeneza lao na kumvika sanda. Hilo lilifanyika pia katika eneo la Nyakunguru alikozikwa marehemu Emmanuel Magige.

Katika Kijiji cha Bonchugu, Serengeti, Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji hicho, Mwikwabe Makena alidai kwamba walilazimika kuzika mwili wa marehemu Chawali Bhoke uliotelekezwa na polisi.


Alidai kwamba kabla ya kuutelekeza, walifyatua mabomu ya machozi na risasi hewani baada ya wananchi waliokuwa wamebeba pinde, mishale, mikuki na mapanga kujaribu kuzuia gari la polisi. Alisema walilazimika kuzika bila kuwapo kwa ndugu wa marehemu waliokuwa wameachwa Tarime.Hata hivyo, Kamanda Massawe na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Robert Boaz hakuwa tayari kuzungumzia madai hayo.

Wednesday, May 25, 2011

Polisi 'wapora' maiti mochwari

*Tundu Lisu akamatwa, afikishwa kortini Tarime

JESHI la Polisi limewakamata na kuwafikisha mahakamani Mbunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) pamoja na maofisa wengine wa chama hicho baada ya kudaiwa kufanya mkusanyiko usio halali na kuzuia watu kuzika ndugu zao.

Sambamba na hatua hiyo jeshi hilo limedaiwa kuingia mochwari ya Hospitali ya Wilaya ya Tarime na kuchukua kwa nguvu maiti nne za watu waliouawa na polisi hivi karibuni na kwenda kuzitelekeza maeneo mbalimbali ili kuzuia mkusanyiko wa kuaga maiti hizo kwa pamoja, kwa kile wanachoeleza ni kuzuia uvunjifu wa amani.

Bw. Lisu na wenzake wanadaiwa kukutwa katika Hosptali ya Wilaya ya mjini hapo wakilinda miili hiyo baada ya kusikia tetesi kuwa polisi walikuwa na mpango wa kuichukua na kuisafirisha kusikojulikana.

Akizungumza na waandishi wa habari nje ya mahakama, Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Bw. Casmil Kria alisema watuhumiwa wanakabiliwa na mashtaka matatu, yaliyosomwa mbele ya Hakimu wa Wilaya, Bw. Yusto Ruboroga.

Mashtaka hayo ni kuingia eneo la hospitali bila kibali, kufanya mkusanyiko usio halali na kuzuia watu kuchukua miili ya ndugu zao.

Watuhumiwa hao ambao wanadaiwa kukutwa eneo hilo saa 4:00 usiku baada ya kusomewa mashtaka na kuyakana, walirudishwa rumande kwa 'sababu za kiusalama', na kesho watafikishwa tena mahakamani kwa ajili ya kupewa dhamana, endapo miili ya waliouawa itakuwa imeshazikwa.

Walioshtakiwa ni Mbunge wa Singida Magharibi, Bw. Tundu Lissu (43), Bw. Mwita Mwikwabe (36), Bw. Stancelaus Nyembea (33), Anderson Deogratias (35), Bw. Andrew Andaru (63), Bw. Mwita Marwa (48) Bw. Bashiri Abdallah Seremani (35) pamoja na Ibrahimu Juma Kimi (27) ambaye ni dereva wa Bw. Lissu.

Wakati huo huo, waandishi wanne wa habari pamoja na Mbunge Viti Maalumu, Bi. Ester Matiko (CHADEMA) nao walishikiliwa na Jeshi la Polisi katika Kituo Kidogo cha Nyamwaga na baadaye kuachiwa huru baada ya mahojiano.

Wandishi hao ni Bi. Beldina Nyakeke wa The Citizen, Anna Mroso (Nipashe), Bw. Anthony Mayunga (Mwananchi) pamoja na Mabere Makubi wa Chanel Ten ambao walikuwa kwenye msafara wa Bi. Matiko.

Waandishi wengine wa habari waliofika katika mahakama ya wilaya kufuatilia tukio hilo walizuiliwa kuingia na kutishiwa kupigwa
risasi na ofisa mmoja wa polisi.

Ofisa huyo ambaye hakufahamika jina aliwatimua waandishi hao, huku akiomba bunduki kutoka kwa askari mwenzake na kuiandaa mithili ya kupambana na adui.

“Toka! Toka! Naombeni bunduki yangu hapa naona nyinyi hamjui kufanya kazi, hatukuja kufanya mchezo hapa waondoe na wale watu upesi mahali hapa wasongee mbali huko hatutaki mtu hapa!” alisema.

Askari hao wakiwa wameziba njia huku ofisa huyo akiendelea kuelekeza bunduki yake kwa raia waliokuwa eneo hilo.