Showing posts with label polisi. Show all posts
Showing posts with label polisi. Show all posts

Monday, August 15, 2011

Kisa na mkasa na Salim Kikeke

Risasi


Bwana mmoja nchini Marekani yuko hospitali baada ya kujipiga risasi kwenye uume wake.
Bwana huyo kutoka Phoenix, Arizona, alijipiga risasi kwa bahati mbaya, wakati akiweka bastoka katika mfuko wake wa suruali.

Polisi katika kiunga cha Chandler wamesema bwana huyo, Joshua Seto mwenye umri wa miaka 27, akiwa na mchumba wake Cara Cristopher walikuwa wakielekea katika dukamoja ndipo walipokutwa na mkasa huo.
Bunduki hiyo ilifyatuka, na risasi kupenya katika uume wa Joshua na kupitiliza hadi kwenye paja la bwana huyo.

Haraka walipiga simu ya dharura, na Bi Cara kuambiwa azuie damu kububujika kwa kutumia shati la mchumba wake huyo.

Kwa mujibu wa mtandao wa Stuff.co.nz polisi wamesema hawana uhakika ni bunduki ya aina gani ilifyatuka.
Aidha kachero wa polisi wa Chandler, Seth Tyler amesema hafahamu bwana huyo atatoka lini hospitali, na iwapo kama ameumia kiasi gani.

Polisi Tyler amewataka watu kutumia mikoba maalum ya kuwekea bastola, badala ya kuziweka mfukoni, au kuzichomeka kwenye mikanda ya suruali.

Kumeza ushahidi


Fundi mmoja wa ujenzi ameburuza mahakamani nchini Marekani baada ya kutuhumiwa kumeza ushahidi.
Shirika la habari la Reuters limesema bwana huyo Wilfredo Gonzalez alimeza pete ya almasi aliyokuwa kitaka kuiiba.

Waendesha mashitaka mjini Chicago wamesema bwana Gonzalez alikuwa akifanya kazi za ujenzi katika mji wa Cicero, huko Illinois, alipofanya wizi huo, wakati mwenye nyumba alipoingia bafuni kuoga.
Baada ya mwenye nyumba huyo kugundua kuwa pete yake imepotea katika mazingira ya kutatanisha, alimuita mume wake.

Gonzalez alipoulizwa alikana, lakini lakini baada ya vuta nikuvute, aliitoa pete hiyo mfukoni na kuimeza.
Polisi waliitwa mara moja, na Gonzalez kupelekwa hospitali, ambapo alipigwa picha za X-ray, na kuonesha jinsi pete hiyo inavyoshuka tumboni taratiibu.

Polisi hatimaye walifanikiwa kuitoa pete hiyo, ingawa haijaelezwa njia gani ilitumika. Bwana Gonzalez anakabiliwa na kifungo cha miaka mitatu jela, iwapo atakutwa na hatia.

Popo

Waumini katika kanisa moja hapa Uingereza wamelazimika kulikimbia kanisa lao, kufuatia popo kutanda katika paa.

Gazeti la daily Mirror limesema popo hao hujisaidia wakati maombi yanaendelea. Taarifa zimesema mwanamama mmoja aliugua kutokana na hali hiyo kiasi kwamba maafisa wa mazingira na afya kulazimika kuitwa kushuhudia. Hata hivyo waumini hao hawana uwezo wa kuwaondoa popo hao kufuatia pingamizi la kisheria lililowekwa na wanaharakati wa mazingira.

Wanaharakati hao wanasema popo hao ni aina ya kipekee na ni adimu, na hivyo haitakiwi wahamishwe au kufukuzwa. Kanisa hilo, saxon Church, lililopo Ellenburn, Yorks kaskazini, limesema linafikiria kuchukua hatua za kisheria.

Mmoja wa wahudumu wa kanisani hapo, Liz Cowley amesema watu hawawezi kuendelea kusali, huku popo wakitoa kinyesi na mikojo. "Ilibidi kukatishe misa" amesema bi Liz.
Msemaji wa wanaharakati wa mazingira wa Natural England amesema popo hao wenye masikio makubwa na rangi ya hudhurungi, wanaweza wakatoweka duniani iwapo hawatapata matunzo mazuri.

Kufutari


Waisilam wanaoishi katika jengo refu zaidi duniani, wanalazimika kusubiri muda zaidi kufutari kuliko waisilam wengine, kwa kuwa jua linachelewa kuzama huko walipo, kutokana na urefu wa jengo hilo. Jengo hilo liitwalo Burj Khalifa liko Dubai.

Kiongozi wa juu wa kidini wa Dubai, Mohammed al-Qubaisi amesema wale wanaoishi zaidi ya ghorofa ya themanini, lazima wasubiri dakika mbili zaidi, baada ya muda kutimia mjini Dubai ili kupata futari yao.
Mwezi wa Ramadhani ulianza wiki moja iliyopita.

Gazeti la Mirror limesema shekhe huyo amesema wale wanaoishi katika ghorofa ya mia moja na hamsini na kuendelea, watalazimika kusubiri dakika tau zaidi ya wenzao.
Jengo hilo, Burj Khalifa, lina ghorofa mia moja na sitini. Waisilam huanza kula futari mara wanapoona jua limezama.

Polisi

Polisi mmoja nchini India alimfukuza mtu aliyekuja kufungua kesi ya kuibiwa mapema asubuhi, akimtaka aje baadaye.

Polisi huyo alisema, akifungua kesi hiyo asubuhi, basi siku nzima atakuwa akipokea kesi kama hizo. Mlalamikaji, Amandeep Saini, wa eneo la Naraingarh alishangazwa na jibu hilo. Bwana huyo alikwenda polisi kushitaki, baada ya kuibiwa simu yake ya mkononi. Gazeti la Times of India limesema polisi huyo alisema hayuko tayari kuanza siku yake kwa kuandikisha kesi ya wizi.
"Tafadhali njoo saa nane mchana" alisema polisi huyo.

Mwizi pochi

Polisi nchini Marekani wamesema mwizi mmoja aliingiwa na imani na kuamua kurejesha pochi aliyoiba.
Gazeti la Eagle Tribune limesema mwizi huyo alikwapua pochi ya mwanamama mmoja katika duka la New Hampshire.

Pochi hiyo ilikuwa na dola tinisi pamoja na kifaa cha kuongozea njia, maarufu kama GPS. Hata hivyo siku chache baadaye, mama huyo mwenye umri wa miaka sitini na moja, aliikuta pochi yake, alipokwenda posta kuchukua barua zake.

Siku chache baadaye, alisikia mtu akigonga mlango wa nyumba yake, na alipofungua, alikutana ma mtu, aliyemuomba radhi, na kurejesha viu vingine vilivyosalia.

Baada ya kuomba radhi mwizi huyo alimpa mwanamama huyo barua, na haraka kutimua mbio. Barua hiyo ilikuwa na maelezo zaidi ya kuomba radhi.

Kaimu kamanda wa polisi kathleen Jones ameliambia gazeti la Eagle Tribune kuwa, ingawa mwanamama huyo amefurahi kurejeshewa vitu vyake, lakini sasa ana wasiwasi, kwa kuwa huyo mwizi anafahamu mahala anapoishi.

Polisi wamesema huenda aliweza kufahamu nyumba hiyo, aada ya kukuta anuani ndani ya pochi aliyoiba.

Busu marufuku

Jumuiya moja inayoshauri watu kuhusu tabia za kijamii nchini Ujerumani, imetoa wito kwa watu kupigwa marufuku kupigana busu wakiwa kazini.

Jumuiya hiyo, Knigge Society imesema, tabia ya kupigana busu katika mashavu kama njia ya kusalimiana kwa wafanyakazi, inawatatiza wajerumani wengi. Mwenyekiti wa jumuiya hiyo hans Michael Klein amesema amepokea barua pepe nyingi zikionesha wasiwasi wa busu kutoka kwa wafanyakazi. Amewashauri watu makazini, kusalia na utamaduni wa kawaidia wa kusalimiana kwa kupeana mikono.

Thursday, June 30, 2011

Ukweli wa vifo vya wapenzi 2 Dar wajulikana

POLISI Jijini Dar es Salaam wamepata ujumbe wa maandishi wa marehemu Nicholaus Maleko (43) aliyeelezwa kujiua pamoja na mpenzi wake, Catherine George (25) Jumapili iliyopita.

Kwa mujibu wa Polisi, Maleko ameandika kuwa, yeye amejiua lakini kifo cha mpenzi wake ni bahati mbaya.

Maleko amedai katika barua hiyo kuwa, amejiua kwa makusudi kukwepa usumbufu wa kuhojiwa baada ya kubaini kifo cha mpenzi wake alichodai kilitokea Catherine alipojisahau na kunywa pombe, wakati akiwa katika dozi ya dawa za ugonjwa uliokuwa ukimsumbua.

Akizungumza na HABARILEO jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela
alisema, barua hiyo ya Nicholaus imeeleza namna vifo hivyo vilivyotokea na itatumika kama sehemu ya ushahidi.

“Pamoja na kuwataja wadai na wadaiwa wake, ameandika namna mali zake zitakavyogawanywa kwa warithi na kufafanua kwa kina jinsi tukio zima lilivyotokea, ambalo kwa ufupi limehusisha uzembe wa mwanamke na makusudi ya Nicholaus,” alisema Kamanda Kenyela.

Kwa mujibu wa Kamanda Kenyela, barua hiyo imemtetea Catherine na kueleza kuwa hakujiua kwa makusudi, ila bahati mbaya kwa kunywa bia aina ya Serengeti wakati akiwa katika dozi ya dawa za binadamu kutibu ugonjwa ambao hata hivyo, Nicholaus hakuutaja.

“Nicholaus, pamoja na kuwapa pole ndugu wa marehemu Catherine na kutuma salamu za rambirambi kwa ndugu na jamaa katika barua hiyo, pia ameeleza namna alivyojaribu kuokoa maisha ya dada huyo ambaye katika barua amemtaja kama mkewe,” alisema.

Kwa maelezo ya Kenyela, sehemu ya barua ya Nicholaus ilisomeka, “mke wangu amejiua kwa bahati mbaya lakini mimi nimejiua kwa makusudi kwa kunywa sumu ya panya kwa sababu sikuona sababu ya kuendelea kuishi na kusumbuliwa kwa yaliyotokea.

“Nilipoona hali yake imebadilika na kukumbuka alikuwa amekunywa dawa, nilimnywesha maziwa lakini hayakusaidia na baada ya hapo niliamua kumpa redbull kwa kudhani ninamsaidia kwa sababu kinywaji hicho ni energizer (cha kuongeza nguvu) lakini kwa bahati mbaya hali ilibadilika na kuzidi kuwa mbaya, akafariki dunia,” Kenyela alisoma barua hiyo.

Tukio hilo lilitokea Boko nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam na kugunduliwa saa 12 asubuhi na mtoto wa marehemu Nicholaus aliyekuwa akienda bafuni kuoga, Masanje Maleko (20) baada ya kusikia baba yao akikoroma kwa sauti ya ajabu.

Mtoto mkubwa, Alexandre Kwilima (21) na ndugu yake Masanje walisema walilazimika kuvunja mlango wa chumbani kwa wawili hao na kukuta mama yao mdogo akiwa amefariki huku baba yao akiwa hajitambui.

“Tuliwafikisha katika hospitali ya MICO iliyoko Tegeta lakini baba alifariki muda mfupi baadaye. Hawakuwa na ugomvi na siku zote walizokuwa pamoja walizoea kunywa pombe huko chumbani kwao,” alisema Kwilima na kufafanua kuwa Catherine waliyeanza kumuona na Nicholaus Januari mwaka huu, alikuwa mama wa kwenda na kuondoka nyumbani hapo. Mtoto huyo alisema muda mrefu aliokaa nyumbani hapo kwa mfululizo ni wiki moja.

Hata hivyo, polisi imechukua sampuli ya maini, damu, utumbo na figo za marehemu hao na kupeleka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kwa uchunguzi zaidi.

“Majibu ya Mkemia Mkuu ndio yatakayo tueleza ukweli kuhusu chanzo cha vifo hivyo kama ni sumu ya dawa ya panya, kuchanganywa dawa na pombe au kitu kingine lakini matapishi ya Nicholaus tuliyoyachukua hospitalini MICO, yana rangi ile ile ya sumu tuliyoipata pale na tumeyakabidhi kwa Mkemia Mkuu pia kwa uchunguzi wa kitaalamu,” alisema.

Katika hatua nyingine, msemaji wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Dar es Salaam, Jezza Waziri alisema uchunguzi wa awali wa marehemu hao umekamilika na kupeleka ripoti Polisi na miili yote miwili bado imehifadhiwa hospitalini hapo.

Watoto wa marehemu walisema kuwa, baba yao atasafirishwa Ijumaa kwenda Marangu, mkoani Kilimanjaro kwa maziko na hawakuwa na taarifa kuhusu mipango ya mazishi ya Catherine.

Tuesday, June 14, 2011

MWANAFUNZI WA SHULE YA LIVINGSTONE NJOMBE ATEKWA ACHINJWA

 
WATU wasiofahamika wamevamia shule ya kimataifa ya Livingston ya wilayani Njombe mkoani Iringa na kumteka mwanafunzi mmoja wa kike katika shue hiyo na kumchinja kwa kumtenganisha kichwa na kiwiliwili.
Imedaiwa kuwa watu hao ambao idadi yao haijafahamika walivamia shule hiyo majira ya saa 10 alfajiri ya kuamkia juzi na kuingia katika bweni la wasichana na kufanikiwa kumteka mwanafunzi huyo aliyefahamika kwa jina la Doris Lutego (12) ambaye ni mkazi wa mtaa wa shule ya Uhuru mjini Makambako wilaya ya Njombe.

Mmoja kati ya mashuhuda wa tukio hilo ambaye aliomba jina lake kuhifadhiwa kwa kuwa si msemaji wa juu wa tukio hilo alisema kuwa mwanafunzi huyo alitekwa usiku wa kuamkia jumapili na kuwa pamoja na jitihada za kumtafuta zilizofanywa na wananchi na viongozi wa shule hiyo jitihada zilishindikana .

“Baada ya taarifa ya kuvamiwa kwa shule hiyo na kutekwa mwanafunzi huyo wananchi tuliendesha msako mkali wa kuwasaka wavamizi hao ila hatukufanikiwa hadi leo asubuhi baada ya wakazi wa eneo la kitongoji cha Kambarage Njombe kufanikiwa kukuta mfuko wa Salfeti ambao ulikuwa na mwili wa mtoto huyo. Mfuko huo ulikutwa nyuma ya nyumba ya balozi wa kitongoji hicho na baada ya kutafuta zaidi ndipo kichwa chake kilikutwa karibu na nyumba ya mwenyekiti wa kitongoji hicho huku kikiwa kimehifadhiwa katika mfuko wa madaftari ya mwanafunzi huyo.
 
Hata hivyo alisema kuwa mbali ya kufanikiwa kukuta mwili wa mwanafunzi huyo ila bado hawajafanikiwa kuwakamata wahusika wa mauwaji hayo ya kinyama . Alisema kuwa mauwaji hayo yamewaweka katika maswali zaidi wakazi wa mji wa Njombe na wilaya nzima kwani inaonyesha wazi wauwaji hao wamefanya hivyo kama sehemu ya kulipiza kisasi katika familia ya mtoto huyo.

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Iringa Evarit Mangalla amethibitisha kutokea tukio hilo na kudai kuwa mtoto huyo alikuwa akisoma darasa la tano katika shule hiyo .

Kamanda Mangalla alisema
kuwa taarifa zilizofika polisi mapema jana zillikuwa ni za kutekwa kwa mtoto huyo na kukutwa kwa baadhi ya meno yake na damu katika kitanda chake na kuwa bado jeshi la polisi linafanya uchunguzi zaidi na kuwasaka wahusika wa tukio hilo.

Monday, June 6, 2011

Hali tete: Chadema, Polisi wakwaruzana

Askari polisi wakilinda kwenye kituo kikuu cha polisi kati anakoshikiliwa mwenyekiti wa Chadema Freeman MbowePicha na Fidelis Felix/Silvan Kiwale


















JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, jana lililazimika kuimarisha ulinzi katika Kituo chake Kikuu (Central) na baadhi ya maeneo ya jiji kukabiliana na tishio la wanachama wa Chadema kuandamana ili kushinikiza Mwenyekiti wao, Freeman Mbowe aliyekamatwa juzi aachiwe.Mbowe ambaye alikamatwa juzi ikiwa ni kutekeleza amri ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha iliyoamuru akamatwe popote alipo na afikishwe hapo kwa kutotii amri ya kufika mahakamani katika kesi inayomkabili, alitarajiwa kupelekwa huko wakati wowote kuanzia jana akiwa chini ya ulinzi.

Jana, vijana wa Chadema walikusanyika katika kituo hicho huku wakilaani kitendo cha kukamatwa kwa mwenyekiti wao huku wengine wakijikusanya katika vikundi vidogovidogo katika maeneo mbalimbali katika Barabara za Morogoro na Nyerere, lengo likiwa kushinikiza kiongozi huyo atolewe rumande na asisafirishwe kupelekwa Arusha.

Taarifa kutoka Arusha ambako kesi ya kiongozi huyo inatarajiwa kuendelea leo asubuhi zinaeleza kuwa polisi jana jioni waliendesha msako wa wanachama wa Chadema waliokuwa wakihamasishana kuhudhuria kwa wingi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Arusha.

Wanachama na mashabiki hao wa Chadema walidai kwamba kitendo cha kukamatwa kwa kiongozi huyo wa kambi ya upinzani bungeni ni mpango uliobuniwa na CCM wa kubinya demokrasia ya vyama vingi nchini.

Mbowe na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Bara, Zitto Kabwe walikamatwa katika maeneo tofauti nchini juzi. Wakati Mbowe alidaiwa kutotii amri ya mahakama, Zitto alidaiwa kuzidisha muda wakati wa kuhutubia mkutano wa hadhara mkoani Singida.

“Tumeongea na polisi, bado wanamng'ang'ania Mbowe. Msimamo wao ni kumpeleka Arusha, tuangalie utaratibu utakaotumika katika kumsafirisha,” alisema Mkurugenzi wa Mambo ya Nje wa Chadema, John Mnyika.

Baada ya kauli hiyo ya Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubunge, vijana wa chama hicho wakiongozwa na Diwani wa Kata ya Ubungo, Boniface Jacob walianza kuimba nyimbo za kulaani kukamatwa kwa mwenyekiti wao huku wakisema muziki wa Chadema polisi hawauwezi.

Ofisa mmoja mwadamizi wa Polisi Ilala ambaye hakujitambulisha jina aliwaambia vijana hao kuwa polisi  walishakubaliana na viongozi wa Chadema kuwa mtuhumiwa huyo amepangiwa utaratibu wa kusafirishwa kwenda Arusha kuhudhuria kesi yake.Ofisa huyo aliwataka wananchi waliokuwa kwenye eneo hilo kuondoka ili kupisha jeshi hilo kuendelea na kazi ya kutoa huduma kwa watu wengine.

“Tumeshaongeza na wakubwa wenu, hiki ni kituo cha polisi watu mbalimbali wanakuja kupata huduma hapa. Mtu haji kuangaliwa kwa aina hii ya hamasa na nyimbo, tunaomba muondoke,” alisema ofisa huyo.Kauli hiyo ilipingwa na vijana hao wakisema ofisa huyo ni mtu wa kawaida hawezi kuwaeleza mambo kama hayo.

“Sisi hapa tuna viongozi wetu mambo kama hayo tungeelezwa na kuelewa kama yangesemwa nao na si mtu wa kawaida kama wewe,”alisikika mmoja wa wanachama hao akisema kwa sauti.

Kauli hiyo ilimshangaza ofisa mwingine wa polisi aliyeibuka na kuhoji: “Mnasema huyu ni mtu wa kawaida? Akajibiwa “ndiyo”, “huyo siyo mtu wa kawaida."Vijana hao waliendelea na msimamo wao: “Sisi tunasema huyo ni mtu wa kawaida kwa sababu siyo kiongozi wetu, ndiyo maana tunasema angekuwa kiongozi wetu tungemwelewa.”

Kauli hiyo ilimlazimisha Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Faustine Shilogile kujitokeza na kuwataka watu hao kuondoka katika eneo hilo kwa sababu kulikuwa na shughuli mbalimbali zilizokuwa zikiendelea.

“Tumeongea na viongozi wenu, tumeshakubaliana tunawaomba mtawanyike na sisi tuendelee na kazi, sitaki mkusanyiko wowote katika kituo cha polisi,” alisema Shilogile. Mara baada ya kauli hiyo gari la maji ya kuwasha lilianza kusogea walipokuwa wafuasi hao wa Chadema likitanguliwa na Polisi wa Kutuliza Ghasia waliokuwa wakiwafukuza katika eneo hilo.

Kundi hilo liliondoka na kuelekea makao makuu ya Chadema ambako Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa alikuwa na mkutano na waandishi wa habari.

Msimamo wa Kamanda Kova
Akizungumzia mvutano huo, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema jeshi lake haliwezi kumwachia Mbowe kwa sababu wanaheshimu amri ya Mahakama.

Kova aliwaambia waandishi wa habari jana kwamba jeshi hilo lilipokea amri ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha ya kumkamata kiongozi huyo wa Chadema na kwamba hawaruhusiwi kuhoji lolote juu ya amri hiyo.

“Sisi kama jeshi la Polisi tumepokea amri ya mahakama ya kumtia hatiani Mheshimiwa Mbowe na hatuna mamlaka ya kumwachia huru hadi mahakama itoe amri ya kumwachia,”alisema.

Alisema sheria hairuhusu kuhoji sababu za amri inayotolewa na mahakama na kufafanua kuwa hizo ni sheria zilizotungwa na wabunge wenyewe. Alisema Mbowe anatarajiwa kusafirishwa chini ya ulinzi wa Polisi kwenda mkoani Arusha kujibu kesi inayomkabili na kwamba taratibu zote za safari tayari zimekamilika.

“Tunachokifanya ni maagizo ambayo yametoka ngazi ya juu kuhusu suala hili kwa hiyo Mbowe atapelekwa Arusha chini ya ulinzi wa polisi muda wowote kuanzia sasa alimradi awahi muda wake wa mahakama,”alisema Kova.

Alisema atapelekwa Arusha chini ya ulinzi wa polisi kwa sababu amekiuka masharti yake ya dhamana na kwamba tayari wamezungumza na baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani waliokwenda kumuona kiongozi huyo wa kambi ya upinzani bungeni jana.

Kova alisema kulingana na taratibu na sheria za Tanzania, mahakama ikitoa amri hakuna mtu anayeweza kuipinga.

Aliwataka wananchi watulie na kuipa fursa mahakama itekeleze sheria zilizotungwa na Bunge. Akizungumzia kukamatwa kwa Mbowe, Mnyika alisema hizo ni njama za kuudhalilisha upinzani na pia mbinu za kumtaka Mbunge huyo wa Hai asihudhurie kwenye Kikao cha Bunge la Bajeti.

“Endapo watashindwa kutumia busara za mazungumzo tuliyoyafanya kumwachia Mbowe, jambo hili tutalirudisha kwa wananchi na nguvu ya umma itatumika kusuluhisha tatizo hilo,” alisema.

Alisema amani ni tunda la haki lakini inaweza kupotea kama haki haitatendeka na kuongeza kuwa kuna watu ambao wanashutuma nzito za ufisadi, lakini hawachukuliwi hatua zozote isipokuwa viongozi wa upinzani.


Tamko la Dk Slaa
Dk Slaa alisema kesi zinazowakabili viongozi wa chama hicho na wabunge wa vyama vya upinzani vinalifedhehesha Bunge la Tanzania kimataifa.

“Ili mtuhumiwa akamatwe sheria iko wazi, notisi zilitakiwa kutolewa kwa mdhamini wake na pia kwa wakili, lakini kwa Mbowe haikuwa hivyo na hiyo inaonyesha ni agizo kutoka mahali Fulani,” alidai.

“Polisi mkoa wa Mwanza wametuma barua kwa Katibu wa Bunge kuomba kibali cha kwenda kumhoji Mbunge wa Jimbo la Busega, Dk Titus Kamani, iweje kwa wabunge wa upinzani kukamatwa bila utaratibu? Alihoji Dk Slaa.

Alisema kutokana na mazingira hayo kama Mbowe hatafikishwa leo mahakamani wabunge wa Chadema hawataingia bungeni.

Kuhusu uwakilishi kwenye kamati ya uongozi alisema hata kama Zitto atakuwa nje ya mahabusu, hataingia kuwakilisha upinzani kwa sababu anayetakiwa kumpa kibali cha kufanya hivyo yupo ndani.

Kuhusu kosa la Zitto kukamatwa na polisi alisema inashangaza kwa sababu alikuwa kwenye mkutano wa hadhara kama mbunge na alizidisha dakika 20 kwenye mkutano huo.

Alisema hiki siyo kipindi cha kampeni na Zitto ni kiongozi mwenye haki ya kufanya hivyo na kusisitiza kilichofanyika kimelenga kufifisha demokrasia nchini.

Friday, June 3, 2011

Mahakama yaamuru Mbowe akamatwe

















 MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Arusha, imetoa amri ya kukamatwa kwa Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe popote alipo na kufikishwa mahakamani hapo kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kutotii amri ya kufika mahakamani hapo. Mahakama hiyo pia imemtaka mdhamini wa Mbowe aliyetajwa kwa jina la Julius Isaya Magwe, kufika mahakamani hapo mara moja ili kuieleza mahakama hiyo sababu za kutotii amri ya mahakama pale anapohitajika.

Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Charles Magesa alisema jana kuwa kimsingi Mahakama inakubaliana na hoja ya wakili upande wa Serikali kuitaka mahakama kutoa amri ya kukamatwa kwa Mbowe kwa sababu ya kutotii amri ya kufika mahakamani au kumtuma mdhamini wake. Alisema sababu iliyotolewa mahakamani hapo kwamba mshtakiwa huyo ni mbunge na yupo kwenye vikao vya Kamati za Bunge haina uzito kwa kuwa hiyo ni moja ya shughuli zake kama ilivyo shughuli nyingine kwa watumishi wa serikali.

“Hivyo basi kama ni shughuli zake za kawaida, haimzuii kutii amri ya mahakama pale anapoitwa bila kujali anaitiwa nini,” alisema Magesa. Hakimu Magesa alisema kuwa anachokumbuka ni kwamba Mahakama hiyo kweli ilipokewa maelezo ya kuwa washtakiwa hawatahudhuria mahakamani hapo Mei 27 mwaka huu kwa sababu ya kuwa katika vikao vya Kamati za Bunge na kuagiza waje wadhamini wao siku kesi inapotajwa. Ndiyo sababu Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini alimpeleka mdhamini wake mahakamani hapo.

Lakini, kabla ya kuhitimisha agizo hilo, hakimu huyo, awali alitoa amri ya kutaka kukamatwa kwa Mbunge wa Moshi Mjini, Philimon Ndesamburo, ambaye naye hakutii amri ya mahakama kwa kutofika Mei 27, 30 na 31 na hata jana.

Hata hivyo, baada ya kutoa amri ya kukamatwa kwa Ndesamburo ambaye naye ni mshtakiwa, ghafla alijitokeza mdhamini wake, Rubeni Ngowi na kuiambia mahakama hiyo kuwa alikuwapo Mei 30, ila hakuweza kusogea mbele kwa sababu ya woga wa mahakama na kwa kuwa hakuitwa. Baada ya maelezo hayo, Hakimu Magesa alimhoji mdhamini huyo akitaka kujua alikuwa wapi Mei 27 mwaka huu kesi hiyo ilipotajwa. Ngowi alijitetea kuwa alikwenda jijini Dar es Salaam kwa familia yake ambayo ilikuwa ina matatizo, lakini Mei 30 alifika mahakamani hapo na kuomba kuondoa amri hiyo ya kukamatwa kwa mshtakiwa wake.

“Basi kwa sababu nakumbuka ulikuwapo Mei 30 na nilikuona hapa mahakamani ukimnong’oneza wakili Kimomogoro, basi naondoa amri hii. Ila naomba utii amri ya mahakama pale mshtakiwa anapokosa uje kutoa sababu za kukosa kwake,” alisema Magesa.

Hakimu Magesa pia alitoa onyo kwa washtakiwa wengine wakiongozwa na Dk Willibrod Slaa wasiache kufika mahakamani, kila siku kesi yao inapotajwa na pale wanapokuwa na sababu ya kutofika, wahakikishe wadhamini wao wanakuwapo kutoa sababu za kukosekana kwao.

Akitoa uamuzi wa hatima ya dhamana za washtakiwa wa kesi inayowakabili viongozi wa Chadema, Godbless Lema, Joseph Selasini na wafuasi wao, Hakimu Mkazi Magesa, alisema Mahakama hiyo imeondoa hati ya kukamatwa kwa washtakiwa hao kama ilivyoamriwa awali na kutupilia mbali ombi la wakili wa serikali la kutaka wafutiwe dhamana.

Alisema kuwa kutokana na kupitia kwa makini maelezo ya utetezi wa pande zote mbili kwa Wakili wa Serikali, Edwin Kakolaki na wakili upande wa utetezi, Medhod Kimomogoro, Mahakama hiyo imeamua kuwapatia dhamana ya kudumu washtakiwa ambao ni Dk Slaa na wenzake, kwa kutii amri ya Mahakama.

“Mahakama hii imeamua kufuta amri ya dhamana ya muda na kuacha dhamana ya awali kwa sababu mara mahakama hii ilipotoa amri ya kuwakamata Mei 27 mwaka huu, washtakiwa hao walifika mahakamani hapa kujisalimisha wenyewe na wengine, akiwamo Mbunge Joseph Selasini, alituma mdhamini wake, hivyo nawaachia dhamana zao,” alisema Magesa.

Kesi hiyo ilifunguliwa na Serikali, Januari 5 mwaka huu ambapo washtakiwa 19 walifikishwa mahakamani hapo na kusomewa shtaka la kufanya kusanyiko pasipo na kibali na kutoa maneno ya uchochezi. Washtakiwa walikana makosa yao na kwa sasa wako nje kwa dhamana hadi Juni 24 mwaka huu kesi hiyo itakapotajwa tena.

Akizungumza na Mwananchi jana jioni, Mbowe alisema anatarajia kutoa tamko kuhusu suala hilo leo saa tano asubuhi jijini Dar es Salaam, lakini alikataa kutaja ni wapi mkutano wake na waandishi wa habari utafanyika.

“Nitatoa tamko kesho, lakini nasikitishwa na tafsiri hii ya Mahakama kwamba mimi nimekaidi amri ya kufika katika vikao vya mahakama. Nasema hivyo kwa sababu mara ya mwisho tulipokuwa mahakamani, tulipewa ruhusa ya kuhudhuria vikao vya Kamati za Bunge,” alisema Mbowe na kuongeza:
“Sasa sijui tafsiri yake ni nini, lakini niseme tu kwamba haya yote kuhusu sakata la Arusha na amri za polisi kuwakamata wabunge wa opposition (upinzani) nitalizungumza kesho (leo) kwa vyombo vya habari”.

Kwa mujibu wa Mbowe, waliomba ruhusa ili kuwawezesha kushiriki vikao vya Kamati za Bunge kutokana na umuhimu wa masuala ya bajeti kwa umma ambayo pia yanawagusa mahakimu na Idara ya Mahakama kwa jumla.

“…hebu kama mnakumbuka, katika Bunge lililopita tulijadili ule muswada wa sheria unaogusa idara ya mahakama sisi wabunge wa upinzani tulitumia nguvu kubwa kuwatetea mahakimu katika mambo mengi. Sasa katika suala hili la bajeti si vizuri tukikosekana kwenye vikao na ndiyo maana tuliomba ruhusa siku ile na tukaruhusiwa, ”alisema Mbowe.

Friday, May 27, 2011

CUF yamtaka Nahodha ajiuzuru

*Ni kutokana na mauaji ya wananchi  watano Tarime 
*Yalaani, yasema huo ni ukiukwaji wa haki za binadamu


BARAZA Kuu la Chama cha Wananchi (CUF) limemtaka Waziri wa Mambo ya Ndani kuwajibika kutokana na mauaji yaliyotokea wilayani Tarime lakini pia kufanyika kwa uchunguzi wa kina juu ya tukio hilo.

Hatua hiyo ilifikiwa Dar es Salaam jana na Mwenyekiti wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mapendekezo mbalimbali yaliyoazimiwa na kikao cha baraza hilo.

Alisema kuwa baraza hilo linalaani vitendo vya ukiukaji na uvunjaji wa haki za binadamu hususan mauaji ya raia yanayofanywa na Jeshi la Polisi ambayo yamekuwa yakiripotiwa kila mara.

"Inatuumiza sana kwa kuwa inaonekana jambo hili ni la kawaida kwa sababu watendaji wake hawachukuliwi hatua yoyote," alisema.

Prof. Lipumba alisema kuwa baraza hilo pia linamtaka Rais Jakaya Kikwete kutambua kuwa jukumu la kuleta maendeleo ya Watanzania ni la watu wote hivyo serikali yake isisite kutumia sera mbadala za CUF kwa maendeleo ya taifa.

Alisema serikali kupitia wizara ya Fedha na Uchumi na Wizara ya Nishati na Madini inatakiwa kuchukua hatua za kuhakikisha nchi na wananchi wake wananufaika na rasilimali za madini zilizopo hapa nchini hususani madini ya dhahabu ambayo bei yake katika soko la dunia imepanda.

"Dhahabu inayouzwa nje ni dola bilioni 1.5 kwa mwaka sawa na  asilimia 40  ya bidhaa za Tanzania zinazouzwa nje ya nchi," alisema.

Alisisitiza kuwa baraza hilo linataka kuona utajiri wa nchi unawanufaisha wananchi na kuisaidia nchi kujikomboa kutoka katika dimbwi la umasikini na kuacha kutegemea misaada kutoka nje ambayo imeifanya nchi kuwa tegemezi kwa miaka mingi.

Aliongeza kuwa baraza hilo linamtaka Waziri wa Nishati na Madini Bw.William Ngeleja kujiuzulu kwa kuwa ameshindwa kutumia vyanzo vya umeme vilivyopo nchini ili kukabiliana na tatizo sugu la nishati linaloikumba nchi yetu kwa sasa.

Alisema nchi imejaliwa vyanzo vingi ya umeme na maeneo mengi ya maporomoko ya maji, makaa ya mawe, madini na hata umeme wa jua ambao hauna gharama kubwa ya kufua.

"Ni miaka 50 tangu tupate uhuru hatuna sababu yoyote  ya kutokuwa na umeme wa uhakika, ni ufisadi tu ambao umekithiri katika serikali yetu," alisema.

Alisisitiza kuwa serikali ni lazima itambue kuwa hali ya kutokuwa na umeme wa uhakika imezorotesha uzalishaji viwanda,biashara,huduma katika hospitali na shule hivyo kusababisha uchumi wa nchi kuzorota.

Aliitaka serikali kuzingatia mapendekezo na hoja zinazotolewa na kamati ya Nishati na Madini ya Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania zinazolenga kupata ufumbuzi wa matatizo ya umeme.

Pia alisema baraza hilo linaitaka serikali kuwa makini katika suala zima la utunzaji na uhifadhi wa silaha nzito za kivita zenye madhara makubwa na kutaka zihifadhiwe mbali na makazi ya watu ili matukio ya milipuko ya mabomu ambayo yameshatokea mara mbili yasijirudie tena.  

Thursday, May 26, 2011

Lissu na wenzake marufuku Nyamongo

Maiti wazikwa, wananchi wataka kurejesha majeneza polisi



 
















MBUNGE wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu, ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Katiba na Sheria, na wenzake saba ambao juzi walifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Tarime na kusomewa mashtaka matatu ya kuingia eneo la hospitali bila kibali, kufanya mkutano na kuzuia watu kufanya kazi, wamepata dhamana lakini wamezuiwa kutembelea maeneo ya Nyamongo hadi kesi inayowakabili itakapokwisha.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya wilaya hiyo, Yusto Roboroga alitoa uamuzi huo akisema ni kwa mujibu wa kifungu cha Sheria Namba 148 cha Makosa ya Jinai, kilichofanyiwa marekebisho mwaka 2002, ambacho kinatoa haki kwa watuhumiwa kupata dhamana. Alitoa uamuzi huo baada ya kupitia pingamizi lililowekwa na upande wa mashtaka kutaka wasipewe dhamana. Hata hivyo, alisema: “Washtakiwa wanazuiwa kutembelea maeneo ya Nyamongo mpaka kesi hiyo itakapokuwa imekwisha."

Hakimu huyo alisema kwa kuwa washtakiwa hao ni viongozi wakubwa wa chama walizuiwa ili kupunguza shinikizo la wanachama kutokana na tukio lililojitokeza, lakini kwa kuwa mazishi yameshafanyika, alisema wanaweza kudhaminiwa kama watakidhi masharti.

Hakimu Ruboroga alitaja masharti  ya dhamana hiyo kuwa ni kusaini mkataba wa dhamana wa Sh5 milioni kwa wadhamini wawili wanaoaminika.

Kwa wasio wakazi wa Tarime, alisema watatakiwa kupeleka mahakamani hati za mali isiyohamishika. Washtakiwa wote walikidhi masharti na kuachiwa kwa dhamana hadi Juni 26, mwaka huu kesi hiyo itakapotajwa tena.

Juzi, Lissu na wenzake, Waitara Mwita Mwikwabe, Stanslaus Nyembea, Anderson Deogratias Chacha, Andrew Andalu Nyandu, Mwita Marwa Maswi, Bashiri Abdalllah Selemani na Ibrahimu Juma Kimu walifikishwa mbele ya mahakama hiyo na kusomewa mashtaka hayo matatu na Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Casmir Kiria ambaye alisema, waliyatenda Mei 23, majira ya saa nne usiku. Wote walikana mashtaka hayo.

Wakati huo huo maiti wote waliokuwa wametelekezwa barabarani wamezikwa na ndugu zao huku baadhi ya familia zikikataa kuwazika kwa majeneza ya polisi na kutumia yale yaliyokuwa yameandaliwa huku wengine wakipanga kuyarudisha kwa Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Tarime, Constantine Massawe.

Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Kewanja, Om’tima Tanzania alisema kuwa mmoja wa marehemu hao, Chacha Ngoka alizikwa na jamii. Hata hivyo, alisema polisi waliweka mwili wake ndani ya jeneza bila kuweka sanda hali ambayo iliwalazimu kumweka ndani ya jeneza lao na kumvika sanda. Hilo lilifanyika pia katika eneo la Nyakunguru alikozikwa marehemu Emmanuel Magige.

Katika Kijiji cha Bonchugu, Serengeti, Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji hicho, Mwikwabe Makena alidai kwamba walilazimika kuzika mwili wa marehemu Chawali Bhoke uliotelekezwa na polisi.


Alidai kwamba kabla ya kuutelekeza, walifyatua mabomu ya machozi na risasi hewani baada ya wananchi waliokuwa wamebeba pinde, mishale, mikuki na mapanga kujaribu kuzuia gari la polisi. Alisema walilazimika kuzika bila kuwapo kwa ndugu wa marehemu waliokuwa wameachwa Tarime.Hata hivyo, Kamanda Massawe na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Robert Boaz hakuwa tayari kuzungumzia madai hayo.

Wednesday, May 25, 2011

Polisi 'wapora' maiti mochwari

*Tundu Lisu akamatwa, afikishwa kortini Tarime

JESHI la Polisi limewakamata na kuwafikisha mahakamani Mbunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) pamoja na maofisa wengine wa chama hicho baada ya kudaiwa kufanya mkusanyiko usio halali na kuzuia watu kuzika ndugu zao.

Sambamba na hatua hiyo jeshi hilo limedaiwa kuingia mochwari ya Hospitali ya Wilaya ya Tarime na kuchukua kwa nguvu maiti nne za watu waliouawa na polisi hivi karibuni na kwenda kuzitelekeza maeneo mbalimbali ili kuzuia mkusanyiko wa kuaga maiti hizo kwa pamoja, kwa kile wanachoeleza ni kuzuia uvunjifu wa amani.

Bw. Lisu na wenzake wanadaiwa kukutwa katika Hosptali ya Wilaya ya mjini hapo wakilinda miili hiyo baada ya kusikia tetesi kuwa polisi walikuwa na mpango wa kuichukua na kuisafirisha kusikojulikana.

Akizungumza na waandishi wa habari nje ya mahakama, Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Bw. Casmil Kria alisema watuhumiwa wanakabiliwa na mashtaka matatu, yaliyosomwa mbele ya Hakimu wa Wilaya, Bw. Yusto Ruboroga.

Mashtaka hayo ni kuingia eneo la hospitali bila kibali, kufanya mkusanyiko usio halali na kuzuia watu kuchukua miili ya ndugu zao.

Watuhumiwa hao ambao wanadaiwa kukutwa eneo hilo saa 4:00 usiku baada ya kusomewa mashtaka na kuyakana, walirudishwa rumande kwa 'sababu za kiusalama', na kesho watafikishwa tena mahakamani kwa ajili ya kupewa dhamana, endapo miili ya waliouawa itakuwa imeshazikwa.

Walioshtakiwa ni Mbunge wa Singida Magharibi, Bw. Tundu Lissu (43), Bw. Mwita Mwikwabe (36), Bw. Stancelaus Nyembea (33), Anderson Deogratias (35), Bw. Andrew Andaru (63), Bw. Mwita Marwa (48) Bw. Bashiri Abdallah Seremani (35) pamoja na Ibrahimu Juma Kimi (27) ambaye ni dereva wa Bw. Lissu.

Wakati huo huo, waandishi wanne wa habari pamoja na Mbunge Viti Maalumu, Bi. Ester Matiko (CHADEMA) nao walishikiliwa na Jeshi la Polisi katika Kituo Kidogo cha Nyamwaga na baadaye kuachiwa huru baada ya mahojiano.

Wandishi hao ni Bi. Beldina Nyakeke wa The Citizen, Anna Mroso (Nipashe), Bw. Anthony Mayunga (Mwananchi) pamoja na Mabere Makubi wa Chanel Ten ambao walikuwa kwenye msafara wa Bi. Matiko.

Waandishi wengine wa habari waliofika katika mahakama ya wilaya kufuatilia tukio hilo walizuiliwa kuingia na kutishiwa kupigwa
risasi na ofisa mmoja wa polisi.

Ofisa huyo ambaye hakufahamika jina aliwatimua waandishi hao, huku akiomba bunduki kutoka kwa askari mwenzake na kuiandaa mithili ya kupambana na adui.

“Toka! Toka! Naombeni bunduki yangu hapa naona nyinyi hamjui kufanya kazi, hatukuja kufanya mchezo hapa waondoe na wale watu upesi mahali hapa wasongee mbali huko hatutaki mtu hapa!” alisema.

Askari hao wakiwa wameziba njia huku ofisa huyo akiendelea kuelekeza bunduki yake kwa raia waliokuwa eneo hilo.

Friday, May 20, 2011

OCD mbaroni kwa kumpiga risasi makalioni mhadhiri wa SUA



MKUU wa Polisi wa Wilaya ya Kibondo mkoani Kigoma, Onesmo Lianga ameshikiliwa na polisi mkoani Morogoro kwa muda na baadaye kuachiwa kwa
tuhuma za kumpiga risasi sehemu ya makalio mwalimu wa kikundi cha sanaa cha Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Dadie Kitururu (42).

Ndugu wa karibu na marafiki wa Bw. Kitururu alipigwa risasi Mei 11, mwaka huu majira ya jioni katika eneo la Forest wakati akiwa njiani kurejea nyumbani kwake, huku wakishangaa kwa nini polisi amtwange mtuhumiwa risasi badala ya kumtia mbaroni.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Bi. Adolphina Chialo alithibitisha kutokea kwa tukio hilo, akisema kuwa siku ya tukio majira ya jioni Bw. Kitururu akiendesha gari alimgonga mpanda baiskeli Salumu Chiga (58), mfanyakazi wa Hospitali ya Mkoa wa Morogoro mkazi wa Kichangani karibu na ofisi za Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) Kilakala na kukimbia.

Alisema kuwa OCD huyo ambaye alikuwa nyuma ya Bw. Kitururu aliyekuwa akiendesha gari lenye namba za usajili T 320 ANQ Suzuki Samurai, naye akiwa na gari lenye namba T 630 BFZ aina ya Rav 4 alimkimbiza Kitururu hadi eneo hilo la Forest.

Kwa mujibu wa RPC, baada ya OCD kuona Kitururu anakimbia zaidi, alifyatua risasi kwa bastola yenye namba PA06897 aina ya Chinese na kupasua taili la mbele na risasi ikapenya hadi kumfikia Kitururu kwenye makalio.

Kamanda Chialo alisema, baada ya tukio hilo OCD alimkamata mtuhumiwa huyo na kumfikisha katika Kituo Kikuu cha Polisi mkoani Morogoro na kuwekwa rumande na baadaye polisi waligundua kuwa mtuhumiwa huyo alikuwa na majeraha baada ya kuona akivuja damu, ndipo alipopelekwa hospitali kwa uchunguzi zaidi.

"Baada ya kufikishwa Hospitali ya Mkoa wa Morogoro mtuhumiwa huyo alilazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi kutokana na hali yake kuwa mbaya na aligundulika kuwa na kipande cha risasi katika makalio na hivyo kupatiwa matibabu," alisema.

Baada ya kugundua hivyo, ndipo polisi walipoamua kumshikilia OCD huyo kwa kwa mahojiano juu ya tukio hilo na kubaini kuwa alipiga tairi risasi likapenya na kumfikia Kitururu.

Wednesday, May 18, 2011

Polisi waua watano


POLISI wameua watu watano na kujeruhi wengine kadhaa katika mgodi wa dhahabu wa North Mara unaomilikiwa na kampuni ya African Barrick Gold, Tarime mkoani Mara.

Habari zilizopatikana kutoka eneo la tukio na kuthibitishwa na Jeshi la Polisi zilisema tukio hilo lilitokea jana alfajiri katika eneo la Nyabirama.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Tarime/Rorya, Constantine Massawe, alisema askari walilazimika kutumia risasi za moto baada ya kutumia mabomu ya machozi bila mafanikio kutawanya kundi la watu waliojaribu kuingia kwa jinai na kupora mawe yenye dhahabu mgodini.

“Askari walilazimika kutumia risasi kukabiliana na watu wanaokadiriwa kuwa kati ya 800 na 1,000 waliokuwa wamevamia mgodi huo ili kuokota mawe yenye dhahabu,” alisema.

Kwa mujibu wa Kamanda Massawe, watu watatu walikufa katika eneo la tukio na wengine wawili walifia katika Hospitali ya Wilaya ya Tarime. Majina yao hayakufahamika mara moja.

Hata hivyo, Kamanda huyo alitaja baadhi ya majina ya majeruhi waliolazwa hospitalini hapo kuwa ni Francis Emmanuel (20) mkazi wa kijiji cha Kewanja, Chacha Mwasi (23) mkazi wa kijiji cha Bisarwi wilayani Tarime na Mwikwabe Marwa (30) mkazi wa Mugumu wilayani Serengeti.

Alidai kwamba polisi wawili waliofika eneo la tukio walijeruhiwa kwa mawe yaliyokuwa yakirushwa kwa kombeo.

Akizungumzia tukio hilo kwa simu kutoka Dar es Salaam, Mbunge wa Tarime, Nyambari Nyangwine (CCM), alilaani mauaji hayo na kuahidi kuchukua hatua.

Alilaani matumizi ya nguvu kubwa yaliyofanywa na polisi kukabiliana na wananchi waliojaribu kuvamia mgodi.
“Ninalaani sana kitendo cha askari kutumia nguvu kubwa ya kuua na kujeruhi wananchi kwa tuhuma za kuvamia mgodi. Nitachukua hatua kali dhidi ya wote waliohusika katika tukio hilo la kusikitisha,” alisema Nyangwine bila kutaja aina hiyo ya nguvu alizoahidi.

Kamanda Massawe alisema ofisi yake inakusudia kuitisha mkutano maalumu wa viongozi wa mgodi wa dhahabu wa North Mara na wakazi wa vijiji vilivyo jirani kutafuta ufumbuzi thabiti wa matukio ya uvamizi na mauaji ambayo yamekuwa yakitokea mgodi hapo.

Alitoa wito kwa wananchi kuepuka vitendo vya uvamizi na uporaji mali katika mgodi huo kwa vile unamilikiwa kihalali na kampuni ya African Barrick Gold.

Wimbi la matukio ya uvamizi, uporaji mawe yenye dhahabu na mauaji ya watu katika mgodi wa dhahabu wa North Mara limeendelea kuwepo, huku baadhi ya askari, walinzi na wafanyakazi wa mgodi huo wakituhumiwa kupokea rushwa ya fedha na kuruhusu watu kuingia kuokota mawe yenye dhahabu.