Showing posts with label maiti. Show all posts
Showing posts with label maiti. Show all posts

Monday, August 1, 2011

Kisa na mkasa na Salim Kikeke

Kutuma ujumbe wa simu kosa...

Jimbo moja nchini Marekani limepiga marufuku watu kutuma ujumbe wa simu huku wakiwa wanatembea barabarani. Mtu atakayekutwa akituma ujumbe mfupi wa maandishi, yaani text messege, huku akiwa anatembea, atapigwa faini ya dola mia moja na ishirini. Taarifa zinasema Jimbo la Pennsylvania limechukua hatua hiyo kukabiliana na tatizo linaloongezeka la watu kutembea huku wakiwa wanatazama simu zao badala ya kutazama wanapokwenda.

Jiji la Philadelphia limesema linataka kupambana pia na madereva wa magari, waendesha baiskeli na watembea kwa miguu ambao muda mwingi huutumia wakituma ujumbe wakiwa barabarani.

Mji wa Rexburg, uliopo Idaho, huwatoza faini ya dola hamsini watu wanaokutwa wakivuka barabara huku wakiwa wanatuma ujumbe wa simu. Hata hivyo naibu meya wa mji huo ametoa taarifa akikanusha madai ya utozaji faini, ingawa ameonya watu kuepuka kutuma text huku wakiwa wanatembea.

Taarifa hizi zimekuja kufuatia msichana mmoja aliyekuwa akituma ujumbe huku akiwa anatembea na kujikuta amedumbukia ndani ya mtaro wa pembezoni mwa barabara. Kutuma ujumbe sio kosa, lakini ni hatari, amesema naibu meya.

Jini au?

Bwana mmoja nchini Afrika Kusini aliyedhaniwa kuwa amekufa, aliamka baada ya kupigwa na baridi kali katika chumba cha kuhifadhia maiti. Bwana huyo mwenye umri wa miaka hamsini alianza kupiga kelele za kuomba msaada. Wafanyakazi wawili wa chumba cha maiti waliposikia kelele hizo walikimbia, wakidhani ni jini, vimeripoti vyombo vya habari vya Afrika Kusini.

"Ndugu zake walidhani amekufa wakampeleka mochuari" amesema Sizwe Kupelo ambaye ni afisa wa wizara ya afya, akizungumza na shirika la habari la Afrika Kusini, Sapa. Shirika la habari la Reuters limesema familia ya bwana huyo katika mji wa Libode, katika jimbo la Eastern Cape iliamua kumpeleka mochuari, baada ya kudhani amekufa.

Baada ya bwana huyo kuendelea kupiga kelele za kuomba msaada, wafanyakazi wawili waliamua kurejea ili kuhakikisha sio jini na kumkuta bwana huyo akiwa hai na mara moja kuita gari la kubebea wagonjwa.
Msemaji wa wizara ya afya amesema mtu huyo alikuwa amekaa kwenye chumba cha baridi kwa karibu saa ishirini na nne.

Afisa huyo amesema watu wasikimbilie kupeleka wagonjwa wao mochuari wakidhani wamekufa.
Amesema madaktari na polisi ndio watu pekee wenye uwezo wa kufanya vipimo na kufahamu kama watu wamekufa au la.

Kuendesha gari bila gurudumu

Dereva mmoja wa basi nchini Uchina aliendesha basi lake kwa umbali mrefu bila kujua kama matairi yote ya nyuma yamechomoka. Kutokana na msongamano wa magari katika jiji la Shaoyang, dereva huyo Shi Shao hata hakuhisi kama gari linaburura kwa sababu ya mwendo mdogo wa foleni.

Gazeti la Metro limesema ingawa alikuwa akisikia mlio usio wa kawaidia, alidhani ni mlio wa kifaa kiitwacho suspension, kimeharibika labda kutokana na mashimo ya barabarani. Hata hivyo, baada ya mlio huo kuendelea, abiria walianza kupatwa na mashaka na wao, na hivyo kutazama tatizo ni nini. Hatimaye abiria waligundua kuwa basi wanalosafiria halina matairi yote ya nyuma, na haraka walimtaarifu dereva. Dereva Shi alisimamisha basi hilo katikati ya barabara ili kusubiri kuvutwa na gari jingine, na hivyo kusababisha msongamano mwingine upya.

Polisi walipowasili hawakuamini macho yao kuona basi limesafiri umbali mrefu bila ya kuwa na matairi ya nyuma.

Yu wapi eh...bwana harusi?

Harusi moja nchini Indonesia ilisimamishwa ghafla bin vuu baada ya kugundulika kuwa bwana harusi ni mwanamke. Wageni waalikwa na wanafamilia walikuwa wamekusanyika katika sherehe ya harusi ya Kiislam, katika eneo la magharibi la Java.

Hata hivyo hali ya wasiwasi ilianza kutanda pale bwana harusi alipowasili peke yake bila ya ndugu na jamaa waliomsindikiza. Pia bwana harusi huyo hakuwa na kitambulisho chochote, zimesema taarifa kutoka Indonesia.

Wasiwasi na mashaka yalizidi pale bwana harusi alipoanza kuzungumza. Sauti iliyokuwa kama ya kiume mara ikaanza kugeuka na kuwa ya kike. "Sauti nzito ghafla ikawa ya kike" amesema mkuu wa polisi wa eneo la Krisnandi. Polisi na wageni waligundua hatimaye kuwa bwana harusi, alikuwa ni mwanamke na hivyo harusi hiyo kusitishwa kwa muda.

Wazazi wa Bi harusi mara moja walimtafuta rafiki wa zamani wa kiume wa bi harusi - yaani ex boyfriend - na kumshawishi amuoe binti yao ili kuokoa jahazi.

Ushoga nchini Indonesia haujapigwa marufuku, lakini ndoa za jinsia moja bado hazijaruhusiwa katika nchi hiyo yenye idadi kubwa ya Waisilam.

Na kwa taarifa yako.... Wanawake hutabasamu zaidi ya wanaume

Thursday, May 26, 2011

Lissu na wenzake marufuku Nyamongo

Maiti wazikwa, wananchi wataka kurejesha majeneza polisi



 
















MBUNGE wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu, ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Katiba na Sheria, na wenzake saba ambao juzi walifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Tarime na kusomewa mashtaka matatu ya kuingia eneo la hospitali bila kibali, kufanya mkutano na kuzuia watu kufanya kazi, wamepata dhamana lakini wamezuiwa kutembelea maeneo ya Nyamongo hadi kesi inayowakabili itakapokwisha.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya wilaya hiyo, Yusto Roboroga alitoa uamuzi huo akisema ni kwa mujibu wa kifungu cha Sheria Namba 148 cha Makosa ya Jinai, kilichofanyiwa marekebisho mwaka 2002, ambacho kinatoa haki kwa watuhumiwa kupata dhamana. Alitoa uamuzi huo baada ya kupitia pingamizi lililowekwa na upande wa mashtaka kutaka wasipewe dhamana. Hata hivyo, alisema: “Washtakiwa wanazuiwa kutembelea maeneo ya Nyamongo mpaka kesi hiyo itakapokuwa imekwisha."

Hakimu huyo alisema kwa kuwa washtakiwa hao ni viongozi wakubwa wa chama walizuiwa ili kupunguza shinikizo la wanachama kutokana na tukio lililojitokeza, lakini kwa kuwa mazishi yameshafanyika, alisema wanaweza kudhaminiwa kama watakidhi masharti.

Hakimu Ruboroga alitaja masharti  ya dhamana hiyo kuwa ni kusaini mkataba wa dhamana wa Sh5 milioni kwa wadhamini wawili wanaoaminika.

Kwa wasio wakazi wa Tarime, alisema watatakiwa kupeleka mahakamani hati za mali isiyohamishika. Washtakiwa wote walikidhi masharti na kuachiwa kwa dhamana hadi Juni 26, mwaka huu kesi hiyo itakapotajwa tena.

Juzi, Lissu na wenzake, Waitara Mwita Mwikwabe, Stanslaus Nyembea, Anderson Deogratias Chacha, Andrew Andalu Nyandu, Mwita Marwa Maswi, Bashiri Abdalllah Selemani na Ibrahimu Juma Kimu walifikishwa mbele ya mahakama hiyo na kusomewa mashtaka hayo matatu na Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Casmir Kiria ambaye alisema, waliyatenda Mei 23, majira ya saa nne usiku. Wote walikana mashtaka hayo.

Wakati huo huo maiti wote waliokuwa wametelekezwa barabarani wamezikwa na ndugu zao huku baadhi ya familia zikikataa kuwazika kwa majeneza ya polisi na kutumia yale yaliyokuwa yameandaliwa huku wengine wakipanga kuyarudisha kwa Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Tarime, Constantine Massawe.

Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Kewanja, Om’tima Tanzania alisema kuwa mmoja wa marehemu hao, Chacha Ngoka alizikwa na jamii. Hata hivyo, alisema polisi waliweka mwili wake ndani ya jeneza bila kuweka sanda hali ambayo iliwalazimu kumweka ndani ya jeneza lao na kumvika sanda. Hilo lilifanyika pia katika eneo la Nyakunguru alikozikwa marehemu Emmanuel Magige.

Katika Kijiji cha Bonchugu, Serengeti, Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji hicho, Mwikwabe Makena alidai kwamba walilazimika kuzika mwili wa marehemu Chawali Bhoke uliotelekezwa na polisi.


Alidai kwamba kabla ya kuutelekeza, walifyatua mabomu ya machozi na risasi hewani baada ya wananchi waliokuwa wamebeba pinde, mishale, mikuki na mapanga kujaribu kuzuia gari la polisi. Alisema walilazimika kuzika bila kuwapo kwa ndugu wa marehemu waliokuwa wameachwa Tarime.Hata hivyo, Kamanda Massawe na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Robert Boaz hakuwa tayari kuzungumzia madai hayo.

Wednesday, May 25, 2011

Polisi 'wapora' maiti mochwari

*Tundu Lisu akamatwa, afikishwa kortini Tarime

JESHI la Polisi limewakamata na kuwafikisha mahakamani Mbunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) pamoja na maofisa wengine wa chama hicho baada ya kudaiwa kufanya mkusanyiko usio halali na kuzuia watu kuzika ndugu zao.

Sambamba na hatua hiyo jeshi hilo limedaiwa kuingia mochwari ya Hospitali ya Wilaya ya Tarime na kuchukua kwa nguvu maiti nne za watu waliouawa na polisi hivi karibuni na kwenda kuzitelekeza maeneo mbalimbali ili kuzuia mkusanyiko wa kuaga maiti hizo kwa pamoja, kwa kile wanachoeleza ni kuzuia uvunjifu wa amani.

Bw. Lisu na wenzake wanadaiwa kukutwa katika Hosptali ya Wilaya ya mjini hapo wakilinda miili hiyo baada ya kusikia tetesi kuwa polisi walikuwa na mpango wa kuichukua na kuisafirisha kusikojulikana.

Akizungumza na waandishi wa habari nje ya mahakama, Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Bw. Casmil Kria alisema watuhumiwa wanakabiliwa na mashtaka matatu, yaliyosomwa mbele ya Hakimu wa Wilaya, Bw. Yusto Ruboroga.

Mashtaka hayo ni kuingia eneo la hospitali bila kibali, kufanya mkusanyiko usio halali na kuzuia watu kuchukua miili ya ndugu zao.

Watuhumiwa hao ambao wanadaiwa kukutwa eneo hilo saa 4:00 usiku baada ya kusomewa mashtaka na kuyakana, walirudishwa rumande kwa 'sababu za kiusalama', na kesho watafikishwa tena mahakamani kwa ajili ya kupewa dhamana, endapo miili ya waliouawa itakuwa imeshazikwa.

Walioshtakiwa ni Mbunge wa Singida Magharibi, Bw. Tundu Lissu (43), Bw. Mwita Mwikwabe (36), Bw. Stancelaus Nyembea (33), Anderson Deogratias (35), Bw. Andrew Andaru (63), Bw. Mwita Marwa (48) Bw. Bashiri Abdallah Seremani (35) pamoja na Ibrahimu Juma Kimi (27) ambaye ni dereva wa Bw. Lissu.

Wakati huo huo, waandishi wanne wa habari pamoja na Mbunge Viti Maalumu, Bi. Ester Matiko (CHADEMA) nao walishikiliwa na Jeshi la Polisi katika Kituo Kidogo cha Nyamwaga na baadaye kuachiwa huru baada ya mahojiano.

Wandishi hao ni Bi. Beldina Nyakeke wa The Citizen, Anna Mroso (Nipashe), Bw. Anthony Mayunga (Mwananchi) pamoja na Mabere Makubi wa Chanel Ten ambao walikuwa kwenye msafara wa Bi. Matiko.

Waandishi wengine wa habari waliofika katika mahakama ya wilaya kufuatilia tukio hilo walizuiliwa kuingia na kutishiwa kupigwa
risasi na ofisa mmoja wa polisi.

Ofisa huyo ambaye hakufahamika jina aliwatimua waandishi hao, huku akiomba bunduki kutoka kwa askari mwenzake na kuiandaa mithili ya kupambana na adui.

“Toka! Toka! Naombeni bunduki yangu hapa naona nyinyi hamjui kufanya kazi, hatukuja kufanya mchezo hapa waondoe na wale watu upesi mahali hapa wasongee mbali huko hatutaki mtu hapa!” alisema.

Askari hao wakiwa wameziba njia huku ofisa huyo akiendelea kuelekeza bunduki yake kwa raia waliokuwa eneo hilo.