Showing posts with label lukuvi. Show all posts
Showing posts with label lukuvi. Show all posts

Wednesday, August 24, 2011

Wabunge- Bunge limedhalilishwa, Pinda kafedheheshwa

BUNGE limesema, Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo amelidhalilisha na pia amemdhalilisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwa kumuamuru Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo arudi kazini.

Wabunge wamesema, taarifa ya uchunguzi ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusu tuhuma kwamba, Jairo alichangisha shilingi bilioni moja ili kuwezesha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini ipitishwe bungeni ilistahili kupelekwa bungeni waijadili kabla Serikali kutoa uamuzi.

Wabunge leo wamejadili kauli ya Luhanjo kama jambo la dharura baada ya wabunge kukubali hoja ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto aliyoitoa asubuhi kabla ya kipindi maswali na majibu na kuifafanua baada ya Kamati ya Bunge ya Uongozi kukutana katika ukumbi wa Spika.

Spika wa Bunge, Anne Makinda aliongoza kikao hicho cha dharura wakati wa kipindi cha maswali na majibu.

Kabla ya kamati hiyo kukutana, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisema, kwa kutumia kifungu cha 51 cha Kanuni za Bunge alichotumia Zitto kuwasilisha hoja yake, inamtaka Mbunge aiwasilishe mapema kwa Spika wa Bunge ili atoe uamuzi.

Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai, alimjibu Lukuvi kwamba, kabla ya kuanza kwa kikao cha leo, Zitto alipeleka taarifa fupi kwa Spika wa Bunge kuhusu hoja hiyo kwa hiyo utaratibu umefuatwa.

“Hoja hii nzito kweli…na ndiyo hoja iliyoungwa mkono” amesema Ndugai baada ya Zitto kuiwasilisha kwa mara ya kwanza kabla ya.

Zaidi ya robo tatu ya wabunge waliokuwa ukumbini wakiwemo kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) wameunga mkono hoja ya Zitto. Ndugai, amesema bungeni kuwa, hoja ya Zitto ni ya msingi kwa kuwa Bunge limedharauliwa.

“Kwa sababu Bunge ni mhimili, hatuwezi kudharauliwa kirahisi”amesema Ndugai na kusisitiza kwamba, Wabunge hawawezi kukaa kimya wakati Waziri Mkuu anadhalilishwa.

“Kama dharau inaweza ikatokea basi huko huko lakini sio ndani ya Bunge hili” amesema Ndugai baada ya wabunge kuijadili hoja ya Zitto na kusisitiza kwamba, kwa kuwa suala hilo lilianzia bungeni, taarifa ya CAG ingepelekwa kwanza kwenye mamlaka hiyo kabla ya uamuzi wa Serikali.

Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Zainab Vullu, wabunge wamepewa jukumu la kuisimamia na kuishauri Serikali kwa niaba ya wananchi hivyo kauli ya Luhanjo imewadhalilisha, na limepokwa mamlaka yake.

Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka, amesema, suala hilo lina maslahi kwa Taifa, taarifa ya CAG ingepelekwa kwanza bungeni itendewe haki.

Sendeka amesema bungeni kuwa, Waziri Mkuu amefedheheshwa kwa kuwa Kiongozi huyo wa Shughuli za Serikali Bungeni alisema, kama angekuwa yeye angemchukilia hatua Jairo, na pia Bunge limedhalilishwa.

Kwa mujibu wa Sendeka, kauli ya Luhanjo imelilidhalilisha Bunge na imekiuka Sheria ya Kinga na Madaraka ya Bunge na ibara ya 100 ya Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.

Mbunge huyo ametumia Kanuni 117 ya Bunge kuomba iundwe kamati teule ya Bunge kuchunguza jambo hilo ukiwemo utaratibu wa Jairo kukusanya fedha za kupitishia bajeti hasa ikizingatiwa kuwa, kila Waziri huwa na fungu la kugharamia bajeti kila idara zikiwemo fedha za kununulia mafuta.

Sendeka aliomba Bunge liunge mkono hoja yake ili kulinda hadhi ya Bunge, takribani wabunge wote walikubali isipokuwa mawaziri na manaibu mawaziri.

Wakati anatoa hoja hiyo, Zitto amesema, kwa kuwa jambo hilo lilianzia bungeni wakati Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo (CCM) alipolieleza Bunge kuwa ana barua ya Jairo kuzitaka idara katika Wizara za Nishati na Madini zichangie shilingi milioni 50 kila moja, wabunge walistahili kuijadili ripoti ya CAG kabla ya Serikali kufanya uamuzi.

Zitto amelieleza Bunge kuwa, kauli ya Luhanjo ni dharau kwa Waziri Mkuu, na imeingilia hadhi, kinga na madaraka ya Bunge kwa kuwa wabunge ndiyo wana mamlaka ya kuisimamia Serikali.

Zitto alipendekeza kwamba, shughuli na hoja zote za Serikali bungeni zisitishwe, kwanza wabunge waijadili taarifa za CAG kwa kuwa Bunge limepokwa nafasi yake.

Ndugai amewaeleza wabunge kuwa, Spika wa Bunge, Makinda, ataunda tume kuchunguza kudharauliwa kwa Bunge, na kukusanywa kwa fedha kwa ajili ya kupitishwa bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2011/2012.

Kwa mujibu wa kiongozi huyo wa Bunge, tume hiyo itapaswa kufanya kazi haraka ili taarifa yake ijadiliwe katika mkutano ujao wa Bunge.

Luhanjo jana alimuagiza Jairo arudi kazini leo aendelee na madaraka yake katika Wizara ya Nishati na Madini kwa kuwa tuhuma zilizotolewa dhidi yake hazikuthibitika.

Leo asubuhi, Jairo alikwenda ofisini kwake wizarani jijini Dar es Salaam, wafanyakazi wakampokea kwa shangwe na vigelegele huku wakiimba kwamba wana imani naye.

Thursday, July 28, 2011

Wabunge waghushi saini ya Pinda

BUNGE la Tanzania linakoelekea sasa si kuzuri. Pengine ndivyo inavyoweza kuzungumzwa kuhusu mambo yanavyokwenda ndani ya chombo hicho cha kutunga sheria na kuisimamia Serikali. Hali hiyo inatokana na tukio la juzi usiku baada ya wabunge au Mbunge asiyefahamika, kughushi saini ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, wakati kikao kikiendelea.

Aliyeweka wazi aibu hiyo ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi, muda mfupi baada ya Bunge kupitisha Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kwa Mwaka 2011/12 yaliyowasilishwa Jumatatu na Waziri Profesa Jumanne Maghembe, ambapo Sh. bilioni 258.3 ziliidhinishwa.

Baada ya Mwenyekiti wa Bunge, ambaye pia ni Mbunge wa Kibakwe, George Simbachawene (CCM) kuzungumzia kupitishwa kwa bajeti hiyo na kumpongeza Waziri na wabunge, huku akijiandaa kusitisha shughuli za Bunge ikiwa ni karibu saa 2:15 usiku, alisimama Waziri Lukuvi na kuomba Mwongozo wa Mwenyekiti.

Katika maelezo yake ya kuomba Mwongozo, Lukuvi alisema kumeibuka tabia ndani ya Bunge ambayo si ya kistarabu, kwani baadhi ya wabunge wamekuwa wakiandika ujumbe kwenye vikaratasi kuonesha mhusika fulani anaitwa wakati hakuna jambo kama hilo.

“Kwa leo (juzi) hapa yametokea matukio mawili ya wabunge Joseph Selasini (Rombo-Chadema) na Leticia Nyerere (Viti Maalumu-Chadema) kupelekewa ujumbe kwa nyakati tofauti ukionesha umesainiwa na Waziri Mkuu akiwaita.

“Lakini jambo la ajabu Waziri Mkuu mwenyewe hajui lolote na anashangaa jambo hili maana hakuandika ujumbe kuwaita,” alisema Waziri Lukuvi na kusababisha mshangao kwa baadhi ya wabunge.  Kutokana na mazingira hayo, aliomba suala hilo liachwe na kwamba si tabia nzuri ambayo imeanza kujitokeza.

Akizungumzia suala hilo, Simbachawene naye alilaani jambo hilo na kusema kwa vile karatasi iliyoandikwa alikuwa nayo, itakuwa rahisi kumbaini mhusika na kumshughulikia.

“Karatasi yenyewe imeandikwa hivi: Mheshimiwa Joseph Selasini, naomba uje kuna jambo tujadili, nahitaji ufafanuzi kutoka kwako - Mizengo Pinda,” alisema Simbachawene na kuongeza kuwa karatasi hiyo imesainiwa kuonesha aliyesaini ni Waziri Mkuu.

“Ndiyo maana nilimwona Mheshimiwa Selasini amekwenda kwa Waziri Mkuu akiwa amejikunyata kistaarabu kuona ameitiwa kitu gani, lakini Mheshimiwa Waziri Mkuu wala alikuwa hamfuatilii, alikuwa ameelekeza mawazo yake katika majibu ya Waziri,” alisema Mwenyekiti huyo.

Alieleza kuwa jambo hilo ni la aibu kubwa kwa wabunge, kufikia hatua ya kughushi saini ya Waziri Mkuu na kusisitiza lazima ichukuliwe uzito unaostahili.

Tangu Bunge la 10 lianze, kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wadau mbalimbali kwamba limepoteza heshima kutokana na baadhi ya wabunge kufanya mambo ambayo hayaendani na chombo hicho – ya kitoto.

Masuala ya kuzomeana, kupigana vijembe na wakati mwingine kuzungumza bila mpangilio, ni baadhi ya mambo yanayopigiwa kelele na wadau kwamba yanakivunjia heshima chombo hicho, ambacho ni moja ya mihimili mikuu mitatu ya Dola.