Showing posts with label zitto. Show all posts
Showing posts with label zitto. Show all posts

Wednesday, August 24, 2011

Wabunge- Bunge limedhalilishwa, Pinda kafedheheshwa

BUNGE limesema, Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo amelidhalilisha na pia amemdhalilisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwa kumuamuru Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo arudi kazini.

Wabunge wamesema, taarifa ya uchunguzi ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusu tuhuma kwamba, Jairo alichangisha shilingi bilioni moja ili kuwezesha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini ipitishwe bungeni ilistahili kupelekwa bungeni waijadili kabla Serikali kutoa uamuzi.

Wabunge leo wamejadili kauli ya Luhanjo kama jambo la dharura baada ya wabunge kukubali hoja ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto aliyoitoa asubuhi kabla ya kipindi maswali na majibu na kuifafanua baada ya Kamati ya Bunge ya Uongozi kukutana katika ukumbi wa Spika.

Spika wa Bunge, Anne Makinda aliongoza kikao hicho cha dharura wakati wa kipindi cha maswali na majibu.

Kabla ya kamati hiyo kukutana, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisema, kwa kutumia kifungu cha 51 cha Kanuni za Bunge alichotumia Zitto kuwasilisha hoja yake, inamtaka Mbunge aiwasilishe mapema kwa Spika wa Bunge ili atoe uamuzi.

Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai, alimjibu Lukuvi kwamba, kabla ya kuanza kwa kikao cha leo, Zitto alipeleka taarifa fupi kwa Spika wa Bunge kuhusu hoja hiyo kwa hiyo utaratibu umefuatwa.

“Hoja hii nzito kweli…na ndiyo hoja iliyoungwa mkono” amesema Ndugai baada ya Zitto kuiwasilisha kwa mara ya kwanza kabla ya.

Zaidi ya robo tatu ya wabunge waliokuwa ukumbini wakiwemo kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) wameunga mkono hoja ya Zitto. Ndugai, amesema bungeni kuwa, hoja ya Zitto ni ya msingi kwa kuwa Bunge limedharauliwa.

“Kwa sababu Bunge ni mhimili, hatuwezi kudharauliwa kirahisi”amesema Ndugai na kusisitiza kwamba, Wabunge hawawezi kukaa kimya wakati Waziri Mkuu anadhalilishwa.

“Kama dharau inaweza ikatokea basi huko huko lakini sio ndani ya Bunge hili” amesema Ndugai baada ya wabunge kuijadili hoja ya Zitto na kusisitiza kwamba, kwa kuwa suala hilo lilianzia bungeni, taarifa ya CAG ingepelekwa kwanza kwenye mamlaka hiyo kabla ya uamuzi wa Serikali.

Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Zainab Vullu, wabunge wamepewa jukumu la kuisimamia na kuishauri Serikali kwa niaba ya wananchi hivyo kauli ya Luhanjo imewadhalilisha, na limepokwa mamlaka yake.

Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka, amesema, suala hilo lina maslahi kwa Taifa, taarifa ya CAG ingepelekwa kwanza bungeni itendewe haki.

Sendeka amesema bungeni kuwa, Waziri Mkuu amefedheheshwa kwa kuwa Kiongozi huyo wa Shughuli za Serikali Bungeni alisema, kama angekuwa yeye angemchukilia hatua Jairo, na pia Bunge limedhalilishwa.

Kwa mujibu wa Sendeka, kauli ya Luhanjo imelilidhalilisha Bunge na imekiuka Sheria ya Kinga na Madaraka ya Bunge na ibara ya 100 ya Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.

Mbunge huyo ametumia Kanuni 117 ya Bunge kuomba iundwe kamati teule ya Bunge kuchunguza jambo hilo ukiwemo utaratibu wa Jairo kukusanya fedha za kupitishia bajeti hasa ikizingatiwa kuwa, kila Waziri huwa na fungu la kugharamia bajeti kila idara zikiwemo fedha za kununulia mafuta.

Sendeka aliomba Bunge liunge mkono hoja yake ili kulinda hadhi ya Bunge, takribani wabunge wote walikubali isipokuwa mawaziri na manaibu mawaziri.

Wakati anatoa hoja hiyo, Zitto amesema, kwa kuwa jambo hilo lilianzia bungeni wakati Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo (CCM) alipolieleza Bunge kuwa ana barua ya Jairo kuzitaka idara katika Wizara za Nishati na Madini zichangie shilingi milioni 50 kila moja, wabunge walistahili kuijadili ripoti ya CAG kabla ya Serikali kufanya uamuzi.

Zitto amelieleza Bunge kuwa, kauli ya Luhanjo ni dharau kwa Waziri Mkuu, na imeingilia hadhi, kinga na madaraka ya Bunge kwa kuwa wabunge ndiyo wana mamlaka ya kuisimamia Serikali.

Zitto alipendekeza kwamba, shughuli na hoja zote za Serikali bungeni zisitishwe, kwanza wabunge waijadili taarifa za CAG kwa kuwa Bunge limepokwa nafasi yake.

Ndugai amewaeleza wabunge kuwa, Spika wa Bunge, Makinda, ataunda tume kuchunguza kudharauliwa kwa Bunge, na kukusanywa kwa fedha kwa ajili ya kupitishwa bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2011/2012.

Kwa mujibu wa kiongozi huyo wa Bunge, tume hiyo itapaswa kufanya kazi haraka ili taarifa yake ijadiliwe katika mkutano ujao wa Bunge.

Luhanjo jana alimuagiza Jairo arudi kazini leo aendelee na madaraka yake katika Wizara ya Nishati na Madini kwa kuwa tuhuma zilizotolewa dhidi yake hazikuthibitika.

Leo asubuhi, Jairo alikwenda ofisini kwake wizarani jijini Dar es Salaam, wafanyakazi wakampokea kwa shangwe na vigelegele huku wakiimba kwamba wana imani naye.

Tuesday, August 9, 2011

Spika amtwisha Zitto Kabwe zigo la UDA



SAKATA la kuuzwa kwa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA) limezidi kugonganisha vichwa vya mamlaka mbalimbali, baada ya Spika wa Bunge, Anne Makinda kuhamisha mchakato wa uchunguzi huo kutoka Kamati ya Bunge ya Miundombinu kwenda Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC).Utata wa uuzaji wa shirika hilo umesababisha pia mvutano mkubwa kati ya wabunge wa Mkoa wa Dar es Salaam na Meya wa jiji hilo, Dk Didas Masaburi ambaye wiki iliyopita aliwashambulia wawakilishi hao kwa maneno makali huku akitoa vitisho kwamba atalipua tuhuma zao za ufisadi.

Makinda aliikabidhi jukumu hilo POAC Ijumaa ya Agosti 5, Spika na kuliondoa Kamati ya Miundombinu ambako Profesa Juma Kapuya ambaye ni mmoja wa wajumbem, ana maslahi na UDA kutokana na kuwa mmoja wa wanahisa wa Kampuni ya Simon Group.
 
Kaimu Katibu wa Bunge John Joel alithibitisha jana Spika amefanya mabadiliko hayo na kwamba tayari Mwenyekiti wa POAC, Zitto Kabwe amekwishapewa taarifa. "Ndiyo, kimsingi kamati inayopaswa kuchunguza ni Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma na tayari Spika ametoa uamuzi huo na maelekezo kwa kamati husika," alisema.

Tafsiri ya uamuzi wa Spika
Uamuzi huo wa Spika pia unaonekana kutengua ule wa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye wakati akitoa kauli ya Serikali kuhusu UDA alisema, ingeshirikiana na Kamati ya Serukamba (Peter, Mwenyekiti Kamati ya Miundombinu). Kiutendaji, jukumu la ubinafsishaji ni la POAC kama ilivyofafanuliwa katika nyongeza ya 8 ya kanuni za Bunge, ibara ya 13 (e).

Vyanzo vya habari vilifafanua kwamba kama uchunguzi huo ungeachwa chini ya Kamati ya Miundombinu kungeibuka mgongano wa kimaslahi kutokana na ubia wa Profesa Kapuya na Simon Group, iliyonunua shirika hilo.

"Uamuzi wa Spika kuhamisha jukumu hilo kutoka kamati ya miundombinu kwenda POAC umelenga kuondoa mgongano wa kimaslahi, kule kuna Kapuya ambaye ni mbia wa Simon Group kwa hiyo kitendo chochote cha uchunguzi kufanywa na miundombinu kingeathiri mchakato huo, " kilifafanua chanzo hicho.

Kauli ya Zitto Kabwe
Kwa upande wake Zitto akifafanua jukumu hilo zito alilotwisha alisema kimsingi kamati yake ndiyo yenye dhamana na ubinafsishaji na kuweka bayana kwamba ataunda kamati ndogo kutokana na uwiano wa vyama na Dar es Salaam kupewa mbunge mmoja.

Alifafanua kwamba, kutoka Dar es Salaam atapaswa kumchagua mbunge mmoja kuingia katika kamati hiyo ndogo huku pia kukiwa na wawakilishi kutoka CUF, NCCR-Mageuzi na CCM.

Alisema ataunda kamati kwa kuzingatia maeneo ya msingi ambayo wajumbe pia wataweza kutoka Katiba na Sheria kwani jambo hilo ni la kisheria, Kamati ya Miundombinu, Serikali za Mitaa kutokana na kugusa Halmashauri ya Jiji na wengine POAC.

Alisema tayari amepata taarifa kutoka Ofisi ya Bunge kuhusu agizo hilo lakini anasubiri taarifa rasmi zitakazomwelekeza namna mchakato huo unavyopaswa kufanywa hadi kukamilika.

"Nimeambiwa lakini sijapata barua rasmi, nasubiri taarifa rasmi kutoka Ofisi ya Spika. Lakini, kimsingi jukumu la ubinafsishaji liko chini ya kamati yangu ya mashirika ya umma," alisema Zitto, ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni.
 
Zitto alisema kama atapata taarifa rasmi hadi jana jioni, leo atatangaza kikosi kazi chake hicho ambacho kitafanya uchunguzi huo kwa undani kuona mchakato mzima ulivyo.


Mpango wa kuizima POAC
Vyanzo vya habari vilidokeza kwamba kumekuwa na juhudi za makusudi kuhakikisha suala hilo linabaki Kamati ya Miundombinu na kuzuia lisifike POAC, ili kulizima 'kiana'.

Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, baadhi ya wahusika wanataka kutumia mwavuli wa Kamati ya Miundombinu ambayo ina baadhi ya wajumbe wenye maslahi na Simon Group kuzima suala hilo huku pia wakitumia mwavuli wa uchunguzi uliotangazwa na Pinda.

Zitto alipoulizwa kuhusu mpango huo Zitto alisema hakuwa akiufahamu kwani mamlaka ya kuunda kamati na majukumu yake ni jukumu lililo chini ya Spika kwa mujibu wa Kanuni za Bunge.

Alisema hata kama Waziri Mkuu ametangaza uchunguzi, bado Bunge likiwa mhimili huru wa dola linapaswa kufanya uchunguzi wake. Alisema uchunguzi wa Serikali na vyombo vyake ni wake lakini Bunge nalo linapaswa kufanya uchunguzi wake huru kuhakikisha linapata kile ambacho linataka.

"Uchunguzi wa Serikali ni wa kwao serikalini lakini Bunge nalo uchunguzi wake ni wake. Kwa hiyo hata kama Serikali inachunguza bado Bunge nalo halifungwi kufanya uchunguzi wake, " alisema.

Utata wa uuzwaji wa shirika hilo uliibuka baada ya Dk Masaburi kufumua menejimenti ya shirika hilo. Suala hilo lilifika bungeni baada ya kuibuliwa wakati wa mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka 2011/12, ambayo wabunge wengi waliochangia walionekana kustushwa na uuzwaji wake.

Saturday, July 16, 2011

Lowassa aweka mambo hadharani

MBUNGE wa Monduli, Edward Lowassa, amesema atatangaza uamuzi kuhusu nyadhifa zake ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), wakati muafaka ukifika. Amesema ameshitushwa na kitendo cha aliyekuwa mbunge wa Igunga, Rostam Aziz, kutangaza kuachia nafasi hiyo na ya ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM.

Lowassa aliyewahi kuwa waziri mkuu wa Serikali ya Muungano, alisema hayo baada ya kutakiwa kutoa maoni kuhusu uamuzi wa Rostam kujiuzulu nyadhifa hizo. "Ninachoweza kusema ni kuwa, Rostam kujiuzulu ni haki yake lakini nimeshituka kuona amejiuzulu na ubunge. Nimeguswa pia na wananchi wake walivyopokea uamuzi huo," alisema. Rostam akitangaza uamuzi wa kuachia ngazi juzi, alisema amefikia uamuzi huo ili kulinda maslahi ya Chama. Kwa upande wake, Lowassa alipoulizwa ana mpango gani wa yeye kujiuzulu alisema: "Nitazungumza wakati muafaka ukifika."

Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama, kwa upande wake alisema kwa kufuata utaratibu wa kawaida ndani ya Chama, hakina taarifa za kujiuzulu Rostam. Hata hivyo, alisema jambo hilo litazungumzwa katika vikao vya juu vya Chama na baadaye taarifa zitatolewa.  "Chama hakina taarifa yoyote, tumeona kwenye vyombo vya habari ametangaza kujiuzulu kwake akiwa Igunga," alisema Mukama na kuongeza kuwa, CCM bado inalihitaji jimbo la Igunga.

Naye mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (CHADEMA), aliibuka bungeni na kuomba muongozo wa Spika Anne Makinda, akitaka atangaze kuwa jimbo la Igunga lipo wazi. Spika Anne alisema hana taarifa rasmi kuhusu kujiuzulu kwa Rostam, na kama ilivyo kwa wengine ameona habari hizo kwenye mitandao.
"Sisi tuna taratibu zetu, Rostam hajaniandikia barua, tutatoa taarifa wakati muafaka utakapowadia," alisema. Katika hatua nyingine, wanasiasa na wasomi nchini wameendelea kuwa na maoni tofauti kuhusu uamuzi wa Rostam, wengine wakipongeza hatua hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti , walisema uamuzi huo ni mzuri ingawa umechelewa.  Mwenyekiti wa TLP na mbunge wa Vunjo, Augustino Mrema, alisema Rostam amechukua uamuzi mzuri. “Ni uamuzi mzuri ingawa amechelewa,  hasa kutokana na tuhuma zake kuwa za muda mrefu,’’ alisema. Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Hajji Semboja, alisema Rostam anapaswa kupigiwa mfano na wafanyabiashara wengine.
“Ni sawa tu kuondoka, nina hakika CCM haiwezi kuyumba, ikizingatiwa kuwa wameondoka wakongwe kama hayati Julius Nyerere na Mzee Rashidi Kawawa na CCM bado ipo,’’ alisema. Alisema CCM ni chama chenye wanachama wengi, hivyo kinachopaswa kufanyika ni kwa wafanyabiashara wengine kujitoa na kuwaachia watu wa siasa.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Mohamed Bakari, alisema CCM inapaswa kuwa makini kutokana na Rostam kushika nafasi kubwa, hivyo ni lazima alikuwa na wafuasi. “Suala hili ni kubwa na lina faida na hasara, hivyo kinachotakiwa ni kujipanga vyema ili kuepusha matatizo yatakayoweza kujitokeza baadaye,’’ alisema.

Friday, June 17, 2011

Allowances here to stay, says PM


Prime Minister Mizengo Pinda yesterday ruled out the possibility of allowances budgeted for in the 2011/12 financial year being scrapped.Answering a question in Parliament, Mr Pinda said those advocating the scrapping of allowance allocations in the Budget should understand that it was a constitutional issue.
“This is a constitutional issue, and there is no way the government can act without following due procedure, which can take a long time,” Mr Pinda said when answering Mr Mohamed Habib Mnyaa (Mkanyageni-CUF), who had asked the Prime Minister to state the government’s stand on the debate on whether or not MPs should receive sitting allowance.

Mr Pinda said Article 73 of the Constitution talked about MPs’ benefits, making parliamentarians’ sitting allowances a constitutional matter that could not be changed through the pressure of one person. He added, however, there was no problem if an MP chose to forfeit his or her allowance, saying the money could be used for other purposes.

“I think there is no problem if an MP directs that his or her allowance be kept by the Treasury for other uses... this is not the first time that such a decision has been made,” Mr Pinda said. Chadema legislators, led by Mr Zitto Kabwe, have been demanding for the scrapping of sitting allowance, saying it was not justified.

Mr Kabwe, the Kigoma North MP, has argued that MPs and civil servants were being paid salaries monthly, and do not deserve extra payment when they go about their official duties. But Mr Pinda said he doubted whether Chadema arrived at the decision out of patriotism. Earlier, Mr Mnyaa said the allowance debate had caused hostility between MPs and voters, with the latter thinking that parliamentarians were squandering public resources.

He accused some MPs and the media of misleading the public, and asked the Prime Minister to clarify on the matter. Mr Pinda said there were two types of allowances –discretionary and non-discretionary. He added that the government had no powers to suspend payment of discretionary allowances, but could do so with discretionary allowances.

Mr Pinda said MPs’ sitting allowance was discretionary, and was recognised under the law and therefore could not be scrapped arbitrarily. The Prime Minister said Chadema MPs were being insincere by claiming that they do not need allowances.
“Chadema MPs may be supporting the idea, but they know deep down that they desperately need the money,” he said, adding that there was nothing wrong if MPs used their allowances to help their voters. On whether the government would take legal measures against those opposed to allowances, which were enshrined in the Constitution, Mr Pinda said there was no need to reach that stage.

“I don’t think that we need to reach that stage as the issue is not as big as some people think…it is a very minor issue.”Mr Pinda added his voice to the debate that has attracted the attention of a number of prominent individuals, including former German president Horst Kohler, who on Wednesday warned that the government’s image was at stake.

Prof Kohler said in Dar es Salaam that donors were closely monitoring the debate, adding that it might end up tarnishing the government’s image before development partners if it was not handled properly. Responding to a question during a dialogue at Movenpick Hotel, he said the debate did not present a good picture of the country’s expenditure priorities.

Prof Kohler felt that it was not in order for a country like Tanzania, which received substantial assistance from donor countries, to set aside huge sums as allowances for government officials, who were also being paid salaries. Giving an example of his own country, he said: “In Germany, such officials have to foot their own bills while attending official duties.” He added that payment of allowances was not a proper way of spending taxpayers’ money.

Prof Kohler said at the Maendeleo Dialogue, organised by Konrad Adenauer Stiftung (KAS) and the Tanzania Development Initiative Programme (Tadip), that Western countries were likely to react once they had all the facts on the allowances debate.

Opposition MP Zitto Kabwe has written to the Clerk of National Assembly, declining sitting allowance during Parliament’s ongoing Budget meeting in Dodoma.

Prof Kohler urged the government to uphold transparency and accountability.  He noted that Tanzania had made great strides in development, but added that a lot more needed to be done to promote the rule of law, saying this would enhance the public’s confidence in the government.

Thursday, June 16, 2011

Upinzani waifumua Bajeti ya Serikali

  • WAFUTA POSHO, WATANGAZA KIMA CHA CHINI SH 315,000



KAMBI ya Upinzani Bungeni imetangaza bajeti mbadala ya Sh14 trilioni na kubainisha upungufu mkubwa katika Bajeti ya Serikali, huku ikipendekeza kufutwa kwa misamaha ya kodi kwa kampuni za uchimbaji wa madini na mafuta na posho za vikao kwa watumishi wa umma, wakiwamo wabunge. Akiwasilisha bajeti hiyo bungeni, Waziri Kivuli wa Fedha na Uchumi, Zitto Kabwe alisema hatua hiyo imelenga kuongeza mapato ya Serikali na kupunguza matumizi yasiyokuwa ya lazima.

Katika bajeti hiyo mbadala, kambi hiyo imesisitiza umuhimu wa ushiriki mkubwa zaidi wa umma na uchunguzaji wa utungaji na utekelezaji wa Bajeti, ili kuboresha uwajibikaji na kuziba mianya zaidi ya ufisadi na matumizi mabaya ya rasilimali za nchi.

Kambi ya Upinzani inapendekeza kupunguza misamaha ya kodi ikitaka isizidi asilimia moja ya Pato la Taifa, kupunguza kodi na tozo kwenye mafuta ya petroli na dizeli ili kupunguza mfumuko wa bei na ukali wa maisha.

Pia imependekeza kufanya marekebisho katika mfumo wa malipo serikalini kwa kuondoa posho za vikao kwa watumishi na viongozi wa umma na kuelekeza sehemu ya tozo ya kuendeleza ujuzi (skills development levy) kwenye Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu.

Kuhusu kodi za mafuta, Zitto alisema Kambi ya Upinzani Bungeni inapinga pendekezo la sasa la kuondoa msamaha wa kodi ya mafuta kwa kampuni za utafutaji mafuta na gesi kwani mikataba ya kazi hiyo imezingatia suala hilo.

"Msamaha huu hauna mantiki kwani kampuni za utafutaji mafuta na gesi kwa mujibu wa mikataba yao (production sharing agreements) wataweza kurejeshewa gharama hizi mara baada ya mafuta na gesi kupatikana," alisema Zitto.

Pia Kambi ya Upinzani kupitia bajeti yake hiyo, inapendekeza kufuta kabisa msamaha wa kodi kwenye mafuta kwa kampuni za madini na za ujenzi kwani imethibitika kuwa msamaha huo husababisha upotevu wa fedha za umma.

Zitto alisema takwimu zinaonyesha kuwa kupitia misamaha hiyo, jumla ya lita 133 milioni za dizeli ambazo ni sawa na asilimia 20 ya dizeli yote iliyoingizwa nchini, zilikuwa za kampuni tano za migodi ya dhahabu ambazo zililipa ushuru wa dola 200,000 tu.

"Mafuta mengi yanayoingia kupitia msamaha huu hurudi kwenye soko na kuuzwa rejareja. Misamaha hii ifutwe bila kujali mikataba iliyopo," alisema.

Misamaha ya kodi

Kuhusu misamaha ya kodi, Zitto alisema kiwango kinachotolewa na Tanzania ni kikubwa ikilinganishwa na nchi jirani za Uganda na Kenya na kwamba kati ya miaka ya 2005/06 na 2007/08, misamaha ya kodi nchini ilikadiriwa kuwa wastani wa asilimia 3.9 ya Pato la Taifa.

"Mwaka 2008/09, misamaha ya kodi ilikuwa asilimia 2.8 ya Pato la Taifa na mwaka 2009/10 asilimia 2.3 ikilinganishwa na Kenya na Uganda ambako misamaha ilifikia asilimia moja na 0.4 ya pato la taifa katika kila nchi husika kwa mtiririko huo," alisema Zitto.

Alisema iwapo Tanzania ingerekebisha kiwango cha misamaha ya kodi ili kulingana na kile kilichofikiwa na Kenya, zaidi ya Sh600 bilioni zingeokolewa kwa mwaka 2007/08 pekee na kwamba fedha hizo zinaweza kuwa sawa na kiasi cha fedha ambacho serikali hushidwa kukikusanya kutokana na kodi.

Alitoa mfano wa mwaka 2008/09 na 2009/10 ambao Serikali haikutimiza lengo lake la mapato kwa wastani wa Sh453 bilioni wakati misamaha ya kodi iliyotolewa ilifikia wastani wa Sh724 bilioni.

Alisema misamaha ya kodi imekuwa ikiendelea kutolewa na kuathiri mapato ya nchi akisema kwa mujibu wa taarifa ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa Kamati ya Fedha na Uchumi ya Bunge, hadi kufikia Juni mwaka huu, msamaha wa kodi unakadiriwa kuwa Sh930 bilioni.

Zitto anasema upungufu katika ukusanyaji wa mapato unasababishwa kwa kiasi kikubwa na misamaha ya kodi kwani kama ingetolewa katika kiwango kinachofanana na cha misamaha ya kodi Kenya, Sh 484 bilioni zingeokolewa mwaka 2008/09 na Sh 302 bilioni kwa mwaka 2009/10.

Pamoja na kuipongeza Serikali kwa kukubali wazo la kupunguza misamaha ya kodi mpaka kufikia asilimia moja ya Pato la Taifa, Kambi ya Upinzani imependekeza kupitiwa upya kwa vivutio vinavyotolewa na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kwa wawekezaji kwa kupiga marufuku msamaha wowote wa kodi kwa bidhaa zinazozalishwa nchini ili kulinda viwanda vya ndani.

Posho serikalini

Katika hotuba yake, Zitto pia alirejea hoja inayopendekeza kufutwa kwa posho za vikao kwa watumishi wote wa umma hasa wabunge akisema wanatakiwa kuwa mfano katika kutekeleza pendekezo hilo.

Kambi hiyo ilishauri kufanya marejeo ya mfumo wa posho na wa mishahara kwa watumishi wa umma na kupendekeza kwamba hatua zianze kuchukuliwa sasa katika Bajeti inayojadiliwa ili kuwaonyesha Watanzania kuwa wabunge wanajali hali zao.

Alisema posho za vikao ni rushwa ya kitaasisi wanaojipa watu wenye mamlaka na kwamba wakati viongozi wakilipwa posho hizo katika vikao vya kufanya uamuzi ambao ni wajibu wao, polisi halipwi posho kwa kulinda, mwalimu halipwi posho kwa kuingia darasani na wala muuguzi halipwi posho kwa kusafisha vidonda vya wagonjwa.

Alisema Kambi ya Upinzani haipingi posho za kujikimu ambazo viongozi au maofisa wa umma hulipwa wanaposafiri nje ya vituo vyao vya kazi bali, zirekebishwe kuendana na gharama za maisha za sasa lakini akasisitiza:

"Posho za vikao zifutwe mara moja. Iwapo sisi tukiendelea kujilipa posho za kukaa humu ndani na kwenye kamati zetu, tunakuwa tunatoa ruhusa kwa watumishi wa Serikali kulipana posho hizi na hatutakuwa na mamlaka ya kuwahoji na kuwawajibisha."

Waziri huyo Kivuli wa Fedha na Uchumi, amekuwa katika malumbano ya muda mrefu na Spika wa Bunge, Anne Makinda na Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo kutokana na msimamo wake wa kukataa kulipwa posho za vikao, malipo ambayo Bunge na Serikali wanasema yapo kisheria hivyo lazima apewe.

Alisema kauli ya Serikali kwamba inakusudia kupunguza posho katika mwaka ujao wa fedha si ya kweli akisema hotuba ya Waziri Mkulo inapendekeza kufutwa kwa kodi katika posho hizo na wakati huohuo, Serikali katika Bajeti imeomba kiasi cha Sh 987 bilioni sawa na asilimia 13 ya bajeti nzima kwa ajili ya malipo ya posho mbalimbali.

"Katika hotuba yake ukurasa wa 66, anapendekeza (Waziri) kufanywa kwa marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Mapato Sura 332 na anasema kwenye (i) kusamehe kodi ya mapato kwenye posho wanazolipwa wafanyakazi wa serikali na wanaofanya kazi kwenye taasisi zinazopata ruzuku kutoka kwenye bajeti ya serikali.”

"Sasa tumeanza kusikia vilio kutoka sekta binafsi kwamba na wao wapate unafuu huu wa kodi. Kambi ya upinzani inapendekeza mfumo mzima wa kulipana posho za vikao (sitting allowances) uondoke katika utumishi wa umma."

Sekta ya madini


Hotuba hiyo ya wapinzani pia imezungumzia kwa undani sekta ya madini na kubainisha kwamba taarifa za Serikali zinathibitisha kwamba haichangii mapato ya ndani.

Alisema ipo haja ya kuhakikisha taifa linakusanya mapato ya kutosha katika sekta hiyo ili kuleta maendeleo ya wananchi:
"Katika mwaka huu wa fedha, taifa letu litakusanya Sh 99.5 bilioni kutoka katika mrabaha kwenye madini yanayochimbwa nchini kwetu. Mapato haya kwa mwaka ujao wa fedha ni asilimia 4.5 tu ya mauzo ya dhahabu peke yake nje ya nchi."

Alisema ni vigumu kujua kiasi cha kodi nyingine zinazokusanywa kutoka katika sekta ya madini kutokana na kampuni zote kurundikwa katika kapu moja la idara ya walipa kodi wakubwa.

Alisema takwimu za Mwaka 2009/2010 zinaonyesha kuwa mapato yote ya kodi pamoja na mrabaha na malipo kwa mifuko ya pensheni (ambayo siyo kodi) katika sekta ya madini yalikaribia Sh 256 bilioni ambazo zilikuwa sawa na asilimia 16 ya thamani ya mauzo ya madini nje ya nchi.

Kodi za mafuta
Kuhusu kodi zitakazopunguzwa kwenye mafuta, Zitto alisema Kambi ya Upinzani inapendekeza kuwa ushuru wa barabara (road toll) usipunguzwe ili kubakia na fedha za kutosha kukarabati barabara ambazo zinajengwa kwa kasi.

Alisema maeneo ambako kodi hiyo inaweza kupunguzwa ni ushuru wa bidhaa kwenye mafuta kwa asilimia 40 na tozo nyingine zote kwenye mafuta zipunguzwe kwa asilimia 40 pia.

Hata hivyo, Zitto alisema hatua ya kupunguza kodi za mafuta ni kama dharura tu kwani bado inaweza isiwe na maana iwapo bei za mafuta zitaendelea kupanda katika soko la dunia.

"Hivyo tunahitaji njia endelevu; nayo ni kuhakikisha mafuta yanaagizwa kwa wingi na hivyo kupunguza gharama za usafirishaji. Mpango wa ununuzi wa mafuta kwa wingi umekuwa ukisemwa bila kutekelezwa kwa muda mrefu kutokana na nguvu kubwa ya rushwa waliyonayo matajiri katika sekta ya mafuta. Ni lazima tuishinde nguvu hii hata kama itakuwa ni kwa baadhi yetu kupoteza maisha."

Sura ya bajeti mbadala

Sura ya bajeti hiyo mbadala inaonyesha kuwepo kwa uwezekano wa mapato ya Serikali katika mwaka wa fedha 2011/12 kufikia Sh14.16 trilioni ikilinganishwa na kiasi cha Sh13.525 trilioni kilichopendekezwa katika Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka huo.

Zitto ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni alibainisha kuwa fedha hizo ni mapato ya ndani Sh8.68 trilioni kutoka Sh6.7trilioni za serikali, mapato ya halmashauri Sh351 bilioni, mikopo na misaada ya nje Sh3.924 trilioni na mikopo ya ndani Sh1.204 trilioni.

Kwa upande wa matumizi, Zitto alisema kambi yake inapendekeza matumizi ya kawaida Sh.7.913trilioni ikilinganishwa na yale ya Serikali ambayo ni Sh 8.600 trilioni
wakati kwa upande wa matumizi ya maendeleo, wapinzani wanapendekeza kaisi cha Sh6.247 trilioni zikiwamo fedha za ndani Sh3.193trilioni na fedha za nje Sh3.054 trilioni.

Bajeti ya Serikali imetenga kiasi cha Sh4.925 trilioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo ambapo fedha za ndani ni Sh1.871 trilioni wakati fedha za nje ni Sh3.054 trilioni.

Ili kukidhi mahitaji ya fedha za mapendekezo yaliyomo katika bajeti yake, Zitto alisema Kambi ya Upinzani, inapendekezo kufanya marekebisho ya kodi katika maeneo kadhaa ambayo yataingiza kaisi cha Sh1.905 trilioni na kuongeza fedha hizo katika bajeti.

Marekebisho hayo ni kodi ya misitu ambayo itawezesha kupatikana kwa Sh100 bilioni, misamaha ya kodi (Sh658 bilioni), mauzo ya hisa za Serikali (Sh 550 bilioni), kodi katika sekta ya madini (Sh240 bilioni), kuimarisha usimamizi wa mapato ya wanyamapori (Sh81 bilioni), kuondoa msamaha wa ushuru wa mafuta kampuni za madini (Sh59 bilioni), usimamizi wa mapato katika utalii (Sh68 bilioni) na kuimarika kwa biashara na nchi za Afrika Mashariki (Sh150 bilioni).

Pia kambi hiyo inapendekeza kuanzishwa kwa kodi mpya inayotokana na fedha ambazo wenye nyumba wanazipangisha. Alipendekeza kuanzishwa kwa chombo maalumu cha kusimamia kazi hiyo.

Chanzo: Mwananchi 16/6/2011

Wednesday, June 15, 2011

CCM WAFUTA POSHO ZA VIKAO


HOJA ya kutaka kufutwa kwa posho za vikao za wabunge na watumishi wengine wa umma imechukua sura mpya baada ya jana Mbunge wa Bumbuli (CCM), Januari Makamba kuliambia Bunge mjini hapa kuwa suala la kufutwa kwa posho ni la kitaifa na ni sehemu ya Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano uliowasilishwa na serikali.

Kauli hiyo ya Makamba ambaye pia ni Katibu wa Mambo ya Nje wa Sekretarieti ya CCM imekuja huku kukiwa na malumbano makali baina ya Spika wa Bunge, Anne Makinda na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe kuhusu suala hilo la posho za vikao vya wabunge.

Juzi, Spika Makinda alisema Zitto ambaye ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, anaweza kufukuzwa ubunge kwa kutosaini karatasi za mahudhurio, hatua ambayo Zitto alisema ataichukua ili asilipwe posho za vikao.

Spika alisema Zitto anaweza kukumbwa na adhabu hiyo iwapo hatasaini karatasi za mahudhurio ambazo ndizo zinathibitsha uwepo wa mbunge katika mikutano na vikao vya bunge na kwamba kanuni zinamwadhibu mbunge kwa kumfukuza asipohudhuria mikutano mitatu. Hata hivyo, Zitto amepuuza kauli hiyo ya Spika kwa kusema kwamba kama ni kwa ajili ya kukataa posho, yuko tayari kufukuzwa bungeni.

"Nitafanya hivyo tuone, Kanuni inasema mikutano mitatu mfululizo na siyo vikao vitatu mfululizo. Nitatumia uzoefu wangu wa siasa za wanafunzi kukwepa mtego wake. Lakini kama anadhani ni sawa kunifukuza ubunge kwa kukataa posho, nipo tayari," alisema.

Kauli ya jana ya Makamba pia inaonekana kutofautina na mawazo ya wabunge wengi wa CCM akiwamo Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo ambaye amesema wanashabikia suala hilo wanajitafutia umaarufu.

Akichangia huo wa maendeleo wa miaka mitano jana, Makamba alionekana kupigia chapuo suala la kufutwa au kuangaliwa upya kwa posho za vikao huku akisema kwamba ni la kitaifa na ni sehemu ya mpango huo.

Makamba alisema kuwa suala la nidhamu na usimamizi wa matumizi ya fedha za umma ni muhimu na kwamba mpango huo umeliona katika ukurasa wa 17 wa kitabu kilichochapishwa kwa Kiingereza na kutoa mapendekezo ya kufutwa kwa posho za vikao na zile za usafiri.

"Mpango unabainisha kwamba kuna umuhimu wa kufutwa kwa posho za vikao na usafiri hivyo iwapo wabunge mtalisikia likiwasilishwa hapa kwa mbwembwe kesho (leo), basi msije mkashangaa kwani ni sehemu ya mpango huu," alisema Makamba.

Kujadiliwa bungeni leo

Mjadala kuhusu malipo ya posho ambao umekuwa ukiendelea kwa wiki moja sasa hasa zaidi nje ya Bunge, leo unatarajiwa kuingizwa rasmi bungeni wakati Bajeti ya Serikali iliyowasilishwa na Mkulo Jumatano iliyopita itakapoanza kujadiliwa.

Suala hilo ni dhahiri litajitokeza katika bajeti mbadala itakayowasilishwa na kambi ya Upinzani Bungeni na Waziri Kivuli wa Fedha, Zitto Kabwe ambaye amekuwa katika mvutano usio rasmi na Spika kutokana na kukataa kulipwa posho za kikao.

Mwenyekiti wa Chadema ambaye pia ni Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe alisema jana kuwa kambi yake inatarajiwa kutoa ushauri mgumu ambao haujazoeleka kwa watendaji wa serikali na kwamba suala la kufutwa kwa posho ni sehemu ya mapendekezo hayo.

Alisema kufutwa kwa posho hizo kunaweza kuokoa zaidi ya Sh900 bilioni ambazo zinaweza kuelekezwa katika maeneo mengine ya huduma kwa wananchi.

Uhalisia posho za wabunge

Mmoja wa wabunge wa CCM ambaye hakutaka kutaandikwa jina lake alisema anasikia kuhukumiwa katika nafsi yake kutokana na kupokea posho za vikao ambazo kimsingi ni sawa na "kuwaibia wananchi".

"Ujue bwana sisi ndani ya CCM mambo hayaendi kama kwa wenzetu (Chadema), wale wanaweza kukaa leo na kuamua, sisi ni tofauti lazima kuwepo na mchakato lakini ukweli ni kwamba hoja yao ni nzuri," alisema mbunge huyo.

Uchunguzi uliofanywa umebaini kuwa malipo ya wabunge yamegawanyika katika sehemu nne ambazo ni pamoja na mshahara ambao ni Sh2,300,000 kwa mwezi, posho ya ubunge kila mwezi ambayo ni Sh5 milioni, posho ya kujikimu (per-diem) Sh80,000 wawapo nje ya majimbo yao kikazi na posho ya vikao (sitting allowance) ambayo huwa ni Sh70,000 kwa kila mbunge.

Kwa maana hiyo, kwa kawaida mbunge hulipwa Sh7.3 milioni kila mwezi kabla ya kukatwa kodi na wawapo Dodoma na Dar es Salaam kwa ajili ya vikao vya kamati na bunge au mikoani kwa ajili ya kukagua shughuli zilizopo chini ya kamati zao. Hulipwa kiasi cha Sh150,000 kila mmoja kwa siku ambazo ni Sh70,000 kwa ajili ya vikao na Sh80,000 kwa ajili ya kujikimu.

Kwa maana hiyo bunge linatarajiwa kutumia kiasi cha Sh1.788 bilioni kwa ajili ya kugharamia vikao 73 vya Bunge la Bajeti iwapo wabunge wote 350 waliopo watahudhuria vikao hivyo.

Kwa hesabu hizo, kila mbunge katika mkutano wa Bunge la Bajeti anatarajiwa kuondoka na kikita cha Sh5.1 milioni mbali na Sh 5.58 milioni ambazo ni malipo kwa ajili ya kujikimu, fedha ambazo ni mbali na mshahara wake kwa mwezi na posho ya ubunge.

CCM yakataa posho

Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeanza machakato wa kufuta posho hizo ikiwa ni hatua ya kupunguza matumizi yasiyo ya lazima. Habari kutoka ndani ya CCM, Dodoma na Dar es Salaam zinasema kuwa mkakati wa kufutwa kwa posho ulianzishwa takriban mwezi mmoja uliopita na sekretarieti mpya inayoongozwa na Katibu Mkuu, Wilson Mukama.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, baadhi ya wajumbe wa sekretarieti walihoji uhalali wa posho wanazolipwa hata pale vikao vinapofanyika katika sehemu ambako ni makazi yao na kwamba hoja hizo ndizo zilizozaa wazo la kufutwa kwa posho katika vikao.

"Hoja ilikuwa kwamba kama chama hakina fedha na tunataka kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, basi posho za vikao zifutwe kwa sababu hakuna ulazima wa posho hizo hasa kwa wajumbe wa sekretarieti ambao kazi zao ni za kila siku," kilieleza chanzo chetu na kuongeza:

"Hivi sasa mpango huo uko kwenye mchakato wa kuwekewa mwongozo na nadhani baada ya kupitia katika vikao vyetu utaanza kutekelezwa. Lakini kimsingi ni kama utekelezaji wake umeshaanza kwa sababu baadhi ya wajunbe wamekataa kabisa kusaini posho hizo."

Habari zaidi zinadai kuwa waraka wa mapendekezo ya kupunguza matumizi ndani ya CCM unakwenda mbali zaidi hadi katika matumizi ya magari na kwamba pale usafiri unapohitaji wa kuelekea kwenye mkutano mmoja, basi viongozi watumie magari machache kwa maana ya usafiri wa pamoja badala ya utaratibu wa sasa ambao unamruhusu kila kiongozi kutumia usafiri wake.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipoulizwa kuhusu sekretarieti kufuta posho katika vikao vyake, hakukanusha wala kuthibitisha, badala yake akadai kuwa hayo ni mambo ya ndani ya chama ambayo hayana faida yoyote kwa umma.

"Hivi ninyi waandishi wa habari, haya mambo mnayapata kwa nani! Haya ni mambo ya ndani ya chama sidhani kama yana tija yoyote kwa umma, maana haiwezi kusaidia chochote," alisema Nape kwa kwa simu.

Alipoelezwa kwamba suala hilo lina uhusiano na sakata linaloendelea bungeni, Nape alisema: "Bunge ni bunge na chama ni chama. Kila taasisi inajitegemea na ina uamuzi wake, lakini pia sisi kama chama tulishatoa kauli mara nyingi kwamba suala la posho kwa wabunge na watumishi wengine wa serikali linazungumzika, ni la kisera na wanaohusika wapo waulizeni hao."

Mwishoni mwa wiki iliyopita Nape akizungumzia malumbano miongoni mwa wabunge kuhusu suala la posho alisema suala hilo linajadilika na kwamba si vyema kulipinga kwa sababu tu linatokea kambi ya upinzani.

Kwa upande wake, Makamba alipoulizwa kuhusu kufutwa kwa posho katika vikao vya Sekretarieti ya CCM naye kama ilivyokuwa kwa Nape, hakukanusha wala kuthibitisha.

"Wewe si unamfahamu msemaji wa chama ni nani? Mwulizeni Nape tena nadhani anakuja Dodoma. Akija mwulizeni, mimi siwezi kulizungumzia.... lakini ninyi waandishi haya mambo ya ndani ya chama huwa mnayapata wapi? Anyway, mwulizeni mwenezi atawaambia," alisema Makamba.

Chanzo: Mwananchi 15/6/2011

Monday, June 6, 2011

Hali tete: Chadema, Polisi wakwaruzana

Askari polisi wakilinda kwenye kituo kikuu cha polisi kati anakoshikiliwa mwenyekiti wa Chadema Freeman MbowePicha na Fidelis Felix/Silvan Kiwale


















JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, jana lililazimika kuimarisha ulinzi katika Kituo chake Kikuu (Central) na baadhi ya maeneo ya jiji kukabiliana na tishio la wanachama wa Chadema kuandamana ili kushinikiza Mwenyekiti wao, Freeman Mbowe aliyekamatwa juzi aachiwe.Mbowe ambaye alikamatwa juzi ikiwa ni kutekeleza amri ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha iliyoamuru akamatwe popote alipo na afikishwe hapo kwa kutotii amri ya kufika mahakamani katika kesi inayomkabili, alitarajiwa kupelekwa huko wakati wowote kuanzia jana akiwa chini ya ulinzi.

Jana, vijana wa Chadema walikusanyika katika kituo hicho huku wakilaani kitendo cha kukamatwa kwa mwenyekiti wao huku wengine wakijikusanya katika vikundi vidogovidogo katika maeneo mbalimbali katika Barabara za Morogoro na Nyerere, lengo likiwa kushinikiza kiongozi huyo atolewe rumande na asisafirishwe kupelekwa Arusha.

Taarifa kutoka Arusha ambako kesi ya kiongozi huyo inatarajiwa kuendelea leo asubuhi zinaeleza kuwa polisi jana jioni waliendesha msako wa wanachama wa Chadema waliokuwa wakihamasishana kuhudhuria kwa wingi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Arusha.

Wanachama na mashabiki hao wa Chadema walidai kwamba kitendo cha kukamatwa kwa kiongozi huyo wa kambi ya upinzani bungeni ni mpango uliobuniwa na CCM wa kubinya demokrasia ya vyama vingi nchini.

Mbowe na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Bara, Zitto Kabwe walikamatwa katika maeneo tofauti nchini juzi. Wakati Mbowe alidaiwa kutotii amri ya mahakama, Zitto alidaiwa kuzidisha muda wakati wa kuhutubia mkutano wa hadhara mkoani Singida.

“Tumeongea na polisi, bado wanamng'ang'ania Mbowe. Msimamo wao ni kumpeleka Arusha, tuangalie utaratibu utakaotumika katika kumsafirisha,” alisema Mkurugenzi wa Mambo ya Nje wa Chadema, John Mnyika.

Baada ya kauli hiyo ya Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubunge, vijana wa chama hicho wakiongozwa na Diwani wa Kata ya Ubungo, Boniface Jacob walianza kuimba nyimbo za kulaani kukamatwa kwa mwenyekiti wao huku wakisema muziki wa Chadema polisi hawauwezi.

Ofisa mmoja mwadamizi wa Polisi Ilala ambaye hakujitambulisha jina aliwaambia vijana hao kuwa polisi  walishakubaliana na viongozi wa Chadema kuwa mtuhumiwa huyo amepangiwa utaratibu wa kusafirishwa kwenda Arusha kuhudhuria kesi yake.Ofisa huyo aliwataka wananchi waliokuwa kwenye eneo hilo kuondoka ili kupisha jeshi hilo kuendelea na kazi ya kutoa huduma kwa watu wengine.

“Tumeshaongeza na wakubwa wenu, hiki ni kituo cha polisi watu mbalimbali wanakuja kupata huduma hapa. Mtu haji kuangaliwa kwa aina hii ya hamasa na nyimbo, tunaomba muondoke,” alisema ofisa huyo.Kauli hiyo ilipingwa na vijana hao wakisema ofisa huyo ni mtu wa kawaida hawezi kuwaeleza mambo kama hayo.

“Sisi hapa tuna viongozi wetu mambo kama hayo tungeelezwa na kuelewa kama yangesemwa nao na si mtu wa kawaida kama wewe,”alisikika mmoja wa wanachama hao akisema kwa sauti.

Kauli hiyo ilimshangaza ofisa mwingine wa polisi aliyeibuka na kuhoji: “Mnasema huyu ni mtu wa kawaida? Akajibiwa “ndiyo”, “huyo siyo mtu wa kawaida."Vijana hao waliendelea na msimamo wao: “Sisi tunasema huyo ni mtu wa kawaida kwa sababu siyo kiongozi wetu, ndiyo maana tunasema angekuwa kiongozi wetu tungemwelewa.”

Kauli hiyo ilimlazimisha Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Faustine Shilogile kujitokeza na kuwataka watu hao kuondoka katika eneo hilo kwa sababu kulikuwa na shughuli mbalimbali zilizokuwa zikiendelea.

“Tumeongea na viongozi wenu, tumeshakubaliana tunawaomba mtawanyike na sisi tuendelee na kazi, sitaki mkusanyiko wowote katika kituo cha polisi,” alisema Shilogile. Mara baada ya kauli hiyo gari la maji ya kuwasha lilianza kusogea walipokuwa wafuasi hao wa Chadema likitanguliwa na Polisi wa Kutuliza Ghasia waliokuwa wakiwafukuza katika eneo hilo.

Kundi hilo liliondoka na kuelekea makao makuu ya Chadema ambako Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa alikuwa na mkutano na waandishi wa habari.

Msimamo wa Kamanda Kova
Akizungumzia mvutano huo, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema jeshi lake haliwezi kumwachia Mbowe kwa sababu wanaheshimu amri ya Mahakama.

Kova aliwaambia waandishi wa habari jana kwamba jeshi hilo lilipokea amri ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha ya kumkamata kiongozi huyo wa Chadema na kwamba hawaruhusiwi kuhoji lolote juu ya amri hiyo.

“Sisi kama jeshi la Polisi tumepokea amri ya mahakama ya kumtia hatiani Mheshimiwa Mbowe na hatuna mamlaka ya kumwachia huru hadi mahakama itoe amri ya kumwachia,”alisema.

Alisema sheria hairuhusu kuhoji sababu za amri inayotolewa na mahakama na kufafanua kuwa hizo ni sheria zilizotungwa na wabunge wenyewe. Alisema Mbowe anatarajiwa kusafirishwa chini ya ulinzi wa Polisi kwenda mkoani Arusha kujibu kesi inayomkabili na kwamba taratibu zote za safari tayari zimekamilika.

“Tunachokifanya ni maagizo ambayo yametoka ngazi ya juu kuhusu suala hili kwa hiyo Mbowe atapelekwa Arusha chini ya ulinzi wa polisi muda wowote kuanzia sasa alimradi awahi muda wake wa mahakama,”alisema Kova.

Alisema atapelekwa Arusha chini ya ulinzi wa polisi kwa sababu amekiuka masharti yake ya dhamana na kwamba tayari wamezungumza na baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani waliokwenda kumuona kiongozi huyo wa kambi ya upinzani bungeni jana.

Kova alisema kulingana na taratibu na sheria za Tanzania, mahakama ikitoa amri hakuna mtu anayeweza kuipinga.

Aliwataka wananchi watulie na kuipa fursa mahakama itekeleze sheria zilizotungwa na Bunge. Akizungumzia kukamatwa kwa Mbowe, Mnyika alisema hizo ni njama za kuudhalilisha upinzani na pia mbinu za kumtaka Mbunge huyo wa Hai asihudhurie kwenye Kikao cha Bunge la Bajeti.

“Endapo watashindwa kutumia busara za mazungumzo tuliyoyafanya kumwachia Mbowe, jambo hili tutalirudisha kwa wananchi na nguvu ya umma itatumika kusuluhisha tatizo hilo,” alisema.

Alisema amani ni tunda la haki lakini inaweza kupotea kama haki haitatendeka na kuongeza kuwa kuna watu ambao wanashutuma nzito za ufisadi, lakini hawachukuliwi hatua zozote isipokuwa viongozi wa upinzani.


Tamko la Dk Slaa
Dk Slaa alisema kesi zinazowakabili viongozi wa chama hicho na wabunge wa vyama vya upinzani vinalifedhehesha Bunge la Tanzania kimataifa.

“Ili mtuhumiwa akamatwe sheria iko wazi, notisi zilitakiwa kutolewa kwa mdhamini wake na pia kwa wakili, lakini kwa Mbowe haikuwa hivyo na hiyo inaonyesha ni agizo kutoka mahali Fulani,” alidai.

“Polisi mkoa wa Mwanza wametuma barua kwa Katibu wa Bunge kuomba kibali cha kwenda kumhoji Mbunge wa Jimbo la Busega, Dk Titus Kamani, iweje kwa wabunge wa upinzani kukamatwa bila utaratibu? Alihoji Dk Slaa.

Alisema kutokana na mazingira hayo kama Mbowe hatafikishwa leo mahakamani wabunge wa Chadema hawataingia bungeni.

Kuhusu uwakilishi kwenye kamati ya uongozi alisema hata kama Zitto atakuwa nje ya mahabusu, hataingia kuwakilisha upinzani kwa sababu anayetakiwa kumpa kibali cha kufanya hivyo yupo ndani.

Kuhusu kosa la Zitto kukamatwa na polisi alisema inashangaza kwa sababu alikuwa kwenye mkutano wa hadhara kama mbunge na alizidisha dakika 20 kwenye mkutano huo.

Alisema hiki siyo kipindi cha kampeni na Zitto ni kiongozi mwenye haki ya kufanya hivyo na kusisitiza kilichofanyika kimelenga kufifisha demokrasia nchini.