Showing posts with label ndugai. Show all posts
Showing posts with label ndugai. Show all posts

Wednesday, August 24, 2011

Wabunge- Bunge limedhalilishwa, Pinda kafedheheshwa

BUNGE limesema, Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo amelidhalilisha na pia amemdhalilisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwa kumuamuru Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo arudi kazini.

Wabunge wamesema, taarifa ya uchunguzi ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusu tuhuma kwamba, Jairo alichangisha shilingi bilioni moja ili kuwezesha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini ipitishwe bungeni ilistahili kupelekwa bungeni waijadili kabla Serikali kutoa uamuzi.

Wabunge leo wamejadili kauli ya Luhanjo kama jambo la dharura baada ya wabunge kukubali hoja ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto aliyoitoa asubuhi kabla ya kipindi maswali na majibu na kuifafanua baada ya Kamati ya Bunge ya Uongozi kukutana katika ukumbi wa Spika.

Spika wa Bunge, Anne Makinda aliongoza kikao hicho cha dharura wakati wa kipindi cha maswali na majibu.

Kabla ya kamati hiyo kukutana, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisema, kwa kutumia kifungu cha 51 cha Kanuni za Bunge alichotumia Zitto kuwasilisha hoja yake, inamtaka Mbunge aiwasilishe mapema kwa Spika wa Bunge ili atoe uamuzi.

Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai, alimjibu Lukuvi kwamba, kabla ya kuanza kwa kikao cha leo, Zitto alipeleka taarifa fupi kwa Spika wa Bunge kuhusu hoja hiyo kwa hiyo utaratibu umefuatwa.

“Hoja hii nzito kweli…na ndiyo hoja iliyoungwa mkono” amesema Ndugai baada ya Zitto kuiwasilisha kwa mara ya kwanza kabla ya.

Zaidi ya robo tatu ya wabunge waliokuwa ukumbini wakiwemo kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) wameunga mkono hoja ya Zitto. Ndugai, amesema bungeni kuwa, hoja ya Zitto ni ya msingi kwa kuwa Bunge limedharauliwa.

“Kwa sababu Bunge ni mhimili, hatuwezi kudharauliwa kirahisi”amesema Ndugai na kusisitiza kwamba, Wabunge hawawezi kukaa kimya wakati Waziri Mkuu anadhalilishwa.

“Kama dharau inaweza ikatokea basi huko huko lakini sio ndani ya Bunge hili” amesema Ndugai baada ya wabunge kuijadili hoja ya Zitto na kusisitiza kwamba, kwa kuwa suala hilo lilianzia bungeni, taarifa ya CAG ingepelekwa kwanza kwenye mamlaka hiyo kabla ya uamuzi wa Serikali.

Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Zainab Vullu, wabunge wamepewa jukumu la kuisimamia na kuishauri Serikali kwa niaba ya wananchi hivyo kauli ya Luhanjo imewadhalilisha, na limepokwa mamlaka yake.

Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka, amesema, suala hilo lina maslahi kwa Taifa, taarifa ya CAG ingepelekwa kwanza bungeni itendewe haki.

Sendeka amesema bungeni kuwa, Waziri Mkuu amefedheheshwa kwa kuwa Kiongozi huyo wa Shughuli za Serikali Bungeni alisema, kama angekuwa yeye angemchukilia hatua Jairo, na pia Bunge limedhalilishwa.

Kwa mujibu wa Sendeka, kauli ya Luhanjo imelilidhalilisha Bunge na imekiuka Sheria ya Kinga na Madaraka ya Bunge na ibara ya 100 ya Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.

Mbunge huyo ametumia Kanuni 117 ya Bunge kuomba iundwe kamati teule ya Bunge kuchunguza jambo hilo ukiwemo utaratibu wa Jairo kukusanya fedha za kupitishia bajeti hasa ikizingatiwa kuwa, kila Waziri huwa na fungu la kugharamia bajeti kila idara zikiwemo fedha za kununulia mafuta.

Sendeka aliomba Bunge liunge mkono hoja yake ili kulinda hadhi ya Bunge, takribani wabunge wote walikubali isipokuwa mawaziri na manaibu mawaziri.

Wakati anatoa hoja hiyo, Zitto amesema, kwa kuwa jambo hilo lilianzia bungeni wakati Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo (CCM) alipolieleza Bunge kuwa ana barua ya Jairo kuzitaka idara katika Wizara za Nishati na Madini zichangie shilingi milioni 50 kila moja, wabunge walistahili kuijadili ripoti ya CAG kabla ya Serikali kufanya uamuzi.

Zitto amelieleza Bunge kuwa, kauli ya Luhanjo ni dharau kwa Waziri Mkuu, na imeingilia hadhi, kinga na madaraka ya Bunge kwa kuwa wabunge ndiyo wana mamlaka ya kuisimamia Serikali.

Zitto alipendekeza kwamba, shughuli na hoja zote za Serikali bungeni zisitishwe, kwanza wabunge waijadili taarifa za CAG kwa kuwa Bunge limepokwa nafasi yake.

Ndugai amewaeleza wabunge kuwa, Spika wa Bunge, Makinda, ataunda tume kuchunguza kudharauliwa kwa Bunge, na kukusanywa kwa fedha kwa ajili ya kupitishwa bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2011/2012.

Kwa mujibu wa kiongozi huyo wa Bunge, tume hiyo itapaswa kufanya kazi haraka ili taarifa yake ijadiliwe katika mkutano ujao wa Bunge.

Luhanjo jana alimuagiza Jairo arudi kazini leo aendelee na madaraka yake katika Wizara ya Nishati na Madini kwa kuwa tuhuma zilizotolewa dhidi yake hazikuthibitika.

Leo asubuhi, Jairo alikwenda ofisini kwake wizarani jijini Dar es Salaam, wafanyakazi wakampokea kwa shangwe na vigelegele huku wakiimba kwamba wana imani naye.

Wednesday, July 6, 2011

Vinara kashfa ya rada watajwa

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Mathias Chikawe amesema Mbunge wa Bariadi Magharibi, Endrew Chenge (CCM), hahusiki kwa namna yoyote na kashfa ya uuzaji wa rada liyoligharimu Taifa pauni milioni 28 ambazo sasa Serikali inataka zirejeshwe.

Mbali na Chenge ambaye pia anatakiwa kujivua gamba ndani ya chama chake kwa kashfa hiyo, Chikawe alisema bungeni jana kuwa, hakuna Mtanzania hata mmoja anayetuhumiwa kwa hilo ndio maana hawajamshitaki mtu.

Akitoa majumuisho ya hotuba ya Ofisi ya Rais Utawala Bora, Chikawe alisema Serikali ililiita Shirika la Serious Fraud Office (SFO) la Uingereza kuja kumchunguza Chenge kwa kushirikiana na Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) na katika uchunguzi huo Chenge hakukutwa na hatia.

Aliwataja wahusika kuwa ni Sailesh Vithlan, dalali wa rada hiyo Jonathan Callman, Meneja Biashara wa Kampuni ya BAE Systems ya Uingereza iliyouza rada hiyo na Meneja Masoko wa kampuni hiyo, aliyejulikana kwa jina moja la Christopher.

"Kama kuna mtu ana ushahidi dhidi ya Chenge au mtu mwingine atupe na tutampeleka mtuhumiwa huyo mahakamani kesho.

"Kama hakuna, basi tufanye kama kanisani (wakati wa kufunga ndoa) kuwa yeyote mwenye neno naye (Chenge), aseme sasa na kama hakuna basi kila mtu anyamaze," alisema Chikawe.

Alifafanua kuwa Serikali haijamshitaki Chenge wala mtu yeyote na kufafanua kuwa haiwezi kwenda mahakamani kwa hisia na hata wanasheria wanafahamu hilo.

Hii ni mara ya tatu kwa Chenge kusafishwa na tuhuma hizo; mara ya kwanza aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Utawala Bora, Sophia Simba alikaririwa akisema kuwa Chenge alisafishwa na SFO.

Mara ya pili, Chenge mwenyewe alijitokeza mbele ya vyombo vya habari alipokuwa akigombea nafasi ya Spika wa Bunge na kufafanua kuwa SFO na Takukuru walimsafisha baada ya kukosa ushahidi dhidi yake.

Lakini Ubalozi wa Uingereza ulitoa tamko kuwa suala hilo halijakamilika wala halijafikiwa muafaka na Chenge hakupaswa kudai kuwa hana hatia.

Hata hivyo wakati wa Kamati ya Matumizi Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani, Tundu Lissu alisimama na kusema anayo barua inayoonesha kwamba Andrew Chenge na Dk. Idris Rashid walihusika katika ununuzi wa rada hiyo na Chenge alipata dola milioni 1 alizopeleka katika akaunti iliyopo nje ya nchi na Dk. Rashid alipata pauni za Kiingereza laki sita.

Hata hivyo Waziri Chikawe alisimama na kusema kwamba aliwaomba wabunge kama wana ushahidi dhidi ya Chenge waulete ili waende mahakamani hata kesho na akaomba Tundu Lissu ampatie ushahidi huo.

Lakini Lissu alisema ushahidi huo ni barua kutoka SFO kwenda kwa Mwanasheria Mkuu wa Tanzania na hivyo Serikali isiwahadae wananchi kwa sababu wanao ushahidi.

Kashfa hiyo hiyo, itakumbukwa kuwa ilichangia Chenge kujiuzulu nafasi yake kama Waziri wa Miundombinu baada ya kutuhumiwa kumiliki fedha zilizodaiwa kuwa mgawo wake katika uuzaji wa rada; dola milioni moja, zaidi ya Sh bilioni moja nje ya nchi.

Lakini jana kabla ya kutangazwa kuwa Chenge hana hatia, Serikali ilitupiwa zigo la kuwachukulia hatua za kisheria Watanzania waliohusika kupora fedha za umma katika ununuzi wa rada katika Mahakama ya Tanzania kwa kuwa katika Mahakama ya Uingereza, watuhumiwa hao hawatakuwa na hatia.

Ujumbe wa Bunge uliokwenda Uingereza kuwakilisha Watanzania kudai fedha hizo maarufu 'chenji' , umeweka wazi kuwa Kampuni ya BAE Systems inayotuhumiwa kushirikiana na watuhumiwa wa Tanzania katika uporaji huo na SFO, wameweka mazingira ya kutoshitakiwa kwa watuhumiwa hao huko Uingereza.

Wakizungumza baada ya kukabidhi ripoti ya kazi waliyoifanya huko Uingereza kwa Spika wa Bunge, Anne Makinda, wajumbe hao walioongozwa na Naibu Spika, Job Ndugai, walisema wamefanikiwa kushawishi Waingereza kuona umuhimu wa fedha hizo pauni milioni 29.5, kurudishwa kupitia Serikali ya Tanzania.

Lakini pia waliituhumu kampuni hiyo na SFO kwa kupanga mazingira hayo ya kutoshitakiwa kwa watuhumiwa kwa kutumia mwanya wa mazungumzo nje ya Mahakama.

Ndugai alisema baada ya SFO kuishitaki kampuni hiyo, kampuni hiyo iliomba mazungumzo nje ya Mahakama na yalipokamilika, Mwanasheria wa kampuni hiyo, ambayo ndiyo mtuhumiwa, alitengeneza makubaliano ya mazungumzo hayo na kuzuia watuhumiwa wasishitakiwe na kuyasajili mahakamani.

Ndugai alisema kuwa mwanasheria huyo alihakikisha anailinda kampuni hiyo na watuhumiwa wengine.

"Kwa kweli jaji aliyetoa hukumu ile, alikuwa na 'moral pressure' msukumo wa kibinadamu, akaona gharama za kesi ni kubwa akasema nitapunguza gharama za kesi na kuongeza katika tuzo itakayopewa Watanzania," alisema Ndugai.

Alifafanua kuwa katika hilo, badala ya kuamuru fedha nyingi ziwe gharama za kesi hizo ambazo zingetumiwa na SFO au kampuni hiyo; jaji huyo alitoa pauni laki tano tu kama gharama za kesi na pauni milioni 29.5 akaamuru zirejeshwe kwa Watanzania walioibiwa.