Showing posts with label mwakyembe. Show all posts
Showing posts with label mwakyembe. Show all posts

Wednesday, August 17, 2011

Magufuli amkomalia aliyejenga barabara ya Kilwa

SERIKALI inachunguza kiini cha barabara ya Kilwa kutoka Mivinjeni hadi Mbagala jijini Dar es Salaam kujengwa chini ya kiwango ili aliyehusika airekebishe kwa gharama zake.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe amelieleza Bunge mjini Dodoma kuwa, Mhandisi, Mhandisi Mshauri na wataalamu kutoka Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) wanachunguza ili kufahamu kiini cha tatizo.

Mwakyembe amewaeleza wabunge kuwa, viongozi wa Wizara hiyo wamekuwa wakali katika kusimamia ubora wa barabara zinazojengwa na ametoa mifano ya barabara kadhaa ambazo zinachunguzwa na nyingine waliosababisha zijengwe chini ya kiwango wametakiwa kuzirekebisha kwa gharama zao.

Kwa mujibu wa Mwakyembe, Mkandarasi aliyejenga barabara ya Nangurukuru- Mbwemkulu ametakiwa kuirekebisha kwa gharama zake.

Amesema, barabara ya Sekenke- Selui inachunguzwa ili aliyesababisha ijengwe chini ya kiwango awajibike.

Amebainisha kwamba, kwa kawaida barabara za lami, baada ya kukamilika kujengwa huwa chini ya uangalizi kwa mwaka mmoja lakini sasa Serikali imeongeza hadi miaka mitatu, na barabara za changarawe zinakuwa kwenye uangalizi kwa miezi sita.

Dk. Mwakyembe ameyasema hayo wakati anajibu swali la nyongeza la Mbunge wa Chonga, Haroub Mohammed Shamis aliyetaka kufahamu kauli ya Serikali baada ya Waziri wa Ujenzi, John Magufuli kuikataa barabara ya kutoka Mivinjeni hadi Mbagala kwa maelezo kuwa imejengwa chini ya kiwango.

Mbunge huyo pia alisema, kwa kuwa bidhaa zinazokuwa chini ya kiwango huchomwa moto na nyingine hupondwa na tingatinga, je barabara zinazokuwa chini ya kiwango hufanywaje?

Awali Mbunge huyo aliuliza, ni vigezo gani vinavyotumika kumpata mshauri huyo wa ufundi na ni kwa nini baadhi ya miradi inaharibika mara tu baada kukabidhiwa.

Dk. Mwakyembe amewaeleza wabunge kuwa, kazi ya ujenzi wa miradi ya barabara inahitaji maandalizi yanayohusisha upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na tathimini ya athari kwa mazingira na kijamii.

“Aidha, wakati wa ujenzi unahitajika usimamizi thabiti ili kukidhi ubora kulingana na usanifu wa viwango vilivyoko kwenye mkataba” amesema Mwakyembe.

Ametaja vigezo vya kumpata Mhandisi Mshauri kuwa ni pamoja na uzoefu wa kampuni ya ushauri wa kulinganisha na mradi husika, uzoefu wa kiwango cha elimu kwa wataalamu wanaohitajika kufanya kazi husika, na gharama iliyopendekezwa na mshauri kwa ajili ya kufanya kazi husika.

“Barabara inaweza kuharibika mapema baada ya ujenzi kutokana na mkandarasi kujenga barabara chini ya ubora katika viwango vilivyowekwa na Mhandishi Mshauri kukosa umakini katika kusimamia na kudhibiti ubora wa kazi wakati wa ujenzi. Aidha, usanifu hafifu wa barabara husika nao unaweza kuwa sababu” amesema.

Monday, August 8, 2011

JK amuangukia Rostam

Rais Kikwete na Rostam Aziz

RAIS Jakaya Kikwete sasa anapanga kumuangukia aliyekuwa Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz, MwanaHALISI limeelezwa.

Taarifa kutoka ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) zinasema tayari chama hicho kimepanga kumuita Rostam katika mkutano wa Kamati Kuu (CC) uliopangwa kufanyika 30 Julai 2011 kwa lengo la kumwangukia.

Kada mmoja wa chama hicho aliye karibu na Rostam anasema kumekuwapo na shinikizo kutoka kwa baadhi ya viongozi wajuu wa CCM na serikali wakitaka Rais Kikwete awasiliane na Rostam ili amwombe kuhudhuria kikao cha CC kwa lengo la kumwomba msamaha ili hatimaye asaidie kampeni za uchaguzi mdogo katika jimbo la Igunga utakapotangazwa.

“Ni kweli kuna mpango wa kumuita katika Kamati Kuu. Lengo ni kumuomba atusaidie kufanikisha kampeni za Igunga, ambako kwa kweli CCM kinakabiliwa na kibarua kigumu kutetea kiti hicho kutokana na kutokuwa na maandalizi ya uchaguzi katika kipindi hiki,” ameeleza mtoa taarifa wa gazeti hili.

Kuibuka kwa taarifa hizi kumekuja wiki mbili baada ya mwanasiasa huyo kujiuzulu nyadhifa zake zote za uongozi ndani ya chama hicho kwa madai ya kuchoshwa na siasa uchwara. Mara baada Rostam kujivua nyadhifa hizo na kuandika barua kwa Spika wa Bunge la Jamhuri Anne Makinda na Rais Kikwete, akiwataarifu uamuzi wake huo aliokwishautangaza mbele ya vyombo vya habari, aliondoka nchini kuelekea Uswisi kwa kile kilichoitwa “safari ya mapumziko.”

Rostam aliondoka tarehe 14 Julai 2011 saa 10.40 alasiri, kwa ndege Na. EK 725 ya Shirika la Ndege la Emirates la Nchi za Falme za Kiarabu, siku moja baada ya kutangaza kujiuzulu ubunge na ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya chama chake.

Kiongozi mmoja wa ngazi ya juu ndani ya CCM aliliambia gazeti hili: “Uamuzi wa Rostam kuachia nafasi zake zote za uongozi umelenga kupeleka ujumbe maalum kwa Rais Kikwete, kwamba hakufurahishwa na hatua yake ya kumtumia Nape Nnauye kumshambulia yeye na wenzake majukwaani.”

Rostam alikuwa mbunge wa Igunga, mkoani Tabora tangu mwaka 1994 na mjumbe wa NEC kwa vipindi viwili.

Hata hivyo, habari zinasema hata kama mkakati wa kumuita kada huyo kwenye CC utashindwa kufanikiwa, Rais Kikwete ataendelea kumuomba asaidie kampeni za uchaguzi mdogo wa Igunga.

Tayari Makinda ameijulisha Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kujiuzulu kwa Rostam, na hivyo kuwapo uwezekano mkubwa wa kufanyika uchaguzi wa jimbo hilo ndani ya kipindi cha miezi mitatu ijayo.

MwanaHALISI limenukuu vyanzo kadhaa vya taarifa, akiwamo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano ya Umma), Steven Wasira, akitaka Rostam aitwe kusaidia kampeni za CCM. Wasira, ambaye alikuwa mstari wa mbele kutaka Rostam aondoke kwenye chama hicho, alimweleza mjumbe mmoja wa NEC, siku moja baada ya Rostam kujiuzulu, “…Kama tunataka kushinda Igunga, sharti tumuombe Rostam atusaidie. Nimeongea naye na amekubali kusaidia kampeni za Igunga.”

Hata hivyo, wachambuzi wa mambo ya kisiasa wanasema hatua ya CCM kutaka kumuangukia mwanasiasa huyu anayekabiliwa na tuhuma za ufisadi kutazidi kukichafua chama hicho mbele ya wananchi na jumuiya ya kimataifa.

Hata hivyo, zipo taarifa kuwa Rostam hataki kabisa kujihusisha na uchaguzi mdogo wa Igunga. Inaeleweka kuwa ndiye amekuwa nguzo ya CCM mkoani Tabora, kwa kutumia ushawishi wake na nguvu ya kipesa kuhakikisha wapinzani hawapiti.

Hofu ya makada na viongozi wa CCM inatokana na ukweli kwamba Rostam aliwashtukiza, kwani walipokuwa wakimtaka aondoke kwenye NEC, hawakutarajia kwamba angejiondoa kwenye ubunge.
Kutokana na hali hiyo, sasa wameanza kushikwa na ‘kigugumizi’ cha kuwachukulia hatua makada wengine wawili, Edward Lowassa na Andrew Chenge ambao, kama Rostam, wamekuwa wanashambuliwa na kuambiwa waondoke, kama njia ya utekelezaji wa dhana ya kujivua gamba.

Lowassa na Chenge wanadai Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, anatumia vibaya dhana hiyo kuwashambulia. Habari zinasema Lowassa hatafuata nyayo za Rostam za kuachia ngazi, lakini kama chama kitaamua kumfukuza atajivua nafasi zote za uongozi ndani ya chama hicho, ukiwamo ubunge wa Monduli.
Iwapo hilo litatokea, CCM kitakuwa kimejiingiza katika mgogoro kama wa Igunga.

Kwa uchache, habari zinasema wabunge tisa wakiwamo waziri mmoja na manaibu mawaziri wawili wameapa kumfuata Lowassa. Majina ya mawaziri na manaibu mawaziri hao tunayahifadhi kwa sasa.

Wakati Lowassa akiapa kutoachia ngazi, habari zinasema CCM inajiandaa kumlazimisha ajiuzulu. Aliyepangwa kuendesha kampeni ya kusimamia hatua hiyo ni Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa Msuya.
Hata hivyo, wapo wanaodai iwapo Lowassa ataondolewa kwenye uongozi kutaibuka mgogoro ndani ya Bunge kwani ana ushawishi mkubwa miongoni mwa wabunge wengi wa CCM. Baadhi ya maswahiba zake ni wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya Bunge. Kwa sasa Lowassa yuko safarini nje ya nchi kikazi. Anatarajiwa kurejea nchini kabla ya vikao vya chama vinavyotarajia kumjadili.

Wakati hayo yakitendeka, mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Vijana (UV-CCM), uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita mjini Dodoma, ulimalizika kwa wajumbe wa pande za Lowassa na Kikwete kushambuliana. Wakati kundi la Kikwete likitaka chama kichukue hatua kwa kupongeza maamuzi ya NEC ya kujivua gamba, upande wa Lowassa ulipinga kwa madai kuwa dhana ya kujivua gamba imetafsiriwa vibaya, na inakiangamiza chama.

Mtoa taarifa aliyekuwa ndani ya mkutano huo amemweleza mwandishi wa habari hizi kuwa mvutano huo uliishia kwa wajumbe “kumshambulia” kwa maneno makali Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama.
Miongoni mwa wengi, mjumbe wa Baraza Kuu, John Nchimbi, alinukuliwa akimweleza Mukama amejiingiza katika vita ya makundi bila ya kujua.

“Umekuja hapa kuponda kauli ya Mheshimiwa Lowassa juu ya serikali kushindwa kufanya maamuzi magumu, ukatoa mfano wa kesi ya City Water. Umesema kesi ile imegharimu serikali Sh.9 bilioni zikiwa gharama za kulipa wanasheria. Lakini mbona hukusema kiasi ambacho serikali imelipwa kutokana na kushinda shauri hilo mahakamani?” alihoji Nchimbi kwa sauti ya ukali.

Alisema, “Acheni unafiki. Mtaangamiza chama. Kama wewe ni mkweli, mbona hujasema kama serikali ilishinda kesi ile na imelipwa mamilioni ya shilingi? Au kwa sababu, Mheshimiwa Lowassa amesema serikali haifanyi maamuzi magumu?”

Nchimbi pia alisema Nape ni “mropokaji” anayevuruga chama.
Wengine walioshupaliwa kwa kuchangia kukidhoofisha chama ni Samwel Sitta na Dk. Harrison Mwakyembe ambao ni miongoni mwa waasisi wa Chama cha Jamii (CCJ) huku wakiwa bado viongozi na wanachama wa CCM. Hata hivyo, CCJ kilinyimwa usajili wa kudumu.
Aliyetoa hoja hiyo ni Hussen Bashe ambaye anajitambulisha ni kutoka kundi la Lowassa na Rostam. Habari zinasema kwamba Mukama alimwita Bashe na kumwomba agombee ubunge Igunga, lakini Bashe alimgomea kwa maelezo kuwa hana mizizi ya kisiasa katika jimbo hilo.
“Nilitaka ubunge wa Nzega, si Igunga. Huko si kwetu. Siwezi kwenda Igunga kwa sababu nataka mshindwe ili tuheshimiane,” Bashe alinukuliwa akimweleza Mukama.

Vile vile, vijana hao walimtaka Mukama aagize serikali imwondoe Sitta katika nyumba ya spika, kwa maelezo kwamba kitendo chake kung’ang’ania nyumba hiyo huku akijua alishaachia uspika ni kinyume cha utaratibu, na kinagombanisha wananchi na serikali yao.

Wednesday, June 8, 2011

LEO NI BAJETI

Mawaziri wapigia debe bajeti 

MACHO na masikio ya mamilioni ya Watanzania na wadau wa nje, leo yanaelekezwa Dodoma ambako Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2011/12 itasomwa. Wananchi wengi wamekuwa na shauku ya kujua mwelekeo wa bajeti hiyo hasa katika kipindi hiki ambacho wanakabiliwa na hali ngumu ya maisha iliyotokana na kupanda kwa bei vyakula na bidhaa za mafuta.

Kwa takriban wiki nzima iliyopita, baadhi ya wananchi wamekuwa wakituma ujumbe mfupi wa maandishi kwa simu katika vyombo vya habari, wakiisihi serikali kuhakikisha kuwa bajeti ya mwaka huu inawaondoa katika hali ngumu ya maisha.

Bajeti hiyo itakayosomwa bungeni na Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo itatangazwa kwa wakati mmoja na bajeti za serikali za nchi zote za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), katika mtazamo wa kuimarisha mshimakano na umoja wa nchi hizo.

Kwa kawaida na mazoea ya muda mrefu, bajeti ya serikali imekuwa ikisomwa siku za Alhamisi ya wiki ya kwanza ya Juni, lakini mwaka huu imebadilika ikielezwa kwamba hiyo ni kutokana na siku hiyo kuangukia siku ya Uhuru wa Uganda.

Akizungumza bungeni jana asubuhi, Spika wa Bunge, Anne Makinda alisema bajeti hiyo itatanguliwa na hotuba ya hali ya uchumi itakayosomwa pia na Waziri Mkulo. Alisema hotuba hiyo itasomwa asubuhi, wakati ile ya bajeti itasomwa jioni.

Baadhi ya mawaziri akiwamo Mkulo wameifagilia bajeti hiyo huku Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania (CTI) likitoa mapendekezo na matumaini yake.

CTI: Tunataka bajeti ya uchumi wa viwanda

Shirikisho hilo limesema kuwa linaisubiri kwa hamu bajeti hiyo likitaka iwe ya kukuza uchumi na kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji. Kauli ya CTI huku likilalamikia kupanda kwa gharama za uzalishaji zilizotokana na mgawo wa umeme wa Tanesco.

Mkurugenzi Mtendaji wa CTI, Christine Kilindu alisema jana kwamba serikali inapaswa kutoa bajeti ambayo pia itaondoa kodi zinazoumiza uzalishaji mkubwa. Alisema kodi kubwa zisizo za msingi zinachangia kupanda kwa gharama za uzalishaji ambao mwishowe husababisha kupanda kwa gharama za maisha kwa mwananchi wa kawaida. 

"Tunataka bajeti ambayo itaondoa kodi zinazokwamisha uzalishaji mkubwa na ukuaji uchumi, tunataka bajeti itakayopunguza makali ya maisha kwa mwananchi kwa kumwezesha kupata bidhaa kwa urahisi," alisema Kilindu.

Alisema bajeti hiyo inapaswa pia kuweka mazingira mazuri na yanavyovutia kibiashara ili kuifanya Tanzania kuwa kituo muhimu cha uwekezaji. Alisema kwamba anategemea kuona umeme ukiwekewa mazingira ya kukuza uchumi na uwekezaji nchini, akisema bila kufanya hivyo hakuna kitu kitakachofanyika.

"Bila umeme hakuna kitu chochote, serikali inapaswa kuongeza nguvu na msukumo kuona umeme siyo tu unamulika maisha ya watu kwa kutoa mwanga, bali iwe ni nguvu ya kusukuma ukuaji wa uchumi wa nchi."

Mawaziri wapigia debe bajeti

Katika kujiwekea mazingira mazuri na kuzuia kubanwa na wabunge, baadhi ya mawaziri wamepigia debe bajeti za wizara zao huku Mkulo, akiahidi kuwa malimbikizo ya vyombo vya usalama yatalipwa mwezi huu.

Mara kwa mara baadhi ya wabunge wamekuwa wakitishia kukwamisha baadhi ya bajeti za wizara, kutokana na kukosa majibu ya msingi kwa mambo mbalimbali ya msingi. Jana asubuhi baadhi ya mawaziri walipokuwa wakijibu maswali bungeni walisisitiza kuwa mambo mengi waliyokuwa wakiulizwa yamezingatiwa katika bajeti.

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Balozi Hamis Kagasheki, akijibu swali kuhusu malipo ya malimbikizo ya posho za polisi ikiwamo za wakati wa uhamisho, alisema wizara yake imeandaa mwongozo wa kisera wa namna ya kulipatia ufumbuzi tatizo hilo.Alisema katika mwongozo huo ambao tayari ulikubaliwa na Wizara ya Fedha na Uchumi, wizara yake imejipangia utaratibu wa kutatua kero hiyo kuanzia kwenye bajeti ya mwaka huu.

Balozi Kagasheki alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Mji Mkongwe (CUF), Mohammed Sanya, ambaye alitaka kujua mkakati huo ukoje kutokana na tatizo hilo kuwa ni la muda mrefu. Baada ya majibu hayo, Waziri Mkulo alisimama na kukuongeza kuwa siyo malimbikizo ya polisi pekee, bali ya vyombo vyote vya usalama na kwamba serikali imejipanga kuhakikisha yanalipwa kabla ya mwezi huu kumalizika.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk Harrison Mwakyembe naye alipigia debe bajeti ya wizara yake ambayo tayari ilisifiwa na Kamati ya Bunge ya Miundombinu, kutokana na kugusa kila eneo huku ikitajwa kuandaliwa kwa weledi wa hali ya juu.

Akijibu maswali likiwamo lililohusu ujenzi wa Barabara ya Babati, Dareda hadi Minjingu na kuhusu kero za barabara katika Jimbo la Ludewa linaloongozwa na Profesa Raphael Mwalyosi, Naibu Waziri huyo alisisitiza kuwa wizara yake ni sikivu na mambo mengi yatazingatiwa ndani ya bajeti.

Alisema wizara iko makini na Bajeti ya Ujenzi imezingatia mambo mengi ya msingi huku akitupa kete ya kuomba uungwaji mkono kwa wabunge ili waipitishe.