Showing posts with label mukama. Show all posts
Showing posts with label mukama. Show all posts

Monday, August 8, 2011

JK amuangukia Rostam

Rais Kikwete na Rostam Aziz

RAIS Jakaya Kikwete sasa anapanga kumuangukia aliyekuwa Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz, MwanaHALISI limeelezwa.

Taarifa kutoka ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) zinasema tayari chama hicho kimepanga kumuita Rostam katika mkutano wa Kamati Kuu (CC) uliopangwa kufanyika 30 Julai 2011 kwa lengo la kumwangukia.

Kada mmoja wa chama hicho aliye karibu na Rostam anasema kumekuwapo na shinikizo kutoka kwa baadhi ya viongozi wajuu wa CCM na serikali wakitaka Rais Kikwete awasiliane na Rostam ili amwombe kuhudhuria kikao cha CC kwa lengo la kumwomba msamaha ili hatimaye asaidie kampeni za uchaguzi mdogo katika jimbo la Igunga utakapotangazwa.

“Ni kweli kuna mpango wa kumuita katika Kamati Kuu. Lengo ni kumuomba atusaidie kufanikisha kampeni za Igunga, ambako kwa kweli CCM kinakabiliwa na kibarua kigumu kutetea kiti hicho kutokana na kutokuwa na maandalizi ya uchaguzi katika kipindi hiki,” ameeleza mtoa taarifa wa gazeti hili.

Kuibuka kwa taarifa hizi kumekuja wiki mbili baada ya mwanasiasa huyo kujiuzulu nyadhifa zake zote za uongozi ndani ya chama hicho kwa madai ya kuchoshwa na siasa uchwara. Mara baada Rostam kujivua nyadhifa hizo na kuandika barua kwa Spika wa Bunge la Jamhuri Anne Makinda na Rais Kikwete, akiwataarifu uamuzi wake huo aliokwishautangaza mbele ya vyombo vya habari, aliondoka nchini kuelekea Uswisi kwa kile kilichoitwa “safari ya mapumziko.”

Rostam aliondoka tarehe 14 Julai 2011 saa 10.40 alasiri, kwa ndege Na. EK 725 ya Shirika la Ndege la Emirates la Nchi za Falme za Kiarabu, siku moja baada ya kutangaza kujiuzulu ubunge na ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya chama chake.

Kiongozi mmoja wa ngazi ya juu ndani ya CCM aliliambia gazeti hili: “Uamuzi wa Rostam kuachia nafasi zake zote za uongozi umelenga kupeleka ujumbe maalum kwa Rais Kikwete, kwamba hakufurahishwa na hatua yake ya kumtumia Nape Nnauye kumshambulia yeye na wenzake majukwaani.”

Rostam alikuwa mbunge wa Igunga, mkoani Tabora tangu mwaka 1994 na mjumbe wa NEC kwa vipindi viwili.

Hata hivyo, habari zinasema hata kama mkakati wa kumuita kada huyo kwenye CC utashindwa kufanikiwa, Rais Kikwete ataendelea kumuomba asaidie kampeni za uchaguzi mdogo wa Igunga.

Tayari Makinda ameijulisha Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kujiuzulu kwa Rostam, na hivyo kuwapo uwezekano mkubwa wa kufanyika uchaguzi wa jimbo hilo ndani ya kipindi cha miezi mitatu ijayo.

MwanaHALISI limenukuu vyanzo kadhaa vya taarifa, akiwamo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano ya Umma), Steven Wasira, akitaka Rostam aitwe kusaidia kampeni za CCM. Wasira, ambaye alikuwa mstari wa mbele kutaka Rostam aondoke kwenye chama hicho, alimweleza mjumbe mmoja wa NEC, siku moja baada ya Rostam kujiuzulu, “…Kama tunataka kushinda Igunga, sharti tumuombe Rostam atusaidie. Nimeongea naye na amekubali kusaidia kampeni za Igunga.”

Hata hivyo, wachambuzi wa mambo ya kisiasa wanasema hatua ya CCM kutaka kumuangukia mwanasiasa huyu anayekabiliwa na tuhuma za ufisadi kutazidi kukichafua chama hicho mbele ya wananchi na jumuiya ya kimataifa.

Hata hivyo, zipo taarifa kuwa Rostam hataki kabisa kujihusisha na uchaguzi mdogo wa Igunga. Inaeleweka kuwa ndiye amekuwa nguzo ya CCM mkoani Tabora, kwa kutumia ushawishi wake na nguvu ya kipesa kuhakikisha wapinzani hawapiti.

Hofu ya makada na viongozi wa CCM inatokana na ukweli kwamba Rostam aliwashtukiza, kwani walipokuwa wakimtaka aondoke kwenye NEC, hawakutarajia kwamba angejiondoa kwenye ubunge.
Kutokana na hali hiyo, sasa wameanza kushikwa na ‘kigugumizi’ cha kuwachukulia hatua makada wengine wawili, Edward Lowassa na Andrew Chenge ambao, kama Rostam, wamekuwa wanashambuliwa na kuambiwa waondoke, kama njia ya utekelezaji wa dhana ya kujivua gamba.

Lowassa na Chenge wanadai Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, anatumia vibaya dhana hiyo kuwashambulia. Habari zinasema Lowassa hatafuata nyayo za Rostam za kuachia ngazi, lakini kama chama kitaamua kumfukuza atajivua nafasi zote za uongozi ndani ya chama hicho, ukiwamo ubunge wa Monduli.
Iwapo hilo litatokea, CCM kitakuwa kimejiingiza katika mgogoro kama wa Igunga.

Kwa uchache, habari zinasema wabunge tisa wakiwamo waziri mmoja na manaibu mawaziri wawili wameapa kumfuata Lowassa. Majina ya mawaziri na manaibu mawaziri hao tunayahifadhi kwa sasa.

Wakati Lowassa akiapa kutoachia ngazi, habari zinasema CCM inajiandaa kumlazimisha ajiuzulu. Aliyepangwa kuendesha kampeni ya kusimamia hatua hiyo ni Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa Msuya.
Hata hivyo, wapo wanaodai iwapo Lowassa ataondolewa kwenye uongozi kutaibuka mgogoro ndani ya Bunge kwani ana ushawishi mkubwa miongoni mwa wabunge wengi wa CCM. Baadhi ya maswahiba zake ni wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya Bunge. Kwa sasa Lowassa yuko safarini nje ya nchi kikazi. Anatarajiwa kurejea nchini kabla ya vikao vya chama vinavyotarajia kumjadili.

Wakati hayo yakitendeka, mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Vijana (UV-CCM), uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita mjini Dodoma, ulimalizika kwa wajumbe wa pande za Lowassa na Kikwete kushambuliana. Wakati kundi la Kikwete likitaka chama kichukue hatua kwa kupongeza maamuzi ya NEC ya kujivua gamba, upande wa Lowassa ulipinga kwa madai kuwa dhana ya kujivua gamba imetafsiriwa vibaya, na inakiangamiza chama.

Mtoa taarifa aliyekuwa ndani ya mkutano huo amemweleza mwandishi wa habari hizi kuwa mvutano huo uliishia kwa wajumbe “kumshambulia” kwa maneno makali Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama.
Miongoni mwa wengi, mjumbe wa Baraza Kuu, John Nchimbi, alinukuliwa akimweleza Mukama amejiingiza katika vita ya makundi bila ya kujua.

“Umekuja hapa kuponda kauli ya Mheshimiwa Lowassa juu ya serikali kushindwa kufanya maamuzi magumu, ukatoa mfano wa kesi ya City Water. Umesema kesi ile imegharimu serikali Sh.9 bilioni zikiwa gharama za kulipa wanasheria. Lakini mbona hukusema kiasi ambacho serikali imelipwa kutokana na kushinda shauri hilo mahakamani?” alihoji Nchimbi kwa sauti ya ukali.

Alisema, “Acheni unafiki. Mtaangamiza chama. Kama wewe ni mkweli, mbona hujasema kama serikali ilishinda kesi ile na imelipwa mamilioni ya shilingi? Au kwa sababu, Mheshimiwa Lowassa amesema serikali haifanyi maamuzi magumu?”

Nchimbi pia alisema Nape ni “mropokaji” anayevuruga chama.
Wengine walioshupaliwa kwa kuchangia kukidhoofisha chama ni Samwel Sitta na Dk. Harrison Mwakyembe ambao ni miongoni mwa waasisi wa Chama cha Jamii (CCJ) huku wakiwa bado viongozi na wanachama wa CCM. Hata hivyo, CCJ kilinyimwa usajili wa kudumu.
Aliyetoa hoja hiyo ni Hussen Bashe ambaye anajitambulisha ni kutoka kundi la Lowassa na Rostam. Habari zinasema kwamba Mukama alimwita Bashe na kumwomba agombee ubunge Igunga, lakini Bashe alimgomea kwa maelezo kuwa hana mizizi ya kisiasa katika jimbo hilo.
“Nilitaka ubunge wa Nzega, si Igunga. Huko si kwetu. Siwezi kwenda Igunga kwa sababu nataka mshindwe ili tuheshimiane,” Bashe alinukuliwa akimweleza Mukama.

Vile vile, vijana hao walimtaka Mukama aagize serikali imwondoe Sitta katika nyumba ya spika, kwa maelezo kwamba kitendo chake kung’ang’ania nyumba hiyo huku akijua alishaachia uspika ni kinyume cha utaratibu, na kinagombanisha wananchi na serikali yao.

Saturday, July 16, 2011

Lowassa aweka mambo hadharani

MBUNGE wa Monduli, Edward Lowassa, amesema atatangaza uamuzi kuhusu nyadhifa zake ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), wakati muafaka ukifika. Amesema ameshitushwa na kitendo cha aliyekuwa mbunge wa Igunga, Rostam Aziz, kutangaza kuachia nafasi hiyo na ya ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM.

Lowassa aliyewahi kuwa waziri mkuu wa Serikali ya Muungano, alisema hayo baada ya kutakiwa kutoa maoni kuhusu uamuzi wa Rostam kujiuzulu nyadhifa hizo. "Ninachoweza kusema ni kuwa, Rostam kujiuzulu ni haki yake lakini nimeshituka kuona amejiuzulu na ubunge. Nimeguswa pia na wananchi wake walivyopokea uamuzi huo," alisema. Rostam akitangaza uamuzi wa kuachia ngazi juzi, alisema amefikia uamuzi huo ili kulinda maslahi ya Chama. Kwa upande wake, Lowassa alipoulizwa ana mpango gani wa yeye kujiuzulu alisema: "Nitazungumza wakati muafaka ukifika."

Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama, kwa upande wake alisema kwa kufuata utaratibu wa kawaida ndani ya Chama, hakina taarifa za kujiuzulu Rostam. Hata hivyo, alisema jambo hilo litazungumzwa katika vikao vya juu vya Chama na baadaye taarifa zitatolewa.  "Chama hakina taarifa yoyote, tumeona kwenye vyombo vya habari ametangaza kujiuzulu kwake akiwa Igunga," alisema Mukama na kuongeza kuwa, CCM bado inalihitaji jimbo la Igunga.

Naye mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (CHADEMA), aliibuka bungeni na kuomba muongozo wa Spika Anne Makinda, akitaka atangaze kuwa jimbo la Igunga lipo wazi. Spika Anne alisema hana taarifa rasmi kuhusu kujiuzulu kwa Rostam, na kama ilivyo kwa wengine ameona habari hizo kwenye mitandao.
"Sisi tuna taratibu zetu, Rostam hajaniandikia barua, tutatoa taarifa wakati muafaka utakapowadia," alisema. Katika hatua nyingine, wanasiasa na wasomi nchini wameendelea kuwa na maoni tofauti kuhusu uamuzi wa Rostam, wengine wakipongeza hatua hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti , walisema uamuzi huo ni mzuri ingawa umechelewa.  Mwenyekiti wa TLP na mbunge wa Vunjo, Augustino Mrema, alisema Rostam amechukua uamuzi mzuri. “Ni uamuzi mzuri ingawa amechelewa,  hasa kutokana na tuhuma zake kuwa za muda mrefu,’’ alisema. Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Hajji Semboja, alisema Rostam anapaswa kupigiwa mfano na wafanyabiashara wengine.
“Ni sawa tu kuondoka, nina hakika CCM haiwezi kuyumba, ikizingatiwa kuwa wameondoka wakongwe kama hayati Julius Nyerere na Mzee Rashidi Kawawa na CCM bado ipo,’’ alisema. Alisema CCM ni chama chenye wanachama wengi, hivyo kinachopaswa kufanyika ni kwa wafanyabiashara wengine kujitoa na kuwaachia watu wa siasa.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Mohamed Bakari, alisema CCM inapaswa kuwa makini kutokana na Rostam kushika nafasi kubwa, hivyo ni lazima alikuwa na wafuasi. “Suala hili ni kubwa na lina faida na hasara, hivyo kinachotakiwa ni kujipanga vyema ili kuepusha matatizo yatakayoweza kujitokeza baadaye,’’ alisema.

Wednesday, June 15, 2011

CCM WAFUTA POSHO ZA VIKAO


HOJA ya kutaka kufutwa kwa posho za vikao za wabunge na watumishi wengine wa umma imechukua sura mpya baada ya jana Mbunge wa Bumbuli (CCM), Januari Makamba kuliambia Bunge mjini hapa kuwa suala la kufutwa kwa posho ni la kitaifa na ni sehemu ya Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano uliowasilishwa na serikali.

Kauli hiyo ya Makamba ambaye pia ni Katibu wa Mambo ya Nje wa Sekretarieti ya CCM imekuja huku kukiwa na malumbano makali baina ya Spika wa Bunge, Anne Makinda na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe kuhusu suala hilo la posho za vikao vya wabunge.

Juzi, Spika Makinda alisema Zitto ambaye ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, anaweza kufukuzwa ubunge kwa kutosaini karatasi za mahudhurio, hatua ambayo Zitto alisema ataichukua ili asilipwe posho za vikao.

Spika alisema Zitto anaweza kukumbwa na adhabu hiyo iwapo hatasaini karatasi za mahudhurio ambazo ndizo zinathibitsha uwepo wa mbunge katika mikutano na vikao vya bunge na kwamba kanuni zinamwadhibu mbunge kwa kumfukuza asipohudhuria mikutano mitatu. Hata hivyo, Zitto amepuuza kauli hiyo ya Spika kwa kusema kwamba kama ni kwa ajili ya kukataa posho, yuko tayari kufukuzwa bungeni.

"Nitafanya hivyo tuone, Kanuni inasema mikutano mitatu mfululizo na siyo vikao vitatu mfululizo. Nitatumia uzoefu wangu wa siasa za wanafunzi kukwepa mtego wake. Lakini kama anadhani ni sawa kunifukuza ubunge kwa kukataa posho, nipo tayari," alisema.

Kauli ya jana ya Makamba pia inaonekana kutofautina na mawazo ya wabunge wengi wa CCM akiwamo Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo ambaye amesema wanashabikia suala hilo wanajitafutia umaarufu.

Akichangia huo wa maendeleo wa miaka mitano jana, Makamba alionekana kupigia chapuo suala la kufutwa au kuangaliwa upya kwa posho za vikao huku akisema kwamba ni la kitaifa na ni sehemu ya mpango huo.

Makamba alisema kuwa suala la nidhamu na usimamizi wa matumizi ya fedha za umma ni muhimu na kwamba mpango huo umeliona katika ukurasa wa 17 wa kitabu kilichochapishwa kwa Kiingereza na kutoa mapendekezo ya kufutwa kwa posho za vikao na zile za usafiri.

"Mpango unabainisha kwamba kuna umuhimu wa kufutwa kwa posho za vikao na usafiri hivyo iwapo wabunge mtalisikia likiwasilishwa hapa kwa mbwembwe kesho (leo), basi msije mkashangaa kwani ni sehemu ya mpango huu," alisema Makamba.

Kujadiliwa bungeni leo

Mjadala kuhusu malipo ya posho ambao umekuwa ukiendelea kwa wiki moja sasa hasa zaidi nje ya Bunge, leo unatarajiwa kuingizwa rasmi bungeni wakati Bajeti ya Serikali iliyowasilishwa na Mkulo Jumatano iliyopita itakapoanza kujadiliwa.

Suala hilo ni dhahiri litajitokeza katika bajeti mbadala itakayowasilishwa na kambi ya Upinzani Bungeni na Waziri Kivuli wa Fedha, Zitto Kabwe ambaye amekuwa katika mvutano usio rasmi na Spika kutokana na kukataa kulipwa posho za kikao.

Mwenyekiti wa Chadema ambaye pia ni Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe alisema jana kuwa kambi yake inatarajiwa kutoa ushauri mgumu ambao haujazoeleka kwa watendaji wa serikali na kwamba suala la kufutwa kwa posho ni sehemu ya mapendekezo hayo.

Alisema kufutwa kwa posho hizo kunaweza kuokoa zaidi ya Sh900 bilioni ambazo zinaweza kuelekezwa katika maeneo mengine ya huduma kwa wananchi.

Uhalisia posho za wabunge

Mmoja wa wabunge wa CCM ambaye hakutaka kutaandikwa jina lake alisema anasikia kuhukumiwa katika nafsi yake kutokana na kupokea posho za vikao ambazo kimsingi ni sawa na "kuwaibia wananchi".

"Ujue bwana sisi ndani ya CCM mambo hayaendi kama kwa wenzetu (Chadema), wale wanaweza kukaa leo na kuamua, sisi ni tofauti lazima kuwepo na mchakato lakini ukweli ni kwamba hoja yao ni nzuri," alisema mbunge huyo.

Uchunguzi uliofanywa umebaini kuwa malipo ya wabunge yamegawanyika katika sehemu nne ambazo ni pamoja na mshahara ambao ni Sh2,300,000 kwa mwezi, posho ya ubunge kila mwezi ambayo ni Sh5 milioni, posho ya kujikimu (per-diem) Sh80,000 wawapo nje ya majimbo yao kikazi na posho ya vikao (sitting allowance) ambayo huwa ni Sh70,000 kwa kila mbunge.

Kwa maana hiyo, kwa kawaida mbunge hulipwa Sh7.3 milioni kila mwezi kabla ya kukatwa kodi na wawapo Dodoma na Dar es Salaam kwa ajili ya vikao vya kamati na bunge au mikoani kwa ajili ya kukagua shughuli zilizopo chini ya kamati zao. Hulipwa kiasi cha Sh150,000 kila mmoja kwa siku ambazo ni Sh70,000 kwa ajili ya vikao na Sh80,000 kwa ajili ya kujikimu.

Kwa maana hiyo bunge linatarajiwa kutumia kiasi cha Sh1.788 bilioni kwa ajili ya kugharamia vikao 73 vya Bunge la Bajeti iwapo wabunge wote 350 waliopo watahudhuria vikao hivyo.

Kwa hesabu hizo, kila mbunge katika mkutano wa Bunge la Bajeti anatarajiwa kuondoka na kikita cha Sh5.1 milioni mbali na Sh 5.58 milioni ambazo ni malipo kwa ajili ya kujikimu, fedha ambazo ni mbali na mshahara wake kwa mwezi na posho ya ubunge.

CCM yakataa posho

Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeanza machakato wa kufuta posho hizo ikiwa ni hatua ya kupunguza matumizi yasiyo ya lazima. Habari kutoka ndani ya CCM, Dodoma na Dar es Salaam zinasema kuwa mkakati wa kufutwa kwa posho ulianzishwa takriban mwezi mmoja uliopita na sekretarieti mpya inayoongozwa na Katibu Mkuu, Wilson Mukama.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, baadhi ya wajumbe wa sekretarieti walihoji uhalali wa posho wanazolipwa hata pale vikao vinapofanyika katika sehemu ambako ni makazi yao na kwamba hoja hizo ndizo zilizozaa wazo la kufutwa kwa posho katika vikao.

"Hoja ilikuwa kwamba kama chama hakina fedha na tunataka kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, basi posho za vikao zifutwe kwa sababu hakuna ulazima wa posho hizo hasa kwa wajumbe wa sekretarieti ambao kazi zao ni za kila siku," kilieleza chanzo chetu na kuongeza:

"Hivi sasa mpango huo uko kwenye mchakato wa kuwekewa mwongozo na nadhani baada ya kupitia katika vikao vyetu utaanza kutekelezwa. Lakini kimsingi ni kama utekelezaji wake umeshaanza kwa sababu baadhi ya wajunbe wamekataa kabisa kusaini posho hizo."

Habari zaidi zinadai kuwa waraka wa mapendekezo ya kupunguza matumizi ndani ya CCM unakwenda mbali zaidi hadi katika matumizi ya magari na kwamba pale usafiri unapohitaji wa kuelekea kwenye mkutano mmoja, basi viongozi watumie magari machache kwa maana ya usafiri wa pamoja badala ya utaratibu wa sasa ambao unamruhusu kila kiongozi kutumia usafiri wake.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipoulizwa kuhusu sekretarieti kufuta posho katika vikao vyake, hakukanusha wala kuthibitisha, badala yake akadai kuwa hayo ni mambo ya ndani ya chama ambayo hayana faida yoyote kwa umma.

"Hivi ninyi waandishi wa habari, haya mambo mnayapata kwa nani! Haya ni mambo ya ndani ya chama sidhani kama yana tija yoyote kwa umma, maana haiwezi kusaidia chochote," alisema Nape kwa kwa simu.

Alipoelezwa kwamba suala hilo lina uhusiano na sakata linaloendelea bungeni, Nape alisema: "Bunge ni bunge na chama ni chama. Kila taasisi inajitegemea na ina uamuzi wake, lakini pia sisi kama chama tulishatoa kauli mara nyingi kwamba suala la posho kwa wabunge na watumishi wengine wa serikali linazungumzika, ni la kisera na wanaohusika wapo waulizeni hao."

Mwishoni mwa wiki iliyopita Nape akizungumzia malumbano miongoni mwa wabunge kuhusu suala la posho alisema suala hilo linajadilika na kwamba si vyema kulipinga kwa sababu tu linatokea kambi ya upinzani.

Kwa upande wake, Makamba alipoulizwa kuhusu kufutwa kwa posho katika vikao vya Sekretarieti ya CCM naye kama ilivyokuwa kwa Nape, hakukanusha wala kuthibitisha.

"Wewe si unamfahamu msemaji wa chama ni nani? Mwulizeni Nape tena nadhani anakuja Dodoma. Akija mwulizeni, mimi siwezi kulizungumzia.... lakini ninyi waandishi haya mambo ya ndani ya chama huwa mnayapata wapi? Anyway, mwulizeni mwenezi atawaambia," alisema Makamba.

Chanzo: Mwananchi 15/6/2011

Friday, May 27, 2011

Tamko la Vijana Arusha lazidi kuivuruga CCM

















TAMKO la baadhi ya vijana wa UVCCM, Mkoa wa Arusha kutaka mafisadi wafukuzwe, limezidi kukivuruga chama hicho baada ya Katibu Mkuu, Wilson Mukama kusema hawezi kujiingiza 'kichwa kichwa' kuzungumzia suala hilo, huku baadhi ya watuhumiwa wakikataa kulizungumzia. Mukama alisema CCM inafuatilia kwa karibu mgogoro huo, lakini haiwezi kuuzungumzia sasa kwa kuwa hajapata taarifa rasmi kutoka umoja wa vijana.

Kwa mujibu wa Mukama, UVCCM ni jumuiya halali ya chama tawala yenye mamlaka kamili ya kuzungumzia matatizo yake, hivyo yeye kusema chochote itakuwa ni kuingilia kazi za jumuiya hiyo.
“Chama chetu kina utaratibu wake, UVCCM ni jumuiya ndani yake, hayo yaliyotokea kule Arusha siwezi kuyazungumzia, ila kesho (leo) tuna kikao, hivyo wao vijana watatupa taarifa zao,” alisema Mukama, huku akisoma ujumbe mfupi wa simu (sms) alioandikiwa na katibu mkuu wa umoja huo, Martin Shigella kuwa watatoa taarifa ya yaliyotokea Arusha.

“Suala la Arusha tunalifuatilia kwa ukaribu sana, ila utendaji tunawaachia wao (UV-CCM), nasi tukishapata taarifa zao ndio tutaweza kulizungumzia suala hilo, ila kwa sasa mtafute Shigella,” alielekeza Mukama.
Alipotafutwa kwa simu jana kuzungumzia tuhuma hizo, Shigella alisema kuwa hawezi kutolea ufafanuzi kwa kuwa alikuwa nje ya nchi kikazi. “Sikuwapo nchini, kwa hiyo sitaweza kuzungumza lolote, kuna mtu alikuwa akikaimu nafasi yangu, hivyo nikipata maelezo kutoka kwake nitakuwa tayari kuzungumza, nitafute kesho (leo),”alisema Shigella.

Naye makamu mwenyekiti wa umoja huo taifa, Benno Malisa alisema wamesikitishwa na kauli zilizotolewa na vijana wenzao wa Arusha, hivyo watatuma kamati ya maadili kwenda kuzungumza na makundi yanayolumbana. “Hivi karibuni Kamati ya Utekelezaji ya UVCCM itakaa na kutoa uamuzi, lakini ni baada ya Kamati ya Maadili itakayotumwa kuzungumza na wanachama wanaolumbana huko Arusha kuleta ripoti makao makuu ya umoja wetu,”Alisema Malisa.

Akizungumzia adhabu wanazoweza kupewa wanachama wa umoja huo, Malisa alisema adhabu hizo zitatokana na aina ya makosa watakayokutwa nayo. “Suala hili liko ndani ya uwezo wetu na tutalifanyia kazi na kuchukua hatua kwa mujibu wa kanuni za UVCCM, kama kutakuwa na makosa makubwa zaidi yatapelekwa  ngazi za juu zaidi,”alisema Malisa.

Juzi, UVCCM Mkoa wa Arusha waliuomba uongozi wa juu wa chama tawala kuwafukuza uanachama viongozi watatu, wakiwamo Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa na mwenzake wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge wanaotuhumiwa kwa ufisadi.

Vijana hao pia walikishauri chama hicho kupitia kamati yake ya maadili kuwaita na kuwahoji makada hao maarufu na baadaye kuwachukulia hatua, zikiwamo za kuwafukuza kwa maslahi ya chama na taifa. Tamko hilo lililosomwa na mjumbe wa baraza la umoja huo mkoani Arusha, Ali Babu lilitaka watuhumiwa hao waliowaita mapacha watatu, kuwa ndio chanzo cha kudhoofika kwa chama hicho tawala.

"Pia, tunasisitiza Andrew Chenge aondolewe kwenye Kamati ya Maadili ya CCM mara moja na kumtaka mtuhumiwa mwingine (jina tunalo) aondolewe pia kwenye uongozi wa ndani ya umoja wetu," ilieleza sehemu ya taarifa hiyo. Lakini, alipotafutwa jana kuzungumzia tuhuma hizo, Chenge alijibu kwa ufupi: "Kwa sasa sitaki kuzungumzia masuala hayo. Kila la heri."

Naye Lowassa alipotafutwa alisema kwa ufupi: ‘no comment’ akimaanisha kuwa hawezi kulizungumzia suala hilo.

Hata hivyo, wakati makada hao wakigoma kuzungumzia suala hilo, mwenyekiti wa umoja huo Mkoa wa Arusha, James ole Milya anayeshinikizwa kujiuzulu wadhifa huo, jana aliibuka na kudai kuwa tamko hilo lilitolewa na kundi la vijana aliowaita wahuni wa mitaani na wasiokuwa na kazi.

“Wale ni wahuni, hawana chochote wala lolote, wanapenda kukaa vijiweni hawana kazi za kufanya, tuna taarifa kwamba walitumwa na baadhi ya viongozi hapa Arusha kupindisha na kuvuruga hoja za umoja wetu mkoani  Arusha,” alisema Milya

Alisema kuwa vijana hao wakiongozwa na Ali Babu hawatambuliki ndani ya umoja huo, huku akisisitiza  kwamba hoja na malalamiko yote hupitishwa katika ngazi husika ili ziweze kufanyiwa kazi na sio kuibuka na kutoa matamshi yasiyo na tija.

Millya aliendeleza msimamo wake wa kutaka Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalumu aondoke madarakani kwa madai ya kusababisha jimbo kwenda upinzani (Chadema), huku akimtaka katibu huyo asikilize kilio chao (UVCCM) cha kumtaka aondoke. Alisema kuwa endapo kiongozi huyo ataendelea kung'ang'ania nafasi yake, basi atang’olewa kwa maandamano ya vijana yasiyokuwa na kikomo ambayo yatafanywa na wanachama wa umoja huo.

“Msimamo wetu uko pale pale, Chatanda ni lazima aondoke kwa kuwa amekivuruga chama chetu, ametuchonganisha na viongozi wa dini, lakini pia amesababisha Jimbo la Arusha Mjini liangukie upinzani kwa kukimbilia Tanga kusaka ubunge wa viti maalumu kipindi cha uchaguzi,”alisisitzia Milya.

Juzi,  katika mkutano wao wenye malengo makuu sita, vijana hao wa Mkoa wa Arusha walisema wanaunga mkono falsafa ya CCM ya kujivua gamba."Tunaipongeza na kuiunga mkono Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kwa kutambua kwamba mafisadi wamechangia sana kukidhoofisha na kukipotezea mvuto chama chetu mbele ya umma wa Watanzania," ilisema taarifa hiyo na kuongeza:
"Kwa mantiki hiyo tunatamka kwa kauli moja kwamba mapacha hao watatu wa ufisadi (wakiwataja kwa majina) na vibaraka wao wafukuzwe mara moja kwa maslahi ya CCM na Watanzania."