Showing posts with label spika. Show all posts
Showing posts with label spika. Show all posts

Monday, August 8, 2011

JK amuangukia Rostam

Rais Kikwete na Rostam Aziz

RAIS Jakaya Kikwete sasa anapanga kumuangukia aliyekuwa Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz, MwanaHALISI limeelezwa.

Taarifa kutoka ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) zinasema tayari chama hicho kimepanga kumuita Rostam katika mkutano wa Kamati Kuu (CC) uliopangwa kufanyika 30 Julai 2011 kwa lengo la kumwangukia.

Kada mmoja wa chama hicho aliye karibu na Rostam anasema kumekuwapo na shinikizo kutoka kwa baadhi ya viongozi wajuu wa CCM na serikali wakitaka Rais Kikwete awasiliane na Rostam ili amwombe kuhudhuria kikao cha CC kwa lengo la kumwomba msamaha ili hatimaye asaidie kampeni za uchaguzi mdogo katika jimbo la Igunga utakapotangazwa.

“Ni kweli kuna mpango wa kumuita katika Kamati Kuu. Lengo ni kumuomba atusaidie kufanikisha kampeni za Igunga, ambako kwa kweli CCM kinakabiliwa na kibarua kigumu kutetea kiti hicho kutokana na kutokuwa na maandalizi ya uchaguzi katika kipindi hiki,” ameeleza mtoa taarifa wa gazeti hili.

Kuibuka kwa taarifa hizi kumekuja wiki mbili baada ya mwanasiasa huyo kujiuzulu nyadhifa zake zote za uongozi ndani ya chama hicho kwa madai ya kuchoshwa na siasa uchwara. Mara baada Rostam kujivua nyadhifa hizo na kuandika barua kwa Spika wa Bunge la Jamhuri Anne Makinda na Rais Kikwete, akiwataarifu uamuzi wake huo aliokwishautangaza mbele ya vyombo vya habari, aliondoka nchini kuelekea Uswisi kwa kile kilichoitwa “safari ya mapumziko.”

Rostam aliondoka tarehe 14 Julai 2011 saa 10.40 alasiri, kwa ndege Na. EK 725 ya Shirika la Ndege la Emirates la Nchi za Falme za Kiarabu, siku moja baada ya kutangaza kujiuzulu ubunge na ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya chama chake.

Kiongozi mmoja wa ngazi ya juu ndani ya CCM aliliambia gazeti hili: “Uamuzi wa Rostam kuachia nafasi zake zote za uongozi umelenga kupeleka ujumbe maalum kwa Rais Kikwete, kwamba hakufurahishwa na hatua yake ya kumtumia Nape Nnauye kumshambulia yeye na wenzake majukwaani.”

Rostam alikuwa mbunge wa Igunga, mkoani Tabora tangu mwaka 1994 na mjumbe wa NEC kwa vipindi viwili.

Hata hivyo, habari zinasema hata kama mkakati wa kumuita kada huyo kwenye CC utashindwa kufanikiwa, Rais Kikwete ataendelea kumuomba asaidie kampeni za uchaguzi mdogo wa Igunga.

Tayari Makinda ameijulisha Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kujiuzulu kwa Rostam, na hivyo kuwapo uwezekano mkubwa wa kufanyika uchaguzi wa jimbo hilo ndani ya kipindi cha miezi mitatu ijayo.

MwanaHALISI limenukuu vyanzo kadhaa vya taarifa, akiwamo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano ya Umma), Steven Wasira, akitaka Rostam aitwe kusaidia kampeni za CCM. Wasira, ambaye alikuwa mstari wa mbele kutaka Rostam aondoke kwenye chama hicho, alimweleza mjumbe mmoja wa NEC, siku moja baada ya Rostam kujiuzulu, “…Kama tunataka kushinda Igunga, sharti tumuombe Rostam atusaidie. Nimeongea naye na amekubali kusaidia kampeni za Igunga.”

Hata hivyo, wachambuzi wa mambo ya kisiasa wanasema hatua ya CCM kutaka kumuangukia mwanasiasa huyu anayekabiliwa na tuhuma za ufisadi kutazidi kukichafua chama hicho mbele ya wananchi na jumuiya ya kimataifa.

Hata hivyo, zipo taarifa kuwa Rostam hataki kabisa kujihusisha na uchaguzi mdogo wa Igunga. Inaeleweka kuwa ndiye amekuwa nguzo ya CCM mkoani Tabora, kwa kutumia ushawishi wake na nguvu ya kipesa kuhakikisha wapinzani hawapiti.

Hofu ya makada na viongozi wa CCM inatokana na ukweli kwamba Rostam aliwashtukiza, kwani walipokuwa wakimtaka aondoke kwenye NEC, hawakutarajia kwamba angejiondoa kwenye ubunge.
Kutokana na hali hiyo, sasa wameanza kushikwa na ‘kigugumizi’ cha kuwachukulia hatua makada wengine wawili, Edward Lowassa na Andrew Chenge ambao, kama Rostam, wamekuwa wanashambuliwa na kuambiwa waondoke, kama njia ya utekelezaji wa dhana ya kujivua gamba.

Lowassa na Chenge wanadai Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, anatumia vibaya dhana hiyo kuwashambulia. Habari zinasema Lowassa hatafuata nyayo za Rostam za kuachia ngazi, lakini kama chama kitaamua kumfukuza atajivua nafasi zote za uongozi ndani ya chama hicho, ukiwamo ubunge wa Monduli.
Iwapo hilo litatokea, CCM kitakuwa kimejiingiza katika mgogoro kama wa Igunga.

Kwa uchache, habari zinasema wabunge tisa wakiwamo waziri mmoja na manaibu mawaziri wawili wameapa kumfuata Lowassa. Majina ya mawaziri na manaibu mawaziri hao tunayahifadhi kwa sasa.

Wakati Lowassa akiapa kutoachia ngazi, habari zinasema CCM inajiandaa kumlazimisha ajiuzulu. Aliyepangwa kuendesha kampeni ya kusimamia hatua hiyo ni Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa Msuya.
Hata hivyo, wapo wanaodai iwapo Lowassa ataondolewa kwenye uongozi kutaibuka mgogoro ndani ya Bunge kwani ana ushawishi mkubwa miongoni mwa wabunge wengi wa CCM. Baadhi ya maswahiba zake ni wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya Bunge. Kwa sasa Lowassa yuko safarini nje ya nchi kikazi. Anatarajiwa kurejea nchini kabla ya vikao vya chama vinavyotarajia kumjadili.

Wakati hayo yakitendeka, mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Vijana (UV-CCM), uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita mjini Dodoma, ulimalizika kwa wajumbe wa pande za Lowassa na Kikwete kushambuliana. Wakati kundi la Kikwete likitaka chama kichukue hatua kwa kupongeza maamuzi ya NEC ya kujivua gamba, upande wa Lowassa ulipinga kwa madai kuwa dhana ya kujivua gamba imetafsiriwa vibaya, na inakiangamiza chama.

Mtoa taarifa aliyekuwa ndani ya mkutano huo amemweleza mwandishi wa habari hizi kuwa mvutano huo uliishia kwa wajumbe “kumshambulia” kwa maneno makali Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama.
Miongoni mwa wengi, mjumbe wa Baraza Kuu, John Nchimbi, alinukuliwa akimweleza Mukama amejiingiza katika vita ya makundi bila ya kujua.

“Umekuja hapa kuponda kauli ya Mheshimiwa Lowassa juu ya serikali kushindwa kufanya maamuzi magumu, ukatoa mfano wa kesi ya City Water. Umesema kesi ile imegharimu serikali Sh.9 bilioni zikiwa gharama za kulipa wanasheria. Lakini mbona hukusema kiasi ambacho serikali imelipwa kutokana na kushinda shauri hilo mahakamani?” alihoji Nchimbi kwa sauti ya ukali.

Alisema, “Acheni unafiki. Mtaangamiza chama. Kama wewe ni mkweli, mbona hujasema kama serikali ilishinda kesi ile na imelipwa mamilioni ya shilingi? Au kwa sababu, Mheshimiwa Lowassa amesema serikali haifanyi maamuzi magumu?”

Nchimbi pia alisema Nape ni “mropokaji” anayevuruga chama.
Wengine walioshupaliwa kwa kuchangia kukidhoofisha chama ni Samwel Sitta na Dk. Harrison Mwakyembe ambao ni miongoni mwa waasisi wa Chama cha Jamii (CCJ) huku wakiwa bado viongozi na wanachama wa CCM. Hata hivyo, CCJ kilinyimwa usajili wa kudumu.
Aliyetoa hoja hiyo ni Hussen Bashe ambaye anajitambulisha ni kutoka kundi la Lowassa na Rostam. Habari zinasema kwamba Mukama alimwita Bashe na kumwomba agombee ubunge Igunga, lakini Bashe alimgomea kwa maelezo kuwa hana mizizi ya kisiasa katika jimbo hilo.
“Nilitaka ubunge wa Nzega, si Igunga. Huko si kwetu. Siwezi kwenda Igunga kwa sababu nataka mshindwe ili tuheshimiane,” Bashe alinukuliwa akimweleza Mukama.

Vile vile, vijana hao walimtaka Mukama aagize serikali imwondoe Sitta katika nyumba ya spika, kwa maelezo kwamba kitendo chake kung’ang’ania nyumba hiyo huku akijua alishaachia uspika ni kinyume cha utaratibu, na kinagombanisha wananchi na serikali yao.

Wednesday, July 6, 2011

Vinara kashfa ya rada watajwa

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Mathias Chikawe amesema Mbunge wa Bariadi Magharibi, Endrew Chenge (CCM), hahusiki kwa namna yoyote na kashfa ya uuzaji wa rada liyoligharimu Taifa pauni milioni 28 ambazo sasa Serikali inataka zirejeshwe.

Mbali na Chenge ambaye pia anatakiwa kujivua gamba ndani ya chama chake kwa kashfa hiyo, Chikawe alisema bungeni jana kuwa, hakuna Mtanzania hata mmoja anayetuhumiwa kwa hilo ndio maana hawajamshitaki mtu.

Akitoa majumuisho ya hotuba ya Ofisi ya Rais Utawala Bora, Chikawe alisema Serikali ililiita Shirika la Serious Fraud Office (SFO) la Uingereza kuja kumchunguza Chenge kwa kushirikiana na Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) na katika uchunguzi huo Chenge hakukutwa na hatia.

Aliwataja wahusika kuwa ni Sailesh Vithlan, dalali wa rada hiyo Jonathan Callman, Meneja Biashara wa Kampuni ya BAE Systems ya Uingereza iliyouza rada hiyo na Meneja Masoko wa kampuni hiyo, aliyejulikana kwa jina moja la Christopher.

"Kama kuna mtu ana ushahidi dhidi ya Chenge au mtu mwingine atupe na tutampeleka mtuhumiwa huyo mahakamani kesho.

"Kama hakuna, basi tufanye kama kanisani (wakati wa kufunga ndoa) kuwa yeyote mwenye neno naye (Chenge), aseme sasa na kama hakuna basi kila mtu anyamaze," alisema Chikawe.

Alifafanua kuwa Serikali haijamshitaki Chenge wala mtu yeyote na kufafanua kuwa haiwezi kwenda mahakamani kwa hisia na hata wanasheria wanafahamu hilo.

Hii ni mara ya tatu kwa Chenge kusafishwa na tuhuma hizo; mara ya kwanza aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Utawala Bora, Sophia Simba alikaririwa akisema kuwa Chenge alisafishwa na SFO.

Mara ya pili, Chenge mwenyewe alijitokeza mbele ya vyombo vya habari alipokuwa akigombea nafasi ya Spika wa Bunge na kufafanua kuwa SFO na Takukuru walimsafisha baada ya kukosa ushahidi dhidi yake.

Lakini Ubalozi wa Uingereza ulitoa tamko kuwa suala hilo halijakamilika wala halijafikiwa muafaka na Chenge hakupaswa kudai kuwa hana hatia.

Hata hivyo wakati wa Kamati ya Matumizi Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani, Tundu Lissu alisimama na kusema anayo barua inayoonesha kwamba Andrew Chenge na Dk. Idris Rashid walihusika katika ununuzi wa rada hiyo na Chenge alipata dola milioni 1 alizopeleka katika akaunti iliyopo nje ya nchi na Dk. Rashid alipata pauni za Kiingereza laki sita.

Hata hivyo Waziri Chikawe alisimama na kusema kwamba aliwaomba wabunge kama wana ushahidi dhidi ya Chenge waulete ili waende mahakamani hata kesho na akaomba Tundu Lissu ampatie ushahidi huo.

Lakini Lissu alisema ushahidi huo ni barua kutoka SFO kwenda kwa Mwanasheria Mkuu wa Tanzania na hivyo Serikali isiwahadae wananchi kwa sababu wanao ushahidi.

Kashfa hiyo hiyo, itakumbukwa kuwa ilichangia Chenge kujiuzulu nafasi yake kama Waziri wa Miundombinu baada ya kutuhumiwa kumiliki fedha zilizodaiwa kuwa mgawo wake katika uuzaji wa rada; dola milioni moja, zaidi ya Sh bilioni moja nje ya nchi.

Lakini jana kabla ya kutangazwa kuwa Chenge hana hatia, Serikali ilitupiwa zigo la kuwachukulia hatua za kisheria Watanzania waliohusika kupora fedha za umma katika ununuzi wa rada katika Mahakama ya Tanzania kwa kuwa katika Mahakama ya Uingereza, watuhumiwa hao hawatakuwa na hatia.

Ujumbe wa Bunge uliokwenda Uingereza kuwakilisha Watanzania kudai fedha hizo maarufu 'chenji' , umeweka wazi kuwa Kampuni ya BAE Systems inayotuhumiwa kushirikiana na watuhumiwa wa Tanzania katika uporaji huo na SFO, wameweka mazingira ya kutoshitakiwa kwa watuhumiwa hao huko Uingereza.

Wakizungumza baada ya kukabidhi ripoti ya kazi waliyoifanya huko Uingereza kwa Spika wa Bunge, Anne Makinda, wajumbe hao walioongozwa na Naibu Spika, Job Ndugai, walisema wamefanikiwa kushawishi Waingereza kuona umuhimu wa fedha hizo pauni milioni 29.5, kurudishwa kupitia Serikali ya Tanzania.

Lakini pia waliituhumu kampuni hiyo na SFO kwa kupanga mazingira hayo ya kutoshitakiwa kwa watuhumiwa kwa kutumia mwanya wa mazungumzo nje ya Mahakama.

Ndugai alisema baada ya SFO kuishitaki kampuni hiyo, kampuni hiyo iliomba mazungumzo nje ya Mahakama na yalipokamilika, Mwanasheria wa kampuni hiyo, ambayo ndiyo mtuhumiwa, alitengeneza makubaliano ya mazungumzo hayo na kuzuia watuhumiwa wasishitakiwe na kuyasajili mahakamani.

Ndugai alisema kuwa mwanasheria huyo alihakikisha anailinda kampuni hiyo na watuhumiwa wengine.

"Kwa kweli jaji aliyetoa hukumu ile, alikuwa na 'moral pressure' msukumo wa kibinadamu, akaona gharama za kesi ni kubwa akasema nitapunguza gharama za kesi na kuongeza katika tuzo itakayopewa Watanzania," alisema Ndugai.

Alifafanua kuwa katika hilo, badala ya kuamuru fedha nyingi ziwe gharama za kesi hizo ambazo zingetumiwa na SFO au kampuni hiyo; jaji huyo alitoa pauni laki tano tu kama gharama za kesi na pauni milioni 29.5 akaamuru zirejeshwe kwa Watanzania walioibiwa.

Wednesday, June 29, 2011

Mbunge aibua Deci bungeni

NAIBU Waziri wa Fedha, Gregory Teu, leo ameshindwa kujibu swali lililomtaka aeleze hatua zilizochukuliwa na Serikali kuhusu maofisa walioshindwa kutekeleza wajibu wao hadi taasisi ya Development Entrepreneurship for Community Initiative (DECI) ikafanya shughuli zake kinyume cha sheria.

Swali hilo liliulizwa na Mbunge wa Kawe Halima Mdee (Chadema) ambaye awali aliuliza swali la msingi kuhusu DECI.

Katika swali hilo la nyongeza, Mdee alisema, DECI ilifanya shughuli zake kwa miaka mitatu za kuchukua amana za wananchi bila kuwa na kibali cha kufanya hivyo.

“Serikali inatoa kauli gani juu ya maafisa wake ambao walikuwa wanajua suala hilo
lakini hawakuchukua hatua zozote? alihoji Mdee.

Katika swali lingine la nyongeza Mbunge huyo aliuliza kuwa, kwa kuwa fedha zinazoshikiliwa ni za wanachama na waliofanya uhalifu huo ni watu watano, na kwa vile thamani ya fedha inashuka kwa nini wanachama ambao hawakuwahi kuvuna hata mara moja wasikabidhiwe fedha hizo?

Katika majibu yake alisema: “Fedha zinazodaiwa na wanachama ni nyingi wakati fedha zilizoko kwenye akaunti za wakurugenzi ni kidogo.”

Baada ya kujibu hivyo alienda kukaa ndipo Spika wa Bunge Anne Makinda akamkumbusha kuwa hajajibu sehemu nyingine ya swali hilo kuwa maofisa wa serikali ambao walizembea hadi Deci wakaendesha shughuli zao kinyume cha sheria wamechukuliwa hatua gani?

Ndipo Naibu huyo aliporudi kwenye eneo la kujibia na kusema “Nafikiri walikuwa bado
hawajaandikishwa,” alisema naibu waziri huyo na kuwafanya wabunge kuangua kicheko.

Awali akijibu swali la msingi la Mbunge huyo, Teu alisema Serikali haijachukua fedha za Deci bali fedha hizo, Sh bilioni 14.81 zimezuiliwa katika akaunti zilizomilikiwa na wakurugenzi wa Deci katika benki mbalimbali nchini.

Katika swali hilo Mdee alitaka kufahamu hatma ya fedha za wananchi. Alisema fedha hizo ni asilimia 37.77 ya ambazo zinadaiwa na wanachama wa Deci ambazo ni Sh bilioni 39.3.

Alisema, uamuzi wa kuzizuia uliotolewa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ikiwa ni hatua mojawapo ya uchunguzi dhidi ya Deci ambayo ilikuwa inaendesha mchezo wa upatu.

“Napenda kuliarifu Bunge lako kuwa kesi ya Deci iliyofunguliwa mwaka juzi katika mahakama ya Kisutu inaendelea kusikilizwa,” alisema Teu na kuongeza: “Hivyo hatma ya fedha hizo za wananchi itategemea hatma ya kesi hiyo kwani Deci ilikuwa na matawi 40 katika mikoa 18 ya Tanzania Bara”.

Alisema, usikilizwaji wa mashahidi wa Dar es Salaam umekamilika na hatua za kuwapata mashahidi kutoka mikoa mingine zimeanza.

Alisema, Deci ilikuwa na wanachama 649,859 na sehemu ya wanachama hao watahitajika kutoa ushahidi mahakamani.

Thursday, June 16, 2011

Upinzani waifumua Bajeti ya Serikali

  • WAFUTA POSHO, WATANGAZA KIMA CHA CHINI SH 315,000



KAMBI ya Upinzani Bungeni imetangaza bajeti mbadala ya Sh14 trilioni na kubainisha upungufu mkubwa katika Bajeti ya Serikali, huku ikipendekeza kufutwa kwa misamaha ya kodi kwa kampuni za uchimbaji wa madini na mafuta na posho za vikao kwa watumishi wa umma, wakiwamo wabunge. Akiwasilisha bajeti hiyo bungeni, Waziri Kivuli wa Fedha na Uchumi, Zitto Kabwe alisema hatua hiyo imelenga kuongeza mapato ya Serikali na kupunguza matumizi yasiyokuwa ya lazima.

Katika bajeti hiyo mbadala, kambi hiyo imesisitiza umuhimu wa ushiriki mkubwa zaidi wa umma na uchunguzaji wa utungaji na utekelezaji wa Bajeti, ili kuboresha uwajibikaji na kuziba mianya zaidi ya ufisadi na matumizi mabaya ya rasilimali za nchi.

Kambi ya Upinzani inapendekeza kupunguza misamaha ya kodi ikitaka isizidi asilimia moja ya Pato la Taifa, kupunguza kodi na tozo kwenye mafuta ya petroli na dizeli ili kupunguza mfumuko wa bei na ukali wa maisha.

Pia imependekeza kufanya marekebisho katika mfumo wa malipo serikalini kwa kuondoa posho za vikao kwa watumishi na viongozi wa umma na kuelekeza sehemu ya tozo ya kuendeleza ujuzi (skills development levy) kwenye Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu.

Kuhusu kodi za mafuta, Zitto alisema Kambi ya Upinzani Bungeni inapinga pendekezo la sasa la kuondoa msamaha wa kodi ya mafuta kwa kampuni za utafutaji mafuta na gesi kwani mikataba ya kazi hiyo imezingatia suala hilo.

"Msamaha huu hauna mantiki kwani kampuni za utafutaji mafuta na gesi kwa mujibu wa mikataba yao (production sharing agreements) wataweza kurejeshewa gharama hizi mara baada ya mafuta na gesi kupatikana," alisema Zitto.

Pia Kambi ya Upinzani kupitia bajeti yake hiyo, inapendekeza kufuta kabisa msamaha wa kodi kwenye mafuta kwa kampuni za madini na za ujenzi kwani imethibitika kuwa msamaha huo husababisha upotevu wa fedha za umma.

Zitto alisema takwimu zinaonyesha kuwa kupitia misamaha hiyo, jumla ya lita 133 milioni za dizeli ambazo ni sawa na asilimia 20 ya dizeli yote iliyoingizwa nchini, zilikuwa za kampuni tano za migodi ya dhahabu ambazo zililipa ushuru wa dola 200,000 tu.

"Mafuta mengi yanayoingia kupitia msamaha huu hurudi kwenye soko na kuuzwa rejareja. Misamaha hii ifutwe bila kujali mikataba iliyopo," alisema.

Misamaha ya kodi

Kuhusu misamaha ya kodi, Zitto alisema kiwango kinachotolewa na Tanzania ni kikubwa ikilinganishwa na nchi jirani za Uganda na Kenya na kwamba kati ya miaka ya 2005/06 na 2007/08, misamaha ya kodi nchini ilikadiriwa kuwa wastani wa asilimia 3.9 ya Pato la Taifa.

"Mwaka 2008/09, misamaha ya kodi ilikuwa asilimia 2.8 ya Pato la Taifa na mwaka 2009/10 asilimia 2.3 ikilinganishwa na Kenya na Uganda ambako misamaha ilifikia asilimia moja na 0.4 ya pato la taifa katika kila nchi husika kwa mtiririko huo," alisema Zitto.

Alisema iwapo Tanzania ingerekebisha kiwango cha misamaha ya kodi ili kulingana na kile kilichofikiwa na Kenya, zaidi ya Sh600 bilioni zingeokolewa kwa mwaka 2007/08 pekee na kwamba fedha hizo zinaweza kuwa sawa na kiasi cha fedha ambacho serikali hushidwa kukikusanya kutokana na kodi.

Alitoa mfano wa mwaka 2008/09 na 2009/10 ambao Serikali haikutimiza lengo lake la mapato kwa wastani wa Sh453 bilioni wakati misamaha ya kodi iliyotolewa ilifikia wastani wa Sh724 bilioni.

Alisema misamaha ya kodi imekuwa ikiendelea kutolewa na kuathiri mapato ya nchi akisema kwa mujibu wa taarifa ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa Kamati ya Fedha na Uchumi ya Bunge, hadi kufikia Juni mwaka huu, msamaha wa kodi unakadiriwa kuwa Sh930 bilioni.

Zitto anasema upungufu katika ukusanyaji wa mapato unasababishwa kwa kiasi kikubwa na misamaha ya kodi kwani kama ingetolewa katika kiwango kinachofanana na cha misamaha ya kodi Kenya, Sh 484 bilioni zingeokolewa mwaka 2008/09 na Sh 302 bilioni kwa mwaka 2009/10.

Pamoja na kuipongeza Serikali kwa kukubali wazo la kupunguza misamaha ya kodi mpaka kufikia asilimia moja ya Pato la Taifa, Kambi ya Upinzani imependekeza kupitiwa upya kwa vivutio vinavyotolewa na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kwa wawekezaji kwa kupiga marufuku msamaha wowote wa kodi kwa bidhaa zinazozalishwa nchini ili kulinda viwanda vya ndani.

Posho serikalini

Katika hotuba yake, Zitto pia alirejea hoja inayopendekeza kufutwa kwa posho za vikao kwa watumishi wote wa umma hasa wabunge akisema wanatakiwa kuwa mfano katika kutekeleza pendekezo hilo.

Kambi hiyo ilishauri kufanya marejeo ya mfumo wa posho na wa mishahara kwa watumishi wa umma na kupendekeza kwamba hatua zianze kuchukuliwa sasa katika Bajeti inayojadiliwa ili kuwaonyesha Watanzania kuwa wabunge wanajali hali zao.

Alisema posho za vikao ni rushwa ya kitaasisi wanaojipa watu wenye mamlaka na kwamba wakati viongozi wakilipwa posho hizo katika vikao vya kufanya uamuzi ambao ni wajibu wao, polisi halipwi posho kwa kulinda, mwalimu halipwi posho kwa kuingia darasani na wala muuguzi halipwi posho kwa kusafisha vidonda vya wagonjwa.

Alisema Kambi ya Upinzani haipingi posho za kujikimu ambazo viongozi au maofisa wa umma hulipwa wanaposafiri nje ya vituo vyao vya kazi bali, zirekebishwe kuendana na gharama za maisha za sasa lakini akasisitiza:

"Posho za vikao zifutwe mara moja. Iwapo sisi tukiendelea kujilipa posho za kukaa humu ndani na kwenye kamati zetu, tunakuwa tunatoa ruhusa kwa watumishi wa Serikali kulipana posho hizi na hatutakuwa na mamlaka ya kuwahoji na kuwawajibisha."

Waziri huyo Kivuli wa Fedha na Uchumi, amekuwa katika malumbano ya muda mrefu na Spika wa Bunge, Anne Makinda na Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo kutokana na msimamo wake wa kukataa kulipwa posho za vikao, malipo ambayo Bunge na Serikali wanasema yapo kisheria hivyo lazima apewe.

Alisema kauli ya Serikali kwamba inakusudia kupunguza posho katika mwaka ujao wa fedha si ya kweli akisema hotuba ya Waziri Mkulo inapendekeza kufutwa kwa kodi katika posho hizo na wakati huohuo, Serikali katika Bajeti imeomba kiasi cha Sh 987 bilioni sawa na asilimia 13 ya bajeti nzima kwa ajili ya malipo ya posho mbalimbali.

"Katika hotuba yake ukurasa wa 66, anapendekeza (Waziri) kufanywa kwa marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Mapato Sura 332 na anasema kwenye (i) kusamehe kodi ya mapato kwenye posho wanazolipwa wafanyakazi wa serikali na wanaofanya kazi kwenye taasisi zinazopata ruzuku kutoka kwenye bajeti ya serikali.”

"Sasa tumeanza kusikia vilio kutoka sekta binafsi kwamba na wao wapate unafuu huu wa kodi. Kambi ya upinzani inapendekeza mfumo mzima wa kulipana posho za vikao (sitting allowances) uondoke katika utumishi wa umma."

Sekta ya madini


Hotuba hiyo ya wapinzani pia imezungumzia kwa undani sekta ya madini na kubainisha kwamba taarifa za Serikali zinathibitisha kwamba haichangii mapato ya ndani.

Alisema ipo haja ya kuhakikisha taifa linakusanya mapato ya kutosha katika sekta hiyo ili kuleta maendeleo ya wananchi:
"Katika mwaka huu wa fedha, taifa letu litakusanya Sh 99.5 bilioni kutoka katika mrabaha kwenye madini yanayochimbwa nchini kwetu. Mapato haya kwa mwaka ujao wa fedha ni asilimia 4.5 tu ya mauzo ya dhahabu peke yake nje ya nchi."

Alisema ni vigumu kujua kiasi cha kodi nyingine zinazokusanywa kutoka katika sekta ya madini kutokana na kampuni zote kurundikwa katika kapu moja la idara ya walipa kodi wakubwa.

Alisema takwimu za Mwaka 2009/2010 zinaonyesha kuwa mapato yote ya kodi pamoja na mrabaha na malipo kwa mifuko ya pensheni (ambayo siyo kodi) katika sekta ya madini yalikaribia Sh 256 bilioni ambazo zilikuwa sawa na asilimia 16 ya thamani ya mauzo ya madini nje ya nchi.

Kodi za mafuta
Kuhusu kodi zitakazopunguzwa kwenye mafuta, Zitto alisema Kambi ya Upinzani inapendekeza kuwa ushuru wa barabara (road toll) usipunguzwe ili kubakia na fedha za kutosha kukarabati barabara ambazo zinajengwa kwa kasi.

Alisema maeneo ambako kodi hiyo inaweza kupunguzwa ni ushuru wa bidhaa kwenye mafuta kwa asilimia 40 na tozo nyingine zote kwenye mafuta zipunguzwe kwa asilimia 40 pia.

Hata hivyo, Zitto alisema hatua ya kupunguza kodi za mafuta ni kama dharura tu kwani bado inaweza isiwe na maana iwapo bei za mafuta zitaendelea kupanda katika soko la dunia.

"Hivyo tunahitaji njia endelevu; nayo ni kuhakikisha mafuta yanaagizwa kwa wingi na hivyo kupunguza gharama za usafirishaji. Mpango wa ununuzi wa mafuta kwa wingi umekuwa ukisemwa bila kutekelezwa kwa muda mrefu kutokana na nguvu kubwa ya rushwa waliyonayo matajiri katika sekta ya mafuta. Ni lazima tuishinde nguvu hii hata kama itakuwa ni kwa baadhi yetu kupoteza maisha."

Sura ya bajeti mbadala

Sura ya bajeti hiyo mbadala inaonyesha kuwepo kwa uwezekano wa mapato ya Serikali katika mwaka wa fedha 2011/12 kufikia Sh14.16 trilioni ikilinganishwa na kiasi cha Sh13.525 trilioni kilichopendekezwa katika Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka huo.

Zitto ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni alibainisha kuwa fedha hizo ni mapato ya ndani Sh8.68 trilioni kutoka Sh6.7trilioni za serikali, mapato ya halmashauri Sh351 bilioni, mikopo na misaada ya nje Sh3.924 trilioni na mikopo ya ndani Sh1.204 trilioni.

Kwa upande wa matumizi, Zitto alisema kambi yake inapendekeza matumizi ya kawaida Sh.7.913trilioni ikilinganishwa na yale ya Serikali ambayo ni Sh 8.600 trilioni
wakati kwa upande wa matumizi ya maendeleo, wapinzani wanapendekeza kaisi cha Sh6.247 trilioni zikiwamo fedha za ndani Sh3.193trilioni na fedha za nje Sh3.054 trilioni.

Bajeti ya Serikali imetenga kiasi cha Sh4.925 trilioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo ambapo fedha za ndani ni Sh1.871 trilioni wakati fedha za nje ni Sh3.054 trilioni.

Ili kukidhi mahitaji ya fedha za mapendekezo yaliyomo katika bajeti yake, Zitto alisema Kambi ya Upinzani, inapendekezo kufanya marekebisho ya kodi katika maeneo kadhaa ambayo yataingiza kaisi cha Sh1.905 trilioni na kuongeza fedha hizo katika bajeti.

Marekebisho hayo ni kodi ya misitu ambayo itawezesha kupatikana kwa Sh100 bilioni, misamaha ya kodi (Sh658 bilioni), mauzo ya hisa za Serikali (Sh 550 bilioni), kodi katika sekta ya madini (Sh240 bilioni), kuimarisha usimamizi wa mapato ya wanyamapori (Sh81 bilioni), kuondoa msamaha wa ushuru wa mafuta kampuni za madini (Sh59 bilioni), usimamizi wa mapato katika utalii (Sh68 bilioni) na kuimarika kwa biashara na nchi za Afrika Mashariki (Sh150 bilioni).

Pia kambi hiyo inapendekeza kuanzishwa kwa kodi mpya inayotokana na fedha ambazo wenye nyumba wanazipangisha. Alipendekeza kuanzishwa kwa chombo maalumu cha kusimamia kazi hiyo.

Chanzo: Mwananchi 16/6/2011

Wednesday, June 15, 2011

CCM WAFUTA POSHO ZA VIKAO


HOJA ya kutaka kufutwa kwa posho za vikao za wabunge na watumishi wengine wa umma imechukua sura mpya baada ya jana Mbunge wa Bumbuli (CCM), Januari Makamba kuliambia Bunge mjini hapa kuwa suala la kufutwa kwa posho ni la kitaifa na ni sehemu ya Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano uliowasilishwa na serikali.

Kauli hiyo ya Makamba ambaye pia ni Katibu wa Mambo ya Nje wa Sekretarieti ya CCM imekuja huku kukiwa na malumbano makali baina ya Spika wa Bunge, Anne Makinda na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe kuhusu suala hilo la posho za vikao vya wabunge.

Juzi, Spika Makinda alisema Zitto ambaye ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, anaweza kufukuzwa ubunge kwa kutosaini karatasi za mahudhurio, hatua ambayo Zitto alisema ataichukua ili asilipwe posho za vikao.

Spika alisema Zitto anaweza kukumbwa na adhabu hiyo iwapo hatasaini karatasi za mahudhurio ambazo ndizo zinathibitsha uwepo wa mbunge katika mikutano na vikao vya bunge na kwamba kanuni zinamwadhibu mbunge kwa kumfukuza asipohudhuria mikutano mitatu. Hata hivyo, Zitto amepuuza kauli hiyo ya Spika kwa kusema kwamba kama ni kwa ajili ya kukataa posho, yuko tayari kufukuzwa bungeni.

"Nitafanya hivyo tuone, Kanuni inasema mikutano mitatu mfululizo na siyo vikao vitatu mfululizo. Nitatumia uzoefu wangu wa siasa za wanafunzi kukwepa mtego wake. Lakini kama anadhani ni sawa kunifukuza ubunge kwa kukataa posho, nipo tayari," alisema.

Kauli ya jana ya Makamba pia inaonekana kutofautina na mawazo ya wabunge wengi wa CCM akiwamo Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo ambaye amesema wanashabikia suala hilo wanajitafutia umaarufu.

Akichangia huo wa maendeleo wa miaka mitano jana, Makamba alionekana kupigia chapuo suala la kufutwa au kuangaliwa upya kwa posho za vikao huku akisema kwamba ni la kitaifa na ni sehemu ya mpango huo.

Makamba alisema kuwa suala la nidhamu na usimamizi wa matumizi ya fedha za umma ni muhimu na kwamba mpango huo umeliona katika ukurasa wa 17 wa kitabu kilichochapishwa kwa Kiingereza na kutoa mapendekezo ya kufutwa kwa posho za vikao na zile za usafiri.

"Mpango unabainisha kwamba kuna umuhimu wa kufutwa kwa posho za vikao na usafiri hivyo iwapo wabunge mtalisikia likiwasilishwa hapa kwa mbwembwe kesho (leo), basi msije mkashangaa kwani ni sehemu ya mpango huu," alisema Makamba.

Kujadiliwa bungeni leo

Mjadala kuhusu malipo ya posho ambao umekuwa ukiendelea kwa wiki moja sasa hasa zaidi nje ya Bunge, leo unatarajiwa kuingizwa rasmi bungeni wakati Bajeti ya Serikali iliyowasilishwa na Mkulo Jumatano iliyopita itakapoanza kujadiliwa.

Suala hilo ni dhahiri litajitokeza katika bajeti mbadala itakayowasilishwa na kambi ya Upinzani Bungeni na Waziri Kivuli wa Fedha, Zitto Kabwe ambaye amekuwa katika mvutano usio rasmi na Spika kutokana na kukataa kulipwa posho za kikao.

Mwenyekiti wa Chadema ambaye pia ni Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe alisema jana kuwa kambi yake inatarajiwa kutoa ushauri mgumu ambao haujazoeleka kwa watendaji wa serikali na kwamba suala la kufutwa kwa posho ni sehemu ya mapendekezo hayo.

Alisema kufutwa kwa posho hizo kunaweza kuokoa zaidi ya Sh900 bilioni ambazo zinaweza kuelekezwa katika maeneo mengine ya huduma kwa wananchi.

Uhalisia posho za wabunge

Mmoja wa wabunge wa CCM ambaye hakutaka kutaandikwa jina lake alisema anasikia kuhukumiwa katika nafsi yake kutokana na kupokea posho za vikao ambazo kimsingi ni sawa na "kuwaibia wananchi".

"Ujue bwana sisi ndani ya CCM mambo hayaendi kama kwa wenzetu (Chadema), wale wanaweza kukaa leo na kuamua, sisi ni tofauti lazima kuwepo na mchakato lakini ukweli ni kwamba hoja yao ni nzuri," alisema mbunge huyo.

Uchunguzi uliofanywa umebaini kuwa malipo ya wabunge yamegawanyika katika sehemu nne ambazo ni pamoja na mshahara ambao ni Sh2,300,000 kwa mwezi, posho ya ubunge kila mwezi ambayo ni Sh5 milioni, posho ya kujikimu (per-diem) Sh80,000 wawapo nje ya majimbo yao kikazi na posho ya vikao (sitting allowance) ambayo huwa ni Sh70,000 kwa kila mbunge.

Kwa maana hiyo, kwa kawaida mbunge hulipwa Sh7.3 milioni kila mwezi kabla ya kukatwa kodi na wawapo Dodoma na Dar es Salaam kwa ajili ya vikao vya kamati na bunge au mikoani kwa ajili ya kukagua shughuli zilizopo chini ya kamati zao. Hulipwa kiasi cha Sh150,000 kila mmoja kwa siku ambazo ni Sh70,000 kwa ajili ya vikao na Sh80,000 kwa ajili ya kujikimu.

Kwa maana hiyo bunge linatarajiwa kutumia kiasi cha Sh1.788 bilioni kwa ajili ya kugharamia vikao 73 vya Bunge la Bajeti iwapo wabunge wote 350 waliopo watahudhuria vikao hivyo.

Kwa hesabu hizo, kila mbunge katika mkutano wa Bunge la Bajeti anatarajiwa kuondoka na kikita cha Sh5.1 milioni mbali na Sh 5.58 milioni ambazo ni malipo kwa ajili ya kujikimu, fedha ambazo ni mbali na mshahara wake kwa mwezi na posho ya ubunge.

CCM yakataa posho

Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeanza machakato wa kufuta posho hizo ikiwa ni hatua ya kupunguza matumizi yasiyo ya lazima. Habari kutoka ndani ya CCM, Dodoma na Dar es Salaam zinasema kuwa mkakati wa kufutwa kwa posho ulianzishwa takriban mwezi mmoja uliopita na sekretarieti mpya inayoongozwa na Katibu Mkuu, Wilson Mukama.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, baadhi ya wajumbe wa sekretarieti walihoji uhalali wa posho wanazolipwa hata pale vikao vinapofanyika katika sehemu ambako ni makazi yao na kwamba hoja hizo ndizo zilizozaa wazo la kufutwa kwa posho katika vikao.

"Hoja ilikuwa kwamba kama chama hakina fedha na tunataka kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, basi posho za vikao zifutwe kwa sababu hakuna ulazima wa posho hizo hasa kwa wajumbe wa sekretarieti ambao kazi zao ni za kila siku," kilieleza chanzo chetu na kuongeza:

"Hivi sasa mpango huo uko kwenye mchakato wa kuwekewa mwongozo na nadhani baada ya kupitia katika vikao vyetu utaanza kutekelezwa. Lakini kimsingi ni kama utekelezaji wake umeshaanza kwa sababu baadhi ya wajunbe wamekataa kabisa kusaini posho hizo."

Habari zaidi zinadai kuwa waraka wa mapendekezo ya kupunguza matumizi ndani ya CCM unakwenda mbali zaidi hadi katika matumizi ya magari na kwamba pale usafiri unapohitaji wa kuelekea kwenye mkutano mmoja, basi viongozi watumie magari machache kwa maana ya usafiri wa pamoja badala ya utaratibu wa sasa ambao unamruhusu kila kiongozi kutumia usafiri wake.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipoulizwa kuhusu sekretarieti kufuta posho katika vikao vyake, hakukanusha wala kuthibitisha, badala yake akadai kuwa hayo ni mambo ya ndani ya chama ambayo hayana faida yoyote kwa umma.

"Hivi ninyi waandishi wa habari, haya mambo mnayapata kwa nani! Haya ni mambo ya ndani ya chama sidhani kama yana tija yoyote kwa umma, maana haiwezi kusaidia chochote," alisema Nape kwa kwa simu.

Alipoelezwa kwamba suala hilo lina uhusiano na sakata linaloendelea bungeni, Nape alisema: "Bunge ni bunge na chama ni chama. Kila taasisi inajitegemea na ina uamuzi wake, lakini pia sisi kama chama tulishatoa kauli mara nyingi kwamba suala la posho kwa wabunge na watumishi wengine wa serikali linazungumzika, ni la kisera na wanaohusika wapo waulizeni hao."

Mwishoni mwa wiki iliyopita Nape akizungumzia malumbano miongoni mwa wabunge kuhusu suala la posho alisema suala hilo linajadilika na kwamba si vyema kulipinga kwa sababu tu linatokea kambi ya upinzani.

Kwa upande wake, Makamba alipoulizwa kuhusu kufutwa kwa posho katika vikao vya Sekretarieti ya CCM naye kama ilivyokuwa kwa Nape, hakukanusha wala kuthibitisha.

"Wewe si unamfahamu msemaji wa chama ni nani? Mwulizeni Nape tena nadhani anakuja Dodoma. Akija mwulizeni, mimi siwezi kulizungumzia.... lakini ninyi waandishi haya mambo ya ndani ya chama huwa mnayapata wapi? Anyway, mwulizeni mwenezi atawaambia," alisema Makamba.

Chanzo: Mwananchi 15/6/2011

Wednesday, June 8, 2011

LEO NI BAJETI

Mawaziri wapigia debe bajeti 

MACHO na masikio ya mamilioni ya Watanzania na wadau wa nje, leo yanaelekezwa Dodoma ambako Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2011/12 itasomwa. Wananchi wengi wamekuwa na shauku ya kujua mwelekeo wa bajeti hiyo hasa katika kipindi hiki ambacho wanakabiliwa na hali ngumu ya maisha iliyotokana na kupanda kwa bei vyakula na bidhaa za mafuta.

Kwa takriban wiki nzima iliyopita, baadhi ya wananchi wamekuwa wakituma ujumbe mfupi wa maandishi kwa simu katika vyombo vya habari, wakiisihi serikali kuhakikisha kuwa bajeti ya mwaka huu inawaondoa katika hali ngumu ya maisha.

Bajeti hiyo itakayosomwa bungeni na Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo itatangazwa kwa wakati mmoja na bajeti za serikali za nchi zote za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), katika mtazamo wa kuimarisha mshimakano na umoja wa nchi hizo.

Kwa kawaida na mazoea ya muda mrefu, bajeti ya serikali imekuwa ikisomwa siku za Alhamisi ya wiki ya kwanza ya Juni, lakini mwaka huu imebadilika ikielezwa kwamba hiyo ni kutokana na siku hiyo kuangukia siku ya Uhuru wa Uganda.

Akizungumza bungeni jana asubuhi, Spika wa Bunge, Anne Makinda alisema bajeti hiyo itatanguliwa na hotuba ya hali ya uchumi itakayosomwa pia na Waziri Mkulo. Alisema hotuba hiyo itasomwa asubuhi, wakati ile ya bajeti itasomwa jioni.

Baadhi ya mawaziri akiwamo Mkulo wameifagilia bajeti hiyo huku Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania (CTI) likitoa mapendekezo na matumaini yake.

CTI: Tunataka bajeti ya uchumi wa viwanda

Shirikisho hilo limesema kuwa linaisubiri kwa hamu bajeti hiyo likitaka iwe ya kukuza uchumi na kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji. Kauli ya CTI huku likilalamikia kupanda kwa gharama za uzalishaji zilizotokana na mgawo wa umeme wa Tanesco.

Mkurugenzi Mtendaji wa CTI, Christine Kilindu alisema jana kwamba serikali inapaswa kutoa bajeti ambayo pia itaondoa kodi zinazoumiza uzalishaji mkubwa. Alisema kodi kubwa zisizo za msingi zinachangia kupanda kwa gharama za uzalishaji ambao mwishowe husababisha kupanda kwa gharama za maisha kwa mwananchi wa kawaida. 

"Tunataka bajeti ambayo itaondoa kodi zinazokwamisha uzalishaji mkubwa na ukuaji uchumi, tunataka bajeti itakayopunguza makali ya maisha kwa mwananchi kwa kumwezesha kupata bidhaa kwa urahisi," alisema Kilindu.

Alisema bajeti hiyo inapaswa pia kuweka mazingira mazuri na yanavyovutia kibiashara ili kuifanya Tanzania kuwa kituo muhimu cha uwekezaji. Alisema kwamba anategemea kuona umeme ukiwekewa mazingira ya kukuza uchumi na uwekezaji nchini, akisema bila kufanya hivyo hakuna kitu kitakachofanyika.

"Bila umeme hakuna kitu chochote, serikali inapaswa kuongeza nguvu na msukumo kuona umeme siyo tu unamulika maisha ya watu kwa kutoa mwanga, bali iwe ni nguvu ya kusukuma ukuaji wa uchumi wa nchi."

Mawaziri wapigia debe bajeti

Katika kujiwekea mazingira mazuri na kuzuia kubanwa na wabunge, baadhi ya mawaziri wamepigia debe bajeti za wizara zao huku Mkulo, akiahidi kuwa malimbikizo ya vyombo vya usalama yatalipwa mwezi huu.

Mara kwa mara baadhi ya wabunge wamekuwa wakitishia kukwamisha baadhi ya bajeti za wizara, kutokana na kukosa majibu ya msingi kwa mambo mbalimbali ya msingi. Jana asubuhi baadhi ya mawaziri walipokuwa wakijibu maswali bungeni walisisitiza kuwa mambo mengi waliyokuwa wakiulizwa yamezingatiwa katika bajeti.

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Balozi Hamis Kagasheki, akijibu swali kuhusu malipo ya malimbikizo ya posho za polisi ikiwamo za wakati wa uhamisho, alisema wizara yake imeandaa mwongozo wa kisera wa namna ya kulipatia ufumbuzi tatizo hilo.Alisema katika mwongozo huo ambao tayari ulikubaliwa na Wizara ya Fedha na Uchumi, wizara yake imejipangia utaratibu wa kutatua kero hiyo kuanzia kwenye bajeti ya mwaka huu.

Balozi Kagasheki alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Mji Mkongwe (CUF), Mohammed Sanya, ambaye alitaka kujua mkakati huo ukoje kutokana na tatizo hilo kuwa ni la muda mrefu. Baada ya majibu hayo, Waziri Mkulo alisimama na kukuongeza kuwa siyo malimbikizo ya polisi pekee, bali ya vyombo vyote vya usalama na kwamba serikali imejipanga kuhakikisha yanalipwa kabla ya mwezi huu kumalizika.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk Harrison Mwakyembe naye alipigia debe bajeti ya wizara yake ambayo tayari ilisifiwa na Kamati ya Bunge ya Miundombinu, kutokana na kugusa kila eneo huku ikitajwa kuandaliwa kwa weledi wa hali ya juu.

Akijibu maswali likiwamo lililohusu ujenzi wa Barabara ya Babati, Dareda hadi Minjingu na kuhusu kero za barabara katika Jimbo la Ludewa linaloongozwa na Profesa Raphael Mwalyosi, Naibu Waziri huyo alisisitiza kuwa wizara yake ni sikivu na mambo mengi yatazingatiwa ndani ya bajeti.

Alisema wizara iko makini na Bajeti ya Ujenzi imezingatia mambo mengi ya msingi huku akitupa kete ya kuomba uungwaji mkono kwa wabunge ili waipitishe.