Showing posts with label chenge. Show all posts
Showing posts with label chenge. Show all posts

Monday, August 8, 2011

JK amuangukia Rostam

Rais Kikwete na Rostam Aziz

RAIS Jakaya Kikwete sasa anapanga kumuangukia aliyekuwa Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz, MwanaHALISI limeelezwa.

Taarifa kutoka ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) zinasema tayari chama hicho kimepanga kumuita Rostam katika mkutano wa Kamati Kuu (CC) uliopangwa kufanyika 30 Julai 2011 kwa lengo la kumwangukia.

Kada mmoja wa chama hicho aliye karibu na Rostam anasema kumekuwapo na shinikizo kutoka kwa baadhi ya viongozi wajuu wa CCM na serikali wakitaka Rais Kikwete awasiliane na Rostam ili amwombe kuhudhuria kikao cha CC kwa lengo la kumwomba msamaha ili hatimaye asaidie kampeni za uchaguzi mdogo katika jimbo la Igunga utakapotangazwa.

“Ni kweli kuna mpango wa kumuita katika Kamati Kuu. Lengo ni kumuomba atusaidie kufanikisha kampeni za Igunga, ambako kwa kweli CCM kinakabiliwa na kibarua kigumu kutetea kiti hicho kutokana na kutokuwa na maandalizi ya uchaguzi katika kipindi hiki,” ameeleza mtoa taarifa wa gazeti hili.

Kuibuka kwa taarifa hizi kumekuja wiki mbili baada ya mwanasiasa huyo kujiuzulu nyadhifa zake zote za uongozi ndani ya chama hicho kwa madai ya kuchoshwa na siasa uchwara. Mara baada Rostam kujivua nyadhifa hizo na kuandika barua kwa Spika wa Bunge la Jamhuri Anne Makinda na Rais Kikwete, akiwataarifu uamuzi wake huo aliokwishautangaza mbele ya vyombo vya habari, aliondoka nchini kuelekea Uswisi kwa kile kilichoitwa “safari ya mapumziko.”

Rostam aliondoka tarehe 14 Julai 2011 saa 10.40 alasiri, kwa ndege Na. EK 725 ya Shirika la Ndege la Emirates la Nchi za Falme za Kiarabu, siku moja baada ya kutangaza kujiuzulu ubunge na ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya chama chake.

Kiongozi mmoja wa ngazi ya juu ndani ya CCM aliliambia gazeti hili: “Uamuzi wa Rostam kuachia nafasi zake zote za uongozi umelenga kupeleka ujumbe maalum kwa Rais Kikwete, kwamba hakufurahishwa na hatua yake ya kumtumia Nape Nnauye kumshambulia yeye na wenzake majukwaani.”

Rostam alikuwa mbunge wa Igunga, mkoani Tabora tangu mwaka 1994 na mjumbe wa NEC kwa vipindi viwili.

Hata hivyo, habari zinasema hata kama mkakati wa kumuita kada huyo kwenye CC utashindwa kufanikiwa, Rais Kikwete ataendelea kumuomba asaidie kampeni za uchaguzi mdogo wa Igunga.

Tayari Makinda ameijulisha Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kujiuzulu kwa Rostam, na hivyo kuwapo uwezekano mkubwa wa kufanyika uchaguzi wa jimbo hilo ndani ya kipindi cha miezi mitatu ijayo.

MwanaHALISI limenukuu vyanzo kadhaa vya taarifa, akiwamo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano ya Umma), Steven Wasira, akitaka Rostam aitwe kusaidia kampeni za CCM. Wasira, ambaye alikuwa mstari wa mbele kutaka Rostam aondoke kwenye chama hicho, alimweleza mjumbe mmoja wa NEC, siku moja baada ya Rostam kujiuzulu, “…Kama tunataka kushinda Igunga, sharti tumuombe Rostam atusaidie. Nimeongea naye na amekubali kusaidia kampeni za Igunga.”

Hata hivyo, wachambuzi wa mambo ya kisiasa wanasema hatua ya CCM kutaka kumuangukia mwanasiasa huyu anayekabiliwa na tuhuma za ufisadi kutazidi kukichafua chama hicho mbele ya wananchi na jumuiya ya kimataifa.

Hata hivyo, zipo taarifa kuwa Rostam hataki kabisa kujihusisha na uchaguzi mdogo wa Igunga. Inaeleweka kuwa ndiye amekuwa nguzo ya CCM mkoani Tabora, kwa kutumia ushawishi wake na nguvu ya kipesa kuhakikisha wapinzani hawapiti.

Hofu ya makada na viongozi wa CCM inatokana na ukweli kwamba Rostam aliwashtukiza, kwani walipokuwa wakimtaka aondoke kwenye NEC, hawakutarajia kwamba angejiondoa kwenye ubunge.
Kutokana na hali hiyo, sasa wameanza kushikwa na ‘kigugumizi’ cha kuwachukulia hatua makada wengine wawili, Edward Lowassa na Andrew Chenge ambao, kama Rostam, wamekuwa wanashambuliwa na kuambiwa waondoke, kama njia ya utekelezaji wa dhana ya kujivua gamba.

Lowassa na Chenge wanadai Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, anatumia vibaya dhana hiyo kuwashambulia. Habari zinasema Lowassa hatafuata nyayo za Rostam za kuachia ngazi, lakini kama chama kitaamua kumfukuza atajivua nafasi zote za uongozi ndani ya chama hicho, ukiwamo ubunge wa Monduli.
Iwapo hilo litatokea, CCM kitakuwa kimejiingiza katika mgogoro kama wa Igunga.

Kwa uchache, habari zinasema wabunge tisa wakiwamo waziri mmoja na manaibu mawaziri wawili wameapa kumfuata Lowassa. Majina ya mawaziri na manaibu mawaziri hao tunayahifadhi kwa sasa.

Wakati Lowassa akiapa kutoachia ngazi, habari zinasema CCM inajiandaa kumlazimisha ajiuzulu. Aliyepangwa kuendesha kampeni ya kusimamia hatua hiyo ni Waziri Mkuu Mstaafu, Cleopa Msuya.
Hata hivyo, wapo wanaodai iwapo Lowassa ataondolewa kwenye uongozi kutaibuka mgogoro ndani ya Bunge kwani ana ushawishi mkubwa miongoni mwa wabunge wengi wa CCM. Baadhi ya maswahiba zake ni wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya Bunge. Kwa sasa Lowassa yuko safarini nje ya nchi kikazi. Anatarajiwa kurejea nchini kabla ya vikao vya chama vinavyotarajia kumjadili.

Wakati hayo yakitendeka, mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Vijana (UV-CCM), uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita mjini Dodoma, ulimalizika kwa wajumbe wa pande za Lowassa na Kikwete kushambuliana. Wakati kundi la Kikwete likitaka chama kichukue hatua kwa kupongeza maamuzi ya NEC ya kujivua gamba, upande wa Lowassa ulipinga kwa madai kuwa dhana ya kujivua gamba imetafsiriwa vibaya, na inakiangamiza chama.

Mtoa taarifa aliyekuwa ndani ya mkutano huo amemweleza mwandishi wa habari hizi kuwa mvutano huo uliishia kwa wajumbe “kumshambulia” kwa maneno makali Katibu Mkuu wa CCM, Wilson Mukama.
Miongoni mwa wengi, mjumbe wa Baraza Kuu, John Nchimbi, alinukuliwa akimweleza Mukama amejiingiza katika vita ya makundi bila ya kujua.

“Umekuja hapa kuponda kauli ya Mheshimiwa Lowassa juu ya serikali kushindwa kufanya maamuzi magumu, ukatoa mfano wa kesi ya City Water. Umesema kesi ile imegharimu serikali Sh.9 bilioni zikiwa gharama za kulipa wanasheria. Lakini mbona hukusema kiasi ambacho serikali imelipwa kutokana na kushinda shauri hilo mahakamani?” alihoji Nchimbi kwa sauti ya ukali.

Alisema, “Acheni unafiki. Mtaangamiza chama. Kama wewe ni mkweli, mbona hujasema kama serikali ilishinda kesi ile na imelipwa mamilioni ya shilingi? Au kwa sababu, Mheshimiwa Lowassa amesema serikali haifanyi maamuzi magumu?”

Nchimbi pia alisema Nape ni “mropokaji” anayevuruga chama.
Wengine walioshupaliwa kwa kuchangia kukidhoofisha chama ni Samwel Sitta na Dk. Harrison Mwakyembe ambao ni miongoni mwa waasisi wa Chama cha Jamii (CCJ) huku wakiwa bado viongozi na wanachama wa CCM. Hata hivyo, CCJ kilinyimwa usajili wa kudumu.
Aliyetoa hoja hiyo ni Hussen Bashe ambaye anajitambulisha ni kutoka kundi la Lowassa na Rostam. Habari zinasema kwamba Mukama alimwita Bashe na kumwomba agombee ubunge Igunga, lakini Bashe alimgomea kwa maelezo kuwa hana mizizi ya kisiasa katika jimbo hilo.
“Nilitaka ubunge wa Nzega, si Igunga. Huko si kwetu. Siwezi kwenda Igunga kwa sababu nataka mshindwe ili tuheshimiane,” Bashe alinukuliwa akimweleza Mukama.

Vile vile, vijana hao walimtaka Mukama aagize serikali imwondoe Sitta katika nyumba ya spika, kwa maelezo kwamba kitendo chake kung’ang’ania nyumba hiyo huku akijua alishaachia uspika ni kinyume cha utaratibu, na kinagombanisha wananchi na serikali yao.

Wednesday, July 6, 2011

Vinara kashfa ya rada watajwa

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Mathias Chikawe amesema Mbunge wa Bariadi Magharibi, Endrew Chenge (CCM), hahusiki kwa namna yoyote na kashfa ya uuzaji wa rada liyoligharimu Taifa pauni milioni 28 ambazo sasa Serikali inataka zirejeshwe.

Mbali na Chenge ambaye pia anatakiwa kujivua gamba ndani ya chama chake kwa kashfa hiyo, Chikawe alisema bungeni jana kuwa, hakuna Mtanzania hata mmoja anayetuhumiwa kwa hilo ndio maana hawajamshitaki mtu.

Akitoa majumuisho ya hotuba ya Ofisi ya Rais Utawala Bora, Chikawe alisema Serikali ililiita Shirika la Serious Fraud Office (SFO) la Uingereza kuja kumchunguza Chenge kwa kushirikiana na Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) na katika uchunguzi huo Chenge hakukutwa na hatia.

Aliwataja wahusika kuwa ni Sailesh Vithlan, dalali wa rada hiyo Jonathan Callman, Meneja Biashara wa Kampuni ya BAE Systems ya Uingereza iliyouza rada hiyo na Meneja Masoko wa kampuni hiyo, aliyejulikana kwa jina moja la Christopher.

"Kama kuna mtu ana ushahidi dhidi ya Chenge au mtu mwingine atupe na tutampeleka mtuhumiwa huyo mahakamani kesho.

"Kama hakuna, basi tufanye kama kanisani (wakati wa kufunga ndoa) kuwa yeyote mwenye neno naye (Chenge), aseme sasa na kama hakuna basi kila mtu anyamaze," alisema Chikawe.

Alifafanua kuwa Serikali haijamshitaki Chenge wala mtu yeyote na kufafanua kuwa haiwezi kwenda mahakamani kwa hisia na hata wanasheria wanafahamu hilo.

Hii ni mara ya tatu kwa Chenge kusafishwa na tuhuma hizo; mara ya kwanza aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Utawala Bora, Sophia Simba alikaririwa akisema kuwa Chenge alisafishwa na SFO.

Mara ya pili, Chenge mwenyewe alijitokeza mbele ya vyombo vya habari alipokuwa akigombea nafasi ya Spika wa Bunge na kufafanua kuwa SFO na Takukuru walimsafisha baada ya kukosa ushahidi dhidi yake.

Lakini Ubalozi wa Uingereza ulitoa tamko kuwa suala hilo halijakamilika wala halijafikiwa muafaka na Chenge hakupaswa kudai kuwa hana hatia.

Hata hivyo wakati wa Kamati ya Matumizi Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani, Tundu Lissu alisimama na kusema anayo barua inayoonesha kwamba Andrew Chenge na Dk. Idris Rashid walihusika katika ununuzi wa rada hiyo na Chenge alipata dola milioni 1 alizopeleka katika akaunti iliyopo nje ya nchi na Dk. Rashid alipata pauni za Kiingereza laki sita.

Hata hivyo Waziri Chikawe alisimama na kusema kwamba aliwaomba wabunge kama wana ushahidi dhidi ya Chenge waulete ili waende mahakamani hata kesho na akaomba Tundu Lissu ampatie ushahidi huo.

Lakini Lissu alisema ushahidi huo ni barua kutoka SFO kwenda kwa Mwanasheria Mkuu wa Tanzania na hivyo Serikali isiwahadae wananchi kwa sababu wanao ushahidi.

Kashfa hiyo hiyo, itakumbukwa kuwa ilichangia Chenge kujiuzulu nafasi yake kama Waziri wa Miundombinu baada ya kutuhumiwa kumiliki fedha zilizodaiwa kuwa mgawo wake katika uuzaji wa rada; dola milioni moja, zaidi ya Sh bilioni moja nje ya nchi.

Lakini jana kabla ya kutangazwa kuwa Chenge hana hatia, Serikali ilitupiwa zigo la kuwachukulia hatua za kisheria Watanzania waliohusika kupora fedha za umma katika ununuzi wa rada katika Mahakama ya Tanzania kwa kuwa katika Mahakama ya Uingereza, watuhumiwa hao hawatakuwa na hatia.

Ujumbe wa Bunge uliokwenda Uingereza kuwakilisha Watanzania kudai fedha hizo maarufu 'chenji' , umeweka wazi kuwa Kampuni ya BAE Systems inayotuhumiwa kushirikiana na watuhumiwa wa Tanzania katika uporaji huo na SFO, wameweka mazingira ya kutoshitakiwa kwa watuhumiwa hao huko Uingereza.

Wakizungumza baada ya kukabidhi ripoti ya kazi waliyoifanya huko Uingereza kwa Spika wa Bunge, Anne Makinda, wajumbe hao walioongozwa na Naibu Spika, Job Ndugai, walisema wamefanikiwa kushawishi Waingereza kuona umuhimu wa fedha hizo pauni milioni 29.5, kurudishwa kupitia Serikali ya Tanzania.

Lakini pia waliituhumu kampuni hiyo na SFO kwa kupanga mazingira hayo ya kutoshitakiwa kwa watuhumiwa kwa kutumia mwanya wa mazungumzo nje ya Mahakama.

Ndugai alisema baada ya SFO kuishitaki kampuni hiyo, kampuni hiyo iliomba mazungumzo nje ya Mahakama na yalipokamilika, Mwanasheria wa kampuni hiyo, ambayo ndiyo mtuhumiwa, alitengeneza makubaliano ya mazungumzo hayo na kuzuia watuhumiwa wasishitakiwe na kuyasajili mahakamani.

Ndugai alisema kuwa mwanasheria huyo alihakikisha anailinda kampuni hiyo na watuhumiwa wengine.

"Kwa kweli jaji aliyetoa hukumu ile, alikuwa na 'moral pressure' msukumo wa kibinadamu, akaona gharama za kesi ni kubwa akasema nitapunguza gharama za kesi na kuongeza katika tuzo itakayopewa Watanzania," alisema Ndugai.

Alifafanua kuwa katika hilo, badala ya kuamuru fedha nyingi ziwe gharama za kesi hizo ambazo zingetumiwa na SFO au kampuni hiyo; jaji huyo alitoa pauni laki tano tu kama gharama za kesi na pauni milioni 29.5 akaamuru zirejeshwe kwa Watanzania walioibiwa.

Friday, May 27, 2011

Tamko la Vijana Arusha lazidi kuivuruga CCM

















TAMKO la baadhi ya vijana wa UVCCM, Mkoa wa Arusha kutaka mafisadi wafukuzwe, limezidi kukivuruga chama hicho baada ya Katibu Mkuu, Wilson Mukama kusema hawezi kujiingiza 'kichwa kichwa' kuzungumzia suala hilo, huku baadhi ya watuhumiwa wakikataa kulizungumzia. Mukama alisema CCM inafuatilia kwa karibu mgogoro huo, lakini haiwezi kuuzungumzia sasa kwa kuwa hajapata taarifa rasmi kutoka umoja wa vijana.

Kwa mujibu wa Mukama, UVCCM ni jumuiya halali ya chama tawala yenye mamlaka kamili ya kuzungumzia matatizo yake, hivyo yeye kusema chochote itakuwa ni kuingilia kazi za jumuiya hiyo.
“Chama chetu kina utaratibu wake, UVCCM ni jumuiya ndani yake, hayo yaliyotokea kule Arusha siwezi kuyazungumzia, ila kesho (leo) tuna kikao, hivyo wao vijana watatupa taarifa zao,” alisema Mukama, huku akisoma ujumbe mfupi wa simu (sms) alioandikiwa na katibu mkuu wa umoja huo, Martin Shigella kuwa watatoa taarifa ya yaliyotokea Arusha.

“Suala la Arusha tunalifuatilia kwa ukaribu sana, ila utendaji tunawaachia wao (UV-CCM), nasi tukishapata taarifa zao ndio tutaweza kulizungumzia suala hilo, ila kwa sasa mtafute Shigella,” alielekeza Mukama.
Alipotafutwa kwa simu jana kuzungumzia tuhuma hizo, Shigella alisema kuwa hawezi kutolea ufafanuzi kwa kuwa alikuwa nje ya nchi kikazi. “Sikuwapo nchini, kwa hiyo sitaweza kuzungumza lolote, kuna mtu alikuwa akikaimu nafasi yangu, hivyo nikipata maelezo kutoka kwake nitakuwa tayari kuzungumza, nitafute kesho (leo),”alisema Shigella.

Naye makamu mwenyekiti wa umoja huo taifa, Benno Malisa alisema wamesikitishwa na kauli zilizotolewa na vijana wenzao wa Arusha, hivyo watatuma kamati ya maadili kwenda kuzungumza na makundi yanayolumbana. “Hivi karibuni Kamati ya Utekelezaji ya UVCCM itakaa na kutoa uamuzi, lakini ni baada ya Kamati ya Maadili itakayotumwa kuzungumza na wanachama wanaolumbana huko Arusha kuleta ripoti makao makuu ya umoja wetu,”Alisema Malisa.

Akizungumzia adhabu wanazoweza kupewa wanachama wa umoja huo, Malisa alisema adhabu hizo zitatokana na aina ya makosa watakayokutwa nayo. “Suala hili liko ndani ya uwezo wetu na tutalifanyia kazi na kuchukua hatua kwa mujibu wa kanuni za UVCCM, kama kutakuwa na makosa makubwa zaidi yatapelekwa  ngazi za juu zaidi,”alisema Malisa.

Juzi, UVCCM Mkoa wa Arusha waliuomba uongozi wa juu wa chama tawala kuwafukuza uanachama viongozi watatu, wakiwamo Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa na mwenzake wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge wanaotuhumiwa kwa ufisadi.

Vijana hao pia walikishauri chama hicho kupitia kamati yake ya maadili kuwaita na kuwahoji makada hao maarufu na baadaye kuwachukulia hatua, zikiwamo za kuwafukuza kwa maslahi ya chama na taifa. Tamko hilo lililosomwa na mjumbe wa baraza la umoja huo mkoani Arusha, Ali Babu lilitaka watuhumiwa hao waliowaita mapacha watatu, kuwa ndio chanzo cha kudhoofika kwa chama hicho tawala.

"Pia, tunasisitiza Andrew Chenge aondolewe kwenye Kamati ya Maadili ya CCM mara moja na kumtaka mtuhumiwa mwingine (jina tunalo) aondolewe pia kwenye uongozi wa ndani ya umoja wetu," ilieleza sehemu ya taarifa hiyo. Lakini, alipotafutwa jana kuzungumzia tuhuma hizo, Chenge alijibu kwa ufupi: "Kwa sasa sitaki kuzungumzia masuala hayo. Kila la heri."

Naye Lowassa alipotafutwa alisema kwa ufupi: ‘no comment’ akimaanisha kuwa hawezi kulizungumzia suala hilo.

Hata hivyo, wakati makada hao wakigoma kuzungumzia suala hilo, mwenyekiti wa umoja huo Mkoa wa Arusha, James ole Milya anayeshinikizwa kujiuzulu wadhifa huo, jana aliibuka na kudai kuwa tamko hilo lilitolewa na kundi la vijana aliowaita wahuni wa mitaani na wasiokuwa na kazi.

“Wale ni wahuni, hawana chochote wala lolote, wanapenda kukaa vijiweni hawana kazi za kufanya, tuna taarifa kwamba walitumwa na baadhi ya viongozi hapa Arusha kupindisha na kuvuruga hoja za umoja wetu mkoani  Arusha,” alisema Milya

Alisema kuwa vijana hao wakiongozwa na Ali Babu hawatambuliki ndani ya umoja huo, huku akisisitiza  kwamba hoja na malalamiko yote hupitishwa katika ngazi husika ili ziweze kufanyiwa kazi na sio kuibuka na kutoa matamshi yasiyo na tija.

Millya aliendeleza msimamo wake wa kutaka Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalumu aondoke madarakani kwa madai ya kusababisha jimbo kwenda upinzani (Chadema), huku akimtaka katibu huyo asikilize kilio chao (UVCCM) cha kumtaka aondoke. Alisema kuwa endapo kiongozi huyo ataendelea kung'ang'ania nafasi yake, basi atang’olewa kwa maandamano ya vijana yasiyokuwa na kikomo ambayo yatafanywa na wanachama wa umoja huo.

“Msimamo wetu uko pale pale, Chatanda ni lazima aondoke kwa kuwa amekivuruga chama chetu, ametuchonganisha na viongozi wa dini, lakini pia amesababisha Jimbo la Arusha Mjini liangukie upinzani kwa kukimbilia Tanga kusaka ubunge wa viti maalumu kipindi cha uchaguzi,”alisisitzia Milya.

Juzi,  katika mkutano wao wenye malengo makuu sita, vijana hao wa Mkoa wa Arusha walisema wanaunga mkono falsafa ya CCM ya kujivua gamba."Tunaipongeza na kuiunga mkono Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kwa kutambua kwamba mafisadi wamechangia sana kukidhoofisha na kukipotezea mvuto chama chetu mbele ya umma wa Watanzania," ilisema taarifa hiyo na kuongeza:
"Kwa mantiki hiyo tunatamka kwa kauli moja kwamba mapacha hao watatu wa ufisadi (wakiwataja kwa majina) na vibaraka wao wafukuzwe mara moja kwa maslahi ya CCM na Watanzania."