Showing posts with label rais. Show all posts
Showing posts with label rais. Show all posts

Tuesday, May 31, 2011

Marando: Tunamtaka Rais Kikwete mahakamani
















Kwa mujibu wa gazeti la Mwananchi, WAKILI Mabere Marando anayemtetea Profesa Costa Mahalu aliyekuwa na Balozi wa Tanzania nchini Italia, amesema ataiomba mahakama imlazimishe Rais Jakaya Kikwete kufika mahakamani kumtetea mteja mteja wake iwapo hatakubali kwenda kutoa ushahidi baada ya kuombwa kufanya hivyo kwa barua.Marando ametoa kauli hiyo wakati Profesa Mahalu na mwenzake Grace Martin wakianza kujitetea leo.

Mbali na utetezi wao binafsi, wanatarajia pia kuwa na mashahidi kadhaa wa kuwatetea akiwamo Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa pamoja na Rais Kikwete.Tayari Rais Mkapa amewasilisha mahakamani hapo hati yake ya kiapo akimtetea Profesa Mahalu na mwenzake kuhusiana na tuhuma zinazowakabili huku akibainisha kuwa yuko tayari kufika mahakamani iwapo italazimu.

Lakini hadi jana, Rais Kikwete alikuwa hajajibu barua aliyoandikiwa na Wakili Marando kwa niaba ya wateja wake wakimwomba akubali wa kufika mahakamani kuwatetea au kuwasilisha kiapo chake ambacho kitatumika kama ushahidi wa utetezi dhidi yao.

Marando alisema jana kuwa Rais Kikwete alikuwa hajajibu barua hiyo, lakini akasema ikiwa Profesa Mahalu atamaliza kujitetea pamoja na mashahidi wengine kabla Rais Kikwete hajakubali, wataiomba mahakama imkumbushe.

“Kama atakaidi hata baada ya mahakama kumwandikia, basi tutaomba kesi hiyo iahirishwe hadi mwaka 2016 (wakati atakapokuwa amemaliza muda wake wa urais) ili imlazimishe kuja kutoa ushahidi huo,” alisema Marando.

Mei 3, mwaka huu Wakili Marando alimwandikia barua Rais Kikwete yenye kumbukumbu namba MM/PCRM/2011/1 kupitia kwa Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo, akibainisha kuwa ni miongoni mwa mashahidi muhimu ambao wateja wao wamewaagiza wamwite.

Barua hiyo inabainisha kuwa umuhimu wa Rais Kikwete katika ushahidi huo wa utetezi unatokana na ukweli kwamba nyumba hiyo ya Ubalozi wa Italia ilinunuliwa wakati akiwa Waziri wa Mambo ya Nje na kwamba alikuwa na taarifa zote kuhusu mchakato wa ununuzi wake.

Mchakato huo, kwa mujibu wa barua hiyo ni pamoja na nguvu ya kisheria aliyopewa mteja wao ambayo ilisainiwa na Rais Kikwete wakati huo akiwa Waziri Septemba 24, 2004 pamoja na hotuba yake aliyoitoa Bungeni Agosti 3, 2004 akithibitisha kuwa ununuzi wa jengo hilo haukuwa na mushkeli wowote.

Pia barua hiyo inaweka wazi kuwa kuna barua nyingi tu ambazo Profesa Mahalu alimwandikia Kikwete akiwa waziri, pamoja na katibu mkuu wa wizara hiyo, ambazo anapaswa kuzitambua mahakamani wakati wa utetezi.

“Kwa hiyo tunaomba kwa unyenyekevu kabisa, uweke barua yetu hii mbele ya Mh. Rais wa Jamhuri ya Muungano Tanzania; aisome na akueleze utujibu kama hana pingamizi kuja kueleza ukweli mahakamani. Kama muda wake hauruhusu, kulingana na ratiba zake za kitaifa, tunaomba aturuhusu tumwandalie kiapo (affidavit) kitakachoeleza yaliyotekea ili tukiwasilishe mahakamani badala ya kumwita yeye mahakamani”, inasisitiza barua hiyo na kuongeza kuwa hakuna kifungu cha Katiba kinachozuia Rais kuitwa kutoa ushahidi mahakamani.

Katika kiapo chake alichokiwasilisha mahakamani, Mkapa anamtetea Mahalu na akidai kuwa amefanya naye kazi kwa muda mrefu na anamjua kuwa ni mtu mwaminifu, mtiifu na mchakapakazi. Mkapa alieleza katika hati yake hiyo kuwa mchakato wa ununuzi wa jengo hilo ulifanyika wakati wa uongozi wake na kwamba alikuwa akijua kila kilichokuwa kikiendelea kuhusiana na ununuzi huo na kwamba ulifanyika kwa mujibu wa sheria.

Alifafanua kuwa mpango wa ununuzi wa jengo hilo ulikuwa ni utekelezaji wa sera ya serikali wa kuwa na majengo yake ya kudumu katika kila ubalozi kwa kununua au kujenga ikiwa ni njia ya kupunguza gharama za upangaji. Aliongeza kuwa serikali yake ilimpa Profesa Mahalu mamlaka yote kupitia nguvu ya kisheria ya kusimamia na kutekeleza mchakato wa ununuzi wa jengo.

Mkapa alisisitiza kuwa kupitia utaratibu wa serikali, alikuwa akijua kuwa taarifa ya uthamini wa jengo hilo iliyofanywa na Wizara ya Ujenzi ilikuwa ni Dola za Marekani 3.0 milioni wakati Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ilikadiriwa Euro 5.5 milioni: “Kupitia utaratibu wa serikali nilifahamu kuwa jengo hilo lilinunuliwa kwa gharama ya Dola za Marekani 3.0milioni sawa na Euro 3,098,741.40,” alisema Mkapa.
Pia Mkapa alisisitiza kuwa alikuwa na bado anatambua taarifa ya serikali bungeni ya Agosti 3, 2004 iliyoeleza na kuthibitisha kuwa taratibu zote za ununuzi wa jengo hilo zilifuatwa kwa mujibu wa maelekezo ya serikali na kwamba dalali alilipwa kikamilifu.

“Kwa kipindi chote ambacho nimefanya kazi na Balozi Mahalu katika nafasi mbalimbali za utumishi wa serikali ameonyesha tabia thabiti na za dhati, uaminifu, utiifu, uchapakazi na ubora," alisema Mkapa.

Alisema kuwa sifa hizo zilimfanya atunukiwe na Rais wa Italia, Tuzo ya Heshima ya Juu wakati wa kuadhimisha Siku ya Taifa hilo, muda mrefu baada ya kuwa ameondoka nchini humo.

Profesa Mahalu na mwenzake, Martin aliyekuwa Ofisa Utawala wa ubalozi huo wanakabiliwa na mashtaka hayo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakidaiwa kuhujumu uchumi kwa kuisababishia Serikali hasara ya Euro 2,065,827.60. Wanadaiwa kusababisha hasara hiyo kupitia mchakato wa ununuzi wa jengo la ubalozi huo, wakati wa utumishi wao.

Kutokana na mashtaka hayo, leo wanadiplomasia hao wanaanza kujitetea baada ya mahakama hiyo kuwaona kuwa wana kesi ya kujibu.Mahalu na Martin wanadaiwa kula njama na kutenda makosa hayo katika tarehe tofauti na katika maeneo tofauti huko Italia, likiwamo la kumpotosha mwajiri wao katika hati ya matumizi.

Miongoni mwa mashtaka hayo ni kwamba Septemba 23, 2002 huko Rome, washtakiwa wakiwa waajiriwa wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, walisaini vocha yenye namba D2/9/23/9/02 ikionyesha kuwa bei ya ununuzi wa jengo la ubalozi ni Euro 3,098,741.58, maelezo ambayo yalikuwa ni ya uongo na yenye nia ya kumdanganya mwajiri wao.

Monday, May 30, 2011

Mtikila: Ridhiwani nenda mahakamani




Mchungaji Christopher Mtikila
LICHA ya mtoto wa Rais Jakaya Kikwete, Ridhiwani kuwaandikia barua ya kusudio la siku 10 kuwafikisha mahakamani Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa na Mwenyekiti wa Democratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila, ameambiwa aende huko mahakamani.

Katika kusudio lake Ridhiwani amedai kuwa endapo watashindwa kumwomba radhi na kumlipa Sh2 bilioni atakwenda mahakamani.Katika kusudio hilo, Ridhiwani amewataka wanasiasa hao wamwombe radhi na kumlipa fidia hiyo ndani ya siku kumi kuanzia Mei 13, kwa madai waliyoyatoa hadharani kuwa yeye ni bilionea aliyetajirika kifisadi.

Katika kusudio hilo, Ridhiwani pia amehusisha gazeti la Tanzania Daima ambalo amedai limechangia kumchafua kwa kuripoti madai ya wanasiasa hao dhidi yake.

“Tumeelekezwa na mteja wetu kuwataka wote kwa pamoja kukanusha na kusahihisha tuhuma zote na kuchapisha habari hiyo ya kuomba radhi kwa uzito na herufi kubwa (bold print) katika kurasa za mbele  wa gazeti hilo (Tanzania Daima) kwa siku tatu mfululizo hadi Mei 23, 2011," alieleza wakili Sam Mapande wa Law Associates, anayemwakilisha Ridhiwani.Wakili huyo aliendelea, "Pia, wote kwa pamoja mnatakiwa kulipa fidia ya Sh2 bilioni kwa madhara ya jumla aliyopata mteja wetu.”

Barua hiyo ya kurasa sita  imetaja baadhi ya maneno yaliyoandikwa kwenye matoleo mawili ya gazeti la Tanzania Daima yakimkariri Dk Slaa na Mchungaji Mtikila, wakimhusisha pia Rais Jakaya Kikwete na mwanaye (Ridhwani) na watu wengine walio karibu yake na matukio ya ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka na ofisi ya umma. Kwa mujibu wa Ridhiwani, madai hayo yamemchafulia jina, kumdhalilisha, kumshushia hadhi na heshima yake katika jamii inayomzunguka.

Mhariri wa gazeti la Tanzania Daima, Absalom Kibanda amekiri kupokea barua hiyo, lakini akasema hawezi kusema chochote kwa jambo ambalo ni la kisheria. “Kwa kuwa bado hatujafikishwa mahakamani, siwezi kusema tumejiunga vipi. Tunasubiri tufikishwe mahakamani kwanza,” alisema Kibanda.

Mchungaji Christopher Mtikila amemtaka mtoto huyo wa rais kwenda mahakamani haraka akidai kuwa hana shaka kwa kuwa ana ushahidi mzito kuthibitisha madai yake.Mtikila aliwaambia waandishi wa habari mjini Arusha jana kuwa, kesi hiyo itakuwa ni ukombozi kwa taifa kwa sababu itampa yeye na mwenzake, Dk Slaa muda wa kueleza kile alichokiita madudu yanayofanywa na mtoto huyo wa rais.
Mtikila aliendelea kudai kuwa Ridhwani anatumia vibaya ofisi na madaraka ya baba yake (Rais Kikwete) kujilimbikizia mali kinyume cha sheria.

“Kitendo cha Ridhwani kutaka aombwe radhi na fidia ni njia na ngazi muhimu itakayosaidia mambo mengi yaliyojificha kuwekwa hadharani," alisema Mtikila na kuongeza:"Tutatumia sheria zilizopo kuwabana wote ambao majina yao yameandikishwa kwenye mali za vigogo nchini waeleze walivyopata mali hizo na hapo ndipo watakapowataja wahusika halisi,” alisema Mtikila.

Kiongozi huyo wa DP aliendelea kudai kuwa viongozi wengi nchini wamejilimbikizia mali kupitia wizi na ufisadi, wakitumia nafasi zao za umma huku wakiandikisha majina ya watu wengine kwenye mali hizo kuficha umiliki wao.

Alidai kuwa kesi anayotaka kuifungua Ridhiwani itaibua mambo mengi kwani walioandikishwa majina kwenye mali hizo, watawataja wamiliki halisi badala ya kufungwa jela kwa kumiliki mali inayodhaniwa kuwa ya wizi au kupatikana isivyo halali.

Kwa upande wake, Dk Slaa jana hakupatikana kuzungumzia kusudio hilo la Ridhiwani kutokana na simu yake ya kiganjani kutopatikana kwa siku nzima.

Jana, Ridhiwani alipotakiwa kueleza nini kinafuata baada ya muda aliotoa kuisha alijibu kwa ufupi kuwa asingependa kuzungumzia suala hilo kwa kuwa ni jambo la kisheria na kwamba sheria ina kanuni zake.

"Ndugu yangu, sitaki kuzungumzia hili kwa kuwa sheria ina kanuni zake. Hili litazungumzwa mahakamani."
Dk Slaa na Mtikila walikaririwa mwanzo wa Mei wakisema kuwa mtoto huyo wa rais ana utajiri mkubwa licha ya kumaliza shule miaka ya karibuni huku wakimtuhumu kutumia cheo na madaraka ya baba yake kujitajirisha.