Showing posts with label slaa. Show all posts
Showing posts with label slaa. Show all posts

Monday, August 8, 2011

Chadema yafukuza madiwani 5 Arusha

KAMATI Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), imewafukuza uanachama madiwani watano wa chama hicho mkoani Arusha kwa kutotekeleza maagizo ya kamati hiyo na hivyo kuweka wazi kata tano za mkoa huo kwa ajili ya uchaguzi mdogo.

Aidha, madiwani watano watiifu wa chama hicho, wameamriwa kutohudhuria vikao vya Baraza la Madiwani la Jiji hilo hadi hapo muafaka mpya wa mgogoro wa umeya unaoendelezwa katika jiji hilo utakapopatikana.

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alitangaza adhabu hiyo jana aliyoiita kuwa ni uamuzi mgumu wa chama hicho katika kikao na waandishi huku akisema katika uamuzi huo, chama hakikufurahi.

“Uamuzi huu ni mzito na wa majonzi, hata chama hakikufurahi kuyafanya, ila kwa kuwa tunasimamia utashi wa chama, ikifikia hatua kama hii hatuna budi kuchukua hatua,” alisema Mbowe.

Hakufafanua kutofurahi huko kwa chama na mantiki ya neno utashi katika ujenzi wa demokrasia, lakini katika duru za kisiasa, kumekuwa na hoja; kuhusu madaraka ya chama cha siasa katika kumuondoa kiongozi aliyechaguliwa na wananchi, kama ndiyo demokrasia ya kweli.

Baadhi ya wasomi na wazee, akiwemo hata Waziri Mkuu mstaafu, Joseph Warioba, alifikia hatua ya kuwataka Watanzania katika mjadala ujao wa Katiba mpya, kuhoji uhalali wa madaraka ya vyama vya siasa, vyenye wanachama wachache kutengua uamuzi wa wananchi walio wengi.

Mbali na hukumu hiyo, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa alisema Kamati Kuu inaendelea na msimamo wake wa kutomtambua Meya wa Arusha, Gaudance Lyimo (CCM) hadi hapo mazungumzo ya muafaka mpya yatakapopatikana.

Katika hilo, wajumbe wa Kamati hiyo, akiwemo Dk. Slaa na Naibu Katibu Mkuu, Kabwe Zitto Alhamisi wiki hii watafanya mkutano wa hadhara kufafanua hukumu hiyo kwa wananchi.

Waathirika wa hukumu hiyo ni aliyekuwa Naibu Meya na Diwani wa Kimandolu, Estomih Mallah; Diwani wa Elerai, John Bayo; Diwani wa Themi, Reuben Ngowi; Diwani wa Kaloleni, Charles Mpanda na Diwani wa Viti Maalumu Rehema Mohamed.

Diwani wa Kata ya Sekei, Crispin Tarimo yeye hukumu yake imesogezwa mbele ili apate nafasi ya kujitetea mbele ya Kamati hiyo kwa kuwa wakati wenzake wakijitetea mjini hapa, alitoa udhuru kuwa ni mgonjwa.

Hata hivyo, wakati akina Dk. Slaa wanajipanga kufanya mkutano wa hadhara Alhamisi wiki hii, Bayo mbali na kueleza nia ya kukata rufaa, alisema mgogoro si kati ya madiwani hao na Kamati Kuu; bali na Mbunge wa Arusha, Godbless Lema (Chadema).

Aliongeza kuwa na wao watakwenda kufanya mikutano ya hadhara kuwaeleza wananchi waliowachagua kilichowatokea. Mallah alipoulizwa kwa simu, alisema anasubiri barua ya kufukuzwa uanachama na kuweka wazi kuwa hajaridhika na atakata rufaa.

Safari ya kisiasa ya kuwang’oa madiwani hao ilianzia kwa Lema (Chadema), ambaye alikuwa wa kwanza kupinga muafaka wa kisiasa kati ya Chadema na CCM mkoani Arusha. Baadaye Lema aliungwa mkono na uongozi wa juu wa Chadema, ambao ulitaka madiwani hao kuvunja muafaka huo lakini madiwani hao wakasisitiza lengo lao lilikuwa maslahi ya maendeleo ya Arusha kuliko misuguano ya kisiasa.

Mbowe katika maelezo yake jana, alikumbusha kuwa baada ya madiwani hao kukubali kumtambua Meya Lyimo (CCM) katika muafaka huo, Chadema iliwataka wajiuzulu nafasi zao walizopata baada ya muafaka na kuomba radhi.

Nafasi hizo ni pamoja na ya Naibu Meya ambayo Mallah alichaguliwa kuichukua na uongozi wa Kamati ya Huduma za Uchumi, Elimu na Afya, ambayo Bayo alichaguliwa Mwenyekiti.

Madiwani hao wakiungwa mkono na wenzao walikaidi agizo la kutakiwa kujiuzulu na kuomba radhi kwa madai kuwa hawakutaka kuendeleza msuguano wa kisiasa, walitaka kuweka maslahi ya wananchi mbele na si ya chama.

Pia walilalamikia kauli za baadhi ya viongozi wa kitaifa wa Chadema akiwemo Dk. Slaa, kuwa wamekula rushwa na wakataka kiongozi huyo wa kitaifa kuomba radhi. Mbowe alisisitiza kuwa madiwani hao watapewa barua, kwa kuwa kitendo cha madiwani hao kukaidi agizo hilo ni utomvu wa nidhamu na pia ni kuvunja maadili na kanuni za chama na kuenda kinyume na msingi mama wa Chadema wa uwajibikaji.

Kuhusu kukata rufaa, Dk. Slaa alisema, madiwani hao wanaweza kufanya hivyo kwenye Baraza Kuu la chama hicho.

Katika hatua nyingine, Kamati hiyo imepokea taarifa ya mazungumzo baina ya Mwenyekiti wao na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuhusu nia na azma ya kumaliza mgogoro wa umeya jijini Arusha.

Akielezea mazungumzo hayo, Mbowe alisema wamekubaliana na Waziri Mkuu, Pinda kuunda kamati ya kushughulikia mgogoro wa umeya jijini Arusha itakayojumuisha wajumbe kutoka vyama viwili. Wajumbe hao watatoka CCM na wengine Chadema, na kamati hiyo itakuwa chini ya uenyekiti wa Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, John Tendwa.

Monday, June 6, 2011

Hali tete: Chadema, Polisi wakwaruzana

Askari polisi wakilinda kwenye kituo kikuu cha polisi kati anakoshikiliwa mwenyekiti wa Chadema Freeman MbowePicha na Fidelis Felix/Silvan Kiwale


















JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, jana lililazimika kuimarisha ulinzi katika Kituo chake Kikuu (Central) na baadhi ya maeneo ya jiji kukabiliana na tishio la wanachama wa Chadema kuandamana ili kushinikiza Mwenyekiti wao, Freeman Mbowe aliyekamatwa juzi aachiwe.Mbowe ambaye alikamatwa juzi ikiwa ni kutekeleza amri ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha iliyoamuru akamatwe popote alipo na afikishwe hapo kwa kutotii amri ya kufika mahakamani katika kesi inayomkabili, alitarajiwa kupelekwa huko wakati wowote kuanzia jana akiwa chini ya ulinzi.

Jana, vijana wa Chadema walikusanyika katika kituo hicho huku wakilaani kitendo cha kukamatwa kwa mwenyekiti wao huku wengine wakijikusanya katika vikundi vidogovidogo katika maeneo mbalimbali katika Barabara za Morogoro na Nyerere, lengo likiwa kushinikiza kiongozi huyo atolewe rumande na asisafirishwe kupelekwa Arusha.

Taarifa kutoka Arusha ambako kesi ya kiongozi huyo inatarajiwa kuendelea leo asubuhi zinaeleza kuwa polisi jana jioni waliendesha msako wa wanachama wa Chadema waliokuwa wakihamasishana kuhudhuria kwa wingi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Arusha.

Wanachama na mashabiki hao wa Chadema walidai kwamba kitendo cha kukamatwa kwa kiongozi huyo wa kambi ya upinzani bungeni ni mpango uliobuniwa na CCM wa kubinya demokrasia ya vyama vingi nchini.

Mbowe na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Bara, Zitto Kabwe walikamatwa katika maeneo tofauti nchini juzi. Wakati Mbowe alidaiwa kutotii amri ya mahakama, Zitto alidaiwa kuzidisha muda wakati wa kuhutubia mkutano wa hadhara mkoani Singida.

“Tumeongea na polisi, bado wanamng'ang'ania Mbowe. Msimamo wao ni kumpeleka Arusha, tuangalie utaratibu utakaotumika katika kumsafirisha,” alisema Mkurugenzi wa Mambo ya Nje wa Chadema, John Mnyika.

Baada ya kauli hiyo ya Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubunge, vijana wa chama hicho wakiongozwa na Diwani wa Kata ya Ubungo, Boniface Jacob walianza kuimba nyimbo za kulaani kukamatwa kwa mwenyekiti wao huku wakisema muziki wa Chadema polisi hawauwezi.

Ofisa mmoja mwadamizi wa Polisi Ilala ambaye hakujitambulisha jina aliwaambia vijana hao kuwa polisi  walishakubaliana na viongozi wa Chadema kuwa mtuhumiwa huyo amepangiwa utaratibu wa kusafirishwa kwenda Arusha kuhudhuria kesi yake.Ofisa huyo aliwataka wananchi waliokuwa kwenye eneo hilo kuondoka ili kupisha jeshi hilo kuendelea na kazi ya kutoa huduma kwa watu wengine.

“Tumeshaongeza na wakubwa wenu, hiki ni kituo cha polisi watu mbalimbali wanakuja kupata huduma hapa. Mtu haji kuangaliwa kwa aina hii ya hamasa na nyimbo, tunaomba muondoke,” alisema ofisa huyo.Kauli hiyo ilipingwa na vijana hao wakisema ofisa huyo ni mtu wa kawaida hawezi kuwaeleza mambo kama hayo.

“Sisi hapa tuna viongozi wetu mambo kama hayo tungeelezwa na kuelewa kama yangesemwa nao na si mtu wa kawaida kama wewe,”alisikika mmoja wa wanachama hao akisema kwa sauti.

Kauli hiyo ilimshangaza ofisa mwingine wa polisi aliyeibuka na kuhoji: “Mnasema huyu ni mtu wa kawaida? Akajibiwa “ndiyo”, “huyo siyo mtu wa kawaida."Vijana hao waliendelea na msimamo wao: “Sisi tunasema huyo ni mtu wa kawaida kwa sababu siyo kiongozi wetu, ndiyo maana tunasema angekuwa kiongozi wetu tungemwelewa.”

Kauli hiyo ilimlazimisha Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Faustine Shilogile kujitokeza na kuwataka watu hao kuondoka katika eneo hilo kwa sababu kulikuwa na shughuli mbalimbali zilizokuwa zikiendelea.

“Tumeongea na viongozi wenu, tumeshakubaliana tunawaomba mtawanyike na sisi tuendelee na kazi, sitaki mkusanyiko wowote katika kituo cha polisi,” alisema Shilogile. Mara baada ya kauli hiyo gari la maji ya kuwasha lilianza kusogea walipokuwa wafuasi hao wa Chadema likitanguliwa na Polisi wa Kutuliza Ghasia waliokuwa wakiwafukuza katika eneo hilo.

Kundi hilo liliondoka na kuelekea makao makuu ya Chadema ambako Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa alikuwa na mkutano na waandishi wa habari.

Msimamo wa Kamanda Kova
Akizungumzia mvutano huo, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema jeshi lake haliwezi kumwachia Mbowe kwa sababu wanaheshimu amri ya Mahakama.

Kova aliwaambia waandishi wa habari jana kwamba jeshi hilo lilipokea amri ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha ya kumkamata kiongozi huyo wa Chadema na kwamba hawaruhusiwi kuhoji lolote juu ya amri hiyo.

“Sisi kama jeshi la Polisi tumepokea amri ya mahakama ya kumtia hatiani Mheshimiwa Mbowe na hatuna mamlaka ya kumwachia huru hadi mahakama itoe amri ya kumwachia,”alisema.

Alisema sheria hairuhusu kuhoji sababu za amri inayotolewa na mahakama na kufafanua kuwa hizo ni sheria zilizotungwa na wabunge wenyewe. Alisema Mbowe anatarajiwa kusafirishwa chini ya ulinzi wa Polisi kwenda mkoani Arusha kujibu kesi inayomkabili na kwamba taratibu zote za safari tayari zimekamilika.

“Tunachokifanya ni maagizo ambayo yametoka ngazi ya juu kuhusu suala hili kwa hiyo Mbowe atapelekwa Arusha chini ya ulinzi wa polisi muda wowote kuanzia sasa alimradi awahi muda wake wa mahakama,”alisema Kova.

Alisema atapelekwa Arusha chini ya ulinzi wa polisi kwa sababu amekiuka masharti yake ya dhamana na kwamba tayari wamezungumza na baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani waliokwenda kumuona kiongozi huyo wa kambi ya upinzani bungeni jana.

Kova alisema kulingana na taratibu na sheria za Tanzania, mahakama ikitoa amri hakuna mtu anayeweza kuipinga.

Aliwataka wananchi watulie na kuipa fursa mahakama itekeleze sheria zilizotungwa na Bunge. Akizungumzia kukamatwa kwa Mbowe, Mnyika alisema hizo ni njama za kuudhalilisha upinzani na pia mbinu za kumtaka Mbunge huyo wa Hai asihudhurie kwenye Kikao cha Bunge la Bajeti.

“Endapo watashindwa kutumia busara za mazungumzo tuliyoyafanya kumwachia Mbowe, jambo hili tutalirudisha kwa wananchi na nguvu ya umma itatumika kusuluhisha tatizo hilo,” alisema.

Alisema amani ni tunda la haki lakini inaweza kupotea kama haki haitatendeka na kuongeza kuwa kuna watu ambao wanashutuma nzito za ufisadi, lakini hawachukuliwi hatua zozote isipokuwa viongozi wa upinzani.


Tamko la Dk Slaa
Dk Slaa alisema kesi zinazowakabili viongozi wa chama hicho na wabunge wa vyama vya upinzani vinalifedhehesha Bunge la Tanzania kimataifa.

“Ili mtuhumiwa akamatwe sheria iko wazi, notisi zilitakiwa kutolewa kwa mdhamini wake na pia kwa wakili, lakini kwa Mbowe haikuwa hivyo na hiyo inaonyesha ni agizo kutoka mahali Fulani,” alidai.

“Polisi mkoa wa Mwanza wametuma barua kwa Katibu wa Bunge kuomba kibali cha kwenda kumhoji Mbunge wa Jimbo la Busega, Dk Titus Kamani, iweje kwa wabunge wa upinzani kukamatwa bila utaratibu? Alihoji Dk Slaa.

Alisema kutokana na mazingira hayo kama Mbowe hatafikishwa leo mahakamani wabunge wa Chadema hawataingia bungeni.

Kuhusu uwakilishi kwenye kamati ya uongozi alisema hata kama Zitto atakuwa nje ya mahabusu, hataingia kuwakilisha upinzani kwa sababu anayetakiwa kumpa kibali cha kufanya hivyo yupo ndani.

Kuhusu kosa la Zitto kukamatwa na polisi alisema inashangaza kwa sababu alikuwa kwenye mkutano wa hadhara kama mbunge na alizidisha dakika 20 kwenye mkutano huo.

Alisema hiki siyo kipindi cha kampeni na Zitto ni kiongozi mwenye haki ya kufanya hivyo na kusisitiza kilichofanyika kimelenga kufifisha demokrasia nchini.

Friday, June 3, 2011

Mahakama yaamuru Mbowe akamatwe

















 MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Arusha, imetoa amri ya kukamatwa kwa Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe popote alipo na kufikishwa mahakamani hapo kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kutotii amri ya kufika mahakamani hapo. Mahakama hiyo pia imemtaka mdhamini wa Mbowe aliyetajwa kwa jina la Julius Isaya Magwe, kufika mahakamani hapo mara moja ili kuieleza mahakama hiyo sababu za kutotii amri ya mahakama pale anapohitajika.

Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Charles Magesa alisema jana kuwa kimsingi Mahakama inakubaliana na hoja ya wakili upande wa Serikali kuitaka mahakama kutoa amri ya kukamatwa kwa Mbowe kwa sababu ya kutotii amri ya kufika mahakamani au kumtuma mdhamini wake. Alisema sababu iliyotolewa mahakamani hapo kwamba mshtakiwa huyo ni mbunge na yupo kwenye vikao vya Kamati za Bunge haina uzito kwa kuwa hiyo ni moja ya shughuli zake kama ilivyo shughuli nyingine kwa watumishi wa serikali.

“Hivyo basi kama ni shughuli zake za kawaida, haimzuii kutii amri ya mahakama pale anapoitwa bila kujali anaitiwa nini,” alisema Magesa. Hakimu Magesa alisema kuwa anachokumbuka ni kwamba Mahakama hiyo kweli ilipokewa maelezo ya kuwa washtakiwa hawatahudhuria mahakamani hapo Mei 27 mwaka huu kwa sababu ya kuwa katika vikao vya Kamati za Bunge na kuagiza waje wadhamini wao siku kesi inapotajwa. Ndiyo sababu Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini alimpeleka mdhamini wake mahakamani hapo.

Lakini, kabla ya kuhitimisha agizo hilo, hakimu huyo, awali alitoa amri ya kutaka kukamatwa kwa Mbunge wa Moshi Mjini, Philimon Ndesamburo, ambaye naye hakutii amri ya mahakama kwa kutofika Mei 27, 30 na 31 na hata jana.

Hata hivyo, baada ya kutoa amri ya kukamatwa kwa Ndesamburo ambaye naye ni mshtakiwa, ghafla alijitokeza mdhamini wake, Rubeni Ngowi na kuiambia mahakama hiyo kuwa alikuwapo Mei 30, ila hakuweza kusogea mbele kwa sababu ya woga wa mahakama na kwa kuwa hakuitwa. Baada ya maelezo hayo, Hakimu Magesa alimhoji mdhamini huyo akitaka kujua alikuwa wapi Mei 27 mwaka huu kesi hiyo ilipotajwa. Ngowi alijitetea kuwa alikwenda jijini Dar es Salaam kwa familia yake ambayo ilikuwa ina matatizo, lakini Mei 30 alifika mahakamani hapo na kuomba kuondoa amri hiyo ya kukamatwa kwa mshtakiwa wake.

“Basi kwa sababu nakumbuka ulikuwapo Mei 30 na nilikuona hapa mahakamani ukimnong’oneza wakili Kimomogoro, basi naondoa amri hii. Ila naomba utii amri ya mahakama pale mshtakiwa anapokosa uje kutoa sababu za kukosa kwake,” alisema Magesa.

Hakimu Magesa pia alitoa onyo kwa washtakiwa wengine wakiongozwa na Dk Willibrod Slaa wasiache kufika mahakamani, kila siku kesi yao inapotajwa na pale wanapokuwa na sababu ya kutofika, wahakikishe wadhamini wao wanakuwapo kutoa sababu za kukosekana kwao.

Akitoa uamuzi wa hatima ya dhamana za washtakiwa wa kesi inayowakabili viongozi wa Chadema, Godbless Lema, Joseph Selasini na wafuasi wao, Hakimu Mkazi Magesa, alisema Mahakama hiyo imeondoa hati ya kukamatwa kwa washtakiwa hao kama ilivyoamriwa awali na kutupilia mbali ombi la wakili wa serikali la kutaka wafutiwe dhamana.

Alisema kuwa kutokana na kupitia kwa makini maelezo ya utetezi wa pande zote mbili kwa Wakili wa Serikali, Edwin Kakolaki na wakili upande wa utetezi, Medhod Kimomogoro, Mahakama hiyo imeamua kuwapatia dhamana ya kudumu washtakiwa ambao ni Dk Slaa na wenzake, kwa kutii amri ya Mahakama.

“Mahakama hii imeamua kufuta amri ya dhamana ya muda na kuacha dhamana ya awali kwa sababu mara mahakama hii ilipotoa amri ya kuwakamata Mei 27 mwaka huu, washtakiwa hao walifika mahakamani hapa kujisalimisha wenyewe na wengine, akiwamo Mbunge Joseph Selasini, alituma mdhamini wake, hivyo nawaachia dhamana zao,” alisema Magesa.

Kesi hiyo ilifunguliwa na Serikali, Januari 5 mwaka huu ambapo washtakiwa 19 walifikishwa mahakamani hapo na kusomewa shtaka la kufanya kusanyiko pasipo na kibali na kutoa maneno ya uchochezi. Washtakiwa walikana makosa yao na kwa sasa wako nje kwa dhamana hadi Juni 24 mwaka huu kesi hiyo itakapotajwa tena.

Akizungumza na Mwananchi jana jioni, Mbowe alisema anatarajia kutoa tamko kuhusu suala hilo leo saa tano asubuhi jijini Dar es Salaam, lakini alikataa kutaja ni wapi mkutano wake na waandishi wa habari utafanyika.

“Nitatoa tamko kesho, lakini nasikitishwa na tafsiri hii ya Mahakama kwamba mimi nimekaidi amri ya kufika katika vikao vya mahakama. Nasema hivyo kwa sababu mara ya mwisho tulipokuwa mahakamani, tulipewa ruhusa ya kuhudhuria vikao vya Kamati za Bunge,” alisema Mbowe na kuongeza:
“Sasa sijui tafsiri yake ni nini, lakini niseme tu kwamba haya yote kuhusu sakata la Arusha na amri za polisi kuwakamata wabunge wa opposition (upinzani) nitalizungumza kesho (leo) kwa vyombo vya habari”.

Kwa mujibu wa Mbowe, waliomba ruhusa ili kuwawezesha kushiriki vikao vya Kamati za Bunge kutokana na umuhimu wa masuala ya bajeti kwa umma ambayo pia yanawagusa mahakimu na Idara ya Mahakama kwa jumla.

“…hebu kama mnakumbuka, katika Bunge lililopita tulijadili ule muswada wa sheria unaogusa idara ya mahakama sisi wabunge wa upinzani tulitumia nguvu kubwa kuwatetea mahakimu katika mambo mengi. Sasa katika suala hili la bajeti si vizuri tukikosekana kwenye vikao na ndiyo maana tuliomba ruhusa siku ile na tukaruhusiwa, ”alisema Mbowe.

Monday, May 30, 2011

Mtikila: Ridhiwani nenda mahakamani




Mchungaji Christopher Mtikila
LICHA ya mtoto wa Rais Jakaya Kikwete, Ridhiwani kuwaandikia barua ya kusudio la siku 10 kuwafikisha mahakamani Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa na Mwenyekiti wa Democratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila, ameambiwa aende huko mahakamani.

Katika kusudio lake Ridhiwani amedai kuwa endapo watashindwa kumwomba radhi na kumlipa Sh2 bilioni atakwenda mahakamani.Katika kusudio hilo, Ridhiwani amewataka wanasiasa hao wamwombe radhi na kumlipa fidia hiyo ndani ya siku kumi kuanzia Mei 13, kwa madai waliyoyatoa hadharani kuwa yeye ni bilionea aliyetajirika kifisadi.

Katika kusudio hilo, Ridhiwani pia amehusisha gazeti la Tanzania Daima ambalo amedai limechangia kumchafua kwa kuripoti madai ya wanasiasa hao dhidi yake.

“Tumeelekezwa na mteja wetu kuwataka wote kwa pamoja kukanusha na kusahihisha tuhuma zote na kuchapisha habari hiyo ya kuomba radhi kwa uzito na herufi kubwa (bold print) katika kurasa za mbele  wa gazeti hilo (Tanzania Daima) kwa siku tatu mfululizo hadi Mei 23, 2011," alieleza wakili Sam Mapande wa Law Associates, anayemwakilisha Ridhiwani.Wakili huyo aliendelea, "Pia, wote kwa pamoja mnatakiwa kulipa fidia ya Sh2 bilioni kwa madhara ya jumla aliyopata mteja wetu.”

Barua hiyo ya kurasa sita  imetaja baadhi ya maneno yaliyoandikwa kwenye matoleo mawili ya gazeti la Tanzania Daima yakimkariri Dk Slaa na Mchungaji Mtikila, wakimhusisha pia Rais Jakaya Kikwete na mwanaye (Ridhwani) na watu wengine walio karibu yake na matukio ya ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka na ofisi ya umma. Kwa mujibu wa Ridhiwani, madai hayo yamemchafulia jina, kumdhalilisha, kumshushia hadhi na heshima yake katika jamii inayomzunguka.

Mhariri wa gazeti la Tanzania Daima, Absalom Kibanda amekiri kupokea barua hiyo, lakini akasema hawezi kusema chochote kwa jambo ambalo ni la kisheria. “Kwa kuwa bado hatujafikishwa mahakamani, siwezi kusema tumejiunga vipi. Tunasubiri tufikishwe mahakamani kwanza,” alisema Kibanda.

Mchungaji Christopher Mtikila amemtaka mtoto huyo wa rais kwenda mahakamani haraka akidai kuwa hana shaka kwa kuwa ana ushahidi mzito kuthibitisha madai yake.Mtikila aliwaambia waandishi wa habari mjini Arusha jana kuwa, kesi hiyo itakuwa ni ukombozi kwa taifa kwa sababu itampa yeye na mwenzake, Dk Slaa muda wa kueleza kile alichokiita madudu yanayofanywa na mtoto huyo wa rais.
Mtikila aliendelea kudai kuwa Ridhwani anatumia vibaya ofisi na madaraka ya baba yake (Rais Kikwete) kujilimbikizia mali kinyume cha sheria.

“Kitendo cha Ridhwani kutaka aombwe radhi na fidia ni njia na ngazi muhimu itakayosaidia mambo mengi yaliyojificha kuwekwa hadharani," alisema Mtikila na kuongeza:"Tutatumia sheria zilizopo kuwabana wote ambao majina yao yameandikishwa kwenye mali za vigogo nchini waeleze walivyopata mali hizo na hapo ndipo watakapowataja wahusika halisi,” alisema Mtikila.

Kiongozi huyo wa DP aliendelea kudai kuwa viongozi wengi nchini wamejilimbikizia mali kupitia wizi na ufisadi, wakitumia nafasi zao za umma huku wakiandikisha majina ya watu wengine kwenye mali hizo kuficha umiliki wao.

Alidai kuwa kesi anayotaka kuifungua Ridhiwani itaibua mambo mengi kwani walioandikishwa majina kwenye mali hizo, watawataja wamiliki halisi badala ya kufungwa jela kwa kumiliki mali inayodhaniwa kuwa ya wizi au kupatikana isivyo halali.

Kwa upande wake, Dk Slaa jana hakupatikana kuzungumzia kusudio hilo la Ridhiwani kutokana na simu yake ya kiganjani kutopatikana kwa siku nzima.

Jana, Ridhiwani alipotakiwa kueleza nini kinafuata baada ya muda aliotoa kuisha alijibu kwa ufupi kuwa asingependa kuzungumzia suala hilo kwa kuwa ni jambo la kisheria na kwamba sheria ina kanuni zake.

"Ndugu yangu, sitaki kuzungumzia hili kwa kuwa sheria ina kanuni zake. Hili litazungumzwa mahakamani."
Dk Slaa na Mtikila walikaririwa mwanzo wa Mei wakisema kuwa mtoto huyo wa rais ana utajiri mkubwa licha ya kumaliza shule miaka ya karibuni huku wakimtuhumu kutumia cheo na madaraka ya baba yake kujitajirisha.