Showing posts with label fisadi. Show all posts
Showing posts with label fisadi. Show all posts

Monday, May 30, 2011

Mtikila: Ridhiwani nenda mahakamani




Mchungaji Christopher Mtikila
LICHA ya mtoto wa Rais Jakaya Kikwete, Ridhiwani kuwaandikia barua ya kusudio la siku 10 kuwafikisha mahakamani Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa na Mwenyekiti wa Democratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila, ameambiwa aende huko mahakamani.

Katika kusudio lake Ridhiwani amedai kuwa endapo watashindwa kumwomba radhi na kumlipa Sh2 bilioni atakwenda mahakamani.Katika kusudio hilo, Ridhiwani amewataka wanasiasa hao wamwombe radhi na kumlipa fidia hiyo ndani ya siku kumi kuanzia Mei 13, kwa madai waliyoyatoa hadharani kuwa yeye ni bilionea aliyetajirika kifisadi.

Katika kusudio hilo, Ridhiwani pia amehusisha gazeti la Tanzania Daima ambalo amedai limechangia kumchafua kwa kuripoti madai ya wanasiasa hao dhidi yake.

“Tumeelekezwa na mteja wetu kuwataka wote kwa pamoja kukanusha na kusahihisha tuhuma zote na kuchapisha habari hiyo ya kuomba radhi kwa uzito na herufi kubwa (bold print) katika kurasa za mbele  wa gazeti hilo (Tanzania Daima) kwa siku tatu mfululizo hadi Mei 23, 2011," alieleza wakili Sam Mapande wa Law Associates, anayemwakilisha Ridhiwani.Wakili huyo aliendelea, "Pia, wote kwa pamoja mnatakiwa kulipa fidia ya Sh2 bilioni kwa madhara ya jumla aliyopata mteja wetu.”

Barua hiyo ya kurasa sita  imetaja baadhi ya maneno yaliyoandikwa kwenye matoleo mawili ya gazeti la Tanzania Daima yakimkariri Dk Slaa na Mchungaji Mtikila, wakimhusisha pia Rais Jakaya Kikwete na mwanaye (Ridhwani) na watu wengine walio karibu yake na matukio ya ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka na ofisi ya umma. Kwa mujibu wa Ridhiwani, madai hayo yamemchafulia jina, kumdhalilisha, kumshushia hadhi na heshima yake katika jamii inayomzunguka.

Mhariri wa gazeti la Tanzania Daima, Absalom Kibanda amekiri kupokea barua hiyo, lakini akasema hawezi kusema chochote kwa jambo ambalo ni la kisheria. “Kwa kuwa bado hatujafikishwa mahakamani, siwezi kusema tumejiunga vipi. Tunasubiri tufikishwe mahakamani kwanza,” alisema Kibanda.

Mchungaji Christopher Mtikila amemtaka mtoto huyo wa rais kwenda mahakamani haraka akidai kuwa hana shaka kwa kuwa ana ushahidi mzito kuthibitisha madai yake.Mtikila aliwaambia waandishi wa habari mjini Arusha jana kuwa, kesi hiyo itakuwa ni ukombozi kwa taifa kwa sababu itampa yeye na mwenzake, Dk Slaa muda wa kueleza kile alichokiita madudu yanayofanywa na mtoto huyo wa rais.
Mtikila aliendelea kudai kuwa Ridhwani anatumia vibaya ofisi na madaraka ya baba yake (Rais Kikwete) kujilimbikizia mali kinyume cha sheria.

“Kitendo cha Ridhwani kutaka aombwe radhi na fidia ni njia na ngazi muhimu itakayosaidia mambo mengi yaliyojificha kuwekwa hadharani," alisema Mtikila na kuongeza:"Tutatumia sheria zilizopo kuwabana wote ambao majina yao yameandikishwa kwenye mali za vigogo nchini waeleze walivyopata mali hizo na hapo ndipo watakapowataja wahusika halisi,” alisema Mtikila.

Kiongozi huyo wa DP aliendelea kudai kuwa viongozi wengi nchini wamejilimbikizia mali kupitia wizi na ufisadi, wakitumia nafasi zao za umma huku wakiandikisha majina ya watu wengine kwenye mali hizo kuficha umiliki wao.

Alidai kuwa kesi anayotaka kuifungua Ridhiwani itaibua mambo mengi kwani walioandikishwa majina kwenye mali hizo, watawataja wamiliki halisi badala ya kufungwa jela kwa kumiliki mali inayodhaniwa kuwa ya wizi au kupatikana isivyo halali.

Kwa upande wake, Dk Slaa jana hakupatikana kuzungumzia kusudio hilo la Ridhiwani kutokana na simu yake ya kiganjani kutopatikana kwa siku nzima.

Jana, Ridhiwani alipotakiwa kueleza nini kinafuata baada ya muda aliotoa kuisha alijibu kwa ufupi kuwa asingependa kuzungumzia suala hilo kwa kuwa ni jambo la kisheria na kwamba sheria ina kanuni zake.

"Ndugu yangu, sitaki kuzungumzia hili kwa kuwa sheria ina kanuni zake. Hili litazungumzwa mahakamani."
Dk Slaa na Mtikila walikaririwa mwanzo wa Mei wakisema kuwa mtoto huyo wa rais ana utajiri mkubwa licha ya kumaliza shule miaka ya karibuni huku wakimtuhumu kutumia cheo na madaraka ya baba yake kujitajirisha.
 

Friday, May 27, 2011

Tamko la Vijana Arusha lazidi kuivuruga CCM

















TAMKO la baadhi ya vijana wa UVCCM, Mkoa wa Arusha kutaka mafisadi wafukuzwe, limezidi kukivuruga chama hicho baada ya Katibu Mkuu, Wilson Mukama kusema hawezi kujiingiza 'kichwa kichwa' kuzungumzia suala hilo, huku baadhi ya watuhumiwa wakikataa kulizungumzia. Mukama alisema CCM inafuatilia kwa karibu mgogoro huo, lakini haiwezi kuuzungumzia sasa kwa kuwa hajapata taarifa rasmi kutoka umoja wa vijana.

Kwa mujibu wa Mukama, UVCCM ni jumuiya halali ya chama tawala yenye mamlaka kamili ya kuzungumzia matatizo yake, hivyo yeye kusema chochote itakuwa ni kuingilia kazi za jumuiya hiyo.
“Chama chetu kina utaratibu wake, UVCCM ni jumuiya ndani yake, hayo yaliyotokea kule Arusha siwezi kuyazungumzia, ila kesho (leo) tuna kikao, hivyo wao vijana watatupa taarifa zao,” alisema Mukama, huku akisoma ujumbe mfupi wa simu (sms) alioandikiwa na katibu mkuu wa umoja huo, Martin Shigella kuwa watatoa taarifa ya yaliyotokea Arusha.

“Suala la Arusha tunalifuatilia kwa ukaribu sana, ila utendaji tunawaachia wao (UV-CCM), nasi tukishapata taarifa zao ndio tutaweza kulizungumzia suala hilo, ila kwa sasa mtafute Shigella,” alielekeza Mukama.
Alipotafutwa kwa simu jana kuzungumzia tuhuma hizo, Shigella alisema kuwa hawezi kutolea ufafanuzi kwa kuwa alikuwa nje ya nchi kikazi. “Sikuwapo nchini, kwa hiyo sitaweza kuzungumza lolote, kuna mtu alikuwa akikaimu nafasi yangu, hivyo nikipata maelezo kutoka kwake nitakuwa tayari kuzungumza, nitafute kesho (leo),”alisema Shigella.

Naye makamu mwenyekiti wa umoja huo taifa, Benno Malisa alisema wamesikitishwa na kauli zilizotolewa na vijana wenzao wa Arusha, hivyo watatuma kamati ya maadili kwenda kuzungumza na makundi yanayolumbana. “Hivi karibuni Kamati ya Utekelezaji ya UVCCM itakaa na kutoa uamuzi, lakini ni baada ya Kamati ya Maadili itakayotumwa kuzungumza na wanachama wanaolumbana huko Arusha kuleta ripoti makao makuu ya umoja wetu,”Alisema Malisa.

Akizungumzia adhabu wanazoweza kupewa wanachama wa umoja huo, Malisa alisema adhabu hizo zitatokana na aina ya makosa watakayokutwa nayo. “Suala hili liko ndani ya uwezo wetu na tutalifanyia kazi na kuchukua hatua kwa mujibu wa kanuni za UVCCM, kama kutakuwa na makosa makubwa zaidi yatapelekwa  ngazi za juu zaidi,”alisema Malisa.

Juzi, UVCCM Mkoa wa Arusha waliuomba uongozi wa juu wa chama tawala kuwafukuza uanachama viongozi watatu, wakiwamo Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa na mwenzake wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge wanaotuhumiwa kwa ufisadi.

Vijana hao pia walikishauri chama hicho kupitia kamati yake ya maadili kuwaita na kuwahoji makada hao maarufu na baadaye kuwachukulia hatua, zikiwamo za kuwafukuza kwa maslahi ya chama na taifa. Tamko hilo lililosomwa na mjumbe wa baraza la umoja huo mkoani Arusha, Ali Babu lilitaka watuhumiwa hao waliowaita mapacha watatu, kuwa ndio chanzo cha kudhoofika kwa chama hicho tawala.

"Pia, tunasisitiza Andrew Chenge aondolewe kwenye Kamati ya Maadili ya CCM mara moja na kumtaka mtuhumiwa mwingine (jina tunalo) aondolewe pia kwenye uongozi wa ndani ya umoja wetu," ilieleza sehemu ya taarifa hiyo. Lakini, alipotafutwa jana kuzungumzia tuhuma hizo, Chenge alijibu kwa ufupi: "Kwa sasa sitaki kuzungumzia masuala hayo. Kila la heri."

Naye Lowassa alipotafutwa alisema kwa ufupi: ‘no comment’ akimaanisha kuwa hawezi kulizungumzia suala hilo.

Hata hivyo, wakati makada hao wakigoma kuzungumzia suala hilo, mwenyekiti wa umoja huo Mkoa wa Arusha, James ole Milya anayeshinikizwa kujiuzulu wadhifa huo, jana aliibuka na kudai kuwa tamko hilo lilitolewa na kundi la vijana aliowaita wahuni wa mitaani na wasiokuwa na kazi.

“Wale ni wahuni, hawana chochote wala lolote, wanapenda kukaa vijiweni hawana kazi za kufanya, tuna taarifa kwamba walitumwa na baadhi ya viongozi hapa Arusha kupindisha na kuvuruga hoja za umoja wetu mkoani  Arusha,” alisema Milya

Alisema kuwa vijana hao wakiongozwa na Ali Babu hawatambuliki ndani ya umoja huo, huku akisisitiza  kwamba hoja na malalamiko yote hupitishwa katika ngazi husika ili ziweze kufanyiwa kazi na sio kuibuka na kutoa matamshi yasiyo na tija.

Millya aliendeleza msimamo wake wa kutaka Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda ambaye pia ni Mbunge wa Viti Maalumu aondoke madarakani kwa madai ya kusababisha jimbo kwenda upinzani (Chadema), huku akimtaka katibu huyo asikilize kilio chao (UVCCM) cha kumtaka aondoke. Alisema kuwa endapo kiongozi huyo ataendelea kung'ang'ania nafasi yake, basi atang’olewa kwa maandamano ya vijana yasiyokuwa na kikomo ambayo yatafanywa na wanachama wa umoja huo.

“Msimamo wetu uko pale pale, Chatanda ni lazima aondoke kwa kuwa amekivuruga chama chetu, ametuchonganisha na viongozi wa dini, lakini pia amesababisha Jimbo la Arusha Mjini liangukie upinzani kwa kukimbilia Tanga kusaka ubunge wa viti maalumu kipindi cha uchaguzi,”alisisitzia Milya.

Juzi,  katika mkutano wao wenye malengo makuu sita, vijana hao wa Mkoa wa Arusha walisema wanaunga mkono falsafa ya CCM ya kujivua gamba."Tunaipongeza na kuiunga mkono Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kwa kutambua kwamba mafisadi wamechangia sana kukidhoofisha na kukipotezea mvuto chama chetu mbele ya umma wa Watanzania," ilisema taarifa hiyo na kuongeza:
"Kwa mantiki hiyo tunatamka kwa kauli moja kwamba mapacha hao watatu wa ufisadi (wakiwataja kwa majina) na vibaraka wao wafukuzwe mara moja kwa maslahi ya CCM na Watanzania."

CUF yamtaka Nahodha ajiuzuru

*Ni kutokana na mauaji ya wananchi  watano Tarime 
*Yalaani, yasema huo ni ukiukwaji wa haki za binadamu


BARAZA Kuu la Chama cha Wananchi (CUF) limemtaka Waziri wa Mambo ya Ndani kuwajibika kutokana na mauaji yaliyotokea wilayani Tarime lakini pia kufanyika kwa uchunguzi wa kina juu ya tukio hilo.

Hatua hiyo ilifikiwa Dar es Salaam jana na Mwenyekiti wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mapendekezo mbalimbali yaliyoazimiwa na kikao cha baraza hilo.

Alisema kuwa baraza hilo linalaani vitendo vya ukiukaji na uvunjaji wa haki za binadamu hususan mauaji ya raia yanayofanywa na Jeshi la Polisi ambayo yamekuwa yakiripotiwa kila mara.

"Inatuumiza sana kwa kuwa inaonekana jambo hili ni la kawaida kwa sababu watendaji wake hawachukuliwi hatua yoyote," alisema.

Prof. Lipumba alisema kuwa baraza hilo pia linamtaka Rais Jakaya Kikwete kutambua kuwa jukumu la kuleta maendeleo ya Watanzania ni la watu wote hivyo serikali yake isisite kutumia sera mbadala za CUF kwa maendeleo ya taifa.

Alisema serikali kupitia wizara ya Fedha na Uchumi na Wizara ya Nishati na Madini inatakiwa kuchukua hatua za kuhakikisha nchi na wananchi wake wananufaika na rasilimali za madini zilizopo hapa nchini hususani madini ya dhahabu ambayo bei yake katika soko la dunia imepanda.

"Dhahabu inayouzwa nje ni dola bilioni 1.5 kwa mwaka sawa na  asilimia 40  ya bidhaa za Tanzania zinazouzwa nje ya nchi," alisema.

Alisisitiza kuwa baraza hilo linataka kuona utajiri wa nchi unawanufaisha wananchi na kuisaidia nchi kujikomboa kutoka katika dimbwi la umasikini na kuacha kutegemea misaada kutoka nje ambayo imeifanya nchi kuwa tegemezi kwa miaka mingi.

Aliongeza kuwa baraza hilo linamtaka Waziri wa Nishati na Madini Bw.William Ngeleja kujiuzulu kwa kuwa ameshindwa kutumia vyanzo vya umeme vilivyopo nchini ili kukabiliana na tatizo sugu la nishati linaloikumba nchi yetu kwa sasa.

Alisema nchi imejaliwa vyanzo vingi ya umeme na maeneo mengi ya maporomoko ya maji, makaa ya mawe, madini na hata umeme wa jua ambao hauna gharama kubwa ya kufua.

"Ni miaka 50 tangu tupate uhuru hatuna sababu yoyote  ya kutokuwa na umeme wa uhakika, ni ufisadi tu ambao umekithiri katika serikali yetu," alisema.

Alisisitiza kuwa serikali ni lazima itambue kuwa hali ya kutokuwa na umeme wa uhakika imezorotesha uzalishaji viwanda,biashara,huduma katika hospitali na shule hivyo kusababisha uchumi wa nchi kuzorota.

Aliitaka serikali kuzingatia mapendekezo na hoja zinazotolewa na kamati ya Nishati na Madini ya Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania zinazolenga kupata ufumbuzi wa matatizo ya umeme.

Pia alisema baraza hilo linaitaka serikali kuwa makini katika suala zima la utunzaji na uhifadhi wa silaha nzito za kivita zenye madhara makubwa na kutaka zihifadhiwe mbali na makazi ya watu ili matukio ya milipuko ya mabomu ambayo yameshatokea mara mbili yasijirudie tena.