Symbion, NSSF wapewa miradi ya kuzalisha Nchi nzima
KAMPUNI ya Symbion Power ya Marekani na Shirika la Hifadhi ya Jamii nchini (NSSF) wamepewa zabuni ya kuingiza nchini mitambo ya kuzalisha umeme wa dharura, katika mpango ambao Serikali itauwasilisha bungeni leo.
Symbion Power ni kampuni ambayo ilinunua mitambo iliyokuwa ikimilikiwa na kampuni ya Dowans Tanzania, imepewa zabuni ya kuzalisha megawati 205 za umeme, wakati NSSF wataingiza mitambo yenye uwezo wa kuzalisha megawati 150.
Kwa mujibu wa taarifa ya Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, iliyowasilishwa na kujadiliwa mbele ya Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini ambayo Mwananchi limeiona, mpango wa dharura kati ya Agosti 2011 na Desemba 2012 itaigharimu Serikali Sh1.24 trilioni.
Miradi inayotarajiwa kutekelezwa ni ya dharura itakayozalisha megawati 1,032 zikiwemo 572 kati ya sasa na mwezi Desemba mwaka huu na megawati 460 zaidi ifikapo Desemba 2012.
“Ili kukabiliana na mgawo wa umeme kwa kipindi cha dharura, Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi, pamoja na taasisi za umma itatumia uwezo wa mitambo iliyopo nchini kukodisha na kununua mitambo ya kufua umeme itakayotosheleza mahitaji ya sasa na baadaye,” inaeleza sehemu ya taarifa hiyo ya Ngeleja.
Hata hivyo mpango huo wa Serikali ambao unatarajiwa kujadiliwa bungeni leo, nusura ukataliwe na Kamati husika kutokana na kile wajumbe wa kamati hiyo walichosema kuwa ni kuchelewa kuwasilishwa mbele yake ili ijadiliwe kama Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alivyoahidi.
Kamati hiyo ilikutana na upande wa Serikali kwa mara ya kwanza juzi, zikiwa zimebaki siku mbili kabla Ngeleja hajarejea bungeni leo ili kutafuta ridhaa ya Bunge kupitisha bajeti ya wizara yake, baada ya kufanya marekebisho yenye lengo la kuliwezesha Taifa kuondoka gizani.
Serikali kupitia kwa Waziri Mkuu, Pinda iliondoa bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini bungeni Julai 18, mwaka huu baada ya wabunge wengi, wakiwemo wa upinzani na wale wa CCM kuweka msimamo wa kutoiunga mkono kwa maelezo kwamba haikuwa na majibu ya matatizo ya uhaba wa umeme nchini.
Pinda alitumia kipengele cha 55 (3) (b) pia cha 59(1) vya kanuni za kudumu za bunge toleo la 2007, ambavyo vinampa nafasi ya kuliambia Bunge sababu za kuahirisha bajeti na muda ambao utatumika katika kuirekebisha.
Pinda aliomba muda wa wiki tatu kwa ajili ya Serikali kujipanga upya, kauli ambayo aliitoa wakati Shirika la Umeme nchini (Tanesco) likiwa limetangaza mgawo wa umeme usio na kikomo kutokana na uhaba wa maji kwenye mabwawa ya kuzalishia nishati hiyo.
Ilikuwa ni ahadi ya Pinda kwamba katikia mchakato huo, Serikali ingeshirikiana na wabunge kupitia kamati za kisekta ambazo baadaye zilitajwa kuwa Kamati ya Nishati na Madini, Kamati ya Fedha na Uchumi na Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma, lakini hadi juzi hakuna kamati hata moja ambayo ilikuwa imeshirikishwa katika mkakati huo.
Hali hiyo ndiyo ilisababisha Kamati ya Nishati na Madini juzi kugomea mpango huo wa Serikali kwa maelezo kwamba, haikuwa na muda wa kutosha kuujadili huku baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo wakihoji sababu za kuchelewa kushirikishwa kwao.
"Jana (juzi), huko hali ilikuwa mbaya sana, wajumbe walichachamaa wakawaambia watendaji wa Serikali kuwa wamekaa muda wote huo halafu wanaleta mpango wao wakati zikiwa zimebaki siku mbili tu, wakasema hawataki," kilieleza chanzo chetu cha habari na kuongeza:
"Lakini busara zilitumika ikaonekana kwamba, tujadili tu ili tuone kama kuna jambo la kusaidia, ndo leo (jana) tunaendelea."
Taarifa ambazo Mwananchi limezipata bungeni zilidai kuwa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini inayoongozwa na Mbunge wa Bumbuli (CCM), January Makamba ilishaomba kukutana na uongozi wa Wizara zaidi ya mara tatu, lakini kila walipotaka kufanya hivyo, upande wa Serikali ulisema hauko tayari.
Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, wiki hii aliomba mwongozo wa Spika, akihoji sababu za Serikali kutokutana na kamati husika tangu kuahirishwa kwa mjadala wa hotuba ya Nishati na Madini, lakini Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisema: "muda bado unaruhusu Serikali kukutana na kamati husika”.
Mwananchi limedokezwa kuwa huenda bajeti hiyo ikapata wakati mgumu wakati bunge litakapokaa kama kamati, kutokana na ukweli kwamba ni kamati ya Bunge ya kisekta moja tu iliyopata fursa ya kushiriki mchakato wa maandalizi yake, tena nyakati za mwisho tofauti na matarajio ya awali ya kushirikishwa kwa kamati tatu.
Showing posts with label makamba. Show all posts
Showing posts with label makamba. Show all posts
Saturday, August 13, 2011
Wednesday, June 15, 2011
CCM WAFUTA POSHO ZA VIKAO
HOJA ya kutaka kufutwa kwa posho za vikao za wabunge na watumishi wengine wa umma imechukua sura mpya baada ya jana Mbunge wa Bumbuli (CCM), Januari Makamba kuliambia Bunge mjini hapa kuwa suala la kufutwa kwa posho ni la kitaifa na ni sehemu ya Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano uliowasilishwa na serikali.
Kauli hiyo ya Makamba ambaye pia ni Katibu wa Mambo ya Nje wa Sekretarieti ya CCM imekuja huku kukiwa na malumbano makali baina ya Spika wa Bunge, Anne Makinda na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe kuhusu suala hilo la posho za vikao vya wabunge.
Juzi, Spika Makinda alisema Zitto ambaye ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, anaweza kufukuzwa ubunge kwa kutosaini karatasi za mahudhurio, hatua ambayo Zitto alisema ataichukua ili asilipwe posho za vikao.
Spika alisema Zitto anaweza kukumbwa na adhabu hiyo iwapo hatasaini karatasi za mahudhurio ambazo ndizo zinathibitsha uwepo wa mbunge katika mikutano na vikao vya bunge na kwamba kanuni zinamwadhibu mbunge kwa kumfukuza asipohudhuria mikutano mitatu. Hata hivyo, Zitto amepuuza kauli hiyo ya Spika kwa kusema kwamba kama ni kwa ajili ya kukataa posho, yuko tayari kufukuzwa bungeni.
"Nitafanya hivyo tuone, Kanuni inasema mikutano mitatu mfululizo na siyo vikao vitatu mfululizo. Nitatumia uzoefu wangu wa siasa za wanafunzi kukwepa mtego wake. Lakini kama anadhani ni sawa kunifukuza ubunge kwa kukataa posho, nipo tayari," alisema.
Kauli ya jana ya Makamba pia inaonekana kutofautina na mawazo ya wabunge wengi wa CCM akiwamo Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo ambaye amesema wanashabikia suala hilo wanajitafutia umaarufu.
Akichangia huo wa maendeleo wa miaka mitano jana, Makamba alionekana kupigia chapuo suala la kufutwa au kuangaliwa upya kwa posho za vikao huku akisema kwamba ni la kitaifa na ni sehemu ya mpango huo.
Makamba alisema kuwa suala la nidhamu na usimamizi wa matumizi ya fedha za umma ni muhimu na kwamba mpango huo umeliona katika ukurasa wa 17 wa kitabu kilichochapishwa kwa Kiingereza na kutoa mapendekezo ya kufutwa kwa posho za vikao na zile za usafiri.
"Mpango unabainisha kwamba kuna umuhimu wa kufutwa kwa posho za vikao na usafiri hivyo iwapo wabunge mtalisikia likiwasilishwa hapa kwa mbwembwe kesho (leo), basi msije mkashangaa kwani ni sehemu ya mpango huu," alisema Makamba.
Kujadiliwa bungeni leo
Mjadala kuhusu malipo ya posho ambao umekuwa ukiendelea kwa wiki moja sasa hasa zaidi nje ya Bunge, leo unatarajiwa kuingizwa rasmi bungeni wakati Bajeti ya Serikali iliyowasilishwa na Mkulo Jumatano iliyopita itakapoanza kujadiliwa.
Suala hilo ni dhahiri litajitokeza katika bajeti mbadala itakayowasilishwa na kambi ya Upinzani Bungeni na Waziri Kivuli wa Fedha, Zitto Kabwe ambaye amekuwa katika mvutano usio rasmi na Spika kutokana na kukataa kulipwa posho za kikao.
Mwenyekiti wa Chadema ambaye pia ni Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe alisema jana kuwa kambi yake inatarajiwa kutoa ushauri mgumu ambao haujazoeleka kwa watendaji wa serikali na kwamba suala la kufutwa kwa posho ni sehemu ya mapendekezo hayo.
Alisema kufutwa kwa posho hizo kunaweza kuokoa zaidi ya Sh900 bilioni ambazo zinaweza kuelekezwa katika maeneo mengine ya huduma kwa wananchi.
Uhalisia posho za wabunge
Mmoja wa wabunge wa CCM ambaye hakutaka kutaandikwa jina lake alisema anasikia kuhukumiwa katika nafsi yake kutokana na kupokea posho za vikao ambazo kimsingi ni sawa na "kuwaibia wananchi".
"Ujue bwana sisi ndani ya CCM mambo hayaendi kama kwa wenzetu (Chadema), wale wanaweza kukaa leo na kuamua, sisi ni tofauti lazima kuwepo na mchakato lakini ukweli ni kwamba hoja yao ni nzuri," alisema mbunge huyo.
Uchunguzi uliofanywa umebaini kuwa malipo ya wabunge yamegawanyika katika sehemu nne ambazo ni pamoja na mshahara ambao ni Sh2,300,000 kwa mwezi, posho ya ubunge kila mwezi ambayo ni Sh5 milioni, posho ya kujikimu (per-diem) Sh80,000 wawapo nje ya majimbo yao kikazi na posho ya vikao (sitting allowance) ambayo huwa ni Sh70,000 kwa kila mbunge.
Kwa maana hiyo, kwa kawaida mbunge hulipwa Sh7.3 milioni kila mwezi kabla ya kukatwa kodi na wawapo Dodoma na Dar es Salaam kwa ajili ya vikao vya kamati na bunge au mikoani kwa ajili ya kukagua shughuli zilizopo chini ya kamati zao. Hulipwa kiasi cha Sh150,000 kila mmoja kwa siku ambazo ni Sh70,000 kwa ajili ya vikao na Sh80,000 kwa ajili ya kujikimu.
Kwa maana hiyo bunge linatarajiwa kutumia kiasi cha Sh1.788 bilioni kwa ajili ya kugharamia vikao 73 vya Bunge la Bajeti iwapo wabunge wote 350 waliopo watahudhuria vikao hivyo.
Kwa hesabu hizo, kila mbunge katika mkutano wa Bunge la Bajeti anatarajiwa kuondoka na kikita cha Sh5.1 milioni mbali na Sh 5.58 milioni ambazo ni malipo kwa ajili ya kujikimu, fedha ambazo ni mbali na mshahara wake kwa mwezi na posho ya ubunge.
CCM yakataa posho
Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeanza machakato wa kufuta posho hizo ikiwa ni hatua ya kupunguza matumizi yasiyo ya lazima. Habari kutoka ndani ya CCM, Dodoma na Dar es Salaam zinasema kuwa mkakati wa kufutwa kwa posho ulianzishwa takriban mwezi mmoja uliopita na sekretarieti mpya inayoongozwa na Katibu Mkuu, Wilson Mukama.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, baadhi ya wajumbe wa sekretarieti walihoji uhalali wa posho wanazolipwa hata pale vikao vinapofanyika katika sehemu ambako ni makazi yao na kwamba hoja hizo ndizo zilizozaa wazo la kufutwa kwa posho katika vikao.
"Hoja ilikuwa kwamba kama chama hakina fedha na tunataka kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, basi posho za vikao zifutwe kwa sababu hakuna ulazima wa posho hizo hasa kwa wajumbe wa sekretarieti ambao kazi zao ni za kila siku," kilieleza chanzo chetu na kuongeza:
"Hivi sasa mpango huo uko kwenye mchakato wa kuwekewa mwongozo na nadhani baada ya kupitia katika vikao vyetu utaanza kutekelezwa. Lakini kimsingi ni kama utekelezaji wake umeshaanza kwa sababu baadhi ya wajunbe wamekataa kabisa kusaini posho hizo."
Habari zaidi zinadai kuwa waraka wa mapendekezo ya kupunguza matumizi ndani ya CCM unakwenda mbali zaidi hadi katika matumizi ya magari na kwamba pale usafiri unapohitaji wa kuelekea kwenye mkutano mmoja, basi viongozi watumie magari machache kwa maana ya usafiri wa pamoja badala ya utaratibu wa sasa ambao unamruhusu kila kiongozi kutumia usafiri wake.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipoulizwa kuhusu sekretarieti kufuta posho katika vikao vyake, hakukanusha wala kuthibitisha, badala yake akadai kuwa hayo ni mambo ya ndani ya chama ambayo hayana faida yoyote kwa umma.
"Hivi ninyi waandishi wa habari, haya mambo mnayapata kwa nani! Haya ni mambo ya ndani ya chama sidhani kama yana tija yoyote kwa umma, maana haiwezi kusaidia chochote," alisema Nape kwa kwa simu.
Alipoelezwa kwamba suala hilo lina uhusiano na sakata linaloendelea bungeni, Nape alisema: "Bunge ni bunge na chama ni chama. Kila taasisi inajitegemea na ina uamuzi wake, lakini pia sisi kama chama tulishatoa kauli mara nyingi kwamba suala la posho kwa wabunge na watumishi wengine wa serikali linazungumzika, ni la kisera na wanaohusika wapo waulizeni hao."
Mwishoni mwa wiki iliyopita Nape akizungumzia malumbano miongoni mwa wabunge kuhusu suala la posho alisema suala hilo linajadilika na kwamba si vyema kulipinga kwa sababu tu linatokea kambi ya upinzani.
Kwa upande wake, Makamba alipoulizwa kuhusu kufutwa kwa posho katika vikao vya Sekretarieti ya CCM naye kama ilivyokuwa kwa Nape, hakukanusha wala kuthibitisha.
"Wewe si unamfahamu msemaji wa chama ni nani? Mwulizeni Nape tena nadhani anakuja Dodoma. Akija mwulizeni, mimi siwezi kulizungumzia.... lakini ninyi waandishi haya mambo ya ndani ya chama huwa mnayapata wapi? Anyway, mwulizeni mwenezi atawaambia," alisema Makamba.
Chanzo: Mwananchi 15/6/2011
Subscribe to:
Posts (Atom)
