Showing posts with label simba. Show all posts
Showing posts with label simba. Show all posts

Friday, August 5, 2011

Kazi imeanza UDA Kumekucha


Alisema kutokana na hali iliyojitokeza bungeni kuhusu uuzwaji wa shirika hilo, serikali imeona ni vyema vyombo vyake vikachunguza jambo hilo. Pinda alisema baada ya uchunguzi kukamilika, serikali itachukua hatua kwa wote waliohusika katika uuzaji UDA kwa kufuata sheria na taratibu za nchi.  “Tumeagiza CAG, TAKUKURU na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) kuanza uchunguzi wa jambo hili, utakapokamilika tutatoa taarifa na kuchukua uamuzi wa kisheria kwa wahusika,” alisema.  Katika hatua nyingine, waziri mkuu alisema serikali ina nia ya dhati ya kuhakikisha wastaafu na wanaodai pensheni katika Shirika la TAZARA wanalipwa. Alisema hatua zimeanza kuchukuliwa ili kuhakikisha wastaafu hao kwa upande wa Tanzania, wanalipwa.

Waziri mkuu alitoa maagizo hayo siku moja baada ya wabunge kulalamikia kuuzwa UDA. Waliwahusisha Meya wa Jiji wa Dar es Salaam, Dk. Didas Massaburi, mbunge wa Kaliua, Profesa Juma Kapuya (CCM), anayedaiwa kuwa na hisa 10,000 katika kampuni ya Simon Group iliyonunua UDA na aliyewahi kuwa waziri katika serikali ya awamu ya tatu, Idd Simba, ambaye anadaiwa kuingiza fedha kwenye akaunti yake na nyingine ya asasi ya Pride.

Wabunge kutoka mkoa wa Dar es Salaam, wakizugumza na waandishi wa habari jana, walisema Dk. Massaburi, Mkurugenzi wa Jiji, Bakari Kingobi na watendaji wengine waliohusika na kadhia hiyo wasimamishwe kazi. Kwa mujibu wa wabunge hao, hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi ya Simba, ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya UDA, wajumbe wa bodi na watendaji wa shirika hilo waliohusika na kashfa hiyo.

Mwenyekiti wa wabunge hao, Abass Mtemvu, alisema wanataka mkataba wa uuzaji UDA usitishwe. Alisema Dk. Massaburi na Kingobi walishiriki kikao batili kilichoitwa mkutano maalumu wa wanahisa wa UDA na kufanya uamuzi wa kukabidhi shirika la mali zake kwa Simon Group Limited.

Alisema kikao hicho kilichoitishwa na meya kilifanyika bila kuheshimu maelekezo ya barua ya Ofisi ya Waziri Mkuu ya Februari 28, mwaka huu, yenye Kumb. Na. CAB. 185/295/01/27 iliyoagiza kusitisha mchakato wa kuuza hisa ambazo hazijagawiwa. Nakala ya barua hiyo  iliwasilishwa kwa Kingobi, meneja mkuu wa UDA na wizara nyingine husika.  Mtemvu alisema mkutano huo ulitanguliwa na kikao batili cha bodi ya wakurugenzi ya UDA, chini ya uenyekiti wa Simba, kilichofanyika Januari 28, mwaka huu, kilichoazimia kuuza hisa zisizogawiwa kwa Simon Group bila kuzingatia taratibu, kanuni na sheria.

Alisema serikali itoe tamko kutokana na mgogoro wa kimaslahi ulioelezwa kuhusu kamati ndogo ya Bunge iliyoundwa na Kamati ya Miundombinu, kutokana na kutozingatiwa Kanuni za Bunge katika kutoa majukumu kwa kamati husika kuhusu kashfa ya UDA. Miongoni mwa wajumbe ni Profesa Kapuya.  Wabunge hao na majimbo yao kwenye mabano ni Mtemvu (Temeke – CCM), Mussa Zungu (Ilala - CCM), Iddi Azzan (Kinondoni - CCM), John Mnyika (Ubungo - CHADEMA), Halima Mdee (Kawe – CHADEMA), Dk. Faustine Ndungulile (Kigamboni –CCM), Eugene Mwaiposa (Ukonga – CCM), Dk. Makongoro Mahanga (Segerea –CCM).

Wengine kupitia Viti Maalumu ni Zarina Madabida (CCM), Philipa Mturano (CHADEMA), Mariam Kisangi (CCM), Angellah Kairuki (CCM) na Dk. Fenella Mukangara (CCM).

Friday, July 8, 2011

Simba full shangwe

Image



Mlindalango wa timu ya Simba Juma Kaseja akishangilia kwa kuonesha flana yenye maandishi (There is only one Kaseja) yakimaanisha ‘Kuna Kaseja mmoja tu’ baada ya kudaka penati iliyopigwa na mchezaji wa timu ya El Mereikh ya Sudan kwenye mchezo wa nusu fainali ya kwanza ya Kombe la Castle la Kagame uliochezwa katika Uwanja wa Taifa Dar es Salaam. Simba ilishinda kwa penalti 5-4.









MABINGWA
wa kihistoria wa michuano ya soka ya Kombe la Kagame timu ya Simba jana ilifuzu kutinga kwenye fainali ya michuano hiyo baada ya kuinyuka timu ngumu ya El Mereikh ya Sudan kwa mikwaju ya penati 5-4 katika mchezo mgumu wa nusu fainali ya kwanza uliofanyika kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Mchezo huo ambao ilibidi uende katika muda wa ziada hivyo kuchezwa kwa dakika 120 baada ya dakika 90 za kawaida kumalizika kwa sare ya bao 1-1, ambapo El Mereikh ndio walikuwa wa kwanza kuzifumania nyavu za Simba katika dakika ya 12 kwa bao lililofungwa na Adiko Rime akiunganisha krosi ya Balla Gabir akiwa amezungukwa na mabeki wawili wa Simba .

Simba ilisawazisha bao hilo katika dakika ya 24 kwa bao lililofungwa na Ulimbokwa Mwakingwe kwa kichwa baada ya mpira wa krosi ya Shija Mkina kuokolewa vibaya na kipa Isam Elhadary na kumfikia Mwakingwe aliyeutumbukiza kimiani.

Katika changamoto hiyo ya mikwaju ya penati shujaa wa Wekundu hao wa Msimbazi alikuwa ni kipa Juma Kaseja ambaye aliokoa mkwaju wa Jonas Sakwaha na kuwafanya mashabiki wa Simba waliofurika kwenye uwanja huo kulipuka kwa shangwe na kuimba ‘ Hatubebwi hatubebwi hatubebwi ikiwa ni katika kuwakejeli watani zao Yanga ambao juzi walitinga kwenye hatua hiyo ya nusu fainali kwa matuta dhidi ya Red Sea ya Eritrea ambapo mashabiki wa Simba wanahisi kuwa watani zao hao walipendelewa baada ya penati zao mbili kurudiwa baada ya kuzikosa awali.

Katika hatua hiyo ya upigaji penati tano tano Simba ndio walianza ambapo Jerry Santo aliongoza jahazi la Simba na kufunga penati ya kwanza lakini Faisal Agab Sido alisawazisha na kufanya iwe sare penati ya pili ya Simba ilipigwa na Salum Machaku na kwenda kugonga mwamba wa juu na hivyo kuzua hofu lakini El Mereikh nayo ilikosa penati yake baada ya Mnigeria Collin Kezechi kupaisha mkwaju wake.

Penati zilizofuatia zilipigwa na Salum Kanoni, Nassor Saidi ‘Chollo’ na Patrick Mafisango aliyepiga penati maridadi iliyomwacha kipa Isam El Hadary akichupa kulia na mpira kutinga kushoto kwa upande wa Mereikh Ahmed Elbasha, Bari Eldin Eldod na kipa Elhadary alifunga penati ya tano na hivyo kufanya ziongezwe moja moja.

Ndipo alikwenda kupiga Ulimboka Mwakingwe ambaye mbali ya kucheza kwa juhudi muda wote wa mchezo pia kiwango chake kilikuwa cha juu na kutumbukiza wavuni mkwaju wake na hivyo kazi ikawa kwa El Mereikh ambayo ilimpa jukumu Sakwaha ambaye penati yake iliokolewa na Kaseja na kumwacha ameduwaa uwanjani.

Kutokana na ushindi huo wa penati 5-4 ,Simba imefuzu kutinga fainali kwa jumla ya mabao 6-5 na sasa inamsubiri mshindi wa nusu fainali ya pili inayofanyika leo kati ya mabingwa wa soka wa Tanzania Bara, Yanga dhidi Saint George ya Ethiopia.

Wednesday, July 6, 2011

Vinara kashfa ya rada watajwa

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Mathias Chikawe amesema Mbunge wa Bariadi Magharibi, Endrew Chenge (CCM), hahusiki kwa namna yoyote na kashfa ya uuzaji wa rada liyoligharimu Taifa pauni milioni 28 ambazo sasa Serikali inataka zirejeshwe.

Mbali na Chenge ambaye pia anatakiwa kujivua gamba ndani ya chama chake kwa kashfa hiyo, Chikawe alisema bungeni jana kuwa, hakuna Mtanzania hata mmoja anayetuhumiwa kwa hilo ndio maana hawajamshitaki mtu.

Akitoa majumuisho ya hotuba ya Ofisi ya Rais Utawala Bora, Chikawe alisema Serikali ililiita Shirika la Serious Fraud Office (SFO) la Uingereza kuja kumchunguza Chenge kwa kushirikiana na Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU) na katika uchunguzi huo Chenge hakukutwa na hatia.

Aliwataja wahusika kuwa ni Sailesh Vithlan, dalali wa rada hiyo Jonathan Callman, Meneja Biashara wa Kampuni ya BAE Systems ya Uingereza iliyouza rada hiyo na Meneja Masoko wa kampuni hiyo, aliyejulikana kwa jina moja la Christopher.

"Kama kuna mtu ana ushahidi dhidi ya Chenge au mtu mwingine atupe na tutampeleka mtuhumiwa huyo mahakamani kesho.

"Kama hakuna, basi tufanye kama kanisani (wakati wa kufunga ndoa) kuwa yeyote mwenye neno naye (Chenge), aseme sasa na kama hakuna basi kila mtu anyamaze," alisema Chikawe.

Alifafanua kuwa Serikali haijamshitaki Chenge wala mtu yeyote na kufafanua kuwa haiwezi kwenda mahakamani kwa hisia na hata wanasheria wanafahamu hilo.

Hii ni mara ya tatu kwa Chenge kusafishwa na tuhuma hizo; mara ya kwanza aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Utawala Bora, Sophia Simba alikaririwa akisema kuwa Chenge alisafishwa na SFO.

Mara ya pili, Chenge mwenyewe alijitokeza mbele ya vyombo vya habari alipokuwa akigombea nafasi ya Spika wa Bunge na kufafanua kuwa SFO na Takukuru walimsafisha baada ya kukosa ushahidi dhidi yake.

Lakini Ubalozi wa Uingereza ulitoa tamko kuwa suala hilo halijakamilika wala halijafikiwa muafaka na Chenge hakupaswa kudai kuwa hana hatia.

Hata hivyo wakati wa Kamati ya Matumizi Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani, Tundu Lissu alisimama na kusema anayo barua inayoonesha kwamba Andrew Chenge na Dk. Idris Rashid walihusika katika ununuzi wa rada hiyo na Chenge alipata dola milioni 1 alizopeleka katika akaunti iliyopo nje ya nchi na Dk. Rashid alipata pauni za Kiingereza laki sita.

Hata hivyo Waziri Chikawe alisimama na kusema kwamba aliwaomba wabunge kama wana ushahidi dhidi ya Chenge waulete ili waende mahakamani hata kesho na akaomba Tundu Lissu ampatie ushahidi huo.

Lakini Lissu alisema ushahidi huo ni barua kutoka SFO kwenda kwa Mwanasheria Mkuu wa Tanzania na hivyo Serikali isiwahadae wananchi kwa sababu wanao ushahidi.

Kashfa hiyo hiyo, itakumbukwa kuwa ilichangia Chenge kujiuzulu nafasi yake kama Waziri wa Miundombinu baada ya kutuhumiwa kumiliki fedha zilizodaiwa kuwa mgawo wake katika uuzaji wa rada; dola milioni moja, zaidi ya Sh bilioni moja nje ya nchi.

Lakini jana kabla ya kutangazwa kuwa Chenge hana hatia, Serikali ilitupiwa zigo la kuwachukulia hatua za kisheria Watanzania waliohusika kupora fedha za umma katika ununuzi wa rada katika Mahakama ya Tanzania kwa kuwa katika Mahakama ya Uingereza, watuhumiwa hao hawatakuwa na hatia.

Ujumbe wa Bunge uliokwenda Uingereza kuwakilisha Watanzania kudai fedha hizo maarufu 'chenji' , umeweka wazi kuwa Kampuni ya BAE Systems inayotuhumiwa kushirikiana na watuhumiwa wa Tanzania katika uporaji huo na SFO, wameweka mazingira ya kutoshitakiwa kwa watuhumiwa hao huko Uingereza.

Wakizungumza baada ya kukabidhi ripoti ya kazi waliyoifanya huko Uingereza kwa Spika wa Bunge, Anne Makinda, wajumbe hao walioongozwa na Naibu Spika, Job Ndugai, walisema wamefanikiwa kushawishi Waingereza kuona umuhimu wa fedha hizo pauni milioni 29.5, kurudishwa kupitia Serikali ya Tanzania.

Lakini pia waliituhumu kampuni hiyo na SFO kwa kupanga mazingira hayo ya kutoshitakiwa kwa watuhumiwa kwa kutumia mwanya wa mazungumzo nje ya Mahakama.

Ndugai alisema baada ya SFO kuishitaki kampuni hiyo, kampuni hiyo iliomba mazungumzo nje ya Mahakama na yalipokamilika, Mwanasheria wa kampuni hiyo, ambayo ndiyo mtuhumiwa, alitengeneza makubaliano ya mazungumzo hayo na kuzuia watuhumiwa wasishitakiwe na kuyasajili mahakamani.

Ndugai alisema kuwa mwanasheria huyo alihakikisha anailinda kampuni hiyo na watuhumiwa wengine.

"Kwa kweli jaji aliyetoa hukumu ile, alikuwa na 'moral pressure' msukumo wa kibinadamu, akaona gharama za kesi ni kubwa akasema nitapunguza gharama za kesi na kuongeza katika tuzo itakayopewa Watanzania," alisema Ndugai.

Alifafanua kuwa katika hilo, badala ya kuamuru fedha nyingi ziwe gharama za kesi hizo ambazo zingetumiwa na SFO au kampuni hiyo; jaji huyo alitoa pauni laki tano tu kama gharama za kesi na pauni milioni 29.5 akaamuru zirejeshwe kwa Watanzania walioibiwa.

Monday, June 20, 2011

Simba yazua makubwa Congo

IKIWA ni siku moja tangu iwekwe Uwanja wa Ndege wa Kinshasa kwa saa nne bila msaada, Simba imepata ahueni ikiwa ni pamoja na hoteli nzuri ya kulala.

Simba sasa imepata ulinzi mkali kutoka kwa mashabiki wa AS Vita Club ya Kinshasa, ambao ni wapinzani wakubwa wa Motema Pembe.

Simba ambayo imefikia kwenye hoteli ya Biveri Roger, ilifanya mazoezi yake  Ijumaa asubuhi kwenye Uwanja wa Ssark na kulindwa vikali na mashabiki pamoja na baadhi ya viongozi wa AS Vita.
AS Vita na Motema Pembe ni wapinzani wakubwa kama zilivyo Simba na Yanga na zote hutumia Uwanja wa Martyrs (Stede des Martyrs) unaobeba mashabiki 80,000.

Mashabiki hao wa AS Vita  Ijumaa asubuhi walilinda milango yote ya kuingilia katika Uwanja wa Ssark na kusababisha vurugu kutoka kwa mashabiki wa Motema Pembe ambao walizuiwa kuingia kuona mazoezi hayo ya Simba.

Majaliwa Mbasa, mmoja wa wadau wa Simba ambaye ameambatana na timu hiyo mjini Kinshasa alisema baada ya kupata mapokezi mabovu siku ya Alhamisi, sasa wamekuwa wakipata sapoti kubwa ya mashabiki wa AS Vita.

Alisema katibu wa mashabiki wa AS Vita alikuwa miongoni mwa watu waliokwenda kuwachukua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kinshasa walipokwama kwa saa nne walipokuwa wakiwasili juzi Alhamisi.

"Lakini  tumefurahi sana kwani timu yetu imefanya mazoezi huku wakilindwa na mashabiki wa Vita ambao walikuwapo kwenye milango yote. Walifanya kazi nzuri kiasi kwamba hakuna shabiki wala kiongozi wa Motema Pembe aliyeingia uwanjani kuona mazoezi," alisema Majaliwa.

Alisema katika mazoezi hayo kulikuwa na vurugu kati ya mashabiki wa Vita ambao walikuwa wakiwazuia wale wa Motema Pembe kutoingia uwanjani.

Mashabiki hao wa Vita wameahidi kuendelea kuilinda Simba hata wakati ingefanya mazoezi ya mwisho kwenye Uwanja wa Martyrs, ambako ndiko kutachezwa mechi hiyo  Jumapili.

Hata hivyo, kocha mkuu wa Simba, Moses Basena alilalamikia chakula ambacho wachezaji wake wanapewa katika hoteli hiyo kuwa ni kichache na si kizuri.

Wachezaji hao walikuwa wanapewa wali, samaki na nyama vya kumtosha mtoto wa miaka mitano kabla ya kutafuta hoteli nyingine kwa ajili ya chakula.

Basena ambaye alisema amebadilisha makosa yaliyojitokeza katika mchezo wa kwanza jijini Dar es Salaam, alishauriana na uongozi wa Simba na kuanzia  Ijumaa jioni wachezaji walikuwa wakienda kupata chakula katika hoteli nyingine ila waliendelea kulala hapo hapo walipofikia.