Friday, January 18, 2013

JK amaliza mgogoro Madagascar


Rais Kikwete ambaye ni Mwenyekiti wa Asasi ya Ulinzi na Usalama ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (Sadc)- Troika, awali alikutana na mpinzani mkuu wa Rais Rajoelina ambaye ni Rais wa zamani wa Madagascar, Marc Ravalomanana na kumshawishi kukukubali kurudi nchini kwake baada ya kuwa uhamishoni nchini Afrika Kusini tangu mwaka 2009.


RAIS wa Serikali ya Mpito ya Madagascar, Andry Rajoelina ametangaza kutowania tena katika uchaguzi wa urais wa nchi hiyo unaotarajia kufanyika mwezi Mei mwaka huu.

Uamuzi wa kutogombea tena nafasi hiyo ulitangazwa jana na Rais Jakaya Kikwete mbele ya Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU), Rais wa Benin, Beni Yayi Ikulu jijini Dar es Salaam baada ya mazunguzo baina yao.

Rais Kikwete ambaye ni Mwenyekiti wa Asasi ya Ulinzi na Usalama ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (Sadc)- Troika, awali alikutana na mpinzani mkuu wa Rais Rajoelina ambaye ni Rais wa zamani wa Madagascar, Marc Ravalomanana na kumshawishi kukukubali kurudi nchini kwake baada ya kuwa uhamishoni nchini Afrika Kusini tangu mwaka 2009.

Pia Rais huyo alitangaza kukubali kutokugombea tena ili kuleta amani na utulivu. “Nimezungumza na Rais Rajoelina na amekubali kutogombea uchaguzi ujao kama uamuzi wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (Sadc) yalivyofikiwa katika vikao vyake vya hivi karibuni,” alisema.

Kwa mujibu wa Rais Kikwete, Rais Rajoelina ametangaza rasmi uamuzi huo juzi nchini kwake na kwamba sasa uchaguzi huo utakuwa wa kidemokrasia na utasimamiwa na Umoja wa Afrika (AU) ambapo marais wote wanatakiwa kuheshimu makubaliano ya umoja huo. Awali, Rais Kikwete alisema kuwa migogoro mingi ya Afrika inasababishwa na wanasiasa ambao wanatumiwa na nchi zilizoendelea kwa masilahi yao.

“Unajua hawa wanasiasa wetu ndio wanaotuletea matatizo, wanatumiwa na nchi za Magharibi ili tuendelee kufarakana na tukishafarakana nchi hizo zinafaidika na rasilimali zetu na faida nyingine ambazo wanazijua wao,” alieleza.

Naye Rais Bon Yayi alipongeza uamuzi wa wanasiasa hao ambapo alisema ndiyo njia pekee ya kuleta amani na utulivu katika nchini hiyo.

Kutokana na hali hiyo, mwenyekiti huyo wa AU alizitaka nchi za Afrika kuungana na kufanya kazi pamoja ili kuokoa rasilimali za nchi zao.

Katika hatua nyingine mwenyekiti huyo alisema kuwa tayari umoja huo umepeleka askari wa kulinda amani nchini Mali kwani wamegundua mgogoro uliopo ni wa kigaidi.

“Tumepeleka zaidi ya askari 1500 kwenda kulinda amani nchini Mali, Nigeria imetoa askari 600 Bukinafaso na 500 na Senegal 500, nitazungumza na Rais Kikwete naye atupatie askari ambao watashirikiana na kikosi hicho ili kuinusuru nchi hiyo.”

Mwenyekiti huyo wa AU alimpongeza Rais Kikwete kwa hatua aliyofikia katika kutatua mgogoro wa mpaka ulipo baina ya Tanzania na Malawi ambapo alisema kuwa anaamini utapata suluhu kabla hajamaliza kipindi chake cha Urais.

“Rais kikwete namfahamu vizuri ni mtu mstaarabu na mpenda demokrasia, suala la mgogoro huu naamini litapata suluhu kabla hajamaliza kipindi chake cha uongozi, alisema Rais Yayi huku akimtania Rais Kikiwete kwamba anaamini atakapomaliza kipindi chake cha uongozi atampisha mtu mwengine badala ya kung’ang’ania madaraka huku akisisitiza kuwa yeye akimaliza kipindi chake cha uongozi mwaka 2016 anatarajia kuwa Padri.

Awali Rais Kikwete alikaririwa jijini Dar es Salaam kuwa Rais Ravalomanana anarudi nchini Madagaska bila masharti yoyote na atapewa ulinzi na Serikali ya nchi hiyo ikisaidiana na Jumuiya ya SADC ambayo Rais huyo alihaidi kuheshimu maamuzi yaliyotolewa na SADC kwa lengo la kuisaidia Madagaska kuwa katika hali ya amani.

No comments:

Post a Comment