Tuesday, March 20, 2012

Kisa na Mkasa na Salim Kikeke

Mwizi na 'haja'

DNA
Teknolojia ya DNA
Mwizi mmoja nchini Uchina aliyekuwa na tabia ya kujisaidia haja kubwa katika nyumba anazofanywa wizi wake, hatimaye amekamatwa kutokana na teknolojia ya DNA.
Polisi jijini Cixi, katika jimbo la Zhejiang wamesema mwizi huyo aitwaye Chen mwenye umri wa miaka 29 akiwa na mwenzake walivunja nyumba moja na kuingia jikoni na kula chakula, kabla ya bwana Chen kujisaidia kwenye sakafu karibu na mlango.
Baada ya kufanya hayo, wawili hao wakaanza kutafuta vitu vya kuiba ndani ya nyumba hiyo, lakini kutokana na kukuru kakara zao, mwenye nyumba alishtuka, na wezi hao kukimbia bila ya kuiba chochote. Miezi michache baadaye, wezi hao waliingia katika nyumba nyingine na kuiba kompyuta mpakato-- yaani Laptop na fedha taslimu yuan elfu moja.
Kama kawaida, waliingia jikoni na kujipakulia chakula, na bwana chen kuacha muhuri wake wa kawaida, wa kinyesi chenye harufu kali karibu na mlango wa mbele. Mtandao wa china daily umesema polisi walifanikiwa kulinganisha vipimo vya DNA na mwizi Chen, ambaye aliwahi kutupwa gerezani kwa kosa jingine mwaka 2003. Baada ya kukamatwa, bwana Chen alikiri kujisaidia katika nyumba anazofanya wizi, akisema, amekuwa akisoma katika vitabu mbalimbali jinsi wezi wanayokuwa na mitindo yao ya kipekee, wanapofanya wizi. Polisi bado wanamsaka mwizi mwenzake.

Mwizi arejesha alichoiba

Zawadi
Zawadi za Krismasi

Bwana mmoja aliyeiba zawadi za Krismasi katika nyumba moja nchini Marekani, amerejesha zawadi zote, na kuandika ujumbe wa kuomba radhi. Mike Valloney aliyeibiwa zawadi hizo amesema camera zake zilimrekodi mwizi huyo akiiba. "Alikuwa akitazama huku na huko, akihisi kama kuna mtu anamtazama" amesema bwana Mike.
Hata hivyo kituo cha televisheni cha WPIX kimesema siku mbili baada ya kuiba zawadi hizo, mwizi huyo alirejea tena, na kurudisha kila alichoiba.
Aidha, mwizi huyo pia aliandika ujumbe usemao " Naomba radhi. Heri ya mwaka mpya. Nataka kufanya mambo mazuri mwaka huu" umesema ujumbe huo. Bwana Valloney aliyeibiwa amesema hadhani kama mwizi huyo ataiba tena.

Aiba na kumuuzia aliyemuibia

iPhone
iPhone kama hii

Polisi mjini Florida Marekani wamesema wamemkamata mwizi mmoja aliyejaribu kumuuzia vitu mtu aliyemuibia vitu hivyo.
Polisi katika kiunga cha Miramar, Florida wamesema mwizi huyo baada ya kuiba simu aina ya iPhone na tabiti aina ya iPad, alimpigia alyemuibia siku mbili baadaye akitaka kumuuzia vifaa hivyo hivyo alivyomuibia.
Polisi wa Miramar wamesema bwana Hank Yan aliyeibiwa siku ya Jumatatu, alishikiwa bunduki na watu wawili waliompora simu na tabiti pamoja na dola mia tano taslimu, limeripoti gazeti la South Florida Sentinel. Polisi wamesema bwana Yan alipokea simu siku mbili baada ya kuibuiwa na alitambua sauti ya mtu anayetaka kumuuzia iPad, na hivyo kupanga kukutana naye. Wezi hao, Zachari Swindle na Devonte Suckie walikamatwa na polsi walipojitokeza katika mahala walipokubaliana na mteja wao.

Bibi na bangi

Bangi
Miche kadhaa
Mwanamama mmoja mwenye umri wa miaka sitini na saba nchini Marekani, ameachiliwa huru na mahakama baada ya kushtakiwa kwa kosa la kupanda miche ya bangi katika bustani yake.
Makachero wa polisi wamesema walikuta miche saba yenye afya na yenye urefu wa futi nne katika bustani ya mwanamama huyo mjini Uniontown, Philadelphia. Mama huyo aitwaye Alberta Kelly amesema yeye alirusha mbegu tu kwenye bustani yake baada ya kupewa mbegu hizo na mtu mmoja mwenye madevu lakini asiyemfahamu.
Bi Kelly amesema wala hakufahamu kama ni bangi, na mtu aliyempa mbegu hizo alimwambia ni mbegu za maua. Bi Kelly alikiambia kituo cha Televisheni cha WTAE kuwa majani ni majani tu.

Hujui Beyonce kaolewa na Jay Z?

Beyonce
Beyonce kaolewa na Jay Z
Polisi mjini Parma, Ohio, nchini Marekani wamesema mtu mmoja amechomwa kisu kwa sababu tu hakuwa akifahamu kwamba mwamamuziki Beyonce ameolewa na msanii Jay Z.
Kachero wa polisi Marty Compton wa kituo cha polisi cha Parma amesema mtu mmoja aitwaye Garfield Heights siku ya mwaka mpya alikuwa akibishana na Ronald Deaver, baada ya bwana Deaver kugundua kuwa Bwana Garfield hafahamu kuwa wanamuziki hao mashuhuri wa Marekani ni wanandoa, kimeripoti kituo cha TV cha WJW, siku ya Alhamisi.
Kachero Compton amesema Bwana Deaver alimchoma kisu bwana Garfield nje tu ya nyumba yake majira ya saa tano usiku saa za huko. Bwana huyo aliyechomwa kisu imeripotiwa anaendelea vizuri katika hospitali ya Metro mjini humo alipolazwa.
Bwana Deaver alikamatwa na kushtakiwa kwa kosa la kushambulia.
-----------------------
Na kwa Taarifa yako...
Watu huzungumza takriban maneno mia moja na ishirini kwa dakika moja.
--------------------
Tukutane Wiki Ijayo... Panapo Majaaliwa....

No comments:

Post a Comment