Wednesday, June 15, 2011

CCM WAFUTA POSHO ZA VIKAO


HOJA ya kutaka kufutwa kwa posho za vikao za wabunge na watumishi wengine wa umma imechukua sura mpya baada ya jana Mbunge wa Bumbuli (CCM), Januari Makamba kuliambia Bunge mjini hapa kuwa suala la kufutwa kwa posho ni la kitaifa na ni sehemu ya Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano uliowasilishwa na serikali.

Kauli hiyo ya Makamba ambaye pia ni Katibu wa Mambo ya Nje wa Sekretarieti ya CCM imekuja huku kukiwa na malumbano makali baina ya Spika wa Bunge, Anne Makinda na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe kuhusu suala hilo la posho za vikao vya wabunge.

Juzi, Spika Makinda alisema Zitto ambaye ni Naibu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, anaweza kufukuzwa ubunge kwa kutosaini karatasi za mahudhurio, hatua ambayo Zitto alisema ataichukua ili asilipwe posho za vikao.

Spika alisema Zitto anaweza kukumbwa na adhabu hiyo iwapo hatasaini karatasi za mahudhurio ambazo ndizo zinathibitsha uwepo wa mbunge katika mikutano na vikao vya bunge na kwamba kanuni zinamwadhibu mbunge kwa kumfukuza asipohudhuria mikutano mitatu. Hata hivyo, Zitto amepuuza kauli hiyo ya Spika kwa kusema kwamba kama ni kwa ajili ya kukataa posho, yuko tayari kufukuzwa bungeni.

"Nitafanya hivyo tuone, Kanuni inasema mikutano mitatu mfululizo na siyo vikao vitatu mfululizo. Nitatumia uzoefu wangu wa siasa za wanafunzi kukwepa mtego wake. Lakini kama anadhani ni sawa kunifukuza ubunge kwa kukataa posho, nipo tayari," alisema.

Kauli ya jana ya Makamba pia inaonekana kutofautina na mawazo ya wabunge wengi wa CCM akiwamo Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo ambaye amesema wanashabikia suala hilo wanajitafutia umaarufu.

Akichangia huo wa maendeleo wa miaka mitano jana, Makamba alionekana kupigia chapuo suala la kufutwa au kuangaliwa upya kwa posho za vikao huku akisema kwamba ni la kitaifa na ni sehemu ya mpango huo.

Makamba alisema kuwa suala la nidhamu na usimamizi wa matumizi ya fedha za umma ni muhimu na kwamba mpango huo umeliona katika ukurasa wa 17 wa kitabu kilichochapishwa kwa Kiingereza na kutoa mapendekezo ya kufutwa kwa posho za vikao na zile za usafiri.

"Mpango unabainisha kwamba kuna umuhimu wa kufutwa kwa posho za vikao na usafiri hivyo iwapo wabunge mtalisikia likiwasilishwa hapa kwa mbwembwe kesho (leo), basi msije mkashangaa kwani ni sehemu ya mpango huu," alisema Makamba.

Kujadiliwa bungeni leo

Mjadala kuhusu malipo ya posho ambao umekuwa ukiendelea kwa wiki moja sasa hasa zaidi nje ya Bunge, leo unatarajiwa kuingizwa rasmi bungeni wakati Bajeti ya Serikali iliyowasilishwa na Mkulo Jumatano iliyopita itakapoanza kujadiliwa.

Suala hilo ni dhahiri litajitokeza katika bajeti mbadala itakayowasilishwa na kambi ya Upinzani Bungeni na Waziri Kivuli wa Fedha, Zitto Kabwe ambaye amekuwa katika mvutano usio rasmi na Spika kutokana na kukataa kulipwa posho za kikao.

Mwenyekiti wa Chadema ambaye pia ni Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe alisema jana kuwa kambi yake inatarajiwa kutoa ushauri mgumu ambao haujazoeleka kwa watendaji wa serikali na kwamba suala la kufutwa kwa posho ni sehemu ya mapendekezo hayo.

Alisema kufutwa kwa posho hizo kunaweza kuokoa zaidi ya Sh900 bilioni ambazo zinaweza kuelekezwa katika maeneo mengine ya huduma kwa wananchi.

Uhalisia posho za wabunge

Mmoja wa wabunge wa CCM ambaye hakutaka kutaandikwa jina lake alisema anasikia kuhukumiwa katika nafsi yake kutokana na kupokea posho za vikao ambazo kimsingi ni sawa na "kuwaibia wananchi".

"Ujue bwana sisi ndani ya CCM mambo hayaendi kama kwa wenzetu (Chadema), wale wanaweza kukaa leo na kuamua, sisi ni tofauti lazima kuwepo na mchakato lakini ukweli ni kwamba hoja yao ni nzuri," alisema mbunge huyo.

Uchunguzi uliofanywa umebaini kuwa malipo ya wabunge yamegawanyika katika sehemu nne ambazo ni pamoja na mshahara ambao ni Sh2,300,000 kwa mwezi, posho ya ubunge kila mwezi ambayo ni Sh5 milioni, posho ya kujikimu (per-diem) Sh80,000 wawapo nje ya majimbo yao kikazi na posho ya vikao (sitting allowance) ambayo huwa ni Sh70,000 kwa kila mbunge.

Kwa maana hiyo, kwa kawaida mbunge hulipwa Sh7.3 milioni kila mwezi kabla ya kukatwa kodi na wawapo Dodoma na Dar es Salaam kwa ajili ya vikao vya kamati na bunge au mikoani kwa ajili ya kukagua shughuli zilizopo chini ya kamati zao. Hulipwa kiasi cha Sh150,000 kila mmoja kwa siku ambazo ni Sh70,000 kwa ajili ya vikao na Sh80,000 kwa ajili ya kujikimu.

Kwa maana hiyo bunge linatarajiwa kutumia kiasi cha Sh1.788 bilioni kwa ajili ya kugharamia vikao 73 vya Bunge la Bajeti iwapo wabunge wote 350 waliopo watahudhuria vikao hivyo.

Kwa hesabu hizo, kila mbunge katika mkutano wa Bunge la Bajeti anatarajiwa kuondoka na kikita cha Sh5.1 milioni mbali na Sh 5.58 milioni ambazo ni malipo kwa ajili ya kujikimu, fedha ambazo ni mbali na mshahara wake kwa mwezi na posho ya ubunge.

CCM yakataa posho

Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeanza machakato wa kufuta posho hizo ikiwa ni hatua ya kupunguza matumizi yasiyo ya lazima. Habari kutoka ndani ya CCM, Dodoma na Dar es Salaam zinasema kuwa mkakati wa kufutwa kwa posho ulianzishwa takriban mwezi mmoja uliopita na sekretarieti mpya inayoongozwa na Katibu Mkuu, Wilson Mukama.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, baadhi ya wajumbe wa sekretarieti walihoji uhalali wa posho wanazolipwa hata pale vikao vinapofanyika katika sehemu ambako ni makazi yao na kwamba hoja hizo ndizo zilizozaa wazo la kufutwa kwa posho katika vikao.

"Hoja ilikuwa kwamba kama chama hakina fedha na tunataka kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, basi posho za vikao zifutwe kwa sababu hakuna ulazima wa posho hizo hasa kwa wajumbe wa sekretarieti ambao kazi zao ni za kila siku," kilieleza chanzo chetu na kuongeza:

"Hivi sasa mpango huo uko kwenye mchakato wa kuwekewa mwongozo na nadhani baada ya kupitia katika vikao vyetu utaanza kutekelezwa. Lakini kimsingi ni kama utekelezaji wake umeshaanza kwa sababu baadhi ya wajunbe wamekataa kabisa kusaini posho hizo."

Habari zaidi zinadai kuwa waraka wa mapendekezo ya kupunguza matumizi ndani ya CCM unakwenda mbali zaidi hadi katika matumizi ya magari na kwamba pale usafiri unapohitaji wa kuelekea kwenye mkutano mmoja, basi viongozi watumie magari machache kwa maana ya usafiri wa pamoja badala ya utaratibu wa sasa ambao unamruhusu kila kiongozi kutumia usafiri wake.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipoulizwa kuhusu sekretarieti kufuta posho katika vikao vyake, hakukanusha wala kuthibitisha, badala yake akadai kuwa hayo ni mambo ya ndani ya chama ambayo hayana faida yoyote kwa umma.

"Hivi ninyi waandishi wa habari, haya mambo mnayapata kwa nani! Haya ni mambo ya ndani ya chama sidhani kama yana tija yoyote kwa umma, maana haiwezi kusaidia chochote," alisema Nape kwa kwa simu.

Alipoelezwa kwamba suala hilo lina uhusiano na sakata linaloendelea bungeni, Nape alisema: "Bunge ni bunge na chama ni chama. Kila taasisi inajitegemea na ina uamuzi wake, lakini pia sisi kama chama tulishatoa kauli mara nyingi kwamba suala la posho kwa wabunge na watumishi wengine wa serikali linazungumzika, ni la kisera na wanaohusika wapo waulizeni hao."

Mwishoni mwa wiki iliyopita Nape akizungumzia malumbano miongoni mwa wabunge kuhusu suala la posho alisema suala hilo linajadilika na kwamba si vyema kulipinga kwa sababu tu linatokea kambi ya upinzani.

Kwa upande wake, Makamba alipoulizwa kuhusu kufutwa kwa posho katika vikao vya Sekretarieti ya CCM naye kama ilivyokuwa kwa Nape, hakukanusha wala kuthibitisha.

"Wewe si unamfahamu msemaji wa chama ni nani? Mwulizeni Nape tena nadhani anakuja Dodoma. Akija mwulizeni, mimi siwezi kulizungumzia.... lakini ninyi waandishi haya mambo ya ndani ya chama huwa mnayapata wapi? Anyway, mwulizeni mwenezi atawaambia," alisema Makamba.

Chanzo: Mwananchi 15/6/2011

No comments:

Post a Comment