Wednesday, June 29, 2011

Hawara amuua mwenye mume

MWANAMKE mkazi wa Ronsoti mjini Tarime mkoani Mara, Debora James (30), anatuhumiwa kumuua mwenzake, Teresia Nago, kwa kumchoma kisu katika mauaji yanayohusisha kugombea mwanamume.

Kwa mujibu wa Polisi, Teresia aliuawa jana saa 4.30 asubuhi Bomani mjini Tarime, baada ya kuchomwa visu viwili tumboni na kifuani na mgomvi wake huyo.

Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Rorya/Tarime, Sebastian Zakaria, alisema Debora alikuwa akituhumiwa kuwa na uhusiano na mume wa Teresia, John Nago ambaye ni mtumishi wa Idara ya Ujenzi katika Halmashauri ya Wilaya ya Tarime.

Kaimu Kamanda alisema, wanawake hao wawili walikuwa na ugomvi wa muda mrefu na vurugu wakigombea mwanamume huyo.

Alisema, jana Teresia na Debora walikwenda kusuluhishwa na mzee wa Kanisa ambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja eneo la Bomani.

Lakini wakiwa Bomani, kulitokea vurugu na Debora ambaye alikuwa na kisu alimshambulia Teresia kwa kumchoma kisu kifuani karibu na moyo na tumboni na kusababisha kifo chake papo hapo, baada ya kutokwa damu nyingi naye akajichoma visu sehemu mbalimbali za mwili wake kwa lengo la kujimaliza.

Kamanda Zakaria alisema Debora amelazwa katika hospitali ya wilaya mjini hapa chini ya ulinzi wa Polisi baada ya kujijeruhi.

No comments:

Post a Comment