Wednesday, May 2, 2012

KISA NA KASA NA SALIM KIKEKE

AMSHTAKI MWANAMKE ALIYEMN'GAN'GANIA

Bwana mmoja nchini Ujerumani amesema atafungua mashtaka dhidi ya mwanamke aliyemfungia ndani kwa muda wa saa tano mfululizo na kumalimisha kufanya naye mapenzi.
Bwana huyo anayefahamika kwa jina la Dieter, ameliambia gazeti la TZ la huko kuwa alilazimika kupiga simu plisi waje kumuokoa kutoka nyumbani kwa mwanamke aliyemfungia ndani.
"Yaani ana wazimu wakufanya ngono" amesema bwana huyo. Akizungumza na gazeti hilo bwana huyo amesema awali walikubaliana na mwanamama huyo kuwa na uhusiano baada ya kukutana katika baa moja.
Amesema baadaye waliodoka na kuelekea nyumbani kwa mwanamama huyo. Hata hivyo bwana huyo amedai kuwa alipotaka kuondoka alikuta mlango umefungwa na ufunguo umefichwa. Amesema alipotaka kutokea dirishani alishindwa kwa sababu nyumba ya mwanamama huyo ipo katika ghorofa ya juu.
Amesema mwanamke huyo alimlazimisha kuendelea na mapenzi licha ya kwamba alikuwa hataki tena. Hatimaye mwanamama huyo alipitiwa na usingizi, na bwana huyo kupata upenyo wa kuita polisi. Taarifa zinasema polisi walipowasili, mwanamama huyo alitaka kuwashawishi kwa ngono, lakini polisi walikataa na kumpeleka kituoni, na kumshtaki kwa kumzuilia mtu na kumlazimisha kufanye tendo.

KUKU BILA YAI

Kuku mmoja nchini Si Lanka amezaa kifaranga bila ya kutaga yai. Kwa kawaida kuku hutaga yai na kulitamia kwa muda wa wiki tatu. Hata hivyo kuku huyo hakutaga yai, na badala yake yai lilisalia ndani ya kuku huyo hadi likapasuka na kufaranga kuzaliwa.
Taarifa zinasema kifaranga hicho kipo katika hali nzuri ya kiafya, ingawa kuku mwenyewe alikufa kutokana na majeraha ya ndani. Afisa mifugo wa huko amekiambia kituo cha habari cha AFP kuwa alikuwa akisikia tu matukio kama haya, lakini safari hii amepata nafasi ya kushuhudia mwenyewe.
"Kuku huyo alichanika sehemu za uzazi na kusababisha kifo chake" amesema afisa huyo. "Mtoto anaendelea vizuri" ameongeza afisa huyo. Habari hizo zimegongwa vichwa vya habari na huku watu wengine wakisema kitendawili cha kipi kilitangulia kati ya kuku na yai huenda kimeteguliwa.
Kuku mwingine huko Montana aligonga vichwa vya habari wiki hii baada ya kutaga yai dogo zaidi duniani. Yai hilo lina ukubwa wa sarafu.

TV YA MBWA

Kituo kipya cha Televisheni kinazidi kupata umaarufu nchini Marekani.
Kituo hicho ni maalum kwa ajili ya mbwa. Kituo hicho kiitwacho DogTV kimepata umaarufu mkubwa mjini San Diego na sasa kitasambaa nchi nzima.
Vipindi katika televisheni hiyo vimetengenezwa mahsusi kwa ajili ya kuwaliwaza na kuwatumbuiza mbwa, wakati wenye mbwa wakiwa wamekwenda kazini.
Picha za televishyeni hiyo hupigwa kwa mtazamo wa kimbwa, na hata sauti na muziki umetengenezwa maalum kwa ajili ya mbwa. Mkazi mmoja wa huko Mary Catania amesema mbwa wake ni mshabiki mkubwa wa TV hiyo.
"Huwa najihisi vibaya ninapomuacha nyumbani na upweke" amesema Bi Mary, "Lakini sasa ana kitu cha kumliwaza" amesema msichana huyo.
Hata hivyo amesema mara kadhaa mbwa wake hujaribu kuingia ndani ya TV ili aungane na mbwa anaowaona kwenye kioo cha TV.

MLOWESHA VITI AKAMATWA

Bwana mmoja nchini Marekani amejikuta matatani baada ya kupatwa na hatia ya kulowesha viti vya wenzake kazini.
Bwana huyo mwenye umri wa miaka hamsini na tisa anashikiliwa na vyombo vya dola baada ya wenzake kazini kulalamika kuwa viti vyao ofisini vimekuwa na madoa yasiyoeleweka yanatokea wapi.
Aidha wamesema wamekuwa wakikuta viti vibichi kila asubuhi wanapofika kazini.
Mameneja ofisini hapo waliamua kuweka mtego kwa kupachika kamera za video. Baada ya kuzikagua picha za video zilizorekodiwa kwa siri walimuona bwana huyo akijisaidia haja ndogo juu ya viti vya wafanyakazi wenzake, wakati wakiwa wamemaliza kazi na kwenda majumbani kwao.
Hatma ya bwana huyo bado haijafahamika, lakini amesababisha hasara ya karibu dola elfu nne na mia tano.

DANSI KATIKA MLO

Nchini Uswisi wafanyakazi wamepata njia nyigine ya kujiburudisha wakati wa mapumziko ya chakula cha mchana.
Wafanyakazi hao huenda katika vilabu vya kucheza dansi na disco kabla au baada ya kupata lo wao wa mchana.
Mtindo huo, unaojulikana kama Lunch Beat - yaani mdundo wakati wa maakuli - umeanza kuenea katika miji mingine ya Ulaya. Baada ya kusakata dansi lao wafanyakazi hao hurejea kazini kama kawaida.
Mtindo huu ulianza kwa wafanyakazi wachache waliokuwa wakicheza muziki katika maeneo ya wazi ya kuegeshea magari. Dansi hilo husakatwa kwa muda wa saa moja, halafu hurejea kazini, ingawa hawatakiwi kunywa vinywaji vyenye ulevi.

ATISHA KWA UFAGIO

Bwana Mmoja anayejulikana kama Lawrence Deptola kutoka mji wa New York huko Marikani ametiwa kizibani baada ya kujaribu kuiba pesa kwa nguvu kwenye benki tatu akitumia ufagio wa chooni kuwatisha wafanyakazi kwenye benki.
Bwana huyo aliwatisha wafanyakazi wa benki na ufagio huo akisema ni bunduki.
Polisi waliitwa baada ya Bwana Deptola kuingia katika benki mmoja na ufagio mkononi na kuanza kuwatukana na kuwatisha wafanyakazi wa benki na kuwaamuru wamtilie pesa kwenye mfuko aliyobeba.
Deptola alikamtwa baada ya kutoka na kukimbia huku polisi wakimfuata.
Na kwa taarifa yako............. Saa zilizotengenezwa kabla ya mwaka 1660 zilikuwa na mkono mmoja tu - wa saa.
Tukutane wiki ijayo, panapo majaaliwa....

No comments:

Post a Comment