Friday, September 16, 2011

Chadema wamkamata Mkuu wa Wilaya Igunga

Boniface Meena na Daniel Mjema, Igunga
VURUGU zimezuka jana katika Kata ya Isakamaliwa, wilayani Igunga zikiwahusisha viongozi wa Chadema na Mkuu wa Wilaya ya Igunga, Fatma Kimario.Katika sakata hilo, wanachama wa Chadema walimkamata Mkuu huyo wa Wilaya kwa tuhuma za kuendesha mkutano wa ndani na watendaji wa serikali za vijiji, wakati akijua kuwa kulikuwa na mkutano wa kampeni za chama hicho karibu na eneo hilo.

Msafara wa Chadema ulifika katika eneo la kampeni saa 8.00 mchana na kabla mkutano haujaanza, Meneja Kampeni wa chama hicho, Sylivester Kasulumbai, aliwaambia waandishi wa habari kuwa mkuu wa wilaya ya igunga alikuwa akifanya kikao cha ndani katika eneo hilo kinyume na taratibu, hivyo wanakwenda kumshughulikia.

Kasulumbai ambaye ni Mbunge wa Maswa Mashariki akiwa na Mbunge wa Viti Maalum, Susan Kiwanga, baadhi ya wananchi na vijana wao, walifika katika ofisi ya Mtendaji wa Kata kulikokuwa kunafanyika mkutano huo na kuanza kuhoji aliko Mkuu huyo wa Wilaya.

Mmoja wa wananchi alimnyooshea kidole mama ambaye alikuwa amekaa mbele na kusema; “..yule ndiye Mkuu wa Wilaya”.Kundi hilo la vijana na viongozi wa Chadema, waliingia katika ukumbi huo na kumtoa nje mama huyo huku wakimtaka aeleze kwa nini anafanya vikao vya ndani katika Kata hiyo wakati anajua kuwa chama hicho kilikuwa na mkutano katika eneo hilo.

Kitendo hicho kilizua purukushani na kutokuelewana kati ya waliokuwa kwenye mkutano wa ndani na viongozi wa Chadema, jambo lililovuta umati mkubwa wa watu.

Maelezo ya DC
Baadhi ya vijana wa Chadema walikuwa wamewashikilia watu waliokuwa wakishiriki mkutano huo huku mama huyo akitolewa nje na kuketishwa kwenye kiti alitakiwa atoe maelezo kuhusu mkutano wake.

Baada ya kukaa kwenye kiti huku akionekana kuchanganyikiwa, alisema yeye ni Mkuu wa Wilaya ya Igunga, jina lake ni Fatma Kimario na kwamba, hakuwa na taarifa za mkutano wa kampeni za Chadema.

“Sina ratiba, iko katika ofisi za halmashauri, hivyo sikujua kama kuna mkutano hapa, hata hivyo watu walikuwepo niliwaruhusu waende mkutanoni na mimi nilikuwa naondoka sasa hivi,” alisema na kuongeza:

“Nilichokuwa nafanya ni mkutano wa viongozi wa serikali kwa ajili ya kuangalia hali ya mifugo inayoibwa sana, elimu kwa wote hasa watoto na ujenzi wa nyumba bora na masuala ya amani”.

Kimario aliwasihi wafuasi wa Chadema kusoma karatasi ya ajenda ili wafahamu kilichokuwa kikijadiliwa kwenye kikao hicho.

Karatasi aliyokuwa akiizungumzia Mkuu huyo wa Wilaya ilikuwa na ajenda tano za kikao hicho ambazo ni; Uhamishaji wa mifugo; Kuwa na choo chenye ubora na nyumba bora; Elimu;  Mipaka ya shule na ajenda ya mwisho ilikuwa Uchaguzi mdogo wa ubunge Jimbo la Igunga.

Hata hivyo mbunge Kiwanga alimtaka mkuu huyo wa wilaya aeleze tangu lini kikao cha viongozi wa serikali kikahudhuriwa na wazee maarufu na mabalozi wa nyumba kumi, swali ambalo lilionekana kumchanganya mkuu huyo wa wilaya kwa kutoa majibu tata.

Mkutano wa Chadema
Wakati hayo yakiendelea, mkutano wa kampeni ulikuwa nao ukiendelea, hivyo viongozi hao wa Chadema walimtaka DC huyo afike kwenye mkutano huo ili aweze kuonana na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa.

Kimario alikubali, lakini akataka dereva wake atangulize gari na kwamba yeye angefuata. “Nitakwenda kwani napaswa kuwepo pale kama msimamizi wa usalama, sijahudhuria mkutano wowote hivyo nitakwenda,” alisema.

Akizungumzia tukio hilo kwenye mkutano wa kampeni, Dk Slaa alisema wakuu wa wilaya na mikoa kufanya mikutano wakati wa kampeni ni kinyume cha sheria, hivyo Kimario alienda kuanzisha vurugu.

“Hapaswi kufanya mkutano wowote hapa hasa akijua kuwa sisi tuna mkutano wa kampeni na yeye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama wa Wilaya,” alisema Dk Slaa na kuongeza:

“DC anafanya nini huku wakati hiki ni kipindi cha uchaguzi au ndiyo wanapanga mikakati ya uchakachuaji halafu wanadai sisi ndiyo tunaofanya vurugu?”

Mkutano wa kwanza na wa pili wa Chadema, hakukuwa na ulinzi wa polisi kama ilivyokuwa kwenye mikutano mingine.

Askari wamwagwa
Wakati gari la waandishi wa habari likirejea mjini Igunga, lilipisha na magari mawili ya polisi yakiwa yamejaa askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), ambayo yalikuwa katika mwendo kasi yakielekea eneo la tukio.

Magari hayo yalifuatiwa kwa nyuma na gari aina ya Toyota Landcruiser ambalo lilikuwa na vioo vyeusi yote yakiwa yamewasha taa kuashiria hali ya hatari.

Hata hivyo polisi wilayani Igunga kupitia kwa Mkuu wake (OCD), Issa Maguha, waliliambia Mwananchi kuwa hawakuwa na taarifa ya tukio hilo na kwamba magari hayo yalikuwa katika doria za kawaida.


CCM yawaangukia wananchi

Katika hatua nyingine CCM kimewaangukia wananchi wa Igunga kikiwataka kuacha jazba na hasira kwani madhara ya kuchagua mbunge kwa chuki yataligharimu jimbo hilo kwa miaka minne ijayo.

Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu wa NEC ya CCM Uchumi na Fedha, Mwigulu Nchemba wakati akihutubia mkutano wa kampeni katika kijiji cha Usongo kata ya Nyandekwa kinachoaminika kuwa ngome ya Chadema.

Habari zilizopatikana kijijini hapo kabla ya kuanza kwa mkutano huo zilidokeza kuwa Chadema walitangulia kufanya mkutano wa kampeni kijijini hapo na kumwaga ‘sumu’ ili wananchi waichukie na wasiichague CCM.

Akihutubia mkutano huo, Nchemba alirudia mara kadhaa kusema, “shusheni jazba” na “punguzeni hasira” ambayo ilitafsiriwa na wengi kuwa ni kujaribu kung’oa mizizi ya Chadema.

Katibu huyo alisema Chadema kimekuwa kikipandikiza chuki kwa wananchi kwamba Serikali ya CCM haijafanya lolote katika kipindi cha miaka 50 ya Uhuru. Alisisitiza kuwa huo ni uongo wa karne unaopaswa kupuuzwa.

“Kuwa na vuguvugu la kifikra inaruhusiwa na pia kuwa na mtizamo tofauti inaruhusiwa lakini si katika kipindi hiki ambacho wananchi wa Igunga wanahitaji mgombea wa CCM kuliko kipindi kingine chochote,” alisema.

Nchemba aliendelea kusema: ”kwenye uchaguzi mdogo nawaombeni mshushe jazba.…hata kama ulikuwa tayari na mlengo fulani, basi badilika kwa manufaa ya wana Igunga…, tusishabikie vyama bali tujadili hoja”.

Katibu huyo ambaye pia ni Mbunge wa Iramba Mashariki, aliwasihi wananchi wa kijiji hicho na Jimbo la Igunga kuacha kushabikia mambo ya maendeleo kama wanavyoshabikia timu za soka hata ambazo hawazijui.

Kwa upande wake, mgombea Ubunge wa CCM, Dk Dalaly Kafumu aliahidi kusimamia mradi wa kuvuta maji kutoka Ziwa Victoria hadi Igunga kupitia majimbo ya Kahama na Nzega.

Dk Kafumu aliahidi kutumia utaalamu wake wa madini kuhakikisha kuwa wachimbaji wadogo wanatengewa maeneo yenye madini katika jimbo hilo na kutatua tatizo na kero ya muda mrefu ya daraja la Mbutu.

No comments:

Post a Comment