Saturday, February 4, 2012

Maghorofa Dar es Salaam yadaiwa kujengwa kwa fedha ‘chafu’

BAADHI ya maghorofa yanayochipuka kama uyoga jijini Dar es Salaam na kwingineko nchini, yanatokana na shughuli za usafishaji wa fedha haramu.

Shughuli hiyo inafanyika kwa wafanyabiashara hao kuingiza fedha haramu kutoka nje ya nchi na kununua bidhaa na huduma na kuziuza kihalali nchini kwa muda kabla ya kuzibadilisha katika fedha za kigeni na kuondoka nazo.

Akichangia Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Udhibiti wa Fedha Haramu wa Mwaka 2012 bungeni jana, Kabwe Zitto alidai hata upandaji holela wa bei za viwanja katikati ya miji umekuwa ukisababishwa na wafanyabiashara wa fedha chafu.

Alidai mabilioni ya fedha yalitoroshwa nchini kati ya mwaka 2000 hadi mwaka juzi kwa njia mbalimbali ambapo zinakadiriwa kufikia dola bilioni 2.9 za Marekani. Hali hiyo alidai inachangia pia upandaji holela wa bei za viwanja vya kujenga katikati ya miji hususan Dar es Salaam.

Alidai kuanguka kwa sarafu ya Tanzania kati ya Septemba na Novemba mwaka jana, ni matokeo ya shinikizo la wasafishaji hao wa fedha, ambao walinunua fedha nyingi za kigeni na kuondoka nazo. Muswada huo ambao ulisomwa kwa mara ya pili jana na kuanza kuchangiwa na Zitto kati ya wachangiaji sita walioruhusiwa kabla ya kuhitimishwa, umelenga kufanya marekebisho katika vifungu kadhaa na kutoa adhabu kali kwa wahusika.

Hata hivyo, pamoja na mchango wa Zitto, kambi rasmi ya upinzani katika hotuba yake, ilisema sifa ya Tanzania na nchi jirani kuwa wasafishaji wa fedha haramu inatokana na Taifa kutotumia sheria iliyotungwa mwaka 2006 inavyostahili. Kwenye hotuba hiyo iliyosomwa na Naibu Waziri wa Fedha Kivuli, Christina Mughwai, Upinzani ulihoji Serikali kutaka kufanya mabadiliko katika sheria ambayo haijaona utekelezaji wake.

Mwaka 2006, Bunge lilipitisha Muswada wa Sheria ya Kuzuia Fedha Haramu lakini haikutungiwa kanuni za utekelezaji. “Kwa mfano sheria iliyopo kifungu cha 23 (1) iliweka utaratibu wa fedha ambazo zinaingia na kutoka nje ya nchi, lakini la kustaajabisha, tangu wakati huo kwa kipindi cha miaka sita sasa, mipaka ya nchi imekuwa ‘wazi’ na fedha nyingi zinatoka bila kujulikana, kutokana na kukosekana kwa utekelezwaji wa kifungu hiki cha sheria,“ alisema Waziri Kivuli.

Alisisitiza, kwamba kifungu hicho kilimpa Waziri mwenye dhamana ya fedha, mamlaka ya kuamua ni kiasi gani cha fedha kinaweza kusafirishwa nje ya nchi kikiwa ni kiasi taslimu, ambacho mtu anapaswa kuwa nazo, lakini hakuna kilichofanyika mpaka sasa. Katika hotuba hiyo pamoja na kupendekeza kikomo cha fedha za kigeni anazoruhusiwa mtu kubeba zikiwa taslimu kuwa dola 10,000, walihoji kama kweli Serikali ina dhamira ya kutekeleza sheria hiyo.

Walidai kuwa hata kwenye mkutano wa Maseru (Lesotho), Serikali ilikataa kusaini mkataba wa fedha haramu kwa tuhuma kwamba Tanzania na Malawi ndizo zinatumika sana kusafisha fedha.
Mkutano huo wa Agosti 2009 ulikuwa na lengo la kuangalia namna bora za kukabiliana na fedha haramu ambazo zinatishia uchumi wa nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara.
Upinzani pia ulizungumzia vifungu kadhaa vinavyotakiwa kubadilishwa na kusema vingine havina uhalisia.

Ulitolea mfano kifungu cha 28B kinachopendekeza adhabu ya jumla kwa mtu kuwa faini ya juu Sh milioni 500 na kiwango cha chini Sh milioni 100 au kifungo kisichozidi miaka mitatu jela, wakati kwa kampuni au taasisi kiwango cha adhabu ni kuwa faini isiyo chini ya Sh milioni 500 .

“Utaratibu huu wa kutoza faini ni dhahiri kuwa haukufikiwa kwa kuzingatia kigezo chochote kile, kwani haijabainisha kuwa ni kiwango gani cha fedha kitapaswa kulipiwa faini hiyo na hivyo kinaweza kutumika kama kishawishi katika kuvutia wahalifu na hasa kampuni kutumia mwanya huu kupitisha fedha nyingi haramu,“ alisema Mughwai.

Alisema Kambi ya Upinzani, inaona faini hizo haziko kiuhalisia, hivyo kutaka faini ziwekwe kwa kutumia asilimia ya fedha atakazotuhumiwa nazo na kiwango kiwekewe jedwali.
Muswada huo una marekebisho mbalimbali manane yaliyoombwa na Serikali yashughulikiwe, yakiwamo ya Sheria ya Udhibiti wa Fedha Haramu, sura ya 423 ili iweze kutumika Tanzania Bara pekee na kurekebisha sheria ili kuwezesha Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu (FIU) kujitegemea.

No comments:

Post a Comment