Wednesday, February 8, 2012

Utata wa Sh 3trilioni wagundulika sekta ya madini


Midraji Ibrahim, Dodoma na Boniface Meena
MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe amesema kuna utata wa Sh2.7 trilioni katika sekta ya madini kutokana na ukaguzi uliofanywa kwenye sekta hiyo mwaka jana na Wakala wa Ukaguzi wa Sekta ya Madini (TMAA).

Zitto aliibua upotevu huo matrilioni jana alipokuwa akichangia hoja ya serikali kuhusu Maazimio ya Bunge katika Sekta ya Nishati na Madini iliowasilishwa na Waziri William Ngeleja.

Alisema Wakala wa Ukaguzi wa Sekta ya Madini (TMAA), umegundua utata wa Dola 1.7 bilioni katika sekta ya madini katika ukaguzi wake uliofanyika mwaka jana.

"TMAA wamegundua utata wa Dola 1.7 bilioni katika sekta ya madini hivyo iundwe timu ya wakaguzi kuangalia sekta nyingine kama ya gesi na mafuta ambayo nayo inalalamikiwa na wabunge kupoteza fedha nyingi,"alisema Zitto.

Aliendelea "Nchi inaweza ikaamua kuwa Nigeria ambayo mafuta yanawape fedha nyingi, lakini umaskini wa wananchi wao unazidi kuongezeka. Ni muhimu wananchi wa Mtwara na Tanzania kwa ujumla wakafaidika na gesi inayozalishwa maeneo yao."

Awali wakichangia mjadala huo wabunge wametaka watuhumiwa wote walioshughulika na ufisadi ulioisababishia serikali upotevu wa Dola za Marekani 20.1 bilioni sawa na zaidi ya Sh 30 bilioni, wakamatwe na kufunguliwa kesi ya jinai.

Hatua hiyo inatokana na Kampuni ya Pan African Energy Tanzania Ltd (PAT), inayosafirisha gesi kutoka Songosongo hadi Dar es Salaam kudaiwa kufanya udanganyifu wa makusudi kipindi cha miaka 2004 hadi 2009 na kusababisha Serikali kukosa gawio lake inalostahili.

Mbunge wa Bumbuli, Januari Makamba (CCM), alisema fedha hizo zinatakiwa kurejeshwa kwa sababu hata PAT imekiri kujirejeshea fedha hizo isivyo halali.

“Sasa Serikali imeunda kamati, matarajio yetu kwamba suala hili litafikia mwisho mapema, siyo kama suala lile (Richmond) lingine ambalo halijafikia hatima mpaka leo,” alisema Makamba na kuongeza:

“Kamati tumeelezwa kuna TRA na CAG, lakini tunataka mtu mwingine aingie naye ni DCI, kuna jinai imefanyika hatua ambayo taifa limewekwa reheani na mwekezaji…hatuwezi kuwa wanyonge wa kutetea haki yetu kwa sababu ya kigezo cha kutovuruga mazingira ya uwekezaji, tuwe tayari kutetea haki yetu bila woga.”

Alisema ni kwa upande wa sekta hiyo ni muhimu Shirika la Petroli nchini(TPDC), likaachwa liwe huru ili liweze kufanya kazi zake kwa ufanisi na si kuwekewa vizuizi ikiwa ni pamoja na kuomba ruhusa ya kuajiri watumishi kitu ambacho si sawa.

Mbunge wa Kilwa, Murtaza Mangungu aliilalamikia kampuni ya PAT kwa kufuja fedha za wananchi na kutaka serikali ichukue hatua kutokana na maazimio ya Bunge ili kuwanufaisha wananchi.

"Inashangaza gesi inachibwa Kilwa lakini haiwasaidii wananchi wa eneo hilo na Halmashauri yao, Hii inatokana na hadithi za serikali kutokutekeleza maazimio ya Bunge,"alisema Mangungu

Kangi Lugola ambaye ni mbunge wa Mwibara alisema haiwezekani serikali ikawa inashindana na bunge katika masuala ya ufisadi unaofanyika.

"Serikali ishughulike na kuwachukulia hatua wale wote ambao wametuibia na kuendelea kuwachekea. PanAfrica Energy imekosa sifa na uaminifu haifai kucheka nayo,"alisema Lugola.

Alisema serikali haiitaji kuzungumza nao kwa kuwa wanaiba waondoke kwa kuwa bila kuiangalia kampuni hiyo vizuri itaendelea kuiba zaidi.

Mbunge wa Bariadi Mashariki, John Cheyo (UDP), alitaka kamati ya bunge kuendelea kupitia mikataba mbalimbali ya madini, kwa sababu sekta hiyo ina udanganyifu mkubwa.

Cheyo alisema wamebaini kwa makusudi Serikali imeamua ofisi ya CAG kukaa bila kazi, kutokana na kuunda kamati ya majadiliano (GNT).

“GNT huyu ni nani? Jambo likishaharibika anapatikana wapi? Serikali ingalie jambo hili hasa linalohusu mapesa,” alisema Cheyo.

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema), alisema wanahitaji suala hilo lifikie mwisho, lisiwe kama la Richmond ambalo tangu mwaka 2008 hadi sasa halijapata ufumbuzi na kwamba, kauli ya Serikali ilikuwa nzuri lakini utekelezaji umeshindika.

“Katika taarifa ya Serikali hakuna maelezo yoyote kuhusu kuwawajibisha wale waliohusika na kashfa hii… tusipokuwa makini na haraka kwenye suala la gesi nchi itakwama,” alisema Mnyika.

Mbunge wa Muhambwe, Felix Mkosamali (NCCR-Mageuzi), alisema taratibu ziko wazi mwekezaji anapokiuka masharti, mkataba unatakiwa kuvunjwa na kuhoji kigugumizi inachopata Serikali kufikia uamuzi.

“Bunge tuwe tunatoa maazimio na muda wa utekelezaji, tutaendelea kuunda kamati nyingi Watanzania watazidi kuumia bila utekelezaji wowote… kama watu hawawajibiki tunatoa maazimio Serikali inakaa bila utekelezaji, basi wabunge tutakuwa hatutekelezi wajibu wetu,” alisema Mkosamali.

Mbunge wa Kisarawe, Suleiman Jafo (CCM), alisema tatizo linalojitokeza kwenye mikataba ni watendaji wanaohusika kutokuwa waadilifu.

“Mapunjo ya Serikali yanayofikia dola 20.1 milioni za Marekani yarudishwe mara moja. Serikali ichukue hatua za kufanya uchunguzi wa kijinai kama ilivyopendekezwa na kamati,” alisema Mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage, alipokuwa akisoma maoni ya kamati kuhusu taarifa ya Serikali ya utekelezaji wa maazimio ya Bunge.

Pia, miongoni mwa maazimio ya Bunge linataka Serikali kusitisha mkataba na Pat, huku usitishwaji huo ukienda sambamba na taratibu za za kisheria na mikataba zinazingatiwa, uwapo wa visima na mitambo, uhakika wa upatikanaji wa gesi nchini.

Hata hivyo, Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, alisema Serikali imeunda kamati ya majadiliano itakayoanza kazi Februari 20, mwaka huu itakayotoa mwelekeo wa kufuata juu ya suala hilo kwa kuzingatia athari zake.

Akizungumza na Mwananchi jana, Ngeleja alisema katika kuvunja mikataba hakuna njia ya mkato lazima hatua zilizopendekezwa na Serikali zifuatwe, kwa sababu inaweza ikaligharibu taifa hapo baadaye.

“Hakuna shortcut (mkato) lazima taratibu hizi zifuatwe, mkivunja mjue mtarudishwa huko kwa hiyo ni kuvumiliana tuone tunalifikisha suala hili wapi,” alisema Ngeleja.

No comments:

Post a Comment