Monday, August 15, 2011

Kisa na mkasa na Salim Kikeke

Risasi


Bwana mmoja nchini Marekani yuko hospitali baada ya kujipiga risasi kwenye uume wake.
Bwana huyo kutoka Phoenix, Arizona, alijipiga risasi kwa bahati mbaya, wakati akiweka bastoka katika mfuko wake wa suruali.

Polisi katika kiunga cha Chandler wamesema bwana huyo, Joshua Seto mwenye umri wa miaka 27, akiwa na mchumba wake Cara Cristopher walikuwa wakielekea katika dukamoja ndipo walipokutwa na mkasa huo.
Bunduki hiyo ilifyatuka, na risasi kupenya katika uume wa Joshua na kupitiliza hadi kwenye paja la bwana huyo.

Haraka walipiga simu ya dharura, na Bi Cara kuambiwa azuie damu kububujika kwa kutumia shati la mchumba wake huyo.

Kwa mujibu wa mtandao wa Stuff.co.nz polisi wamesema hawana uhakika ni bunduki ya aina gani ilifyatuka.
Aidha kachero wa polisi wa Chandler, Seth Tyler amesema hafahamu bwana huyo atatoka lini hospitali, na iwapo kama ameumia kiasi gani.

Polisi Tyler amewataka watu kutumia mikoba maalum ya kuwekea bastola, badala ya kuziweka mfukoni, au kuzichomeka kwenye mikanda ya suruali.

Kumeza ushahidi


Fundi mmoja wa ujenzi ameburuza mahakamani nchini Marekani baada ya kutuhumiwa kumeza ushahidi.
Shirika la habari la Reuters limesema bwana huyo Wilfredo Gonzalez alimeza pete ya almasi aliyokuwa kitaka kuiiba.

Waendesha mashitaka mjini Chicago wamesema bwana Gonzalez alikuwa akifanya kazi za ujenzi katika mji wa Cicero, huko Illinois, alipofanya wizi huo, wakati mwenye nyumba alipoingia bafuni kuoga.
Baada ya mwenye nyumba huyo kugundua kuwa pete yake imepotea katika mazingira ya kutatanisha, alimuita mume wake.

Gonzalez alipoulizwa alikana, lakini lakini baada ya vuta nikuvute, aliitoa pete hiyo mfukoni na kuimeza.
Polisi waliitwa mara moja, na Gonzalez kupelekwa hospitali, ambapo alipigwa picha za X-ray, na kuonesha jinsi pete hiyo inavyoshuka tumboni taratiibu.

Polisi hatimaye walifanikiwa kuitoa pete hiyo, ingawa haijaelezwa njia gani ilitumika. Bwana Gonzalez anakabiliwa na kifungo cha miaka mitatu jela, iwapo atakutwa na hatia.

Popo

Waumini katika kanisa moja hapa Uingereza wamelazimika kulikimbia kanisa lao, kufuatia popo kutanda katika paa.

Gazeti la daily Mirror limesema popo hao hujisaidia wakati maombi yanaendelea. Taarifa zimesema mwanamama mmoja aliugua kutokana na hali hiyo kiasi kwamba maafisa wa mazingira na afya kulazimika kuitwa kushuhudia. Hata hivyo waumini hao hawana uwezo wa kuwaondoa popo hao kufuatia pingamizi la kisheria lililowekwa na wanaharakati wa mazingira.

Wanaharakati hao wanasema popo hao ni aina ya kipekee na ni adimu, na hivyo haitakiwi wahamishwe au kufukuzwa. Kanisa hilo, saxon Church, lililopo Ellenburn, Yorks kaskazini, limesema linafikiria kuchukua hatua za kisheria.

Mmoja wa wahudumu wa kanisani hapo, Liz Cowley amesema watu hawawezi kuendelea kusali, huku popo wakitoa kinyesi na mikojo. "Ilibidi kukatishe misa" amesema bi Liz.
Msemaji wa wanaharakati wa mazingira wa Natural England amesema popo hao wenye masikio makubwa na rangi ya hudhurungi, wanaweza wakatoweka duniani iwapo hawatapata matunzo mazuri.

Kufutari


Waisilam wanaoishi katika jengo refu zaidi duniani, wanalazimika kusubiri muda zaidi kufutari kuliko waisilam wengine, kwa kuwa jua linachelewa kuzama huko walipo, kutokana na urefu wa jengo hilo. Jengo hilo liitwalo Burj Khalifa liko Dubai.

Kiongozi wa juu wa kidini wa Dubai, Mohammed al-Qubaisi amesema wale wanaoishi zaidi ya ghorofa ya themanini, lazima wasubiri dakika mbili zaidi, baada ya muda kutimia mjini Dubai ili kupata futari yao.
Mwezi wa Ramadhani ulianza wiki moja iliyopita.

Gazeti la Mirror limesema shekhe huyo amesema wale wanaoishi katika ghorofa ya mia moja na hamsini na kuendelea, watalazimika kusubiri dakika tau zaidi ya wenzao.
Jengo hilo, Burj Khalifa, lina ghorofa mia moja na sitini. Waisilam huanza kula futari mara wanapoona jua limezama.

Polisi

Polisi mmoja nchini India alimfukuza mtu aliyekuja kufungua kesi ya kuibiwa mapema asubuhi, akimtaka aje baadaye.

Polisi huyo alisema, akifungua kesi hiyo asubuhi, basi siku nzima atakuwa akipokea kesi kama hizo. Mlalamikaji, Amandeep Saini, wa eneo la Naraingarh alishangazwa na jibu hilo. Bwana huyo alikwenda polisi kushitaki, baada ya kuibiwa simu yake ya mkononi. Gazeti la Times of India limesema polisi huyo alisema hayuko tayari kuanza siku yake kwa kuandikisha kesi ya wizi.
"Tafadhali njoo saa nane mchana" alisema polisi huyo.

Mwizi pochi

Polisi nchini Marekani wamesema mwizi mmoja aliingiwa na imani na kuamua kurejesha pochi aliyoiba.
Gazeti la Eagle Tribune limesema mwizi huyo alikwapua pochi ya mwanamama mmoja katika duka la New Hampshire.

Pochi hiyo ilikuwa na dola tinisi pamoja na kifaa cha kuongozea njia, maarufu kama GPS. Hata hivyo siku chache baadaye, mama huyo mwenye umri wa miaka sitini na moja, aliikuta pochi yake, alipokwenda posta kuchukua barua zake.

Siku chache baadaye, alisikia mtu akigonga mlango wa nyumba yake, na alipofungua, alikutana ma mtu, aliyemuomba radhi, na kurejesha viu vingine vilivyosalia.

Baada ya kuomba radhi mwizi huyo alimpa mwanamama huyo barua, na haraka kutimua mbio. Barua hiyo ilikuwa na maelezo zaidi ya kuomba radhi.

Kaimu kamanda wa polisi kathleen Jones ameliambia gazeti la Eagle Tribune kuwa, ingawa mwanamama huyo amefurahi kurejeshewa vitu vyake, lakini sasa ana wasiwasi, kwa kuwa huyo mwizi anafahamu mahala anapoishi.

Polisi wamesema huenda aliweza kufahamu nyumba hiyo, aada ya kukuta anuani ndani ya pochi aliyoiba.

Busu marufuku

Jumuiya moja inayoshauri watu kuhusu tabia za kijamii nchini Ujerumani, imetoa wito kwa watu kupigwa marufuku kupigana busu wakiwa kazini.

Jumuiya hiyo, Knigge Society imesema, tabia ya kupigana busu katika mashavu kama njia ya kusalimiana kwa wafanyakazi, inawatatiza wajerumani wengi. Mwenyekiti wa jumuiya hiyo hans Michael Klein amesema amepokea barua pepe nyingi zikionesha wasiwasi wa busu kutoka kwa wafanyakazi. Amewashauri watu makazini, kusalia na utamaduni wa kawaidia wa kusalimiana kwa kupeana mikono.

No comments:

Post a Comment