Thursday, August 11, 2011

SAKATA LA MAFUTA:Wafanyabiashara wasalimu amri


KAMPUNI nne zilizopewa amri na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura), ya kurejesha huduma hiyo mara moja za BP, Oilcom, Engen na Camel Oil zimesalimu amri na kuanza usambazaji na uuzaji wa mafuta katika vituo mbalimbali nchini.Hata hivyo, katika baadhi ya vituo jijini Dares Salaam, utoaji wa huduma hiyo ulikuwa kusuasua hali iliyowafanya baadhi ya vijana kufunga barabara na kuvizingira wakitaka kuhudumiwa kwa nguvu.Mbali ya kufunga barabara na kuzingira vituo, vijana hao pia walikuwa wakiandamana barabarani kuelekea kituo kimoja baada ya kingine hasa vile vilivyopo kando kando ya Barabara ya Mandela.

Polisi waingia vituoniPolisi jana walikuwa wakifuatilia kwa karibu usalama katika vituo vya kuuzia mafuta kwa askari wake kufanya doria vituoni.Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema kutokana na kauli ya Serikali, jeshi hilo limelazimika kulinda usalama na kukagua kuona ni vituo vilivyokuwa vikitii agizo hilo na vile vilivyokaidi.

“Hili suala linahitaji usimamizi wa hali ya juu, unajua tumelazimika kulinda usalama kwa wananchi kutokana na hizo foleni. Pia tunavikagua kujua kama vinatoa huduma,” alisema.

Camel wakutana lakini wauza mafuta
Mmoja wa maofisa wa Kampuni ya Camel ambaye hakutaka kutajwa jina lake gazetini alisema wameanza kutekeleza amri hiyo na tayari malori yalianza kuchukua mafuta na kusambaza katika vituo.

Alisema kazi hiyo ilianza jana mapema asubuhi na kwamba sambamba na hilo, viongozi wa ngazi za juu walikuwa kwenye mkutano wa ndani kujadili namna ya utekelezaji wa agizo hilo.Waandishi wa gazeti hili walifika kwenye hifadhi ya kampuni hiyo, Kurasini na kushuhudia malori makubwa yakipakia shehena ya mafuta kupeleka vituoni.

Engen yajikosha kwa Serikali
Engen, baada ya Mkurugenzi wake, Selan Naidoo kutuhumiwa kuidharau Serikali kwa kuipa saa 24 ifidie hasara itakayopata kutokana na bei mpya elekezi, jana imeibuka na kusema kwamba imekuwa na uhusiano mzuri na Serikali ya Tanzania na wakati wote imekuwa ikishirikiana na taasisi mbalimbali.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Meneja Mkuu wa kampuni hiyo, Wayne Hartmann wakati wote kampuni hiyo imekuwa na malengo chanya kwa Tanzania na kwamba msimamo utakuwa wa kudumu kwao kwa wakati wote watakaokuwa wakiendesha biashara ya mafuta nchini.

Alisema kauli iliyotolewa na Naidoo kuhusu bei mpya za mafuta zilizotangazwa na Serikali kuwa ni msimamo wa kampuni hiyo na haihusiani kwa namna yoyote na kampuni nyingine za mafuta nchini.

Hata hivyo, Hartmann alisema kuwa bei mpya za mafuta zilizoanza kutumika mwanzoni mwa mwezi huu, zimeyaweka makampuni ya mafuta katika wakati mgumu na mengi yamejikuta yakiuza kwa bei ya hasara.

Kwa upande wake Naidoo alisema vituo vingi vinavyomilikiwa na kampuni hiyo vingeanza kutoa huduma hiyo muda wowote kuanzia jioni kwa kuwa nyakati za mchana baadhi havikuweza kutoa huduma hiyo kwa kuwa havikuwa na mafuta.


Oilcom: Tumetekeleza maagizo
Meneja Mkuu wa Kampuni hiyo ya Oilcom, Ahmed Bathawab alisema jana kwamba wametii agizo la Serikali na kusambaza mafuta kwenye vituo vyote vilivyopo chini ya kampuni hiyo.Alisema kampuni hiyo inasambaza mafuta kwa vituo zaidi ya 70 nchini kote, huku baadhi yake vikimilikiwa na kampuni hiyo na nyingine zikiwa chini ya washirika wake wa biashara.

Kuhusu agizo la kujieleza alisema wamepatiwa fomu na kujaza kisha kuzirudisha serikalini.“Tumetekeleza agizo la Serikali pamoja na masharti yake. Tumefungua vituo vyetu vya mafuta na kuhusu kujieleza walituletea fomu, tumejaza na kurudisha,” alisema Bathawab.Alisema kampuni yake imefungua vituo vyake 16 vya jijini Dar es Salaam na zaidi ya 70 vilivyopo nchi nzima na kueleza kwamba wamekubali kuuza kwa bei mpya iliyotangazwa na Ewura licha ya kulalamika kuwa ni bei ya hasara.

Alisema kampuni yake imekuwa ikipata hasara ya Sh117 kwa lita moja ya mafuta ya dizeli wakati hasara katika mafuta ya petroli ni Sh94.“Tumekubali agizo la Serikali siyo kutokana na amri yake pekee bali, hata sisi hatupendi nchi iingie kwenye matatizo. Tutaendelea kuuza kwa hasara hadi hapo tutakapofikia mwafaka,” alisema Bathawab.

Alisema pamoja na hatua hiyo bado wamiliki hao wanaendelea na mkutano na Ewura kujadili hatima ya sakata hilo.

BP yasuasua
Kwa upande wa Kampuni ya BP, jana walikuwa kwenye kikao kujadili agizo hilo la Serikali.Mwandishi wa gazeti hili alifika katika Ofisi za BP, Kurasini na kuelezwa kuwa viongozi walikuwa kikaoni na kwamba hakuna tamko ambalo lingetolewa mpaka kitakapomalizika.Mtumishi mmoja wa kampuni hiyo aliyejitambulisha kwa jina la Agness Nsangalufu alisema: “Kwa sasa hivi hakuna taarifa yoyote kuna kikao kinaendelea labda nikupe namba ambayo ukipiga baadaye utapewa taarifa.”

Hata hivyo, namba hiyo ilipopigwa aliyepokea aliikata mara baada ya mwandishi kujitambulisha na haikupatikana tena hadi tunakwenda mitamboni.Mpaka saa 10 baadhi ya vituo kampuni hiyo vilikuwa havitoi huduma hiyo jambo lililoibua maswali mengi kutoka kwa wananchi hasa ikizingatiwa kwamba Serikali ina hisa katika kampuni hiyo.

Hata hivyo, taarifa iliyotolewa jana na Ofisa Uhusiano Mwandamizi wa Ewura, Titus Kaguo ilisema kampuni hiyo ilikuwa imetoa mafuta ya petroli lita 48,000 na dizeli lita 402,000 kwa ajili ya kuuzwa katika vituo vya rejareja.

Taomac yanywea
Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Kampuni za Kuuza Mafuta Tanzania (Taomac), Salum Bisarara alisema hawezi kuzungumzia kauli iliyotolewa na Serikali juzi kwa sababu ilielekezwa kwa kampuni.

“Serikali jana (juzi) ilielekeza kauli yake kwa kampuni za kuuza mafuta, kwa sasa suala lolote linalohusu bei ya mafuta sisi hatuwezi kulizungumzia, suala hili linatakiwa lizungumzwe na kampuni, sisi haturuhusiwi kupigania mambo ya bei za mafuta kabisa,” alisema na kuongeza:

“Ewura wametutahadharisha tusije tukavunja sheria kwa sababu suala hili limefika pabaya, hata suala la adhabu haturuhusiwi kulizungumzia.”

Mapema wiki hii Ewura iliweka bayana kwamba ingeishauri Tume ya Ushindani wa Kibiashara (FCC) kuifuta Taomac kutokana na kile ilichodai ni kukiuka sheria za biashara ya ushindani baada ya kukaa na kujadiliana kuhusu mgomo.

Wiki iliyopita, Bisarara alikaririwa na vyombo vya habari akisema kwamba kutokana na bei elekezi iliyotolewa na Ewura, wafanyabishara wanapata hasara ya Sh150 mpaka 250 kwa kila lita hivyo kampuni hizo zitaweza kutoa huduma hiyo chini ya mwezi mmoja tu.

Ewura yatoa tamko
Kwa upande wake, Ewura imesema kuanzia jana, kampuni 13 ziliuza petroli na dizeli kwa ajili ya kusambazwa kwenye vituo vya rejareja.Taarifa ya Ewura imesema mbali ya BP, Kampuni ya Camel Oil ilitoa petroli lita 416,500 na dizeli 626,000, OilCom ilitoa petroli lita 353,000 na dizeli lita 382,000, Total ilitoa dizeli lita 163,000  na ORYX ilitoa petroli lita 44,000 na dizeli lita 91,000.

Kampuni ya Gulf Bulk ilitoa petroli lita 86,500 na dizeli 272,000, Engen ilitoa lita 64,000 za petroli na lita 175,000 za dizeli, MGS International ilitoa lita 116,000 za petroli.

Nat Oil ilitoa petroli lita 55,000 na dizeli 79,000. Lake Oil ilitoa lita 65,000 za petroli na dizeli lita 279,500. Gapco ilitoa petroli lita 418,100 na dizeli lita 348,500.

Kampuni ya Hass ilitoa petroli lita 119,000 na dizeli lita 57,500 wakati Kobil ilitoa lita za petroli 37,000 na lita 431,000 za dizeli.

No comments:

Post a Comment