Wednesday, October 26, 2011

Gaddafi azikwa kwa siri jangwani


MISRATA, Libya
MWILI wa aliyekuwa kiongozi wa Libya, Kanali Maummar Gaddafi umezikwa katika sehemu ya siri jana, baada ya kuuawa kwake na wapiganaji waliokuwa wakimpinga wiki iliyopita.

Mmoja wa waopiganaji hao alijitokeza kwa mara ya kwanza jana kupitia mkanda wa video akieleza kwamba yeye ndiye aliyechukua uamuzi wa kufyatua risasi na kumuua Gaddafi, kwa kuwa hakuona haja ya kumshikilia akiwa hai.

Maziko hayo yamefanyika baada ya kuwapo kwa mvutano baina ya wanafamilia wa Kanali Gaddafi na uongozi wa sasa wa Libya ambao ni Baraza la Mpito la Nchi hiyo (NTC) ambalo lilitangaza kuzika mwili huo kwa siri, ili kuficha mahali lilipo kaburi la kiongozi huyo wa Libya kwa miaka 42.

Mwili huo ulichukuliwa na kupelekwa kuzikwa kusikojulikana, baada ya ndugu na watu wake kadhaa wa karibu kuruhusiwa kushiriki katika sala maalum na taratibu zote za Kiislamu.

Mmoja wa wasemaji wa NTC alisema jana kuwa mwili wa Gaddafi, mwanae Mutassim pamoja na mmoja wa wasaidizi wake imezikwa, licha ya kuwapo kwa utata kuhusu pale ilipostahili kuzikwa.

Mvutano uliokuwapo ulitokana na ombi la ndugu wa kabila la Kanali Gaddafi ambao walikuwa wakitaka wapewe mwili wa kiongozi huyo ili wauzike mjini Sirte, alipozaliwa, lakini viongozi wa baraza la kitaifa la mpito walipinga ombi hilo.

Taarifa nyingine zinamnukuu msemaji wa NTC, Ibrahim Beitalmal akisema ndugu wachache wa familia ya Gaddafi walishiriki katika taratibu za ibada ya mazishi ya kiongozi huyo na dua, vilivyofanyika kwa kuzingatia taratibu za dini ya Kiislamu.

Hata hivyo, habari zaidi zinadai kuwa, baada ya sala hiyo, ndugu wa Gaddafi hawakuruhusiwa kuona sehemu ambayo kiongozi huyo amezikwa ambako kunadaiwa kuwa ni katikati ya jangwa.

Baadhi ya watu mjini Misrata wanasema miili ya watu hao watatu iliondolewa usiku kutoka sehemu ilipokiuwa imehifadhiwa katika harakati za kupanga mazishi hayo.

Raia wa Libya wamekuwa wakitembelea eneo hilo la bucha katika mji wa Misrata ambako miili hiyo ilipelekwa na kuhifadhiwa baada ya tangazo la kifo cha kiongozi huyo na baadhi ya walinzi wake, kujionea mwili wake ili kuthibitisha ukweli kuwa ameuawa.

Viongozi wa NTC walikuwa wanahofia kuwa huenda Kanali Gaddafi akizikwa katika sehemu ya wazi, kaburi lake litabadilishwa kuwa pahali patakatifu na wafuasi wake.

Pamoja na hilo, mashirika ya kutetea haki za binadamu yamekuwa yakishinikiza uchunguzi ufanyike kubainisha jinsi alivyouawa Kanali Gaddafi, kwani picha za awali zilionyesha kuwa alikamatwa akiwa hai.

Kiongozi wa NTC, Mustafa Abdul Jalil, ametangaza kuwa uchunguzi utafanyika kuhusu hilo. Hata hivyo, kuna wale wanaohoji ikiwa kweli uchunguzi huo utakuwa wa wazi ikiwa mashirika ya kujitegemea hayakuhusishwa.

Katika video iliyotolewa jana, kwa mujibu wa gazeti la Daily Mail la Uingereza, kijana mpiganaji anayedai kumuua Kanali Gaddafi baada ya kukamatwa akiwa hai kwenye mtaro wa majitaka, alisema hakuona sababu ya kumuacha aendelee kuwa hai na kumkabidhi kwa uongozi wa NTC.

“Tulimkamata, nilimpiga katika paji la uso. Baadhi ya wapiganaji wenzangu walikuwa wakilazimisha kutaka tumpeleke na kumkabidhi akiwa hai. Niliamua kumpiga risasi mbili. Moja kichwani na nyingine kifuani,” alisema.

Katika kutaka kuthibitisha hilo, kijana huyo alionyesha kipande cha nguo ya Gaddafi kikiwa kimetapakaa damu na pete ya dhahabu ambayo alimvua baada ya kumuua.

No comments:

Post a Comment