Waandishi Wetu
ASKOFU Msaidizi wa Jimbo Katoliki  la Bukoba, Mhashamu Methodius Kilaini, amemshangaa Naibu Spika Job  Ndugai kwa kile alichoeleza kuwa amekwepa kujibu hoja ya msingi  ya  Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye inayohusu nyongeza ya posho za  wabunge,  badala yake, ameshambulia kiongozi huyo kama mtu binafsi.
"Sumaye  kama mwanadamu anaweza akawa na upungufu mwingi, lakini alichokisema  kuhusu posho tujihoji kina ukweli gani? Hilo ndilo la msingi.  Alichotakiwa Ndugai ni kufafanua uhalali wa posho na sio kusema aliyetoa  hoja hiyo, hana usafi wa kuhoji."
Katika kuonesha kukerwa na  kauli ya Ndugai, kiongozi huyo wa kiroho alikemea kauli za baadhi ya  wanasiasa kutotaka kukosolewa hata pale wanapofanya makosa  na kutaka  watu waachwe waseme ukweli bila kuzibwa midomo wala kubezwa.
"  Watu waachwe waseme kweli wasibezwe. Kwamba naye (Sumaye) alijiongezea  posho, hilo ni jambo lingine ambalo kama anataka (Ndugai), alianzishe  mjadala watu wajadili. Lakini sasa tunazungumzia suala la posho za  wabunge ambazo sote zinatukera,"alisema Kilaini.
Kwa mujibu wa  Askofu Kilaini, si sahihi mtu kujadili hoja aliyoanzisha mtu kwa  kuangalia udhaifu wa mtoa hoja. "Hakuna hoja ya msingi katika  kumshambulia mtu anayetoa hoja kwa kutumia udhaifu wake, kwani ukweli  utaendelea kuwa ukweli na udhaifu wa mtu ni jambo lingine."
Askofu  Kilaini alisema: "Nataka watu wajue kwamba hakuna mtakatifu hapa, wote  tuna udhaifu, lakini kama mwenzetu kasema ukweli tujadili hoja yake kwa  moyo mkunjufu na sio kumpuuza kwa sababu tu eti aliyeongea ana upungufu  fulani."
Aliongeza;  "Ndugai lazima asome alama za nyakati. Huu  sio wakati wa kutetea posho kwani hakuna atakayemwelewa. Watanzania wa  matabaka yote wamezipinga sasa yeye akianza kuzitetea atabaki peke  yake."
Wanasheria
Kauli hiyo ya Askofu Kilaini, iliungwa mkono  na baadhi ya wanasheria waliozungumzia hoja hiyo jana ambao kwa nyakati  tofauti walisema kitendo cha Ndugai kuponda maoni ya Sumaye,  kimeonyesha kuwa si mtu makini.
Wakili wa kujitegemea, Lupia Augusto  alihoji kama Ndungai alikuwepo bungeni wakati sheria ya kupandisha posho  za viongozi wastaafu zilizomwezesha Sumaye kujiandalia uzee mwema,  kwanini hakupinga. "Iweje aje na hoja hiyo leo?"alihoji.
Augusto  alisema tabia aliyoionyesha  Ndugai inatakiwa kutafsiriwa kama hakujua  majukumu ya ubunge wake  wa kuhoji  na badala yake, alijua  itamnufaisha.Alifafanua kwamba kitendo alichokifanya Ndugai ni ishara  kwamba maoni yake yamekumbatia kujinufaisha na sio kunufaisha wananchi.
Alisema  Ndugai ameanika udhaifu wake kwani hakuna rekodi zinazoonyesha kwamba  alipinga hoja ya kupitisha posho ilipoletwa wakati Sumaye alipokuwa  Waziri Mkuu.Augusto alisema kuna kila dalili kwamba kuna mambo mengi  yanayofanywa kwa siri kwa maslahi ya wachache na kwamba wanapopingana  ndipo mambo hayo hujitokeza wazi.
 “Wananchi wajiulize alifanya  nini kupinga, maana hapa anaazisha malumbano yasiyokuwa na tija baada ya  watu kupinga posho ambazo wabunge wamejipandishia bila kuweka uzalendo  mbele,”alisema
Awakera wananchi
Baadhi ya  wananchi nao wameeleza kukerwa na kauli ya Ndugai dhidi ya Sumaye na  kwamba ni mbinu za kuwatisha viongozi wastaafu wasitetee maslai ya Umma.
Mkazi  wa Dar es Salaam, Kimazi Totera alisema Ndugai anatumia Bunge kama  sehemu ya kutetea matakwa yake binafsi kwa kuziua kauli za viongozi  wastaafu pale wanapotetea maslai ya Umma.
Fatma Haji alisema  Ndugai ana siri kubwa kutokana na kuyajua mazingira ya uongozi ya awamu  ya tatu kwa kudai Sumaye alijiwekea sheria ya viongozi wa juu wastaafu  kulipwa asilimia 80 ya mshahara.
“Yeye kama kiongozi alikuwa wapi  kupinga sheria ya viongozi hawa kulipwa kiwango hicho cha pesa ina maana  naye ana chuki binafsi, tungemwelewa kama angesema mapema,”alisema  Fatma.
Alichosema Sumaye
Jana alipotakiwa  kuzungumzia hoja za Ndugai jana, Sumaye alisema," No comment," nataka  kusoma na kuelewa vizuri alichokisema kwa hiyo unitafute kesho (leo)."
Kilichoamsha  hasira za Ndugai ni kauli ya Sumaye alioyoitoa kupitia kipindi cha  dakika 45 kinachorushwa na Kituo cha Televisheni cha ITV,  kwamba  ongezeko la posho za wabunge linaweza kuchochea makundi mengine kudai  kama Wanajeshi, Polisi, Mahakama na walimu nao kutaka nyongeza, hivyo  kumweka Rais katika wakati mgumu kufanya uamuzi.
“Mwanasiasa  mzuri akifanya jambo akiona limewaudhi wananchi anatakiwa aliache,  lakini pia kwenye hili huu mkanganyiko wa Spika na Katibu wake na huu  ukimya wa Ikulu ni tatizo, tungependa waseme ili umma ujue hali ikoje,”
 alisema Sumaye.
Alisema hatua ya Bunge kujipandishia posho ya kikao kutoka 70,000 hadi 200,000 kwa 
siku  haliingii akilini na kwamba, inakiuka utaratibu uliowekwa na serikali  katika kulipa gharama kwa maofisa wake ikiwa ni pamoja na gharama hizo   za fedha za kujikimu.
“Siyo kwamba napinga posho, wabunge  wanastahili posho, lakini kwa kweli kujiongezea kutoka 70,000 hadi  200,000 siyo sahihi,” alisema Sumaye.
Alisema wakati yeye  alipoteuliwa na Rais Benjamin Mkapa kwa awamu ya pili kushika wadhifa wa  Waziri Mkuu, aligoma kwa sababu alikuwa amekwaruzana  na wabunge kuhusu  nyongeza ya posho.
“Nilimwambia wabunge watanikataa kwa sababu  nimegombana nao sana juu ya suala la posho lakini akasema lazima uwe na  mimi ndipo nikakubali, lazima hili suala liangaliwe mara mbilimbili…,  leo wabunge mmejiongezea kesho jeshi, polisi na walimu nao watataka,  tutafanyaje tusifanye mambo ambayo yatamuweka Rais pabaya,” alisema  Sumaye.
Alisema posho ni jambo ambalo kwa sasa limekuwa tatizo  kwa serikali na kwamba imefika wakati ofisi za serikali zimehamia  hotelini, lengo likiwa ni watumishi wa umma kutafuta mwanya wa kulipana  posho. 
“Ndiyo maana watu wa TRA (Mamlaka ya Mapato Tanzania)  wanakusanya fedha nyingi lakini ni fedha kidogo sana zinakwenda kwenye  huduma za jamii, nadhani hili ni tatizo na ni utawala mbaya kabisa,  lazima kuwepo mabadiliko kama kweli tunataka kuisafisha nchi yetu,”  alisema Sumaye
No comments:
Post a Comment