JAMBAZI sugu mkoani Arusha anayetambuliwa kwa jina la Pokea Samsoni,  amemuua askari kanzu kwa risasi ya shingo na kumjeruhi Mkuu wa Upelelezi  wa Wilaya ya Arusha (OC-CID). 
Mauaji hayo yalifanyika jana saa 10 alfajiri katika Kijiji cha Nambala katika eneo la Shangarai 
wilayani Arumeru mkoani Arusha wakati jambazi huyo alipokuwa akijaribu kuwakimbia polisi. 
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Thobias Andengenye alimtaja  askari aliyeuawa kuwa ni Konstebo Kijanda Mwandu mwenye namba F. 2218. 
Kamanda Andengenye alisema polisi walipata taarifa kutoka kwa raia  wema kuwa nyumba inayomilikiwa na mkazi wa eneo hilo aliyejulikana kwa  jina moja la Agnes, inahifadhi majambazi. 
Alisema walielekezwa kuwa nyumba hiyo ipo barabara ya Peace Point eneo la Shangarai na 
ndipo walipojipanga na kwenda kufanya upekuzi na hatimaye kuwakamata watuhumiwa hao 
wa ujambazi.  
Andengenye alisema askari walipofika karibu na eneo la nyumba hiyo, jambazi hilo liliwahi 
kuwaona na kuanza kurusha risasi ovyo hewani na kwa bahati mbaya risasi moja ikampata 
huyu Konstebo Kijanda akafa papo hapo na nyingine kumpata OC-CID, Faustine Mafwele 
kwenye bega la kushoto.  
Kamanda Andengenye alisema kuwa Mkuu huyo wa Upelelezi amelazwa hospitalini kwa matibabu.  
Baada ya hapo jambazi hilo lilitoroka na msichana Agnes Silasi ili  kuficha maovu yao katika eneo hilo na katika upekuzi katika nyumba hiyo  walikuta risasi 36 za SMG, risasi 12 za shotgun, kitako kimoja cha  shotgun, mtutu mmoja, mtambo mmoja wa bunduki ya shotgun na soksi za  kuvaa usoni nyeusi mbili.  
Baada ya hapo polisi iliwakamata watoto wawili; Daines Msawe (9) mkazi wa Nambala na 
Allex Parumina (13) mkazi wa Nambala ili kuwahoji kwa sababu mmoja wa watoto hao ndiye 
aliyemfungulia mlango jambazi huyo na kutoka nje kufanya mashambulizi dhidi ya Polisi. 
“Kuanzia sasa polisi mkoani Arusha imetangaza donge nono la shilingi  milioni 5 kwa mtu yeyote atakayefanikisha kukamatwa kwa jambazi huyo.
No comments:
Post a Comment