Wednesday, January 4, 2012

Hatima ya Hamad CUF leo

BARAZA Kuu la Chama cha Wananchi (CUF) leo linatarajiwa kukata mzizi wa fitina kwa ama kumfukuza uanachama Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohammed na wenzake 13 au la.

Wakati baraza hilo kuu likitarajiwa kukata mzizi huo wa fitina, tayari mpasuko zaidi umejitokeza ndani yake baada ya uongozi wa chama hicho Mkoa wa Mwanza, kutishia kujiengua endapo Hamad na wenzake watafukuzwa.

Hamad na wanachama wengine 12 wa chama hicho watafikishwa mbele ya Kikao cha Baraza Kuu la uongozi la chama hicho kinachoketi mjini Zanzibar, kusomewa mashtaka na kuhukumiwa.

Katika barua walizopewa kutoka ofisi ya chama hicho, Dar es Salaam za Januari Mosi, mwaka huu na Shaweji Mketo kwa niaba ya Katibu Mkuu, Maalim Seif Shariff Hamad, wanachama hao wanatakiwa kufika kwenye kikao hicho bila kukosa. Barua hiyo inaeleza kuwa kikao hicho kitafanyika leo kuanzia saa 3:00, asubuhi katika Hoteli ya Mazson.

“Kwa mujibu wa Katiba ya CUF, kifungu cha 63 kinachozungumzia wajibu wa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa kifungu cha 63 (1)(d), kinafafanua wajibu huo kuwa ni kulinda na kuendeleza heshima ya chama na Serikali zote halali za nchi,” inasema sehemu ya barua hiyo na kuendelea:

“Kifungu cha 63 (1) (j) kinaeleza wajibu wa kuwachukulia hatua za kinidhamu viongozi na wanachama wanaoshutumiwa kwa makosa mbalimbali, kwa kufuata masharti ya katiba hiyo na kanuni zinazatungwa mara kwa mara.”
Sehemu ya barua hiyo ilifafanua zaidi kwamba kwa kuzingatia hali hiyo, Kamati ya Utendaji ya Taifa imeridhika kwamba kuna haja ya kutumia uwezo iliyopewa chini ya kifungu cha 62(1) cha Katiba ya CUF kuitisha kikao cha dharura cha Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la chama ili kutafakari hali hiyo na kusikiliza tuhuma zinazomkabili kila mmoja wao.

Wanachama hao pia watapata nafasi ya kujitetea ambayo ni ya kikatiba na kisha baraza hilo litatoa uamuzi kwa kadri inavyofaa, kwa mujibu wa katiba ya chama hicho.
CUF Mwanza

Wakati CUF kinajiandaa kutoa uamuzi juu ya mgogoro huo, huko Mwanza chama hicho kimetoa tamko la kutaka maamuzi hayo yawe ya kisayansi na kwa maslahi ya chama na si vinginevyo.

Akisoma tamko hilo kwa niaba ya wanachama wote jana, Mwenyekiti wa CUF Wilaya ya Nyamagana, Hamduni Mercei alisema wanachama hao wataunga mkono uamuzi utaoleta suluhu katika chama na hivyo kuwaweka wanachama na chama chao katika mazingira bora ya kujiimarisha kisiasa.

“Chama hakiko vizuri kimpangilio na tunahitaji juhudi za pamoja kuhakikisha tunarejea tulikotoka na pengine kwenda vizuri zaidi ya jinsi tulivyokuwa kabla na baada ya uchaguzi mkuu uliopita,” alisema Mercie na kuendelea:

“Tunaomba wajumbe na viongozi wetu watilie maanani maoni ambayo yanatolewa na wanachama mbalimbali wanaokitakia chama mafanikio, siasa iwe urafiki, udugu, kuvumiliana, kuheshimiana, kukosoana na kusameheana,” ilisomeka sehemu ya tamko hilo.


Hofu ya Hamad
Akizungumzia kikao hicho jana, Hamad alidai kwamba uamuzi utakaotolewa umeshapangwa na Maalim Seif.
Alisema yupo tayari kwa uamuzi wowote utakaotolewa lakini, hawezi kuhama chama na kwenda kingine kama inavyodhaniwa.

“Mimi nimeshajua wamepanga kutufukuza wanachama watatu mimi na wenzangu Doyo Hassan Doyo na Shoka Khamis Juma ambao tunaonekana ni vinara wa mgogoro ndani ya chama na wengine watapewa karipio,” alisema Hamad.

Wanachama wengine ambao wanadaiwa kwamba watapewa karipio ni Juma Said Saanani, Yasini Mrotwa, Mohamed Albadawi, Mohamed Masaga, Doni Waziri, Yusuph Mungiro, Haji Nanjase, Ahmed Issa, Tamim Omary, Amir Kirungi na Ayub Kimangile.Katika nakala ya barua pepe aliyoipata Hamad iliyotumwa Desemba 14, mwaka jana na Maalim Seif kwenda kwa Mwenyekiti wa CUF, Profesa Lipumba ilieleza kwamba, wameshauriana na makamu na wameona kuna haja ya kuwaita katika kamati ya wanachama hao.

“Nimeshauriana na makamu na tumeona kuna haja ya jamaa yako na genge lake kuitwa katika kamati ya nidhamu na maadili kuhojiwa, ushahidi wa kutosha umekusanywa dhidi yake na wasaidizi wake, Doyo na Shoka na kamati ya maadili ilete taarifa katika kikao kijacho cha Kamati ya Utendaji (KUT)ambacho  kitafanyika mwisho wa mwezi,” ilieleza barua hiyo.

 “Chama ki-act decisively hasa dhidi ya jamaa yako yeye muono wetu tumfukuze kwenye chama na akiamua kwenda mahakamani na mahakama kutoa uamuzi wa kumpendelea yeye mwache awe mbunge wa mahakama kama walivyokuwa wakina Asha Ngede na Naila Majid,” ilisisitiza sehemu ya barua hiyo.

No comments:

Post a Comment