Wednesday, January 4, 2012

Madaktari 229 wagoma Muhimbili

MADAKTARI 229 walioko katika mafunzo kwa njia ya vitendo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, jijini Dar es Salaam, wamegoma wakishinikiza kulipwa jumla ya Sh176 milioni, zikiwa ni posho zao za kijikimu.Mgomo huo ulianza jana mchana na madaktari hao wamesema hautakwisha hadi hapo watakapolipwa fedha zao.

Madaktari hao ni wa kada za tiba ya vinywa, maabara, dawa na wafamasia ambao wametishia mgomo huo utaenea hadi katika Hospitali za Mnazi Mmoja, Zanzibar, Bombo mkoani Tanga, Temeke, Amana na Mount Meru, jijini  Arusha ambako wenzao nao hawajalipwa kwa miezi miwili.

Wakizungumza  mbele ya Mganga Mkuu wa Serikali, Dk Deo Mtasiwa. aliyekwenda Muhimbili kuwasikiliza madai yao,  madakatari hao walisema maisha yao yamekuwa magumu kwa sababu ya kukosa fedha za kujikimu.
 Mmoja wa wataalamu hao,  Dk Frank Kagoro, alisema  tatizo  lililopo ni kukosekana kwa uwajibikaji kwa upande wa Serikali.

“Mnachukulia mambo kirahisi sana tupo katika mafunzo lakini tutawezaje kufanya kazi bila fedha. Tunajua tuna wagonjwa na wanaumia kwa sababu ya hatua hii, hivi nani hapa asiyejua kuwa muda huu alitakiwa kuwa wodini akiwapitia wagonjwa, hivi kweli mnatupa kipaumbele," alihoji Dk Kagoro.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa madaktari hao, Dk Mally Deogratius, alisema madai yao ni zaidi ya Sh176 milioni, zikiwa ni posho za kati ya Novemba na Desemba mwaka jana, kipindi ambacho hawakulipwa.
Hata hivyo, Dk Mtasiwa aliwahakikishia kuwa malipo yao yatafanyika leo na kwamba yamechelewa kutokana na taratibu za Serikali katika malipo.

Mgogomo wa madaktari hao, unakuja wakati wanafunzi wa udaktari waliokufuzwa katika Chuo Kikuu Kishiriki cha Sayansi cha Sayansi za Tiba cha Muhimbili, wakiwa wameomba radhi, kufuatia vurugu walizofanya mwezi uliopita.

Wanafunzi hao walifanya hivyo jana ambapo walisema wametafakari na kujiridhisha kuwa walifanya makosa yaliyosababisha kukosekana kwa amani na utulivu katika chuo hicho.Wanafunzi hao walifanya fujo Desemba 8 na 10 mwaka jana wakishinikiza kusikilizwa kwa madai yao.

No comments:

Post a Comment