Thursday, January 5, 2012

Magufuli awavimbia wabunge wa Dar

Boniface Meena
WAZIRI wa Ujenzi, Dk John Magufuli amepuuza msimamo wa wabunge wa Dar es Salaam wa kumtaka awaombe radhi, akisisitiza kuwa kauli yake ya kupandisha nauli katika kivuko cha Kigamboni hataibadilisha na wabunge hao, waache kupiga siasa.

Dk Magufuli alijikuta kwenye mvutano na wabunge wa Mkoa wa Dar es Salaam kufuatia kauli yake aliyotoa Jumapili iliyopita kwa wakazi wa Kigamboni, kuwa kama wakishindwa kulipa nauli ya Sh200, wapige mbizi habarini au wapite Kongowe ili kuingia katikati ya Jiji vinginevyo, warudi vijijini wakalime. 

Kauli hizo za kejeli ziliwafanya wabunge hao kupitia Mwenyekiti wao Abbas Mtemvu, kumtaka waziri huyo aombe radhi huku wakiwambia wao wanalijua jiji la Dar es Salaam kuliko Magufuli.
Pia walimtaka akafanye ubabe katika Jimbo lake la uchaguzi

Lakini jana akizungumza jijini Dar es Salaam, Dk Magufuli hakutaka kujibu maswali yaliyomtaka aeleze msimamo wake kuhusu msukumo huo wa wabunge, badala yake alisisitiza tu kwamba nauli mpya aliyoitangaza haitabadilika.

 "Waambieni (wabunge wa Dar es Salaam ) waache kupiga siasa, kama wanaona gharama ni kubwa wakajifunze kivuko cha Chato au waombe kukiendesha kivuko hicho kwa kuwa sheria inaruhusu," alisema.

Alisema Ibara ya 26 Ibara ndogo ya 1 na ya 2 inampa kila mtu wajibu wa kufuata sheria na kuongeza kwamba  yeye amefuata sheria kufanya ongezeko hilo la nauli za vivuko na hivyo  nauli hiyo halitabadilika.

"Kwa mujibu wa Farries Act iliyotungwa na kupitishwa na wabunge wenyewe  inanipa nguvu mimi waziri kufanya hivyo kwa hiyo hakuna sheria inayosema nikitaka kupandisha nauli nikawaulize wabunge," alisema Magufuli.


"Dar es Salaam itajengwa na watu wa kuja, Mtemvu na wenzake wajue hilo na tuache  siasa tufanye kazi. Nawaambia wakitaka kuendesha kivuko hicho nitashangilia sana kwani kwa mujibu wa sheria inaweza kuwa hivyo na kama wanapinga wakajifunze Chato watu wanakovuka kwa Sh 3,000," alisisitiza.

Dk Magufuli alisema wakazi wa Kigamboni wametii sheria kwa kuendelea kulipa nauli hiyo ambayo imefanya makusanyo katika kivuko hicho kutoka Sh9 milioni hadi kufikia Sh 18 milioni, fedha ambazo zitasaidia kivuko kujiendesha.

"Hao wanaolalalamika nawashangaa, Kigamboni zamani kitumbua walikuwa wakinunua Sh 50 sasa hivi ni Sh 250 na wananunua. Mnyika katika jimbo lake la Ubungo kuna kituo cha mabasi ya mikoani ambako ukimsindikiza tu mtu kuingia pale ni Sh 200 ananishangaza kweli kwa kupinga ongezeko hili,"alisema Dk Magufuli.

Alisema ni muhimu wabunge hao na wakazi wa Kigamboni wakafahamu kuwa Dar es Salaam ni ya watu wote na si ya watu wakuja tu hivyo ni muhimu ikajengwa kwa mshikamano.

"Ambacho wangetakiwa kikufanya wabunge hawa ni kutupongeza tulivyopambana na mafuriko ya Dar es Salaam na mimi kusitisha likizo kuja kuhakikisha madaraja yaliyoharibika yanajengwa haraka na si kupinga hili," alisema Dk Magufuli.

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika alipotakiwa kuzungumzia kauli hiyo ya Dk Magufuli alisema hawezi kusema chochote mpaka atakapopata taarifa kamili ya kilichozungumzwa.


Jumapili, Dk Magufuli alitsema Serikali imeamua kupandisha nauli kutoka Sh 100 hadi sh 200 kwa safari moja ya kivuko hicho na kwamba hiyo inatokana na gharama za uendeshaji kuwa za  juu.
Magufuli alisema kivuko cha Magogoni kimekuwa kikitoza nauli za chini ikilinganishwa na Chato, kinachotoza sh 300, Pangani Sh 200, Kisorya Sh 300, Lugolora Sh 500, Nyakarilo Sh 3000, Chato-Bukombo Sh 2,000, Kirambo sh 500 na Utete Sh 300, huku wanafunzi wakisafiri bure.Lakini, mbunge wa Kigamboni Dk Faustine Ndugulile alitoa hoja kupinga ongezeko hilo.

No comments:

Post a Comment