Daniel Rutoryo.
BEI ya mchele  imezidi kupanda Jijini Dar es Salaam  kutokana na upatikanaji wa nafaka hiyo kuwa adimu kutoka kwenye vyanzo  vyake  na sasa bidhaa hiyo inauzwa kwa bei ya Sh2500 tofauti na Sh2200  iliyokuwa bei ya mwishoni mwa mwaka 2011.
 Meneja Biashara wa  Soko la Kariakoo, Mrero Mgheni amethibitisha hali hiyo na kusema kuwa  imesababishwa na upatikanaji adimu wa bidhaa hiyo inayotegemea zaidi   msimu na kwamba kwa sasa mahitaji ya mchele ni makubwa kuliko akiba  iliyopo .
“Mchele umekuwa adimu kutokana na kipindi hiki si cha  msimu wa zao hili, hali hii imepelekea upatikanaji wake sokoni kuwa wa  shida sana ndiyo maana bidhaa hii imekuwa ikipanda kutoka mwishoni mwa  mwaka jana”. Alisema
Mrero alisema ukilinganisha  mchele na bidhaa  nyingine  zilizopanda mwishoni mwa mwaka jana kama nyanya, karoti,  maharagwe, viazi mviringo, kabeji na vitunguu, zimeshuka bei na kuwa   bei ya kawaida.
Mrero alielezea hali ya biashara katika soko la  kariakoo na kusema kwa sasa hairidhishi kutokana na wateja kutokuwa  wengi ukilinganisha na siku za nyuma, hali hii inayosababishwa na  maandalizi ya wanafunzi na kupunguza baadhi ya mahitaji kama chakula.
“Hali  ya biashara kwa sasa si nzuri sababu kaya nyingi zinafanya maandalizi  kwa ajili ya wanafunzi kwenda shule, baadhi ya mahitaji  kama chakula  yamepungua”. Alisema Mrero.
Mfanyabiashara katika soko la  Kariakoo,  Aziza Juma kwa upande wake alisema ugumu wa upatikanaji  mchele unatokana na   bidhaa hiyo kutegemewa na wafanyabiashara wengi  kwa kuwa mchele ndiyo chakula kikuu cha wakazi wa Jiji la Dar es Salaam.
“Mchele  ndiyo bidhaa inayouzika kwa wingi kwani haina Sikukuu wala nini lakini  chakushangaza bidhaa hii imekuwa adimu na ghali kupita kiasi  na ndiyo  inayotulazimu kuuza kwa bei ya juu ili nasi tupate kurudisha faida, hali  hii ikiendelea tutakuwa katika wakati mgumu”. Alisema Aziza
Vilevile  aliongeza kuwa kusema kutokana na hali iliyopo wakazi wengi wa jijini  itafika wakati  watashindwa kumudu mahitaji ya familia zao kutokana  kupanda kwa  hali ya maisha huku thamani ya pesa ikishuka .“Lazima  viongozi wetu wachukue hatua za makusudi ili kuimarisha uchumi”. Alisema  Aziza.
No comments:
Post a Comment