Friday, January 20, 2012

Kisa na Mkasa na Salim Kikeke

Mwizi na Mlegezo

Saggy
Mtindo wa Kata K
Mwizi mmoja hapa London aliyekuwa akijaribu kukimbia baada ya kufanya wizi wake, aliuhisi mkono wa sheria ukimkamata baada ya kuanguka, kwa kuwa alikuwa amevaa suruali yake katika mtindo uitwao mlegezo, au kata K.
Gazeti la Metro limesema John O'Dell alisimamishwa na polisi katika eneo la harringey, kaskazini mwa London siku ya Jumapili, lakini badala yake akaamua kukimbia.
Hata hivyo, kwa kuwa alikuwa amevaa suruali yake bila mkanda na katika mtindo wa mlegezo, suruali hiyo iliteremka na kumfanya adondoke na kukamatwa na polisi mara moja. Tukio hilo lilishuhudiwa na wapita njia. Mpita njia Harry Robbins aliyeshuhudia sakata hilo amesema, kwa kuwa hakuwa amevaa mkanda, ilikuwa ni kichekesho jinsi suruali yake mwenyewe ilivyomuangusha na kusababisha kukamatwa. Wote tuliokuwepo tulibaki tukicheka, amesema Robbins. Mwizi huyo baada ya kukamatwa alikiri kuiba laptop ya karibu dola mia tano -- atafikishwa mahakamani Januari 31.

Mimba ya Mochuari

Mochuari
Mfanyakazi wa mochuari

Mwanamama mmoja nchini Marekani anayefanya kazi mochuari ameingia matatani baada ya kupata uja uzito kwa kujamiiana na mtu aliyekufa. Mtandao wa habari wa dead serious news umesema tukio hilo linadhaniwa kutokea katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Mourning Glory, nje ya Lexington, Missouri.
Polisi wa mjini humo wamemshtaki mama huyo aitwaye Felicity Marmaduke kwa kosa la kunajisi na kuchezea maiti. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na polisi, kiungo cha kiume cha mwili wa mtu aliyekufa kilihamasika wakati mwili ukioshwa. Taarifa zinasema, kwa kuwa mwanamama huyo alikuwa peke yake, aliamua kujamiiana na mwili huo.
Kwa mshangao hata wa mwanamama huyo, maiti huyo alitoa mbegu za kiume. Wiki chache baadaye Bi Marmaduke alijikuta ni mja mzito. Baada ya kumwambia daktari wake mfululizo wa matukio, daktari huyo aliwataarifu polisi.
Bi Marmaduke alikamatwa na polisi akiwa nyumabni kwake, si mbali sana na mochuari anayofanyia kazi. Katika tukio la kushangaza zaidi, mwanamama huyo amesema anapanga kudai urithi kutoka kwa familia ya mtu huyo aliyekufa.

Wasiolia kupewa adhabu?

Kim
Mazishi ya Kim Jong-il
Mamlaka za Korea kaskazini zinadaiwa kuwaadhibu wananchi wake kwa kuwapeleka jela na kazi ngumu-- wale wote ambao hawakulia vya kutosha katika msiba wa kiongozi wao Kim Jong-il.
Gazeti la kila siku lenye makao yake makuu Korea Kusini NK limesema yeyote ambaye hakushiriki misa ya kihistoria ya kumuenzi Kim au ambaye alihudhuria lakini hakulia kiasi cha kutosha au kuonekana kulia kwa uongo, atapelekwa katika kambi maalum na kufanyishwa kazi ngumu kwa miezi sita, limeripoti gazeti hilo.
Gazeti hilo limedai huku likikariri chanzo ambacho haikukitaja kuwa yeyote aliyejaribu kutoka nje ya nchi wakati huo atashtakiwa katika mahakama mbele ya kadamnasi. Kwa mujibu wa taarifa zilizochapishwa kwenye mtandao wa cnews.com, wengine watapelekwa katika kambi na kupewa elimu upya ya utaifa.
Hakuna taarifa rasmi kutoka Korea kaskazini iliyothibitisha taarifa hizi. Hata hivyo shirika la habari la Korea Kaskazini limeripoti wiki iliyopita kuwa kifo cha Kim Jong-il kiliombolezwa hadi na wanyama wa porini.
"Dubu mmoja akiwa na wanae walionekana wakiwa wanalia kwa nguvu" imesema taarifa ya shirika hilo. Madubu hao sio wanyama pekee ambao wameripotiwa kumuomboleza kiongozi huyo.
Shirika hilo liliripoti mwezi uliopita kuwa mamia ya kunguru aina ya Magpies walionekana wakipeperuka kuzunguka sanamu la Rais Kim katika wilaya ya Magyondae.

Polisi mwizi

Police
Polisi wa Moscow

Polisi katika mji wa St Petersburg wamesema wamemkamata afisa wa polisi akiwa anaendesha gari la wizi.
Gazeti la RIA Novosti limeripoti siku ya Alhamis kuwa polisi huyo kapteni Andrei Makononeko alikutwa akiendesha gari ya wizi aina ya Lexus na huenda akafunguliwa mashtaka. Kamati ya uchunguzi ya Urusi imesema polisi huyo alikamatwa Januari 10. Gari hilo liliibiwa mwezi Novemba, wamesema polisi. Uchunguzi unafanyika kutazama iwapo mashtaka yafunguliwe dhidi ya afisa huyo.

Usipige 999 hovyo

Police
Polisi wa Uingereza
Polisi wa Uingereza wamewataka wananchi wake kutotumia hovyo namba ya dharura, baada ya mtu mmoja kupiga simu na kuripoti ugomvi uliokuwa ukitokea kwenye TV.
Mtandao wa MSN umesema bwana mmoja alipiga simu polisi baada ya ugomvi kuzuka katika tamthilia aliyokuwa akitazama kwenye TV.
Taarifa zinasema bwana huyo alikuwa akitazama tamthilia maarufu Uingereza iitwayo EastEanders, na kipande hicho chenye mzozano kilirekodiwa mwaka 2009. Taarifa za polisi zimetolewa ili kuwafahamisha wananchi umuhimu wa kutumia simuza dharura, na kuainisha zipi ni dharura na zipi sio dharura.

Na kwa Taarifa yako....

Huwezi kujiua kwa kushikilia pumzi yako mwenyewe.

Tukutane wiki ijayo...... Panapo Majaaliwa...
Taarifa kutoka mitandao mbalimbali ya habari duniani

No comments:

Post a Comment