Wednesday, November 16, 2011

Kesi ya Prof. Mahalu kusikilizwa tena leo

Na Rehema Mohamed

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jana imeshindwa kuendelea kusikiliza kesi ya kuhujumu uchumi na kuipatia serikali hasara ya
sh.bilioni 2 inayomkabili aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia Profesa Costa Mahalu na mwenzake kutokana na hakimu anayesikiliza kesi hiyo kutokuwepo mahakamani..


Ilidaiwa mahakamani hapo jana na hakimu Bw.Mustafa Siyani kuwa hakimu anayesikiliza kesi hiyo Bw.Ilvin Mugeta ana majukumu mengine ya kikazi nje ya mahakama.

Kutokana na hali hiyo kesi hiyo iliahilishwa na itaendelea kusikilizwa  leo.Kesi hiyo ipo katika hatua ya kusikiliza utetezi ambapo mshtakiwa wa kwanza Prof.Mahalu ameanza kujitetea.

Mshitakiwa mwingine katika kesi hiyo ni Bi.Grace Martin aliyekuwa Ofisa Mwandamizi wa ubalozi huo.

Mara ya mwisho upande wa  mashtaka ukiwakilishwa na wakili wa serikali Bw.Ponsiano Lukosi uliiomba mahakama uwape muda wa kukusanya nyaraka mbalimbali ambazo zilikuwa zikilalamikiwa na Prof.Mahalu.

Wakati akitoa ushahidi wake Prof.Mahalu alidai kuna nyaraka 11 alizoomba azitoe mahakamani hapo kama vielelezo katika utetezi wake ambazo ni vivuli kwa sababu alishindwa kupata nakala halisi kutokana na chuki dhidi yake kwa baadhi ya watumishi wa Serikali kwa sababu yeye ni mshitakiwa.

Miongoni mwa nyaraka hizo ni viambatanishi katika barua iliyotolewa na Serikali ambazo upande wa mashtaka ulidai hawana kopi halisi na hawawezi kuvipata kwa sababu sio wao walioziandaa.Upande wa mashtaka leo unatarajiwa kuja na nakala hizo halisi.

No comments:

Post a Comment