Saturday, November 26, 2011

Lowassa apambana

'Fainali’ Uvuaji Gamba CCM

Edward Lowassa
Edward Lowassa
 
Hatima yake na Andrew Chenge mashakani
Wafuasi wake wamfananisha na Rais Jacob Zuma
January amkera Rais Kikwete, hoja yake yazimwa
UVCCM vurugu tupu Dodoma
UPEPO wa hali ya kisiasa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) unazidi kuvuma, na sasa watu wanaotajwa kuwa na nguvu kubwa ndani ya chama hicho, Edward Lowassa na Andrew Chenge, wamebanwa na wanapambana ‘kufa au kupona’.
Japokuwa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye, juzi Jumatatu, alilaumu vyombo vya habari kwa kupandisha joto nchini kuhusiana na matukio  ndani ya chama hicho, ukweli ni kwamba kuna upepo mbaya unavuma ndani ya CCM, na kila kitu kinachofanyika ndani ya vikao kinaleta hisia mchanganyiko.
Tayari imethibitika kwamba Lowassa na Chenge wako vitani kujibu mapigo wakisaidiwa na kundi kubwa la wafuasi wao wakiwamo viongozi wa Umoja wa Vijana wa chama hicho (UVCCM) waliofika Dodoma kuwasaidia kuokoa jahazi, hatua ambayo nayo imeiweka jumuiya hiyo katika hatari ya kuvunjwa kwa muda.
January Makamba amkera Kikwete
Mjumbe mmoja wa  Kamati Kuu ya CCM, January Makamba anaelezwa kuwa aliwasilisha mada, juzi Jumatatu, inayozungumzia hali ya kisiasa nchini akipendekeza uamuzi wa kuwachukulia hatua kina Lowassa na Chenge usitishwe ili kuepuka mgawanyiko ndani ya chama.
Katika kujenga hoja, mjumbe huyo alitoa mfano wa mjadala wa Katiba na nguvu kubwa ya CHADEMA nchi nzima kuwa inabidi CCM iepuke mgawanyiko unaoweza kutokea kwa kuwang’oa wenzao wanaotuhumiwa kwa ufisadi.
Hata hivyo, mapendekezo hayo yalionekana kumkera Mwenyekiti, Rais Kikwete, ambaye alihoji ni nani aliyesababisha mgawanyiko, na nini madhara ya kisiasa kwa CCM kutokua na msimamo katika kukemea uovu.
Rais Kikwete alipoonyesha kupinga moja kwa moja mawazo ya kuahirisha ‘uvuaji gamba’, alibadili hali ya hewa ndani ya kikao hicho kilichoahirishwa Jumatatu usiku na kuendelea Jumanne asubuhi.
Lowassa, Chenge wakataa kujiondoa NEC
Taarifa kutoka kwa watu walio karibu na Lowassa na Chenge, mjini Dodoma, zinaeleza kwamba awali wanasiasa hao walielezwa wazi wazi kujiondoa wenyewe kutoka NEC na kubakia na ubunge, ushauri ambao waliupinga moja kwa moja.
Imeelezwa kwamba pamoja na kukiri udhaifu na kuomba kuwapo kwa suluhu, Lowassa anaelezwa kujitetea kwa kuhoji ni kwa nini achukuliwe hatua peke yake wakati wapo baadhi ya viongozi ambao wanatuhumiwa na wengine wamekwisha kufikishwa mahakamani kwa makosa mbalimbali, na kutoa changamoto kwa Serikali kumchukulia hatua za kisheria kama inaona yeye ni fisadi.
“Wanasema yeye ni fisadi ajivue gamba, yeye akawaambia; mbona kuna wengine hadi mahakama imewatia hatiani lakini hawachukuliwi hatua zozote na kusema kama kweli ana makosa kwanini hafikishwi mahakamani?” , alisema mfuasi mmoja wa Lowassa ambaye yuko mjini Dodoma.
Hata hivyo, utetezi huo wa Lowassa ulikwisha kupatiwa majibu na Nape ambaye aliwaambia waandishi wa habari kwamba suala la ‘uvuaji gamba’ si la watu watatu tu, lakini ni lazima pawepo pa kuanzia.
Utetezi wa Lowassa umekuwa na nguvu kubwa na hapa Dodoma, kuna makundi makubwa ya watu; hasa vijana wanaodai ni wafuasi wa CCM, wakiwa na fedha nyingi, wanaendesha vikao kwenye mahoteli na mabaa na wanataja baadhi ya ajenda zilizowaleta hapa.
Kati ya ajenda hizo ni kuhakikisha kwamba ile dhana ya ‘kujivua gamba’ iliyoasisiswa na Mwenyekiti wao, Rais Jakaya Kikwete, mwanzoni mwa mwaka huu, inakomea hapo ilipofikia, isiwaguse watu wengine, na hasa Lowassa - Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa ya umeme mwaka 2008 na Mbunge wa Monduli; na Andrew Chenge, Mwanasheria Mkuu wa zamani na Mbunge wa Bariadi Magharibi.
Baadhi ya vijana hao wamekuwa wakimfananisha Lowassa na Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma, ambaye aliandamwa na kashfa za rushwa na ukosefu wa maadili kabla ya kushinda kesi mahakamani na baadaye kushinda uchaguzi ndani ya chama chake na kuwa Rais.
Lowassa afananishwa na Zuma
“Wameanza kumfananisha Lowassa na Zuma na kwamba atashinda tuhuma zinazoelekezwa kwake na kuwa Rais wa Tanzania baadaye,” anasema mmoja wa vijana wa UVCCM aliyeko Dodoma.
Vijana hao, wakiwamo viongozi wa karibu mikoa yote wa Umoja wa UVCCM, wanasema wako Dodoma kushinikiza mpango wanaodai unaandaliwa wa kuuvunja umoja wao, uachwe.
Ukiacha taarifa zinazosema kuna hali ya kuvutana ndani ya CCM na hata katika vikao vyake vya juu vilivyoanza hapa mwishoni mwa wiki iliyopita, kuhusu hatua za kuchukuliwa dhidi ya Lowassa na Chenge, ambao maazimio ya mkutano uliopita wa Halimashauri Kuu (NEC) yanasema wachukue hatua ya kujiondoa ama vinginevyo chama kitaamua wao wakishindwa, yapo maoni kwamba UVCCM ya leo haina msaada kwa chama.
Ni umoja unaoonekana kuendeshwa kwa kufuata matakwa ya watu kadhaa ambao wamekuwa wafadhili wakuu wa baadhi ya viongozi wa umoja huo .
Inasemwa kwamba baadhi ya viongozi wa UVCCM sasa nao wana fedha na mali ambazo kwa kazi na kipato chao, hawawezi kuthibitisha wamezipata wapi.
Mwishoni mwa wiki iliyopita na mwanzoni mwa wiki hii, umoja huo ulizua tafrani kubwa hapa Dodoma pale ziliposambazwa taarifa kwamba ulitaka kuitisha kikao cha dharura cha Baraza lake ili kutoa tamko kwamba hauko tayari kuvunjwa, na ikitokea ukavunjwa, basi,vijana wote watahamia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Taarifa za ndani ya CCM zinasema kwamba ni kweli mwenendo wa UVCCM umekuwa hauwaridhishi wengi, na kwa ajili hiyo baadhi ya viongozi wa umoja huo waliitwa mbele ya Kamati ya Maadili kutoa maelezo ya baadhi ya matamshi na matendo yao.
Bashe na wenzake waitwa kuhojiwa
Kati ya wanaotajwa kuitwa mbele ya Kamati ya Maadili Jumapili iliyopita ni Hussein Bashe, mjumbe wa Baraza Kuu la Vijana. Ukiacha nafasi hiyo ndani ya UVCCM, Bashe ni mwajiriwa wa kampuni ya magazeti ya New Habari inayomilikiwa na mfanyabiashara Rostam Aziz na mbunge wa zamani wa Igunga aliyejiondoa katika siasa miezi kadhaa iliyopita akidai amechoshwa na siasa chafu. Bashe ni mtendaji mkuu katika kampuni hiyo ya Rostam.
Kama walivyo Lowassa na Chenge, Rostam naye alikuwa akituhumiwa na chama chake kuwa kwa matendo yake na kutajwa sana katika matukio ya ufisadi; ya kampuni iliyochota fedha Benki Kuu ya Kagoda na kashfa ya kampuni ya kufua umeme ya Richmond, anakikosesha mvuto mbele ya jamii jambo ambalo lilichangia kupungua kwa kura za mgombea wa CCM wa nafasi ya rais, Kikwete, ambaye aliporomoka hadi kufikia kura asilimia 61 katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana kutoka katika asilimia 82 za mwaka 2005.
Bashe amekuwa akidaiwa kwamba alitoa matamshi mabaya dhidi ya chama chake akiwa wilayani Nzega alipoashiria kudai kwamba CCM isingeshinda katika uchaguzi mdogo wa kuziba nafasi ya Rostam, Igunga, na hiyo ingesaidia kuweka heshima.
Imefahamika kwamba kamati hiyo pia ilimwita Katibu wa  Mkoa wa Dar es Salaam, Kirumbe Ng’enda, ambaye anatuhumiwa kusababisha mtafaruku katika zoezi la kura za maoni kiasi cha kumshusha mmoja wa wagombea nafasi za udiwani wa viti maalumu vya wanawake kutoka nafasi ya juu hadi ya chini katika mazingira yanayoashiria ufisadi.
Kamati ya Maadili ina wajumbe wazito, baadhi yao ni: Mwenyekiti Kikwete, Makamu wenyeviti, Pius Msekwa na Amani Karume, Makamu wa Pili wa SMZ, Balozi Seif Iddi,Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Katibu Mkuu, Wilson Mukama na Manaibu Katibu Mkuu, Kapteni mstaafu John Chiligati na Vuai Ali Vuai.
Hakuna taarifa zilizokuwa zimepatikana kuhusiana na hatima ya Bashe na Ng’enda na baadhi ya wanachama wa UVCCM wanaodaiwa kutoa matamshi ya kashfa kwa Mwenyekiti ambao nao waliitwa.
Kwa kawaida, kamati hiyo ina mamlaka ya kuchukua hatua, lakini pia inaweza kupendekeza hatua za kuchukuliwa na vikao vya juu zaidi, yaani Kamati Kuu ambayo sehemu ya wajumbe wake ni haohao wa kwenye Kamati ya Maadili na NEC.
Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya siasa nchini  wanasema kwamba kwa kuchoshwa na matatizo ya UVCCM, CCM inaweza kufanya kama ilivyopata kufanya huko nyuma.
Katika kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1995, UVCCM iliweka msimamo uliokuwa unachagiza wagombea vijana wapewe nafasi ya kuwania urais. Majina yaliyokuwa yakitajwa wakati huo ni pamoja na ya kina Kikwete na Lowassa, waliokuwa wakiungwa mkono na kina Anne Makinda na wengineo. Joto lilipozidi, uongozi wa juu wa UVCCM uliondolewa na hali ikabaki salama.
Baadhi ya waliokuwa katika uongozi wa UVCCM wakati huo ni pamoja na John Guninita ambaye leo ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam. Vijana wengine wa enzi hizo ni pamoja William Lukuvi ambaye sasa ni mjumbe wa Kamati Kuu, Leonidas Gama ambaye sasa ni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro na Muhammed Seif Khatibu, John Henjewele na Said Mwambungu ambaye sasa ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma.
Aidha, wachambuzi hao wanasema hata ‘kujivua gamba’ kulikwishakufanyika ndani ya CCM japo kwa msamiati mwingine, lakini wenye maana karibu na huo.
“Mwaka 1984 walisema hali ya kisiasa ilikuwa imechafuka na kuchafuka huko kukaondoka na aliyekuwa Rais wa Zanzibar, Aboud Jumbe Mwinyi. Baadaye mkono huo wa CCM ukamfikia Maalim Seif Shariff Hamad na wenzake.
“Lakini hata huko nyuma, miaka ile kati ya 1960 watu kama Wilfreim Mwakitwange, Fortunatus Masha, Choga na Kasanga Tumbo  ambao walikuwa wabunge maarufu, walifukuzwa ndani ya TANU na chama hakikutetereka,” anasema mmoja wa wachambuzi hao.
Akizungumza na waandishi wa habari juzi kuhusu joto hilo la kisiasa hapa na nchini kwa ujumla, Nape alisema hakuna haja ya kuwa na hofu ya mageuzi yanayofanyika sasa ndani ya CCM kwa vile yanalenga kukiboresha chama hicho.
"Kama kwa kusimamiavyema  rasilimali na kupiga vita rushwa na ufisadini kutaleta mpasuko, nadhani mpasuko huo utakuwa ni mwema kwa vile utaondoa dhambi ndani ya chama," alisema Nape akiomba vyombo vya habari kuwa na subira.
Aliongeza Nape: “Ikifika hatua ya wananchi kuwa na shaka ya uadilifu wa mtu au chama,ni lazima kuhakikisha shaka hiyo inatoka kwa kufanya mageuzi."
Kikao cha Kamati Kuu kilianza hapa juzi na kilitarajiwa kuendelea jana kabla ya cha  NEC kilichopangwa kuanza leo Jumatano na kukamilika kesho Alhamisi.
NEC inakutana baada ya kikao chake cha mwisho cha Aprili mwaka huu ambacho kiliazimia ya kuwa wanaokishusia chama mvuto wajuvue gamba.
Uamuzi huo ulikuwa umechangiwa kwa kiasi kikubwa na maoni shawishi ya mmoja wa Wenyeviti wa Mikoa, Mwenyekiti  wa Mkoa wa Mara, Charles Makongoro Nyerere, aliyesema watu wa kawaida walikuwa wakishangazwa na CCM kuendelea kukumbatia watu waliokuwa wakionekana  wanashiriki katika ufisadi.
Akichangia wakati huo katika tathmini na mapendekezo ya Kamati Kuu ya kutaka Chenge, Lowassa na Rostam wawajibike, Makongoro  Nyererealisema isingewezekana Chenge, Lowassa na Rostam kuendelea kuwa na nafasi za uongozi ndani ya chama.
Alisema wakati huo mtoa habari wetu: “ Kwanza alianza kwa kumwambia Mwenyekiti kwamba japo yeye ni Mwenyekiti wa Taifa, yeye (Makongoro)  naye ni Mwenyekiti wa Mara na kwamba NEC ndio waajiri wa Mwenyekiti Taifa.
“ Akasema anapokaa Mwenyekiti wa Taifa ni mahala patakatifu na kwa ajili hiyo pasingeweza kusogelewa na shetani, hata kama siku moja Mungu alipata kukutana na shetani barabani.
“ Akasema kule site (kwenye eneo la ujenzi ambako yeye ndiko anakoshinda akichanganya zege na kupiga bati) wanasema na wanataka watuhumiwa wote wa ufisadi watoke kwenye nafasi zao.
“Lowassa ni ndugu yangu.Sina matatizo naye.Najua ananipenda, nami nampenda.Lakini kule site wanasema hapana.Atoke. Tena nawe Mweyekiti ulipokwenda Monduli, ukainua mkono wake juu, ukasema hujapata kuona kama yeye (Lowassa), kule site wakauliza, sasa hii  ndiyo nini?
“Rostam simfahamu vizuri. Ninakotembelea yeye hawezi kuja na  mimi siwezi kwenda anakotembelea. Sina ugomvi naye.Lakini kule site wanasema naye hapana. Ulipokwenda Igunga ukamuamsha mkono ukasema ni kama timu ya mpira iliyokamilika watu kwenye site wakauliza sasa hii ndiyo nini?
“Nasikia Chenge wanamwita Mzee wa Vijisenti. Ni ndugu yangu. Sina hakika kama anavyo vijisenti kiasi hicho. Lakini kwenye site, si mimi, watu wanasema naye hapana, “ alikaririwa akisema Makongoro.
Mifano aliyoitaja Makongoro kwa kumhusisha Kikwete ilijitokeza wakati akiwa katika kampeni za Uchaguzi Mkuu wa 2010, katika majimbo ya Igunga alikokuwa akigombea ubunge Rostam na Monduli alikogombea ubunge Lowassa.
Akiwa katika majimbo hayo, Kikwete aliwanadi viongozi hao waliokuwa wamepitishwa na chama chake kuwania ubunge, licha ya tuhuma za ufisadi zilizokuwa zikielekezwa kwao.
Mwingine ambaye alichangia sana katika uamuzi wa NEC wa Aprili ni Mwanasheria Mkuu, Jaji Frederick Werema, aliyekuwa amealikwa kwenda kusaidia katika fafanuzi kadhaa ndani ya Kamati Kuu.
Ufafanuzi huo wa Werema ulihusu mchakato wa kupata katiba mpya ambao umepitishwa na Bunge wiki iliyopita.
Mpasha habari wetu wakati huo alisema:  “Kuondoka kwakina Lowassa, Rostam na Chenge kimeharakishwa na Werema. Aliletwa na Mwenyekiti kuja kufafanua mambo kadhaa kama mchakato wa katiba mpya.
“Katika mchango wake kama mtu aliyeko nje ya chama alizungumzia mambo ambayo yeye alisema hayaendi sawa ndani ya CCM. Kwanza alianza kwa kusema yeye si mwana CCM japo huko nyuma, kama walivyokuwa wengi, alipata kuwa mwanachama.
“Akasema kwao anakotoka (Jaji Werema anatoka Mkoa wa Mara)  mwanamume anapaswa kusema ukweli hata kama ukweli huo unauma kiasi gani.
“ Akasema kwamba alikuwa anaona tatizo kwamba taarifa nyingi za vikao kama hicho alichokuwa ameitwa kuzungumza, zilikuwa zinavuja sana.
“ Akasema hata hayo ambayo angeyasema, jioni yangekuwa yamewafikia watu wa nje, na wahusika wakubwa wa kuvujisha taarifa hizo walikuwa ndani ya Kamati Kuu hiyo hiyo.
“ Akiachana na hilo akahoji kwa nini, chama hicho kinalialia kuwa haiba yake imeshuka na wakati huo huo kikikumbatia vitu kama Richmond na Dowans ambavyo vinaichefua jamii na ambavyo wahusika wake wakuu wamo katika uongozi wa juu wa chama,” alisema mjumbe mmoja wa Kamati Kuu aliyezungumza na Raia Mwema.
Hadi tunakwenda mitamboni jana hakukuwa na taarifa mpya ya mwenendo wa kikao cha Kamati Kuu na maandalizi ya kikao cha NEC leo.
Raia Mwema hata hivyo ilishuhudia wajumbe kadhaa wa NEC waliokwisha kuwasili na kama ilivyo kawaida ya CCM, walikuwa katika vikundi vikundi wakiteta.

No comments:

Post a Comment